Historia ya Wafransisko

 

Ndugu Wadogo wa Kapelekesi (Mbeya) - Piccoli Fratelli a Kapelekesi (Mbeya) - Little Brothers at Kapelekesi (Mbeya)

 

 

 

Nd. Rikardo Maria, UNWA

 

 

HISTORIA YA WAFRANSISKO

 

 

 

JEDWALI LA FAMILIA YA KIFRANSISKO

 

 

 

 

 

 

 

 

1. UTAWA WA KWANZA

 

 

1.1. NDUGU WADOGO KUPAMBANA HADI KUTENGANISHWA (1226-1517)

 

1.1.1. MWANZO WA MAPAMBANO (1226-1318)

 

Mt. Fransisko alipokuwa hai alisongwa na kundi la Watumishi na wasomi wa utawa wake, likisaidiwa na viongozi wa juu wa Kanisa, ili alegeze masharti ya ufukara na kulinganisha zaidi shirika lake na yale ya zamani. Kwa karama yake ya pekee aliweza kukabili upinzani huo wote. Juhudi yake ya mwisho ya kuzuia shirika lisipotoke ni wasia aliouandika ili kusisitiza msimamo wake, kudai kanuni yake isifafanuliwe, pamoja na kukataza wanashirika wasimuombe Papa hati yoyote. Alipokufa utawa ukabaki mikononi mwa Watumishi hao, wakiongozwa na nd. Elia Bombarone, Mkuu wa shirika miaka 1221-1227, halafu 1232-1239.

Katikati ya hivyo vipindi vyake viwili vya uongozi, Mtumishi mkuu alikuwa nd. Yohane Parenti. Chini yake yalizuka mabishano makali kati ya walioshikilia wasia huo na wale waliotaka shirika lishindane na mashirika mengine. Yeye na Watumishi wengine wakadhani utatuzi unaweza kutokea kwa viongozi wa Kanisa tu. Akipokea ombi lao, Gregori IX (1227-1241) alitoa tamko rasmi la kwanza juu ya kanuni (1230), akitumia mamlaka yake ya Kipapa na pia ujuzi wake wa nia ya Mt. Fransisko (ndiye aliyemsaidia sana kutunga kanuni alipokuwa bado Kardinali, jina lake Ugolino). Upande wa ufukara kwa jumla alitetea msimamo wa mwanzilishi (kwa jinsi alivyomheshimu hata akamtangaza mtakatifu), ila aliulegeza kiasi, kwa lengo la kufanikisha zaidi utume wa Ndugu Wadogo na hivyo kurekebisha Kanisa lililokuwa na hali mbaya kiroho. Kwa ajili hiyo aliwapa hati na ruhusa nyingi za pekee dhidi ya mamlaka ya Maaskofu na maparoko. Kuhusu wasia alitamka kuwa si sheria inayowabana Wafransisko wasiweze kufafanua kanuni yao wala kufafanuliwa na Kanisa, wala kuomba wala kupewa hati na fadhili za Papa. Sababu ya msingi ni kuwa Kanisa liko juu kuliko kanuni.

Hivyo njia ikawa wazi kuligeuza shirika la wadogo walio wote sawa, wanaohubiri toba kwa unyenyekevu chini ya padri yeyote, liwe shirika imara la kikleri, lisilo chini ya Maaskofu isipokuwa kwa machache. Mageuzi hayo yalisababisha kwa muda mrefu upinzani mwingi wa Maaskofu na mapadri wanajimbo. Aliyesukuma sana shirika kufuata njia hiyo ni nd. Elia, ambaye alimjengea Mt. Fransisko kanisa zuri sana, halafu jirani nalo konventi kubwa mno, ili kushindana na abasia za Wabenedikto. Alimgeuza mwanzilishi kuwa fahari ya shirika badala ya kielelezo cha kufuatwa. Mwenye vipawa na elimu, ingawa bradha, aliathiri sana viongozi wa dini (Gregori IX) na wa siasa (Federiko II), alistawisha misheni huko Mashariki na kukuza nyumba za masomo, lakini pia alidhulumu vikali watetezi wa kanuni (hasa alimuacha nd. Kaisari wa Speyer afe kwa njaa kisha kumfunga). Bila ya kutembelea kanda za shirika, alishika uongozi wote mikononi mwake, akichagua Watumishi na walinzi, akihamisha ndugu, akituma wawakilishi wake huko na huko kusimamia kazi ya Watumishi, na akikataa kuitisha mkutano mkuu. Fahari zake binafsi, ushuru aliowatoza mfululizo Watumishi (kwa ajili ya ujenzi n.k.) vilisababisha wafanye njama dhidi yake, hadi Gregori IX akaitisha na kuendesha mkutano mkuu ambao ulimuondoa madarakani na kutunga sheria ili kupunguza mamlaka ya Mtumishi mkuu.

Nd. Aimoni wa Faversham, Mwingereza aliyeongoza upinzani, akaja kuwa Mtumishi mkuu (1240-1244), na kulipatia shirika sura ya kudumu kufuatana na mfano wa Wadominiko upande wa muundo, utume, masomo na liturujia. Taratibu za maisha zikazidi kufuata mitindo ya kimonaki, pamoja na watawa kujitafutia visingizio vya kisheria wasibanwe nazo. Makao ya kifukara ya upwekeni yalizidi kuachwa ili wanashirika wahamie nyumba kubwa za mijini, zenye makanisa makubwa ambamo wafanye utume, wakiwanyang’anya maparoko waamini na sadaka zao. Kama alivyofanya mwenyewe huko Paris, Ndugu Wadogo wakazidi kushika nafasi kwenye vyuo vikuu na vinginevyo, na kuwa na uzito mkubwa ndani ya Kanisa, jambo lililowasogeza mbali na udogo uliowapasa. Mabradha wakanyimwa kabisa nafasi za uongozi na kukubaliwa tu kutoa huduma ndogondogo za nyumbani (bustani n.k.), wakiwaachia raia huduma duni zaidi. Kazi za mikono nje ya konventi zilikatazwa; badala yake ile ya kuombaomba ikaja kusifiwa na kushika nafasi ya kwanza upande wa uchumi. Zilipangwa pia njia za hakika za kupata mahitaji, hasa kwa nyumba za masomo.

Alipokufa, nd. Kreshensi wa Iesi alishika nafasi yake (1244-1247), akatambua hali halisi, lakini hakuweza kuirekebisha (pia kwa sababu ya uzee wake). Akiona kwamba Mt. Fransisko alikuwa bado kielelezo cha wadogo, aliagiza zikusanywe habari zote juu yake, halafu akamuagiza nd. Thoma wa Celano aandike upya maisha ya mwanzilishi. Juhudi zake kwa ajili ya kushika njia ya kati hazikuridhisha wala upande mmoja (wenzi wa Mt. Fransisko na ndugu “wa Kiroho”, yaani wenye nia ya kushika kanuni kadiri ya Roho Mtakatifu) wala upande wa pili (“jumuia”, yaani waliopenda maisha katika konventi kubwa na hali ilivyo). Inosenti IV (1243-1254) alikubali kutoa tamko la pili juu ya kanuni (1245) ili kuilegeza. Hasa alifungua milango ili Ndugu Wadogo wajipatie vitu vingi, akitamka kuwa vyote walivyonavyo, kama si vya wafadhili tena, basi ni vya Papa. Hivyo kwa kutofautisha kutumia vitu na kuvimiliki kisheria, Ndugu Wadogo waliweza kujidai fukara ingawa wanatumia vingi, eti si vya kwao! Lakini wengi hawakuridhika na ujanja huo.

Akachaguliwa M.H. Yohane wa Parma (1247-1257), mtu wa kufaa sana kwa elimu na utakatifu, aliyeongoza hasa kwa mfano wa maisha yake bora. Alikusudia kurudisha shirika katika hali ya mwanzoni kufuatana na wasia, kwa kuheshimu Maaskofu na mapadri na kukataa fadhili za Papa. Alitembelea kwa miguu kanda zote akiamsha nia ya kushika kanuni na wasia. Hivyo mkutano mkuu (1254) ulisimamisha utumiaji wa fadhili kadhaa; lakini, alivyosema M.H. Egidi wa Asizi (+1262), juhudi hizo nzuri zilikuwa zimechelewa zisiweze kurekebisha shirika lote. Wapinzani walimshtaki M.H. Yohane, akalazimika kujiuzulu. Mkutano mkuu ulitaka aendelee, lakini mwenyewe hakurudi nyuma. Hatimaye walimuomba walau amchague mwandamizi wake, naye akamtaja Mt. Bonaventura wa Bagnoregio akaenda kuishi upwekeni.

Mt. Bonaventura (1257-1274), kufuatana na tabia yake, alikubali hali ilivyo na kujitahidi kuepusha shirika na hatari za nje na za ndani alizoziona mapema. Upinzani wa Maaskofu na maparoko dhidi ya Ndugu Wadogo ulikuwa umeungwa mkono na chuo kikuu cha Paris: hapo hazikupingwa tu ruhusa kadhaa walizopewa, bali msingi wenyewe wa mtindo wao na wa Wadominiko. Baada ya Mt. Bonaventura na Mt. Thoma wa Akwino kuutetea, Papa alilaani upinzani na kusifu sana mtindo wa Kiinjili. Mwalimu huyo kuchaguliwa kuwa Mtumishi mkuu kukawa ushindi mwingine mkubwa chuoni.

Mashambulizi ya kutisha zaidi yalitokea ndani, upande wa ndugu “wa Kiroho”. Mt. Bonaventura alijipangia kulinganisha uaminifu kwa kanuni na mabadiliko ya shirika, akionyesha hayo hayaendi kinyume cha nia ya mwanzilishi. Ili athibitishe hayo ilimpasa kuziondolea lawama msingi wowote kwa kupigania uaminifu kwa wito wa shirika. Mwenyewe alikubali bila ya wasiwasi matamko ya Mapapa juu ya kanuni kama ufafanuzi rasmi wa wachungaji wakuu wa Kanisa na wa shirika pia. Kielelezo cha Mt. Fransisko kilitakiwa kuzingatiwa na wote kwa umoja, bila ya kupishana kuhusu namna ya kukitazama. Kwa ajili hiyo alitunga kitabu rasmi cha maisha yake kilichopitishwa na mkutano mkuu hata ukaagiza maandishi yote yaliyotangulia yatekelezwe. Ndivyo shirika lilivyopotewa kwa muda mrefu na habari nyingi muhimu juu ya mwanzilishi. Kitabu alichokiandika, bila ya kusema uongo, kinaleta baadhi tu ya matendo na mafundisho ya Mt. Fransisko yaliyochaguliwa kwa makini ili kumchora kama mfano kamili wa Kristo msulubiwa na kusisitiza mang’amuzi yake bora ya kiroho, lakini kwa kuficha mambo fulanifulani kuhusu kipeo cha udogo. Aliheshimu ufukara kama sifa kuu na utukufu wa shirika, ingawa alijali mabadiliko yaliyotokea, yaani konventi kubwa mijini n.k. Kwake elimu pamoja na utume ni sehemu ya lazima ya utendaji wa Kifransisko. Kwa ajili hiyo alikubali ruhusa lilizopewa shirika, ingawa kwa udogo alipenda kupatana na Maaskofu na maparoko. Basi, chini ya uongozi wake shirika likatulia, kwa jinsi alivyoweza kulinganisha upendo kwa Mt. Fransisko na furaha kwa mabadiliko, hamu ya kuishi upwekeni muda mrefu pamoja na ndugu “wa Kiroho” na utetezi wa konventi za mijini.

Hata kwa nje shirika likazidi kuheshimiwa na kushika nafasi katika maisha ya Kanisa (utume mbalimbali, uchaguzi wa Papa, Mtaguso mkuu). Mt. Bonaventura akafa akiwa Kardinali, wakati wa Mtaguso II wa Lyons, ambao ulionyesha hatari kwa mashirika ya Ombaomba, kwa kuwa ulipitisha hati ya kuyafuta yote isipokuwa Wadominiko na Wafransisko, pamoja na Waaugustino na Wakarmeli. Lakini iliwabidi hao wapatane na wanajimbo kwa kujinyima baadhi ya ruhusa walizopewa. Hata hivyo Mapapa waliofuata wakaendelea kuwarudishia au kuwanyang’anya tena, mpaka Mtaguso wa Vienne (1311-1312) ulipofaulu kuwatungia sheria ya kudumu baada ya miaka mia ya mashindano: kwamba kuhusu maisha yao ya ndani na uongozi watawa wawe chini ya Papa moja kwa moja, ila kuhusu utume nje ya makanisa yao wawe chini ya Maaskofu na maparoko.

Mambo yakawa magumu zaidi ndani ya shirika, hata suala la ndugu “wa Kiroho” likawa zito kwa Kanisa lote. Mwelekeo wao ulianza kutia wasiwasi ulipoingiwa na unabii na mafundisho yaliyolaaniwa ya abati Yohakimu wa Fiore (+1202). Huyo aligawa historia katika nyakati tatu: ule wa Baba tangu Adamu hadi Kristo (ulioongozwa na watu wa ndoa), ule wa Mwana tangu Kristo hadi kipindi cha Yohakimu (ulioongozwa na makleri); hatimaye ule wa Roho Mtakatifu utakaoongozwa na watawa na kupindua Ukristo kwa kufuta uongozi wa Kanisa, sakramenti na sheria ili kuanzisha Kanisa la Kiroho, la furaha, upendo na uhuru kama matunda ya maisha ya kujikatalia. Shirika jipya la watu “wa Kiroho” litakuwa kielelezo cha maisha ya Kikristo. Wakati mpya utatangazwa na malaika wa mhuri wa sita, mwenye alama ya Mungu aliye hai na mleta Injili ya milele, yaani ya Kiroho. Wafransisko wengi wakachangamka na kumuona Fransisko kuwa ndiye malaika mwenye alama ya madonda matakatifu na mleta Injili ya milele, yaani kanuni yake! Ndugu Wadogo wakajiona kuwa shirika hilo jipya ambalo lilete Kanisa la Kiroho lenye kufuata ufukara. Hapo jina “ndugu wa Kiroho” likawa na maana mpya na kuwaelekeza kupinga uongozi wa Kanisa, kuanzia Mtaguso II wa Lyons, walipojiandaa kukataa maagizo waliyoambiwa watapewa kinyume cha haki.

Upinzani ukalipuka hasa baada ya Nikola III (1277-1280) kutoa hati nyingine juu ya kanuni (1279) ili kuwaondolea Ndugu Wadogo wasiwasi wowote kuhusu namna ya kuitekeleza, pamoja na kuwatetea dhidi ya maadui wa nje. Hati hiyo inafuata kabisa msimamo wa Mt. Bonaventura. Jambo muhimu zaidi ni kutofautisha matumizi ya vitu na haki ya kuvitumia: Ndugu Wadogo hawana haki ya kutumia kitu, ila wanaruhusiwa kuwa na matumizi kadiri ya ufukara na uduni. Fundisho hilo likasababisha mabishano makali mno kwa miaka mingi, kuanzia Ufaransa Kusini. Viongozi wa shirika mara walijaribu kukomesha upinzani huo, mara waliuunga mkono. Mapapa walitumia nguvu, isipokuwa Mt. Selestini V (1294), aliyetazamwa kuwa “Papa wa kimalaika” atakayeanzisha Kanisa la Kiroho. Yeye aliwaruhusu waliotaka wajitenge na jumuia na kuishi upwekeni wakifuata kanuni bila ya kujali matamko ya Kanisa. Alipojiuzulu, mwandamizi wake Bonifasi VIII (1295-1303) alimtenga kiongozi wao, nd. Anjelo Klareno (+1337), kama mzushi. Hapo wakaanza kudai ubatili wa kujiuzulu kwa Selestini V na wa kuchaguliwa Bonifasi VIII; halafu wakadai Mapapa waliotoa matamko juu ya kanuni kuwa wazushi. Kinyume na mtangulizi wake, Klemensi V (1305-1314) alipenda kusikiliza wote, halafu akatoa (1312) tamko jipya juu ya kanuni ili kuondoa wasiwasi hasa kwa kubainisha amri za kanuni na kiasi ambacho zinawabana Ndugu Wadogo. Pia akawaweka ndugu “wa Kiroho” chini ya ulinzi wake; viongozi waliowadhulumu waliondolewa, na makosa dhidi ya ufukara yalirekebishwa ili kukwepa farakano. Lakini ikawa bure: mwaka 1317 uasi ukawa wazi usijali kutengwa na Kanisa wala kuchomwa moto. Waklareno wakaendelea hivyo zaidi ya miaka mia mpaka wat. Yohane wa Capestrano na Yakobo wa Marka walipowapatanisha na Kanisa (1430 hivi), nao wakarudi chini ya Mtumishi wa shirika lote (1473).

 

1.1.2. MAREKEBISHO NA UTENGANO (1318-1517)

 

Shirika lilipitia hatari kubwa kuliko zote za historia yake liliposhindana miaka 13 na Yohane XXII (1316-1334). Kiburi kilichowapata Ndugu Wadogo katika karne yao ya kwanza, kutokana na mafanikio yao na mashindano na Maaskofu, kikafikia upeo walipopingwa na Papa pia. Kisa chake ni dhana ya kuwa Kristo na mitume hawakumiliki chochote wala binafsi wala kwa pamoja. Dhana hiyo ililaaniwa na Kanisa, kinyume cha msimamo wa shirika. Badala ya kukubali uamuzi huo, Mtumishi mkuu nd. Mikaeli wa Cesena (1316-1328) na wanashirika karibu wote wakaukataa hata kumtangaza Yohane XXII kuwa mzushi. Mfalme mkuu wa Ujerumani akalipokea shirika chini ya ulinzi wake ili apate nguvu dhidi ya Papa, hata akafanya ndugu mdogo mmojawapo atangazwe kinyume cha sheria kuwa ni Papa badala ya Yohane XXII (bado hai). Baadaye kidogo uasi ukaisha, lakini matokeo ya kwazo kubwa hivi yalichangia sana kudidimia kwa shirika.

Matukio mengine ya nje yaliyochangia ni: vita vya miaka mia (1339-1453) katika sehemu kubwa ya Ulaya; tauni (1348-1350) iliyoua thuluthi mbili za wanashirika (matokeo yake waliobaki walikusanyika katika konventi kubwa zenye hali nzuri zaidi kiuchumi, walipunguza utume na kupokea miito bila ya kuichuja); farakano la Kanisa la Magharibi (1378-1418) lililoleta fujo na utovu wa nidhamu; hatimaye kufifia kwa tunu bora za karne za kati. Upande wa ufukara uamuzi wa Yohane XXII wa kulinganisha Ndugu Wadogo na mashirika mengine ulisababisha hao wasimamie mali na kutumia pesa (hata za binafsi) kinyume cha kanuni. Kilele cha fujo kikawa miaka ya farakano la Magharibi, ambapo kwa wakati mmoja kulikuwa na Watumishi wakuu wawili au watatu, kila mmojawao akimfuata Papa wa Roma, au yule wa Avinyoni au hatimaye yule wa Pisa. Hata hivyo baadhi yao waliongoza vizuri na kuchangia amani ya Kanisa hadi ulipopatikana umoja wake na wa shirika mwaka 1418.

Pamoja na matatizo hayo yote, kuanzia mwaka 1334 baadhi ya wanashirika Italia, halafu Hispania na Ufaransa, walijiombea ruhusa ya Mtumishi mkuu au ya Papa waweze kuishi kijumuia kadiri ya kanuni, bila ya kutumia fadhili za kuilegeza. Wakati huo marekebisho ya namna hiyo yalitokea hata katika mashirika mengine, ingawa kwa kiasi kidogo zaidi. Ni kwamba kati ya Wafransisko kuna utata wa kudumu kuhusu namna ya kulinganisha kipeo asili na maisha halisi, au sehemu mbalimbali za karama ileile: katika karne ya XIV na XV utata huo ulisababisha mapambano ya kishujaa. Walioanzisha urekebisho walikuwa watawa (wengi wao mabradha wasio na elimu) wasioridhika na hali ya shirika. Wakililia hali ya mwanzoni, walilaumu maisha ya wenzao na uongozi wa Watumishi. Hao waliitikia kwa ukali wakijisingizia wanapaswa kudumisha nidhamu na kutetea haki ya walio wengi ya kutumia ruhusa za Kanisa. Kwa kawaida waanzilishi wa marekebisho hawakuwa watakatifu, bali nia yao ilichanganyikana na upungufu wa unyenyekevu na utiifu. Wakidai haki ya kufuata kanuni “Kiroho” kadiri ya sura ya 10, walikimbilia ngazi za juu kwa msaada wa wanasiasa ambao – sawa na watu wa kawaida – kila mara walipendelea urekebisho. Kisha kukubaliwa, marekebisho yakavuta miito bora: k.mf. kati ya mwaka 1402 na 1416 walijiunga na Waoservanti Bernardino wa Siena, Mt.Yohane wa Capestrano, nd. Alberto wa Sarteano na Mt. Yakobo wa Marka ambao wanaitwa “nguzo nne za Oservansya (= kushikakanuni)”. Marekebisho yote, pamoja na kusisitiza ufukara, yalijali sana kimya na sala ya moyo upwekeni. Kama tunda la maisha ya namna hiyo yalifanya pia kazi kubwa tena bora ya kuhubiri, na hivyo kurudisha ule uwiano aliokuwa nao mwanzilishi. Mwishowe haki ya kushika kanuni kiaminifu ikatambulikana na Kanisa.

Mahali pa kwanza walipokusanyika ni makao ya upwekeni ya Brogliano karibu na Asizi. Aliyestawisha zaidi kwanzia mwaka 1368 ni nd. Paolucho Trinci (+1390), bradha aliyefanywa mkurugenzi wa jumuia zilizofuata urekebisho Italia, akiwa na haki ya kupokea wanovisi na kuanzisha nyumba nyingine. Dhidi ya upinzani wa Watumishi, Mtaguso wa Konstans (1415) uliwaruhusu Waoservanti kuenea katika kanda zote za shirika, kupokea wanashirika wote watakaopenda kujiunga nao, tena kuwa na kiongozi maalumu, yaani Watunzaji wao wawe chini ya mmojawao kama makamu wa Mtumishi mkuu badala ya kubaki chini ya Watumishi wa kanda. Hata hivyo marekebisho mengine yaliyokwishaanza (Wavilyakresi, Wakoleta, Waamadei na Waklareno) hayakupenda kujiunga na Waoservanti. Wakonventuali walipinga vikali uamuzi wa Mtaguso, na juhudi za Mapapa hazikuweza kurudisha amani, kwa kuwa hao hawakukubali kurekebishwa, wala Waoservanti kukaa chini yao. Wakati majaribio mbalimbali yalipoendelea kushindikana, Oservansya ikaenea na kustawi, hadi Eugeni IV (1431-1447) alipoiruhusu kujifanyia mikutano mikuu na ya kanda ili kujichagulia viongozi (1446). Ushindi mwingine ukawa tangazo la kuwa Bernardino wa Siena, Mkuu wake wa kwanza, ni mtakatifu (1450).

Leo X (1513-1521) alifanya jaribio la mwisho alipoitisha mkutano mkuu wa wote pamoja (1517), wakiwa na viongozi wa marekebisho mengine. Wakonventuali wakakataa tena shirika lote lisifuate urekebisho wala kuongozwa na Mwoservanti. Basi, Papa akaamua kuwatenganisha moja kwa moja, na kupindua uhusiano kati yao: Waoservanti wawe na hadhi ya kuwa ndio shirika halisi (OFM), wakati waliotetea maisha yaliyofuatwa katika konventi kubwa wakakubaliwa kuendelea nayo kwa kutumia fadhili halali walizopewa, lakini kama tawi tu (OFMConv). Alimlazimisha Mtumishi mkuu wa Wakonventuali kujiuzulu na kukabidhi mhuri wa shirika kwa Waoservanti, ambao Mtumishi wao aitwe Mtumishi mkuu wa shirika lote, likiwa ni pamoja na marekebisho mengine. Wakonventuali wasishiriki tena uchaguzi wa Mtumishi mkuu, wala kiongozi wao asiitwe Mtumishi bali Mwalimu mkuu tu! Hata hivyo wasisumbuliwe kwa kutumia fadhili walizopewa na Kanisa. Waoservanti wabaki na nyumba zao, na Wakonventuali na nyumba zao, bila ya kuvuka toka upande mmoja kwenda upande mwingine.

Ingawa hakuna takwimu ya wanashirika kabla ya karne ya XVII, tunaweza kuwakadiria kutokana na idadi ya nyumba na ya wastani wa ndugu walioishi katika nyumba:

mwaka

ndugu

1226

5000

1300

40000

1400

25000

1517

50000 na zaidi (elfu 20 au 25 Wakonventuali na 30 au 32 Waoservanti)

 

1.1.3. MAISHA NDANI YA SHIRIKA (1226-1517)

 

Kujua maisha ya ndani ya shirika lolote ni muhimu kuliko kujua matukio makuu ya miundo yake. Basi, tuone jamaa ya Ndugu Wadogo ilivyoendelea kwa ndani katika karne tatu za kwanza tulizokwishaziona.

Baada ya kifo cha mwanzilishi wanashirika walizidi kumiminika mijini, katika konventi kubwa zaidi na zaidi, na zenye sura ya kimonaki zaidi na zaidi (kanisa kubwa, ukumbi wa mikutano, ua, bustani na kuta za kandokando…). Kanuni iliendelea kuzingatiwa, lakini kwa mtazamo wa kisheria, kufuatana na matamko ya Mapapa juu yake. Ufukara mkuu ukaja kuwa sifa maalumu za kujitangazia shirika bora kuliko mengine, pamoja na kujipongeza kwa kuwa na mwanzilishi aliye Kristo wa pili, mtakatifu kuliko wengine (tazama ngao ya shirika ya karne ya XV yenye msalaba iliposulibiwa pamoja mikono ya Kristo na Fransisko). Lakini utekelezaji ukawa wa kinafiki sana, k.mf. tendo la ndugu kusafiri na boi ambaye amchukulie pesa asije akazigusa mwenyewe lilihukumiwa tayari na katiba ya Narbona (1260) iliyotungwa kama kinga ya kanuni, halafu ikarekebishwa mara nyingi ili kudhibiti makosa yaliyojitokeza pamoja na kudumisha usawa katika sura ya nje ya watawa na katika matumizi ya kila siku.

Kimya kilichosisitizwa na Mt. Fransisko kama sharti la sala, kikaja kuratibiwa kwa mfano wa monasteri: kwamba kimya kikuu kiwe cha kudumu katika kanisa, maktaba, vyumba vya kulala, ua na mezani wakati wa kula. Zaidi ya hicho, kitunzwe daima na popote kimya cha Kiinjili, yaani kukwepa maneno yoyote yasiyofaa (Math. 12:36). Katiba haikuzungumzia maburudisho, lakini sikukuu zilikuwa na nafasi za kufurahia udugu (vyakula na divai, nyimbo, maigizo na michezo), ingawa ilikatazwa mara nyingi ndugu wasipite kiasi. Hatujui vitendo vya toba vya kijumuia vilipoanza; lakini mwanzoni mwa karne ya XIV Ndugu Wadogo walikuwa wakijipiga mijeledi kila siku ya Kwaresima, halafu mara tatu kwa juma nyakati nyingine. Adhabu alizozitoa mwanzilishi zikaja kuongezwa chini ya nd. Eliya hata kuratibiwa na sheria. Mapema ulifuatwa mfano wa Wadominiko wa konventi zote kuwa na magereza, ila yajali utu. Wasiojirekebisha wafukuzwe shirikani.

Mpaka mwaka 1239 ndugu wakleri na mabradha waliishi kwa usawa alivyotaka Mt. Fransisko. Baadaye shirika likabadilika na kuwa la kikleri. Sababu ni mbalimbali: heshima kubwa ya mwanzilishi kwa mapadri, ongezeko la mapadri kwa idadi na ubora, chuki ya wengi kwa sera ya nd. Eliya aliyependelea mabradha wenzake katika uongozi. Miaka miwili tu baada ya kumuondosha, mabradha wakajikuta hawaruhusiwi tena kuwa na cheo chochote, halafu ikakatazwa wasipokewe tena shirikani, isipokuwa kwa sababu ya pekee. Pia mabradha walifungiwa kabisa mlango wa ukleri kwa kufafanua visivyo maneno ya kanuni yasemayo, “wasio na elimu wasijisumbue kusudi waipate”. Basi, baada ya katazo la kufanya kazi za mikono nje ya konventi kama zamani, sura ya bradha Mfransisko ikawa kwa karne nyingi ile ya mtu ambaye hana sauti wala kura, amekusudiwa kutoa huduma za konventini na kuombaomba, ambaye heshima yake kubwa ni kuwatumikia wanashirika mapadri. Hivyo miito ya namna hiyo haikutoka tena kwa watu wenye elimu wenye kulenga utakatifu wa Kifransisko, bali kwa watu wadogo, wasiojua kusoma, wasio na mbele wala nyuma, ambao wengi wao waliingia utawani kujitafutia tu maisha ya hakika. Hapo ilibidi wachujwe sana. Kwa njia hiyo sura ya ndani ya jamaa ilibadilika sana, kwa kuwa na matabaka yenye kazi tofauti, haki tofauti na malezi tofauti. Ila marekebisho yakajaribu kurudia hali ya mwanzoni.

Baadaye ikatokea migawanyiko mingine kati ya waliopewa na wasiopewa fadhili, yaani ruhusa za pekee. Kwanza zilitolewa kwa walimu na wanafunzi ili kustawisha masomo katika ngazi za juu, halafu katika ngazi ya kati na ya chini. Wakaja kuongezwa waliowahi kuwa na vyeo, wazee na hatimaye wahubiri. Malalamiko yakawa mengi, hasa walionyimwa walipokosa hata mahitaji yao, ingawa wagonjwa waliendelea kushughuliwa vizuri, na haki zao zilitetewa na sheria. Utaratibu wa kimonaki wa kuwapanga watawa kufuatana na muda wa kukaa utawani, uliokataliwa mwanzoni ukajipenyeza shirikani; hata katika hilo, na katika kuwapa viongozi heshima kubwa za nje, marekebisho yakarudia usahili wa mwanzoni.

Mt. Fransisko aliwazoesha wafuasi wake kuwa wazi kati yao, kuelezana habari za safari, kujishtaki kwa unyenyekevu na kuomba msamaha. Ndiyo asili ya “mkutano wa makosa” ambao uliagizwa na katiba (1260) mara moja kwa wiki, ukifuatwa na mkutano wa jumuia uliojadili masuala ya pamoja. Mpango wa mwanzilishi wa kuwatuma wafuasi wake ulimwenguni wawiliwawili uliendelea, ila kwa shabaha ya kulindana bila ya kuaminiana, badala ya kushuhudia umoja wa kidugu na kusaidiana. Malezi kwa jumla yalilenga zaidi maisha ya ndani kuliko kwenda ulimwenguni, jambo lililotarajiwa kuwa la nadra tu. Mipango ya kwanza kwa malezi iliratibiwa na katiba (1260). Walezi walisaidiwa na vitabu kadhaa, hasa “Kielelezo cha Nidhamu” cha Bernardo wa Besse (+1300 hivi) ambacho kinalenga nidhamu, adabu njema, usafi na taratibu za kimonaki kuliko mitindo ya Kifransisko. Baada ya kumaliza unovisi, watawa wapya waliendelea kulelewa walau miaka mitatu, ingawa kazi hiyo ilionekana mapema kuwa ngumu sana. Sehemu mbalimbali (hasa Wakonventuali) walianza kupokea watoto wadogo kama walivyofanya wamonaki.

Toka mwanzo kazi za Ndugu Wadogo zilikuwa tatu: sala, kazi za mikono na mahubiri; uvivu ulikuwa tishio kwa mwanzilishi na viongozi wengine. Mt. Bonaventura alipochaguliwa aliwaandikia mara wanashirika wote ili kuwaonyesha hatari hiyo kubwa, lakini alipinga kabisa watawa kufanya kazi za mikono zenye malipo. Badala yake walitafutiwa kazi nyingine mbalimbali: kusoma, kuimba Zaburi, kutoa huduma za nyumbani, kuombaomba n.k.

Mchango muhimu mmojawapo wa mashirika ya Ombaomba ni kujenga daraja kati ya liturujia ya monasteri na ya makanisa makuu na mahitaji ya kidini ya jamii yenye kubadilika. Ndugu Wadogo, wakitumia haki ya wakati huo ya kila shirika kujitengenezea liturujia yake, walistawisha kalenda na taratibu zao, pamoja na kufuata kimsingi zile za Roma. Walizifupisha kwa faida ya sala ya moyo, na kuzisogeza jirani na haja za mtu binafsi. Ingawa wapinzani walisema kufanya hivyo ni kuvuruga liturujia, Mapapa wakaja kueneza breviari ya Kifransisko katika Kanisa lote la Kilatini. Hata misale ya Kiroma iliyotumiwa na kurekebishwa na Ndugu Wadogo ikaja kuenea: taratibu nyingi za ibada, nyimbo na sikukuu mpya ziliingizwa nao kabla hazijakubaliwa kwa Kanisa lote. Kwa juhudi na mafanikio ya pekee zilistawishwa ibada kwa Ekaristi, jina la Yesu, kuzaliwa kwake na kuteseka (Njia ya Msalaba), Bikira Maria (Kukingiwa Dhambi ya Asili). Kwa ajili hiyo, nje ya ibada walitumia pia maigizo, wakisaidiwa na Utawa III. Baada ya jumuia zote kupata kanisa la kitawa ambapo iliwabidi waadhimishe Sala ya Kanisa, ibada zilizidi kuwa za fahari, hasa kwa lengo la kuwapa kazi ya kufanya ndugu wasiosoma wala kuhubiri. Kwa sababu hiyohiyo, juu ya Sala ya Kanisa vikaongezwa vipindi vingine kwa ajili ya wafu, kwa heshima ya Bikira Maria n.k. Hoja ya msingi ilikuwa kwamba walio wengi wasingefanya bidii katika sala ya binafsi. Kama kawaida, marekebisho yalirudia kusisitiza sala ya moyo na kusoma tu Zaburi, pamoja na kuadhimisha Misa pasipo fahari katika makanisa madogomadogo. Wasio mapadre walihudhuria Misa, ila ilikuwa kawaida kupokea Ekaristi kila baada ya wiki mbili. Kumbe maungamo yalikuwa mara mbili kwa juma.

Kati ya walimu wa kiroho Mt.Bonaventura alishika nafasi ya kwanza. Maandishi yake yote yalilenga maisha ya kiroho, na kuathiri sana shirika na Kanisa lote hadi leo; ndiyo sababu akatangazwa mwalimu wa Kanisa kwa jina la “mwalimu wa kiserafi”. Tukiacha waandishi wengine bora na kuzingatia waliofaulu kuyatekeleza kikamilifu maisha ya kiroho, tunakuta katika karne tatu za kwanza walifariki watakatifu 25 na wenye heri 61: ndio ushahidi bora wa jinsi kipeo cha Kifransisko kinavyofaa. Wa kwanza ni wafiadini wa Moroko (5 wa mwaka 1220, na 7 wa mwaka 1227). Kufuatana na mfano wao alijiunga na shirika Mt. Antoni wa Padua (+1231), “mwalimu wa Kiinjili” mwenye utakatifu usiosemeka kulingana na moyo wa mwanzilishi. Baada ya Mt. Bonaventura kuna askofu mwingine, Mt. Ludoviko wa Tolosa (+1297), aliyekufa kijana kama alivyotamani. Karne ya XIV, iliyojaa wamisionari na wafiadini, ina ndugu wanne kutoka nchi mbalimbali waliotangazwa watakatifu: Nikola Tavelic na wenzake waliouawa Yerusalemu (1391). Watakatifu wote sita wa karne ya XV ni Waoservanti ambao walipigania kanuni na kufanya utume mkubwa: Bernardino wa Siena (+1444), Yohane wa Capestrano (+1456) na Yakobo wa Marka (+1476) toka Italia, Petro Regalado (+1456) na Didakus wa Alkala (+1463) toka Hispania, halafuYohane wa Dukla (+1484) toka Polandi.

 

1.1.4. UTUME (1226-1517)

 

Tangu mashirika ya Wafransisko na Wadominiko yaanzishwe, Mapapa walitambua yanavyohitajika na kufaa kutegemezea Kanisa la Roma ambalo, baada ya kufikia kilele cha fahari na mamlaka wakati wa Inosenti III (1198-1216), lilianza kukabiliana na upinzani mpya wa viongozi wa siasa. Ili waweze kuwatumia watawa hao bila ya pingamizi, Mapapa walijiwekea usimamizi wao wasikae chini ya Maaskofu, wakawapendelea katika tume nyingi. Hivyo toka mwanzo Ndugu Wadogo walifanya kazi katika ofisi za Papa na kupewa vyeo mbalimbali, kinyume cha matakwa ya Mt. Fransisko aliyetaka wabaki “wadogo”. Hasa baada ya Gregori IX, Mapapa waliona ustawi wa Kanisa unastahili uzingatiwe kuliko udogo wa Kifransisko. Ingawa shirika lilijitahidi kuzuia ongezeko la vyeo, katika karne ya XIII waliishi Maaskofu Wafransisko 250, katika ile ya XIV 746, katika ile ya XV 791, na miaka 17 ya kwanza ya karne ya XVI 70. Mabalozi ya Papa jumla walikuwa zaidi ya 300, Makardinali 29, na wawili wakawa Mapapa: Nikola IV (1288-1292) na Sisto IV (1471-1484). Ndugu Wadogo walichangia sana Mitaguso mikuu yote ya karne hizo tatu: Lyons I (1245), Lyons II (1274), Vienne(1311-1312), Konstans (1414-1418), Firenze (1431-1445) na Laterano V (1512-1517). Vilevile ndugu wengine walitetea haki za Papa dhidi ya upinzani, na zaidi ya 200 walipokea hata kazi ya kuwahukumu wazushi, ingawa hiyo haikuwapendeza sana.

Kazi ya kawaida zaidi ilikuwa ile ya kuhubiri. Waliokubaliwa na Watumishi wakaja kuunda tabaka la juu kuliko mapadri wa kawaida (waliosoma Misa tu) na ya mabradha. Ilipobaki kazi ya wasomi tu, ikarudia mitindo ya vyuoni na kuachana na usahili wa mwanzo alioutumia na kuutaka mwanzilishi. Mhubiri mkuu wa kwanza ulikuwa Mt. Antoni ambaye kwa miaka 10 alichangamsha Italia na Ufaransa Kusini akishinda uzushi. Pamoja na kuhubiri, wengine wametuachia kwa maandishi hotuba zao, mifano mingi na maelekezo juu ya namna ya kuhubiri.

Karne ya XV ndiyo bora kwa mahubiri ya Kifransisko, ambapo nguzo za Oservansya walitoka upwekeni wakawashirikisha wote utajiri waliojipatia katika sala. Makanisa hayakutosha kukusanya wasikilizaji; wote waliguswa na wengi wakaongoka. Kutoka Italia wakahubiri nchi mbalimbali hadi Norwe. Tunda mojawapo la utume wa Mt. Yohane wa Capestrano ni ushindi wa Wakristo juu ya Waturuki waliotishia kuvamia Ulaya yote (1456). Huko Italia mahubiri hayo yalipinga mwelekeo mpya wa kuweka pembeni Ukristo katika maisha ya kila siku na kujali ustawi wa kidunia tu. Kitubio kilifuatana na mahubiri; hasa baada ya Mapapa kuruhusu watawa kutoa huduma hiyo, ikaja kuwa mojawapo ya kazi zao kuu.

Shirika likiwa na uhusiano wa pekee na watu wadogo toka mwanzo, daima ni jepesi kutambua hali na haja zao upande wa roho na wa mwili, na kuziitikia vizuri, hata kupitia Utawa III. Kipindi hicho watu walielekea sana kujiundia makundi kadiri ya fani zao n.k. Ndugu Wadogo waliwaelekeza kufanya hivyo bila ya kusahau dini, katika jina na taratibu walivyoyapatia. Walipatanisha mara nyigi wanasiasa wa miji au vyama tofauti, walisaidia maskini na wagonjwa (hata wenye ukoma na tauni), walianzisha hospitali, walilaumu hadharani dhuluma n.k. Kwa ajili hiyo, bila ya kujali upinzani wowote, walianzisha pia benki ambazo zikopeshe pesa kwa riba ndogo sana ili kukomesha waliodai riba pasipo kiasi (hasa Wayahudi).

Kabla hatujaeleza umisionari wa Ndugu Wadogo, tuangalie juhudi zao kwa ajili ya umoja kati ya Waortodoksi na Kanisa la Roma. Kabla Kostantinopoli haujatekwa na Waturuki (1453), udhaifu wa Wagiriki upande wa siasa na jeshi uliwaelekeza kutafuta msaada wa Wakristo wa Magharibi. Hivyo zilipatikana fursa nyingi za kukaribiana na kujaribu kuungana, ambazo Mapapa kila mara waliwatumia Wafransisko na Wadominiko. Kwa namna ya pekee Mtaguso II wa Lyons, kwa juhudi hasa za Mt. Bonaventura, ulifanikiwa kutangaza umoja, ingawa baadaye ukashindikana kwa sababu mbalimbali.

Juhudi nyingine kulingana na mitazamo ya nyakati hizo zilifanywa na Ndugu Wadogo waliosambaa kotekote Mashariki na kutoa mifano bora ya maisha yao, pamoja na kutangaza kwa sauti na kwa maandishi ukweli wa Kanisa katoliki ili kuwavuta Waortodoksi mmojammoja au makundimakundi kuingia katika ushirika kamili nalo. Sehemu fulanifulani matunda yaliridhisha, lakini wengine waliuawa, hasa baada ya Waturuki kuteka Ulaya Mashariki Kusini. Nje ya eneo hilo, utume huo ulifanyika pia Urusi, Georgia, Armenia, Irani, Lebanoni, Misri hata Ethiopia.

Kazi ngumu zaidi ilifanyika kwa wasio Wakristo. Karne ya XIII ilikuwa mwanzo wa umisionari wa aina mpya, ambao unaongozwa na Mapapa kwa kutumia mashirika ya Ombaomba (yaliyofaa sana kwa utayari wa kutumwa na kwa umoja wa miundo yake), unapata wamisionari mchanganyiko kutoka nchi yoyote, unaenea katika bara lote la Asia (ambalo linakuja kujulikana na Wazungu wakati huo) na hauna faida ya uchumi. Mt.Fransisko alichochea hayo kwa mifano na mafundisho yake ambayo alisisitiza kuwa wito huo ni wa Kimungu, kwa hiyo hautakiwi kuzuiwa. Kwa mang’amuzi yake alielekeza kutoa kwanza ushuhuda wa maisha ya Kikristo, halafu tu, kadiri ya mapenzi ya Mungu, kuhubiri wazi imani. Wafuasi wake hawakufuata daima maelekezo hayo, kwa maana wengi waliwachokoza Waislamu ili kuuawa.

Katika historia ya misheni za Kifransisko, tunaona kwanza uenezi mkubwa upande wa Mashariki, halafu karne nyingine ya kufifia, halafu katika karne ya XV msukumo mpya toka kwa Waoservanti, lakini kuelekea maeneo mapana ambayo yalivumbuliwa na Wazungu miaka ya mwisho ya karne hiyo na kuhitaji Injili.

Kuanzia mwaka 1217 Wafransisko wametunza mahali patakatifu pa nchi ya Yesu, ingawa iliwabidi kuvumilia magumu mengi, dhuluma na vifodini; wengi walikufa pia kwa kuwashughulikia wenye tauni. Kuanzia mwaka 1219 wengine walitumwa Afrika Kaskazini, ambapo baadhi walifia dini. Shirika lilianza kupata Maaskofu kwa ajili ya Moroko, ingawa hawakuweza kukaa huko. Kumbe Tunisia na Libya waliruhusiwa kuwaongoa Waislamu wakachuma matunda kwa muda fulani, ingawa vipindi vingine waliweza tu kuwahudumia Wakristo wageni.

Mwaka 1241 Wamongolia, baada ya kujitwalia Asia karibu nzima, walivamia Ulaya na kufadhaisha Wakristo wote, kwa sababu hakuna aliyeamini uwezekano wa kuwashinda. Mapapa walijaribu kuwasimamisha kwa kutuma Wafransisko na Wadominiko (wa kwanza ni nd. Yohane wa Pian del Carpine) waombe masharti ya amani. Ujumbe huo uliposhindikana, walianza kupenya kama wamisionari upande wa Ulaya Mashariki, wakasambaa kwa ruhusa ya watu hao wakatili sana katika utawala wao wote. Nikola IV alimtuma (1291) nd. Yohane wa Montecorvino, mwanzilishi wa misheni za China na Askofu wa kwanza wa Beijing, mwenye majimbo sita chini yake katika ufalme mzima (hadi Urusi). Nyumba za kitawa katika eneo hilo lote likafikia kuzidi 50, baadhi zikiwa na ndugu wasiopungua 20. Inosenti VI (1352-1362) aliomba mkutano mkuu wa mwaka 1353 uongeze wamisionari alivyotaka mfalme wa Mongolia, lakini itikio likawa hafifu, kwa kuwa tauni iliyoua wamisionari wengi, iliua pia watawa wengi Ulaya. Hivyo misheni zikaendelea kwa shida tu mpaka ikaja kufa China ilipojikomboa. Pia, Ndugu Wadogo waliongoa Walitwania, taifa la mwisho la Ulaya kuingia Ukristo (karne ya XIII na XIV).

Karne ya XV ilielekeza umisionari upande mwingine, na Waoservanti waliuchangamkia kuanzia visiwa vya Kanaria vilivyopokea Ukristo haraka kwa juhudi za ndugu waliofikia kuwa 200, mmojawao Mt. Didakus wa Alkala. Kutoka huko umisionari ulienea pwani za Afrika Magharibi. Mzunguko wa Afrika hadi Ras wa Tumaini Jema (Dias, 1488) na India (Da Gama, 1497-1498), na hasa uvumbuzi wa Amerika (Columbus, 1492) ulisisimua sana umisionari kwa maeneo, miundo na mbinu mpya. Wakati ambapo uenezi wa Waturuki Waislamu ulikuja kuzuia njia za Asia, na misheni zilizokuwa chini ya utawala wao zilidumaa, Ndugu Wadogo walistawisha upeo umisionari wao Amerika na Asia Mashariki kupitia baharini (wakati huo Asia Mashariki ilikuwa chini ya Askofu wa Funchal, katika kisiwa cha Afrika Magharibi!). Upande wa miundo wafalme wa Ureno na wa Hispania walipogawana ulimwengu kwa baraka ya Aleksanda VI (1492-1503) walipewa pia usimamizi wa kazi zote za misheni, pamoja na haki ya kuchagua na kutuma wamisionari katika maeneo yao. Hivyo karne ya XVI idadi ya wamisionari OFM ilifikia 6,000, wengi wao wakitokea nchi hizo mbili, kwa sababu mataifa mengine waliweza wakabaguliwa na hata kurudishwa nyumbani.

Ndugu Wadogo 6 wa kwanza walifika Amerika (kisiwa cha Hispaniola, leo Dominikana/Haiti) mwaka 1493 na kuanza kuwahubiria wazalendo. Wengine wakafuata mapema na kuenea kadiri vilivyovumbuliwa visiwa vingine. Kufikia mwaka 1500 walikuwa wameshabatizwa wazalendo 3,000 Hispaniola na wengi zaidi Kuba. Mwaka 1504 yaliundwa majimbo matatu na mwaka 1505 kanda ya shirika. Mwaka 1511 alitawazwa Askofu wa kwanza wa Amerika visiwani (Dominikana) na mwaka 1513 wa bara (Panama), wote wawili wakiwa Wafransisko. Ila barani hatari zikawa nyingi. Waliohamia Brazili (1503) waliuawa baada ya miaka miwili, na wengi wa waliowafuata wakauawa pia. Hata hivyo Wafransisko wakaendelea na umisionari huko, wakiwa peke yao hadi 1549.

Vilevile Ndugu Wadogo ndio wamisionari wa kwanza kufika India kwa meli (1500, baada ya kupitia Brazili); wengine wakafuata. Mabanyani waliwaua 3, lakini wengine waliongoka jumla wakabatizwa pasipo mafundisho kutokana na uhaba wa wamisionari. Safarini, wengine walihubiri kisiwani Sokotra (karibu na Somalia) na kuongoa karibu wote, hata wakageuza msikiti kuwa kanisa la Bikira Maria; lakini Waarabu wakakiteka (1510) wakaharibu kila kitu.

Uenezaji wa Injili unatimia unapopenya utamaduni wa watu. Tuone basi Ufransisko ulivyoathiri Kanisa na jamii, kuanzia elimu, fasihi na sanaa.

Mt. Fransisko hakuwa msomi, tena alihisi uchu wa elimu unavyoweza kuzuia udogo na usawa wa wafuasi wake. Lakini, akitambua njia hiyo haiepukiki, alielekeza namna ya kuifuata bila ya kudhurika. Kwake na kwetu Mt. Antoni wa Padua ndiye kielelezo, kwa jinsi alivyokuwa tayari kuweka pembeni usomi. Ndiyo sababu alimruhusu kuwafundisha ndugu teolojia huko Bologna mradi isizimishwe roho ya sala na ibada. Mwaka 1231 shirika lilikuwa na nyumba za masomo hata Paris na Oxford karibu na vyuo vikuu ili kuwaandaa walimu ambao wafundishe katika konventi muhimu zaidi za kila kanda. Ndipo walipojipatia sifa ya elimu na nafasi mpya za utume, ingawa M.H. Egidi na wengineo walizidi kulaumu Paris kwamba imeharibu shirika. Tangu karne ya XIV katika konventi karibu zote kulikuwa na vipindi vya lazima kwa wasio mabradha. Pia yalianzishwa masomo kwa waliotarajia kupata daraja. Mitindo ya kufundisha ilikuwa sawa na ile ya mashirika mengine na ya vyuo vikuu: vipindi asubuhi na jioni, mijadala, mahubiri ya walimu na ya wanafunzi vilevile.

Shirika halikuwa na mwalimu maalumu na mafundisho ya lazima, ila tabia na mazingira yake yote vilielekeza Ndugu Wadogo kuwaza namna fulani, yaani kusisitiza upendo kuliko ujuzi, na utashi kuliko akili; pia kumuona Mungu kama Wema kuliko kama Ukweli. Falsafa ya Wafransisko ilifuata ile ya Plato kumpitia Mt. Augustino (Mt. Antoni alitoka shirika lake). Kati ya walimu wa vyuo vikuu aliyeelekeza njia ni Aleksanda wa Hales (+1245), aliyemfundisha Mt. Bonaventura huko Paris. Kwa mtakatifu huyo, mwalimu ni Kristo tu, na elimu ni moja tu, ile inayotuunganisha naye, hasa Maandiko Matakatifu, ambayo peke yake yanawafaa Ndugu Wadogo. Baada yake teolojia ikabili mababu wa Kanisa na maandishi ya walimu wa teolojia. Wanafalsafa na waandishi wengine wasomwe tu kwa mpito kadiri wanavyosaidia kuelewa Biblia. Ndiyo njia ya kufikia elimu, lakini mtu akitaka hekima anapaswa kuwa na maisha matakatifu.

Oxford iliwatoa hasa: nd. Roger Bacon (+1292), mtaalamu wa mambo mengi na mwanzilishi wa mtindo wa upimaji kama msingi wa sayansi; M.H. Yohane Duns Scoto (+1308), mwalimu mwenye uchambuzi mkali, anayesifiwa kwa kuonyesha Kristo kuwa kiini cha uumbaji, na kwa kutetea sifa ya Maria kukingiwa dhambi ya asili (Wafransisko wakaendelea kuitetea hadi ikatangazwa na M.H. Pius IX, wa Utawa III, mwaka 1854, kuwa dogma); na nd. Wiliamu wa Ockham (+1347) aliyepotosha falsafa akadai eti, akili haiwezi kujua yanayopita malimwengu: msimamo wake ukaenea sana, ukampa Martin Luther silaha dhidi ya imani katoliki, ukaathiri utamaduni wa Magharibi hadi leo.

Ufransisko uliathiri vilevile mwelekeo wote wa sanaa ya Magharibi. Ukiitikia vizuri matarajio yote ya kidini na ya kijamii ya kipindi cha mageuzi, ulieneza mtazamo mpya wa maisha unaojali mtu na viumbe vyote. Hivyo ulichangia sana upatikanaji wa mitindo mipya na njia mpya za kufurahia uzuri, ingawa bila ya kupotewa na imani. Fasihi ya Kifransisko inapenda kusimulia, tunavyoona katika maisha ya mwanzilishi yaliyoandikwa na wafuasi wake; uchorahi unaonyesha sura halisi ya kwake na ya wengineo; hata ujenzi unafuata njia mpya, hasa kufuatana na kielelezo cha kanisa la Mt. Fransisko huko Asizi. Hata katika ujenzi wa nyumba zao Ndugu Wadogo waliweza kuzingatia ufukara bila ya kupuuzia uzuri, kiasi kwamba upendevu wake unavutia wengi hadi leo.

 

 

1.2. MAREKEBISHO KUENDELEA (1517-1762)

 

1.2.1. MATAWI MAPYA KUCHIPUKA

 

Utengano wa Waoservanti na Wakonventuali ulitatua tatizo moja, lakini haukufaulu kuunganisha makundi yaliyorekebishwa, ingawa Papa alikuwa ameagiza itungwe mara katiba moja kwa yote. Baadhi yalidumu kuwa na kanda zao, Waoservanti wa Italia wakaikataa katiba hiyo wakaendelea kuirekebisha mfululizo ile maalumu ya kwao, na kanda nyingine zilijitungia vilevile na kuzidisha tofauti shirikani. Kilichohatarisha zaidi umoja ni utaifa uliochochewa na serikali mbalimbali kwa faida ya siasa ya nchi zao dhidi ya nyingine. Wafalme waliingilia kwa njama na vitisho masuala ya mikutano mikuu, sawa na walivyoingilia uchaguzi wa Papa, lakini kila mara idadi iliwapa ushindi Wahispania, hata washindani wao (Wafaransa) wakagoma kuhudhuria mara kadhaa.

Matatizo mengine yalihusu maisha yenyewe, hasa ufukara. Waliolazimika kujiunga na Waoservanti, na wale wasioacha kutumia fadhili walizokuwanazo wakiwa Wakonventuali, walikataa kurekebishwa. Kinyume chake, wengine hawakuridhika tena na namna OFM ilivyoshika kanuni, wakadai ruhusa ya kuishika kabisa. Ndivyo walivyofanya watawa wa mashirika mbalimbali, kwa kuwa haja ya urekebisho ilitambulikana na wote katika Kanisa la karne ya XV na ya XVI. Kwa namna ya pekee Ndugu Wadogo walichochewa kufanya hivyo na sura ya X ya kanuni pamoja na wasia. Ndiyo sababu Mt. Bonaventura aliona haja ya kuwepo makao ya upwekeni katika kila kanda ili kuwaachia uhuru wa kuishi hivyo wale wapendao. Kumbe Waoservanti wengi na baadhi ya viongozi wao hawakukubali kuwaachia wenye bidii uhuru huo, kwa sababu ingekuwa sawa na kukiri kwamba wamelegea. Hivyo wakawatenda ndugu hao kama Wakonventuali wa zamani walivyowatenda Waoservanti wa kwanza. Walioamini urekebisho unaweza kutoka kwa viongozi wakaja kujionea haiwezekani. Miundo iliyoanza kama urekebisho ikajikuta inajaribu kuzuia juhudi za waliopenda urekebisho, na viongozi wa shirika lililoanza kwa kushindana na viongozi wakawalaumu waliotaka kufanya vile wakisema eti, ni wakaidi tu! Kwa kukosa busara na wema walisababisha waliotaka urekebisho wakafuate njia zao ili kupata ruhusa walizozihitaji, kwa kumkimbilia Papa au viongozi wa serikali. Mara nyingine Wakonventuali walipokea makundi hayo chini ya ulinzi wao ili kuwakomoa Waoservanti waliokuwa wanawadharau wakijidai ndio wafuasi halisi wa Mt. Fransisko. Ndiyo asili ya matawi mapya, hasa lile la kujitegemea la Wakapuchini.

Mwaka 1525 nd. Mateo wa Bascio alimkimbilia Klementi VII (1523-1534) ili kuruhusiwa ashike kanuni, avae kanzu asili na kuhubiri huko na huko alivyotaka. Alipokubaliwa, walijiunga naye ndugu wawili, Ludoviko na Rafaeli wa Fossombrone. Mtumishi wa kanda aliwatafuta sana, lakini walilindwa vizuri na Katerina Cibo, ndugu wa Papa. Ili kukwepa dhuluma, wakajiunga na Wakonventuali, halafu wakapewa na Klementi VII haki ya kuwa na Mtumishi wao chini ya Mkuu wa Wakonventuali na ya kupokea wanovisi (1528). Mapema walianza kuitwa Wakapuchini kutokana na kofia yao kubwa. Upinzani wa Mkuu wa OFM dhidi yao haukufaulu; kinyume chake, kwa kuwa alitaka kuzuia hata makao ya upwekeni ndani ya shirika, ndugu wengi wenye bidii wakakata tamaa wakajiunga na Wakapuchini. Njama nyingine za kuwakomesha zikashindikana, hivi kwamba mwaka 1535 walikuwa tayari 700. Ndipo aliposhika uongozi wao nd. Bernardino wa Asti aliyelipa shirika jipya sura ya kiroho ya kudumu, hasa kwa njia ya katiba iliyotungwa mwaka huo na kupitishwa mwaka uliofuata.

Hatari nyingine zilitokea ndani ya shirika, kwa ukaidi wa nd. Ludoviko, halafu kwa uzushi wa mwandamizi wa nd. Bernardino. Hatimaye mambo yakatulia na tawi jipya likazidi kustawi kiroho na kitume, ingawa Julius III (1550-1555) alikataza Waoservanti wasihamie tena kwa Wakapuchini. Hivyo hawa wakazidi kujisikia tofauti na Wafransisko wenzao. Mkutano mkuu wa mwaka 1552 ulionyesha kuwa juhudi kali za awali zimeanza kutulia na kujilinganisha na maisha: shirika lilipanga masomo na kuwa na watu maarufu upande wa elimu, utume na uongozi. Jambo muhimu zaidi, lilimzaa mtakatifu wa kwanza, bradha Felix wa Cantalice (+1587), kielelezo cha unyofu. Mtaguso wa Trento (1545-1563) ulisifu tawi hilo kama urekebisho wa kufaa na wenye uaminifu kwa wito wake hata kustahili kutazamwa na Kanisa kwa namna ya pekee. Shirika likazidi kukaza nidhamu ili kuzuia ulegevu, likaanza kuenea ng’ambo ya milima ya Italia Kaskazini (1573). Ulipozuka upinzani wa Wakonventuali, Kanisa lilikuwa limeshang’amua ubora wa Wakapuchini; basi, Paulo V (1605-1621) alitamka kuwa ni Ndugu Wadogo halisi na wana wa Mt. Fransisko sawa na matawi mengine (1608), halafu akawaondoa chini ya Mkuu wa Wakonventuali na kuwapa Mtumishi wa kwao mwenye haki ya kuhesabiwa mwandamizi halali wa mwanzilishi (1619). Kwa wakati huo shirika limeshazaa tena watakatifu Serafino wa Montegranaro (+1604), bradha asiye na vipawa vingi kiutu bali mwenye karama za ajabu, Yosefu wa Leonesa (+1612), padri Mkapuchini wa kwanza kutumwa kwa Waturuki Waislamu halafu mhubiri bora Italia, na Mt. Laurenti wa Brindisi (+1619), “mwalimu wa Kitume”, mtimilifu kuliko Wakapuchini wote kwa utakatifu, elimu na utume. Wakafuata Mt. Fidelis wa Sigmaringen (+1622), wa kwanza kutoka nje ya Italia, na wa kwanza kufia dini kati ya waliotumwa na Idara ya Papa kwa Uenezaji wa Imani, halafu Mt. Bernardo wa Corleone (+1667), mwongofu mwenye toba kali. Pia walipatikana wenye heri 6.

Kipindi hicho ndicho cha ukomavu wa shirika, mitazamo ya Kiitalia ilipopanuka kwa kuenea nje ya nchi na wanashirika waliposhika nafasi muhimu katika Kanisa. Baadaye hakuna matukio ya maana zaidi, isipokuwa mengine ya kufaa na mengine yasiyofaa ambayo yaliathiri shirika: idadi ya watawa na ya shughuli iliongezeka pamoja na sifa kutoka kwa viongozi wa Kanisa na serikali, lakini zilizuka vurugu pia kama ile ya utaifa (1636-1678). Benedikto XIV (1740-1758) aliamua mhubiri wa Papa awe daima Mkapuchini, akasema, “Shirika la Wakapuchini linastahili yoyote yale, kwa kuwa ndilo kielelezo pekee cha ukamilifu wa Kiinjili kilichobaki hadi nyakati zetu”. Kweli urekebisho huo uliendelea kushika kikamilifu kanuni kwa muda mrefu kuliko mengine yote. Nyumba ziliendelea kujengwa ilivyoagizwa toka mwanzo, ndogo sana, nje ya miji na vijiji, zikielekeza ndugu kufuata ufukara na unyofu hata ulimwengu ulipokazania fahari. Watakatifu wa kipindi hicho ni bradha Krispino wa Viterbo (+1750), kielelezo cha furaha ya kiroho, Ignas wa Santhià (+1770), padri mwenye bidii kwa wagonjwa na wakosefu, Ignas wa Lakoni (+1781), bradha ombaomba aliyesaidia sana fukara, na Felix wa Nicosia (+1787), bradha mtiifu ajabu, mbali ya mwenye heri 1.

Vilevile Italia, ndugu waliojikusanya katika makao ya upwekeni kuanzia mwaka 1535 (mkutano mkuu ulipowaruhusu ili kuzuia wengine wengi wasiwakimbilie Wakapuchini), kisha kuongezeka waliwekwa moja kwa moja chini ya Mtumishi mkuu tu (1579), wakapewa katiba maalumu (1595), ruhusa za pekee sana (1596), hatimaye Kiongozi mkuu na mkutano mkuu wa kwao. Hivyo mamlaka ya Mtumishi wa OFM kwao ikawa jina tu. Kati ya hao Wariformati katika kipindi hicho tunawakuta watakatifu mabradha watatu: Mt. Benedikto Mwafrika (+1589), mtoto wa watumwa huko Italia, Mnegro wa kwanza kutangazwa mtakatifu, Mt. Umile wa Bisignano (+1637), mnyenyekevu ajabu, na Mt. Karolo wa Sezze (+1670), aliyeandika vizuri sana kuhusu maisha ya kiroho; halafu mapadri Mt. Pasifiko wa San Severino (+1721), aliyezingatia sana maisha ya sala, na Leonardo wa Portomaurizio (+1751), tunda bora la Kirekebisho kilichoanzia mjini Roma karne ya XVII. Pia walipatikana wenye heri 4.

Huko Hispania, baadhi ya wafuasi wa urekebisho wa Pekupeku, baada ya kuunganishwa na Waoservanti (1517) walimkimbilia Mkuu wa Wakonventuali ili kukwepa vizuio vya OFM, na mmojawao, Mt. Petro wa Alcantara (+1562) akafanywa Mkurugenzi wao (1557). Alipokufa, Pius IV (1560-1565) akawahamisha Waalkantara chini ya Waoservanti lakini bila ya kufuta kanda zao, katiba yao na mavazi yao maalumu. Gregori XIII (1572-1585) akamkataza Mkuu wa OFM asiingilie masuala yao ya ndani (1578), na Urbani VIII (1623-1644) akawaruhusu wasifuate tena katiba ya shirika lote (1642). Jinsi sisitizo la sala na toba linavyozaa matunda imethibitishwa na umisionari wao (Amerika na Asia Mashariki) na hasa na watakatifu 9 wa urekebisho huo, wakiwa ni pamoja na Mt. Paskali Baylon (+1592), mwenye ibada ya pekee kwa Ekaristi, wat. Petro Batista, Martino wa Kupaa na Fransisko Blanco, mapadri, halafu Fransisko wa Mt. Mikaeli, Gonzalo Garcia na Filipo wa Yesu, mabradha, ambao wote walifia dini Japani (+1597), hatimaye Mt. Yohane Yosefu wa Msalaba (+1734), mpenda ufukara mkuu. Pia walipatikana wenye heri 22.

Huko Ufaransa makao ya upwekeni hayakustawi sana hadi mwisho wa karne ya XVI. Mwaka 1601 walioishi huko wakapewa na Kanisa Mkurugenzi mwenye mamlaka pana sana; hapo wakaenea haraka kwa msaada wa mfalme, hata kanda zote za Ujerumani na Uholanzi zikajirekebisha na kujiunga nao, wakaitwa Warekoleti. Mmojawao ni Mt. John Wall (+1679), aliyefia dini huko Uingereza.

Katika karne ya XVI na ya XVII karibu kila mkutano mkuu wa OFM ulizungumzia katiba na kupigania umoja, ambao haukuwa rahisi kutokana na mchanganyiko wa ndugu waliopenda fadhili za Wakonventuali na wengine waliotaka urekebisho. Katika hali hiyo Watumishi wakuu walijitahidi kuhuisha shirika lote, lakini wengi wao walitumwa na Mapapa kama mabalozi kwa wafalme na Maaskofu wa Ulaya, au walipewa uaskofu wa miji muhimu. Shirika halikupendezwa kwa sababu lilikuja kukosa uongozi imara: ndiyo maana mara kadhaa liliwadai kiapo cha kutokubali kazi hizo au walau cha kujiuzulu Utumishi. Watakatifu waliopatikana kipindi hicho ni: Mt. Salvatore wa Horta (+1567), bradha aliyefanya miujiza mingi ajabu (labda milioni moja), wat. Nikolaus Pieck, Jeromu wa Weert, Teodoriko van der Eem, Nikasi wa Heeze, Wilehadi wa Denmaki, Godefrid wa Melveren, Antoni wa Weert, Antoni wa Hoornaert, Fransisko wa Roye, mapadri, halafu Petro wa Assche na Korneli wa Wijk-bij-Durstede (+1572), mabradha, ambao wote walifia dini Uholanzi, Mt. John Jones (+1588), aliyefia dini Uingereza, hatimaye Fransisko Solano (+1610), mmisionari bora Amerika Kusini aliyezunguka kotekote kwa miaka 14, akihubiri na kuimba. Wenye heri wa kipindi hicho ni 17.

Karne ya XVII ikawa ya utulivu na utendaji, lakini ongezeko kubwa mno la watawa lilisababisha matatizo makubwa na ulegevu hata katika marekebisho. Pamoja na utaifa kuzidi, matawi ya Italia yalishindana kwa maandishi makali ya kukwaza. Makwazo mengine yalitokana na desturi ya Watumishi kadhaa kutuma watawa wasiofaa kwenye kanda nyingine au kuwaacha nyumbani mwa marafiki au ndugu. Badala ya juhudi za watawa kwa ajili ya kanuni kama katika karne zilizopita, sanasana tunakuta viongozi wakijitahidi kuwalazimisha washike kanuni, lakini bidii za namna hiyo hazikuweza kufanikiwa kwa kuwa hazikutoka moyoni mwa watawa. Hatimaye mwaka 1676 mkutano mkuu ulikubali na kuagiza kila kanda ianzishe makao 3-4 ya upwekeni ambapo yafanyike malezi ya watakaji na wanovisi wote: baadaye katika mazingira hayo walistawi wat. Thomas wa Cori (+1729), mhubiri maarufu na Teofilo wa Corte (+1740), mwanafunzi wake. Lakini katika karne ya XVIII ilionekana wazi jinsi matazamio ya wengi yalivyolenga kupata kwa visingizio vyovyote fadhili na nafasi za kwanzakwanza. Kupitia mikutano mikuu upuuzi wa namna hiyo uliathiri sheria za shirika. Pia mabadiliko mengi mno ya katiba, badala ya kusaidia nidhamu, yalizidi kuipunguza kwa kusababisha ndugu wasiijali katiba isiyodumu.

Upande wa Wakonventuali, utengano na Waoservanti haukuwaondolea baadhi yao wasiwasi kuhusu utekelezaji wa kanuni, ingawa Mtaguso wa Trento ulitamka (1563) kwamba OFM na Wakapuchini tu hawaruhusiwi kuwa na mali hata kishirika, tofauti na Wakonventuali na mashirika mengine yote. Uhusiano na matawi yaliyokimbilia chini ya Mkuu wao ili kufuata urekebisho ulichochea hamu ya kuwaiga. Ndivyo walivyoanza Wakonventuali wa Urekebisho Hispania: uenezi wao ulichangia uamuzi wa Mt. Pio V (1566-1572) wa kuunganisha na OFM Wakonventuali wote wa Hispania na Ureno (1566-1567). Juhudi za mikutano, za Watumishi wakuu na za watawa wenyewe zilileta nidhamu na ustawi, hasa mmojawao alipochaguliwa kuwa Papa Sisto V (1585-1590) akaanza kuwasaidia kwa kila njia, kama vile kuunganisha chini ya Wakonventuali marekebisho madogo yaliyokuwa yameanza Italia (1562). Ila mwaka 1669 yakaja kutawanywa, baada ya kusumbuliwa sana na Wakonventuali wa kawaida na Wakapuchini (kuhusu sare zao zilizofanana). Kabla ya hapo mkutano mkuu ulitunga katiba mpya kabisa (1625) ili kuondoa misimamo tofauti kuhusu kanuni: katiba hiyo haikufuata matamko ya zamani ya Mapapa juu ya kanuni, bali ilipitisha moja kwa moja desturi za shirika zilivyokuwa. Baada ya kuthibitishwa na Urbani VIII, Wakonventuali wakaanza kuweka nadhiri zao kwa kutamka wazi kuwa watashika kanuni “kadiri ya katiba ya Urbani” tu.

Baada ya kujipatia hivyo msimamo wa kudumu, Wakonventuali wakazaa mwenye heri 1 na watakatifu 2 waliong’aa mmoja hasa upande wa sala, mwingine upande wa utume: Mt. Yosefu wa Copertino (+1663) na Mt. Fransisko Antonio Fasani (+1742), wote mapadri. Pia shirika liliendelea kusifiwa upande wa elimudini likaona mtawa wake mwingine kuwa Papa (Klementi XIV, 1769-1774) ambaye naye alilipendelea sana, k.mf. kwa kuwahamisha Waoservanti wote wa Ufaransa chini ya Wakonventuali. Kwa mara nyingine upendeleo huo ukazaa chuki ya wengine ilivyojitokeza kisha kufa kwake.

Takwimu ya jumla ya Utawa I ni kama ifuatavyo:

 

Matawi

Mwaka 1575 hivi

Mwaka 1700 hivi

Mwaka 1762 hivi

   (Waoservanti)

32,750

36,400

39,900

   (Pekupeku)

1,700

6,600

7,000

   (Wariformati)

500

13,900

19,000

   (Warekoleti)

50

9,200

11,000

OFM jumla

35,000

66,100

76,900

Wakonventuali

12,000

15,200

21,000

Wakapuchini

3,600

27,300

34,000

Jumla kuu

50,600

108,600

131,900

 

Bila ya kujali tofauti kati ya tawi na tawi, karibu 60% walikuwa mapadri, ambao nusu ya idadi yao walikuwa wahubiri, nusu “mapadri wa Misa na sufuria” tu. Ongezeko lilipungua kwanza kutokana na Uprotestanti kuenea na kufuta kanda kadhaa Ulaya Kaskazini, na utawala wa Kiislamu kuenea Ulaya Mashariki Kusini, ingawa pande nyingine zilifidia. Karne yenye ongezeko la kasi zaidi ni ile ya XVII: ndio mwanzo wa wasiwasi na hofu kwa viongozi wa Kanisa na serikali, kwa kuwa mashirika mengine pia yalikua. Kuanzia mwaka 1634 Mapapa walichukua hatua kuzuia upokeaji wa wanovisi na kupunguza konventi (Italia zilifungwa 24.2%), hata kufikiria uwezekano wa kuwapeleka watawa vijana kupigana na Waturuki ili kuwapunguza! Lakini hatua hizo hazikufanikiwa. Kuhusu uenezi, wakati wa kufikia kilele cha idadi ya wanashirika mgawanyo ulikuwa ifuatavyo:

 

Nchi

OFM

OFMConv

OFMCap

Jumla

Italia na visiwa

26,000

10,700

15,700

52,400

Hispania na makoloni

23,000

0

3,100

26,100

Ufaransa

9,500

5,400

6,100

21,000

Ujerumani n.k.

9,600

2,600

8,100

20,300

Ureno na makoloni

4,000

0

0

4,000

Dola la Waturuki

1,700

800

300

2,800

Polandi na Urusi

1,500

1,500

0

3,000

Uingereza na Irelandi

1,600

0

150

1,750

1.2.2. MAISHA NDANI YA SHIRIKA

 

Kadiri ya hati ya utengano (1517) Mkuu wa Waoservanti tu alikubaliwa kuitwa Mtumishi mkuu, wakati yule wa Wakonventuali alipewa jina la Mwalimu Mkuu; vilevile viongozi wa kanda. Lakini jina hilo jipya halikuja kutumika. Mkuu wa Wakapuchini aliitwa Makamu (wa Mkuu wa Wakonventuali aliyetakiwa kumthibitisha baada ya kuchaguliwa). Jina la “Mtumishi mkuu wa Shirika lote” lililotumiwa na Mkuu wa OFM lilichukiwa na kulalamikiwa na Wakonventuali na Wakapuchini, hadi Paulo V alipotamka kuwa hao wote ni wana halisi wa Mt. Fransisko, na Wakuu wao ni waandamizi wake halali (1619). Hata hivyo mabishano ya wazi yakaendelea kuhusu mlolongo wa uandamizi huo, mtindo asili wa kanzu na hasa kofia yake, mpaka Aleksanda VIII (1689-1691) alipokataza maandishi yote juu ya hayo.

Kwanza Kardinali mlinzi alikuwa mmoja kwa wote, halafu Wakapuchini wakakubaliwa kuwa na mmoja wa kwao (1564), na vilevile Wakonventuali (1580). Mara kadhaa waliingilia mno masuala ya shirika hadi kulivuruga na kusababisha Mapapa walazimike kuwazuia. Mamlaka yao ilipungua ilipoanzishwa Idara ya Papa kwa Watawa (1586). Tofauti kati ya matawi kuhusu miundo ya ndani ziliendelea, hasa upande wa mikutano, lakini hazikupata kamwe kuwa kubwa mno, kwa sababu ya kanuni na mapokeo yao kuwa mamoja.

Haikuwa rahisi kwa viongozi kuhuisha kiroho umati mkubwa vile wa watawa, hasa tukizingatia jinsi Wafransisko wasivyopangika. Ili kuleta nidhamu zilitumika mbinu za kisheria: ziara za Mkuu zilizofanyika kwa ukali na adhabu hata ya kufungwa na kufukuzwa. Mbinu mpya (hasa kuanzia katikati ya karne ya XVII) ni mazoezi ya kiroho; pengine zilisambazwa pia barua za Mkuu.

Maisha ya kiroho yalistawi hasa Hispania katika karne ya XVI, Ufaransa katika ile ya XVII, na Italia katika karne za XVI-XVIII. Katika hiyo karne ya dhahabu ya Hispania, Ndugu Wadogo walichanga na wananchi wenzao walioandika juu ya maisha ya kiroho: ufafanuzi kamili wa mang’amuzi ya ndani na teolojia ya kiroho pamoja na ugumu wa maisha, ingawa walifuata mapokeo ya shirika kwa kusisitiza zaidi uhuru wa roho, ubora wa upendo na usahili katika kumuelekea Mungu. Ndugu wa Italia walielekea zaidi utendaji hasa katika huruma, hivyo hawakulenga mirukoruko katika ibada. Hasa Wakapuchini walijitahidi toka mwanzo kuandika vitabu vyenye lengo la kujenga kiroho wasomaji na kuwaelekeza wote katika sala kama njia bora ya kurekebisha maisha. Ndugu wa Ufaransa walizingatia hasa matakwa ya Mungu kama muhtasari wa hatua tatu za maisha ya kiroho.

Katika karne hizo mtindo wa Baroko ulitawala sanaa na maisha ya jamii pia, ukijali sura kuliko undani, vitendo kuliko moyo: hivyo mapambo na madoido yakazidishwa sana. Hiyo ni sababu mojawapo ya marekebisho kusifiwa kadiri yalivyojitokeza katika miguu mitupu, nguo duni, majengo fukara na mwenendo adili. Mambo hayo yalipotokana na msimamo wa moyo yalijenga kweli, tofauti na yalipofanyika kwa nje tu.

Maisha katika marekebisho yalikuwa magumu, si ya kuvutia, ingawa riziki hazikukosekana kwa ukarimu wa walei. Kila mmojawapo mwanzoni ulilenga kuwa na ndugu wachache katika nyumba ili kurahisisha usahili, ufukara na udugu, lakini polepole idadi ikaongezeka kwa faida ya taratibu za kitawa na hasa fahari ya ibada. Mwaka 1680 kwa wastani kulikuwa na ndugu 17 kwa nyumba; mwaka 1762 walifikia 20. Pamoja na mapadri, mafrateri (kwa maana ya wenye kusomea upadri au walau walionyolewa tonsura) na mabradha kulikuwa na Watersyari wa kudumu katika jumuia. Mwanzoni mwa kila urekebisho mabradha walikuwa wengi, halafu wakazidi kupungua kutokana na kuchujwa sana; lakini pia kwa sababu wakazidi kukosa nafasi, wakipangwa hata baada ya wanovisi watakaosomea upadri! Mtaguso wa Trento uliwanyima haki ya kupiga na kupigwa kura, ila Mt. Pio V aliwarudishia Wakapuchini. Hivyo mabradha wengi walijitafutia ruhusa ya kuhamia kati ya mafrateri, kinyume cha sheria. Wasio mapadri walizidi kupokea Komunyo kuliko zamani. Shida kubwa ilikuwa bado namna ya kuwapa kazi mapadri wasio wahubiri, kwa kuwa hawakufanya utume wala kazi za mikono. Shughuli kuu ilikuwa Misa na Sala ya Kanisa iliyoadhimishwa usiku (lakini kwa Wakonventuali si mahali pote) na mchana kwa nyimbo (isipokuwa Wakapuchini na Wariformati walipendelea kuacha nafasi zaidi kwa sala ya moyo).

Haja ya kutafuta miito haikuwepo; kazi ilikuwa kuichuja tu kwa majaribu mengi. Hata desturi ya Wakonventuali ya kupokea watoto ikaja kwisha karne ya XVI. Ili mtu apokewe kama frateri alipaswa kuwa na elimu ya msingi na kujua Kilatini. Hayakufikiriwa makao ya malezi kwa watakaji. Kwa wanovisi Klementi VIII (1592-1605) aliagiza (1596) zichaguliwe tu nyumba ambapo maisha ya kitawa yanashikwa kikamilifu; tena watengewe sehemu maalumu na kuwasiliana na mlezi wao na msaidizi wake tu, pamoja na kushiriki ratiba ya jumuia (sala, milo n.k.). Katika karne ya XVIII zikaanza kutokea nyumba za unovisi kwa mabradha tu, zilizozidisha utengano wa kitabaka ndani ya shirika. Kazi ya mwaka wa jaribio ilikuwa hasa kueleza kanuni na amri zake kadiri ya matamko ya Mapapa; mapokeo ya shirika; nidhamu; juhudi za kiroho; taratibu za ibada (pamoja na kuimba, kwa Wakonventuali na Waoservanti); Sala ya Kanisa; hasa utekelezaji wa sala na maadili. Walezi bora waliandika vizuri juu ya mang’amuzi yao. Baada ya nadhiri (ambazo zilikuwa za daima tu) watawa chipukizi walitakiwa kuendelea na malezi miaka mitatu katika nyumba ya kuaminika. Kulikuwa na maagizo kuhusu malezi ya kudumu pia (vipindi vya mara kwa mara kwa wote).

 

1.2.3. UTUME

 

Mikutano mikuu ilishughulikia utume wa kuhubiri ikisisitiza ndugu waandaliwe na kuchujwa kwa makini, halafu wasiofaa wanyang’anywe ruhusa. Pia zilipangwa ngazi mbalimbali: kuanzia wahubiri wa konventi na wa kanisa lake hadi wahubiri wakuu wa mahali muhimu zaidi alipojiwekea Mtumishi mkuu (Italia palikuwa 30). Lakini mvuto wa elimu ulisababisha huduma za kiroho zisizingatiwe sana na ndugu wenye vipawa vingi zaidi. Basi, ili kuwavuta wakahubiri na kuungamisha Mkuu wa OFM alipewa haki ya kuwapa fadhili na vyeo, kama kawaida ya wakati huo.

Urekebisho wa Wakapuchini ulipinga mitindo ya kuhubiri kwa kurudia unyofu wa Injili, kuhimiza ushuhuda wa maisha na kulenga wongofu wa wasikilizaji. Kwa karne moja na zaidi hao waliendelea kuwa wahubiri bora, kwa jinsi wanavyoelewa watu na kugusa sio akili tu, bali mioyo pia, ya wadogo na hata ya wasomi. Hayo yalikuwa matokeo ya maisha bora ya kiroho, lakini pia ya maandalizi ya mpango chini ya walimu wa hakika. Walipoanza (1650 hivi) kufuata mitindo ya Baroko, matunda yakapungua. Wahubiri waliongoza pia roho binafsi. Wafransiskani waliungamisha sana, kumbe Wakapuchini walisita kupokea kazi hiyo, isije ikavuruga maisha yao ya sala hasa. Walianza kuifanya nje ya Italia (katika mkoa wa Alsasya kati ya mwaka 1740 na 1747 waliungamisha mara 24 milioni!), lakini walitakiwa kuwa na sifa maalumu.

Kati ya mahubiri zilishika nafasi ya pekee wiki za uamsho, hasa kuanzia mwaka 1650 hivi. Waliokusudiwa kuziendesha walidaiwa maandalizi kamili. Baadhi zilifanywa na ndugu 30 hadi 60 kwa pamoja. Kulikuwa na mafundisho maalumu kwa makundi (watoto, vijana, akina baba, akina mama) na pengine mfungo wa siku nne kwa makundi ya pekee. Mbinu zilikuwa mbalimbali, lakini licha ya kufundisha imani na maadili Wakapuchini hawakukosa kuelekeza watu wote namna ya kufanya sala ya moyo. Wahispania walitumia sana maandamano ya toba, rozari za hadhara n.k. Waitalia walikuwa wakipanda msalaba karibu na mji au kijiji uwe kumbukumbu. Maarufu kuliko wote waliofanya kazi hiyo ni Mt. Leonardo wa Portomaurizio, aliyeendesha wiki hizo mara 343, akiongozana kwa kawaida na mapadri 4 na bradha 1. Baada ya wiki mbili za mahubiri kulikuwa na wiki moja ya maungamo. Katika miaka 44 aliokoa watu wengi ajabu, na kuinua hali ya roho ya mapadri wanajimbo na watawa katika Italia karibu nzima. Ndiye mwenezaji mkuu wa Njia ya Msalaba, ibada iliyoanza kustawi katika karne ya XV ikiwa na vituo 7 hadi 37, mpaka ile ya 14 ilipopewa rehema ya pekee (1686) na hivyo kuenea popote. Kumbe kiini cha wiki za uamsho za Wakapuchini kilikuwa ni kuabudu ekaristi kwa saa 40 mfululizo, ibada iliyoanza mwaka 1535 na kutoa nafasi ya kuhubiri kwa nguvu zaidi.

Ndugu Wadogo walieneza ibada nyingine pia, hata kabla Kanisa halijazikubali rasmi, kama vile kwa Moyo wa Yesu, kwa Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili (aliyetangazwa na mkutano mkuu wa mwaka 1645 kuwa msimamizi wa shirika) na ile ya kujifanya watumwa wake. Kuanzia karne ya XV Wakonventuali walieneza rozari ya furaha saba za Bikira Maria, na chama cha kamba ya Kifransisko (ambayo hata watakatifu 4 wasio wanashirika walipenda kuivaa kiunoni).

Ndugu Wadogo waliendelea kushika nafasi muhimu katika Kanisa: 739 walikuwa Maaskofu (kati ya mwaka 1503 na 1710), 16 Makardinali (karne ya XVI hadi ya XVIII), na 2 wakafikia Upapa. Wengine pia waliathiri sana siasa, k.mf. katika vita vya madhehebu, katika kutetea haki za Kanisa dhidi ya serikali, na hasa kama mabalozi wa Mapapa na wa wafalme Wakatoliki.

Hasa Wakapuchini walijihusisha na aina mbalimbali za utume wa kijamii, wakidaiwa na katiba kujitosa hadi ushujaa. Kwa namna ya pekee walifanya hivyo yalipoenea maradhi ya kuambukiza, hasa tauni. Katika karne ya XVI na XVII kila mara walijihatarisha na kufa ili wahudumie kiroho na kimwili walioambukizwa. Ilivutia sana kuona wanajumuia wote kujitolea. Tunafahamu zaidi ya ndugu 2,000 waliokufa hivyo, lakini walikuwa walau mara mbili zaidi, bila ya kuhesabu ndugu wengi wa matawi mengine. Katika miji mingi walikabidhiwa uongozi wa hospitali nzima, hata nje ya nyakati za tauni. Zaidi ya hayo Wakapuchini hasa walihudumia kiroho wagonjwa na walio mahututi, walianzisha vyama vya kutolea huduma hizo, walichapisha vitabu juu yake, walipenya magereza ili kuhudumia wafungwa na waliohukumiwa kufa. Ufaransa walikuwa wazimamoto pia. Hata vita viliwapa nafasi za kujitoa kwa upendo kama mapadri wa wanajeshi, hasa katika kuzuia Waturuki Waislamu wasiteke Ulaya nzima kati ya mwaka 1571 na 1686. Wafalme pia waliwatafuta sana Wakapuchini kama wahudumu wa roho na wa mwili wa askari wao.

Ndugu Wadogo walipambana na mifumo mbalimbali iliyofuatana kuzuka karne hizo na kupotosha imani na maadili, hasa Uprotestanti. Dhidi ya Rinascimento iliyotaka kurudisha Ulaya kwenye mitazamo ya kipagani, marekebisho ya karne ya XVI yalihubiri toba na kushuhudia dharau ya anasa. Dhidi ya Ujanseni shirika lilitetea kwa mahubiri na maandishi kipeo cha Kiinjili na mapokeo ya ibada. Dhidi ya waasi wa dini walioshambulia misingi ya Ukristo, huko Ufaransa walianzisha hata gazeti la kutetea dini.

Ingawa uenezi wa Uprotestanti ulifunga konventi nyingi, hakuna hata moja iliyoasi jumla. Idadi ya Wafransisko waliouingia ni ndogo kulingana na ile ya walioupinga tangu ulipoanza, kabla wengi hawajatambua hatari. Kardinali wa Brandeburg aliwakataza (1519) wasiendelee kuhubiri dhidi ya Martin Luther, kumbe Mtumishi mkuu alipofika Ujerumani aliagiza maandishi yake yachomwe, wahubiri waandaliwe kumshambulia tena na wanashirika wote wasali na kujiandaa kufia imani (kama walivyofanya walau 500 katika miaka 1520-1620). Walutheri walitokeza chuki yao kwa kueneza kitabu cha dhihaka “Kurani ya Pekupeku”. Baadaye Ndugu Wadogo wakawa kati ya mashirika muhimu zaidi katika kurudisha Ukatoliki kwenye miji na vijiji. Wakapuchini walianza kupambana na Uprotestanti kwa mahubiri na katekesi huko Italia usije ukaipenya, wakawa wa kwanza kujitolea kutumwa na Idara ya Papa kwa Uenezaji wa Imani mara ilipoanzishwa (1622). Chini yake juhudi ziliongezeka na kupangwa vizuri zaidi. Chuo chake mjini Roma kilianzishwa (1627) hasa kwa juhudi na ukarimu wa Kardinali Mkapuchini. Idara ilikuwa ikituma wale wote waliopendekezwa na wakubwa wao wakiwa na sifa upande wa maadili na elimu. Katika karne ya XVII idadi kubwa ya waliotumwa ni Wakapuchini. Agizo la shirika lilikuwa kuwasiliana na Waprotestanti kwa kufuata mbinu za Mt. Fransisko wa Sales (+1622), yaani kwa upole, usikivu na ushuhuda wa maisha safi yenye kujitosa. Pia Wakapuchini walishirikisha waamini katika kazi hiyo ngumu, na kuandika vitabu vya mabishano. Huko Uingereza na Irelandi baada ya kufukuzwa wote, kwa karne tatu Wafransiskani wakaendelea kuingia ili kufanya utume kwa siri kutoka Ulaya Bara walipopokea na kulea miito ya visiwa hivyo.

Wakonventuali walifanya kazi hasa kati ya Waortodoksi, wakivuta baadhi yao upande wa Roma na kutunza makundi madogomadogo ya Wakatoliki waliosambaa Mashariki. Pia walizuia Uprotestanti usienee kati ya Waortodoksi, hasa kwa kufaulu kumuondosha Patriarki wa Kostantinopoli aliyetaka kuhalalisha ungamo la imani la Wakalvini. Idara ya Papa ilistawisha pia misheni za Waoservanti chini ya utawala wa Waturuki, ambapo wengi walifia dini. Vilevile Wakapuchini walienea sehemu hizo na Urusi. Katika karne ya XVI Wafransiskani walichuma tunda bora India Kusini walipoungana na Roma Askofu Msiro-Malabari na familia 30,000. Wariformati walifanya kazi miaka 160 Ethiopia wakamwaga damu yao kwa wingi wasikate tamaa.

Kuhusu uenezaji Injili kwa wasio Wakristo, karne ya XVI na XVII zilikuwa na miito mingi ya kimisionari, hata likatokea swali, “Je, Watumishi wanaweza kuzuia watawa wasiende kwenye nchi za misheni?”. Kumbe karne ya XVIII wito huo haukuvutia tena umati wa ndugu wasio na kazi, hata swali likawa tofauti kabisa, “Je, Watumishi wanaweza kuagiza watawa wao waende Amerika?”. Mkuu wa OFM alifikia hatua ya kutangaza atawatenga na Kanisa watakaozuia watawa wasifuate wito huo. Kwa kuwachagua na kuandaa vilikuwa muhimu vyuo vya kimisionari, hasa miito hiyo ilipopungua: pamoja na kuwakusanya, kazi yake ilikuwa kuwafundisha lugha na kuwalea kiroho na kichungaji. Mara kwa mara Wakapuchini walisita kukubali misheni za mbali kwa kuhofia mazingira yatafanya watawa washindwe kufuata maisha ya shirika yaliyopangwa mtindo mmoja; pia umbali utamzuia Mkuu asiwatembelee kama desturi: ndiyo sababu hawakuanzisha miundo ya kudumu huko.

Upande wa Asia, Waturuki Waosmani walipoteka Yerusalemu (1517) walifunga wamisionari wote kwa miaka mingi, wakaendeleza dhuluma za kila aina pamoja na kuchochea ushindani na Waortodoksi kuhusu kumiliki mahali patakatifu hata kusababisha wauane nao. Utaifa uliwavuruga vilevile. Wafransiskani walianzisha kanda huko India (1583) wakazidi kuenea Mashariki hadi Indonesia walipoanzisha kanda nyingine (1622). Misheni za Filipino ni sifa kubwa ya Pekupeku walioanzisha kanda huko (1586) na kulipatia Kanisa (kwa msaada hasa wa Wajesuiti) nchi kubwa pekee ya Kikatoliki katika Asia nzima. Toka huko wakaenea katika nchi zote za kandokando kuanzia China, walipoongoa mtu aliyekuja kuwa Askofu Mchina wa kwanza. Ila mabishano yao na Wajesuiti kuhusu mbinu za umisionari yalikwaza sana hata kudai Papa aingilie kati. Dhuluma zilipoanza (1723), thuluthi moja ya Wakatoliki 300,000 wa China walikuwa chini ya Ndugu Wadogo, ambao wakafichama na kuendelea na kazi yao, bila ya kujali jela na kifo, kama walivyofanya pia Vietinamu na Kampuchia. Hata Japani ulizuka ushindani na Wajesuiti, halafu dhuluma kali za serikali, lakini umisionari ukaendelea na kuongoa wengi zaidi. Baada ya Wafransisko 354 wa Utawa I na III kufia dini, waamini wakaendelea kwa siri bila ya mapadri: wamisionari wapya walipofika (1865) wakakuta Wakristo wenye majina ya Kifransisko! Upande wa Wakapuchini walianzisha misheni India (1632) ambapo walishindana na Wajesuiti kuhusu madhehebu ya Kimalabari hadi mwaka 1744. Sifa kubwa zaidi ilipata misheni ya Tibet (1707-1745) iliyoeneza Injili hadi Nepali, Butani na Bengala.

Tofauti na India, Afrika na Brazili (zilizokabidhiwa na Papa kwa Wareno), sehemu nyingi za Amerika zilikabidhiwa kwa Wahispania. Kanda OFM ya visiwani ilizidi kustawi hata watawa wake kufanya kazi ngumu Venezuela na Guyana (1540); baada ya majaribio kadhaa wakafaulu kupenya kati ya wazalendo wa Panama halafu kuenea Kolombia, ambapo hadi mwisho wa karne ya XVI walibatiza Wahindi Wekundu 200,000. Wakati huo barani kulikuwa na kanda yenye ndugu 145; miaka 100 baadaye walikuwa 338. Wafransiskani 2 walifika Mexico pamoja na wavamizi (1519), lakini kazi rasmi ilianza miaka 5 baadaye, walipotumwa Waguadalupe 12 walioandaliwa vizuri; hao wakatunga sarufi, kamusi na katekisimu kwa lugha ya Kiazteka na kuanzisha shule. Watu waliongoka kwa wingi mkubwa ajabu: 200,000 hadi mwaka 1529, 1,000,000 hadi 1531, 5,000,000 hadi 1536, 9,000,000 hadi 1540 (Wamersedari, halafu Wadominiko na Waagustino walisaidia pia). Ndugu Wadogo walienea Kusini (1525) hadi Gwatemala, Honduras na Nikaragua, na Kaskazini (1527) katika maeneo ambayo sasa ni Marekani Kusini. Kanda ya Mexico iliyoanzishwa mwaka 1535 ikazaa nyingine 7 hadi Marekani Kusini (1612). Pekupeku pia walianzisha kanda (1599). Mwisho wa karne ya XVII kulikuwa na Wafransiskani 2,400, wengi wao wakiwa wananchi. Wavamizi wa Peruu pia waliongozana na Wafransisko katika safari ya kwanza (1527), halafu wakaletwa “mitume 12” waliofanya kazi bora Meksiko (1531), wakifuatwa na wengine wengi kutoka Hispania hata ikaundwa kanda (1553) ambayo nyumba yake mojawapo ilifikia kuhudumia parokia 29 kati ya Wahindi Wekundu: Wafransisko 129 waliuawa nao. Mjini Lima ilianzishwa konventi kubwa ya malezi kwa wamisionari wa Amerika Kusini karibu nzima. Mapema waliingia Ekwador (1533) wakaunda kanda (1565), sawasawa na walivyofanya Chile, ingawa huko hawakuongezeka sana kwa sababu wengi waliuawa katika mapigano ya muda mrefu ya wenyeji dhidi ya wakoloni. Toka Peruu Ndugu Wadogo walifanya umisionari kati ya Wahindi Wekundu wa Bolivia pia hadi mwaka 1793. Walikuwa pia wa kwanza kufika Amerika Kusini Mashariki (Paragwai, Ajentina na Urugwai) ilipoanzishwa kanda (1612). Huko Brazili, kwa miaka 100 Pekupeku walianzisha kanda mbili (1657, 1675). Katika karne ya XVII waliingia pia Wakapuchini na Waoservanti kufanya kazi hasa kwa Wahindi Wekundu, halafu kwa Wanegro na Wazungu. Wafransiskani wengine walifanya kazi katika makoloni ya Waingereza Marekani Magharibi, ingawa mmojammoja tu, halafu Wakapuchini waliingia katika makoloni ya Wafaransa visiwani, Guyana na Marekani ya Kati (1722), wakafanya kazi miaka mingi Panama, Haiti, Trinidad n.k. Hata Kanada wamisionari wa kwanza walikuwa Ndugu Wadogo (Warekoleti kuanzia mwaka 1615, halafu Wakapuchini): misheni zao zilifungwa kila mara maeneo ya Wafaransa yalipotekwa na Waingereza.

Upande wa Afrika, misheni ya Moroko iliendelea hadi alipouawa Mfransiskani wa Italia (1532) ikafunguliwa tena na Wakapuchini (1624-1700), wakifuatwa na Pekupeku (kuanzia 1630). Huko Tunisia Wakapuchini walipojaribu mara ya pili walifaulu kufungua nyumba (1674). Huko Libya Wariformati (1630), halafu Wakapuchini waliendelea muda mrefu kwa matunda mengi. Huko Misri Wafransiskani waliendelea hadi karne ya XIX. Afrika Magharibi (Gine, Kepuvede, Siera Leoni) walifanya kazi zaidi Wakapuchini (kuanzia 1634), ingawa walifukuzwa mara kadhaa. Wafransiskani walianzisha misheni ya kudumu Kabo Verde (1656), iliyoeneza kazi yake hadi Siera Leoni. Misheni bora ni ile ya Wakapuchini Kongo-Angola (1645-1835), ingawa kulikuwa na matatizo mengi (kwa miaka 100 walifia huko wamisionari 144). Aliyeianzisha alikubaliwa kufungua nyingine Nijeria (1651-1693). Wakapuchini walianzisha misheni nyingine ya kudumu katika kisiwa cha Saotome (1686) wakihudumia hata Wakristo wa pwani.

Mtaguso wa Trento ulikuwa fursa kwa kila shirika kutambulisha wasomi wake. Ndugu Wadogo waliuchangia sana kupitia Maaskofu na wanateolojia waliohudhuria: Wakonventuali 67, Waoservanti 57 na Wakapuchini 8. Idadi inaonyesha kuwa upande wa masomo, waliofanya juhudi zaidi ni Wakonventuali, kwa kuwa hawakupatwa kamwe na wasiwasi wa marekebisho yote kuhusu hatari zake. Labda ndiyo kazi kubwa zaidi waliyolifanyia Kanisa, hasa kama washauri wa Idara za Mapapa na kama waandishi wa vitabu. Hata Waoservanti, walipoondoa wasiwasi huo, wakaona masomo kuwa kazi ya lazima kwa shirika, wakaendelea sana katika elimu (karne ya XVI na XVII). Kati ya Wakapuchini elimu ilishirikishwa kibinafsi tu, wasianzishe nyumba za masomo mpaka Mtaguso huo ulipolazimisha kuyapanga. Hapo wakasisitiza ndugu wasisome kwa ajili ya elimu, bali kwa kujirekebisha na kurekebisha wengine. Kwa jumla Ndugu Wadogo, hasa Italia, walikwepa vyuo vikuu na digrii mpaka Sisto V, katika jitihada zake kwa ajili ya Wakonventuali wenzake, alipoanzisha (1587) Chuo cha Mt. Bonaventura kama kiini cha shirika lao upande wa elimu. Mwalimu huyo na M.H. Yohane Duns Scoto ndio waliofuatwa zaidi na Ndugu Wadogo wa karne hizo, ingawa hakuna aliyetangazwa rasmi kuwa afuatwe na shirika katika falsafa na teolojia. Katika nusu ya kwanza ya karne ya XVII walimtetea sana Scoto dhidi ya mashambulizi ya Wadominiko (washabiki wa Mt. Thoma wa Akwino), hata baadhi wakajaribu kumfanya atangazwe hivyo ili shirika lijitukuze kwa wataalamu wake kama mengine yalivyofanya. Mabishano hayakusaidia kujua ukweli, bali yalijenga ukuta kati ya mashirika hayo mawili yenye udugu wa asili. Hatimaye mkutano mkuu ukahimiza (1651) uhusiano mzuri na Wadominiko katika elimudini, shetani asiachiwe nafasi ya kufitini. Wakonventuali na Waoservanti waliujali sana muziki pia, kinyume cha Wakapuchini na Wariformati.

 

 

1.3. NDUGU WADOGO KATIKA ULIMWENGU WA KISASA (1762–2005)

 

1.3.1. MATATIZO YA NDANI NA YA NJE (1762–1869)

 

Ongezeko la watawa lilifikia kilele chake kati ya mwaka 1760 na 1770, likishinda vizuio vilivyowekwa na viongozi wa Kanisa. Kama kawaida, shaka zilizosababishwa na mageuzi ya harakaharaka katika jamii na uchumi zilichangia pia ongezeko la miito ya wasiwasi yenye kutafuta usalama konventini. Kadiri hiyohiyo ilionekana wazi kuwa wingi si hoja na kuwa umati wa watawa haukuhuishwa na vipeo halisi. Uvivu haukuepukika ukazaa ulegevu na maovu mengi. Ingawa watu wadogo waliendelea kuwaheshimu watawa, wasomi walizidi kuwaona vielelezo wa tunu zisizo na maana tena. Jamii ilipokuwa inaelekea kasi matazamio mapya hata upande wa dini, watawa walizidi kujitenga konventini wakijali desturi zao na elimu yao ya kidini bila ya mawasiliano na elimudunia. Kati yao wachache tu walijitahidi kulinganisha imani na sayansi.

Kwa muda mfupi mashirika, hasa ya Ombaomba, yalikuja kudharauliwa na wengi. Kufuatana na mawazo mapya kuhusu uchumi, serikali zilizidi kuyatazama kama mzigo au donda kwa jamii. Bahati mbaya, hali ya mashirika ilistahili lawama nyingi zilizotolewa. Sababu nyingine zilizoleta dhoruba juu ya watawa ni kwamba serikali zilitamani mali za mashirika yao, na maadui wa Kanisa waliwafanya shabaha ya kwanza, kwa kuwa kila mara ndio wanaohakikisha zaidi uimara wa ukatoliki chini ya Papa na dhidi ya utaifa (ambao wakati huo ulichochewa na serikali na kupendeza Maaskofu wengi). Ukweli wa dhati ni kwamba Mungu alitaka kutakasa watu aliowakusudia wawe moyo wa Kanisa.

Katika barua rasmi za miaka hiyo, Watumishi wakuu waliweka wazi matatizo yaliyokuwepo (utaifa, ugomvi, uchu wa vyeo, wivu, malezi ya kulipua, kujiingiza katika masuala ya siasa, utovu wa unyofu na unyenyekevu, utovu wa usafi na nidhamu) pamoja na utabiri wa dhoruba ijayo. Ugumu wa hali unaonekana pia katika miundo mikuu ya utawa kwenda kinyume cha kawaida: OFM toka 1791 karibu mfululizo iliongozwa na Watumishi wakuu Pekupeku na Mriformati badala ya Waoservanti (waliokuwa na msimamo laini); vilevile Wakapuchini toka 1754 hadi 1789 waliongozwa karibu mfululizo na wasio Waitalia (tofauti na wanashirika wenzao, watawa wa nchi hiyo walikuwa wakiridhika zaidi na hali ya shirika na kupinga urekebisho). Pia mikutano mikuu haikufanyika muda mrefu: katika OFM tangu 1768 hadi 1856; kwa Wakonventuali tangu 1789 hadi 1847. Iliwabidi Mapapa wateue Watumishi wakuu.

Utatuzi ulijaribu kuelekea pande mbili: urekebisho wa hiari (kwa watawa wenyewe kujituma, hasa kwa kuanzisha makao ya upwekeni) na wa lazima (kwa viongozi kuimarisha nidhamu). Upande wa urekebisho wa hiari, kwa Waoservanti makao ya upwekeni yalikuwepo rasmi na kuhitaji kuhuishwa tu; kumbe matawi mengine hayakuwanayo. Watumishi wakuu wa Wakapuchini walijitahidi kuyaanzisha Italia na Hispania (huko kwa jina la “vyuo vya kimisionari”, yaani vituo vya sala na malezi ambapo watawa wajiandae kuhubiri) lakini walipingwa sana hata na washauri wao waliodai eti, shirika linafuata kwa umoja katiba yake, hivyo kukubali urekebisho ni kukiri limelegea; tena eti, anayetaka ukamilifu anaweza kuupata popote pale shirikani, hakuna haja ya kujitafutia mazingira ya pekee. Zilipokosekana juhudi za kutoka rohoni ililibidi shirika, hasa katika ngazi ya kanda, lidai vitendo vya nje vilivyopangwa kikamilifu katika vitabu vya taratibu na desturi vilivyoandikwa hasa wakati huo. Hivyo uaminifu ulidhaniwa kuishia katika utekelezaji wa vipengele vingi hivyo, ambavyo tena viliachwa iwezekanavyo vishikwe na vijana na mabradha, huku wengine wakijitafutia fadhili ili kuviepa.

Serikali zilianza kuchukua hatua kali, zikidai haki ya kujihusisha na maisha yote ya Kanisa. Kisha kuwafukuza Wajesuiti kutoka nchi mbalimbali (1759-1768) zilimlazimisha Klementi XIV (1769-1774) kulifuta kabisa shirika lao (1773) lililokuwa kizuio kikubwa kwa serikali kutawala Kanisa mahalia (Maaskofu walikuwa wakiridhika au kunyamaza badala ya kutetea mamlaka ya Papa juu ya majimbo yote duniani). Kuhusu mashirika mengine serikali (kuanzia Ufaransa, 1765) zilitumia mbinu ya kuanzisha “kamati ya urekebisho” chini ya Maaskofu, zikificha hivyo malengo halisi. Hizo kamati zilitunga sheria za kunyongea mashirika: kupunguza au kufunga konventi zote za sehemu fulani au za aina fulani, kukataza kuombaomba, kupandisha umri wa kuingia unovisi, kupanga idadi yao, na hasa kuzuia mahudhurio katika mikutano mikuu kwa kudai mikutano ya kitaifa tu, vilevile katiba ya kitaifa badala ya ile ya shirika lote, uongozi wa kitaifa usio chini ya ule wa shirika lote, kukataza kukata rufaa kwa Papa n.k. Tukiondoa Dola la Kipapa, nchi zote za Ulaya zilipanga kunyonga mashirika. Kwa miaka 13 Ndugu Wadogo wa Ufaransa walipungua 3,756; kwa miaka 9 Hispania walipungua 5,582; kwa miaka 28 Polandi watawa walipungua asilimia 67! Chini ya siasa hiyo mashirika yalielekea kwisha bila ya sifa.

Kumbe mapinduzi ya Kifaransa yalipoanza kutumia nguvu zaidi na kuamua kufuta mashirika yote (1790) watawa wengi walipata taji la kifodini. Kisha kutupwa nje ya konventi, walipaswa kuchagua kati ya kula kiapo haramu cha kutii serikali badala ya Papa, au kuhama nchi au kukatwa kichwa. Wengi walikubali kwa furaha mwaliko wa kuacha utawa na kupewa pensheni; lakini wengiwengi pia walikwenda kuishi kitawa hasa Amerika, au walitoa uhai wao ili kutetea haki za Kanisa: kati ya wafiadini hao Wafransisko ni zaidi ya 250. Jeshi la Ufaransa llilipovamia karibu Ulaya nzima, sheria za namna hiyo zilienezwa Ubelgiji (1796), Italia Kaskazini-Magharibi (1802), Ujerumani Magharibi (1803), Italia Kusini (1809), Hispania (1810). Hata nchi nyingine za Ulaya ya kati zilifuta mashirika au kuyabana zaidi. Katika kipindi hicho waliishi watakatifu Egidi Maria wa Mt.Yosefu (+1812), Pekupeku ombaomba, na Yohane wa Triora, Mwoservanti aliyefia dini China (+1816). Akaja kufuata Mkapuchini Mt. Fransisko Maria wa Camporosso (+1866), bradha ombaomba mwenye upendo mkuu. Pia kuna wenye heri 25.

Wafaransa waliposhindwa, mkutano wa amani wa Vienna (1815) uliamua kurudisha iwezekanavyo hali iliyokuwepo Ulaya kabla ya mapinduzi. Hata mashirika wakajaribu kufanya hivyo, lakini haikuwa rahisi. Mawazo ya mapinduzi yalikuwa yameenea, yakidai uhuru na maendeleo. Watawa waliozoea kwa miaka kadhaa kuishi mmojammoja ulimwenguni, walipolazimishwa na Kanisa kurudi konventini hawakukubali tena nidhamu ya nadhiri. Pia ilikuwa vigumu kwao kuishi pamoja kutokana na misimamo yao tofauti kuhusu mapinduzi. Wasiwasi kuhusu kesho ukaendelea pia kwa sababu serikali mpya zilikuwa na siasa ileile ya kabla ya mapinduzi, hivyo mashirika yakaanza tena kufutwa: Urusi, ukiwa na Polandi chini yake (1831 hadi 1864), Ureno (1832-1890), Hispania (1836-1880), Italia Kaskazini Magharibi (kuanzia 1855), Italia nzima (kuanzia 1866), Ujerumani (1871-1875), Ufaransa (1880 kwa muda mfupi, tena kuanzia 1903). Wakati huo makoloni ya Amerika ya Kilatini yalijipatia uhuru (1820-1824): watawa wananchi walisimama wote upande wa mapinduzi, kumbe wamisionari (hasa Wahispania) waliyapinga wakateswa hadi kuuawa. Baada ya ushindi jamhuri mpya pia zilianza kudhulumu mashirika hata karibu kuyakomesha (k.mf. Brazili konventi zote ziliagizwa kufungwa mwaka 1822, Mexico mashirika yote yalifutwa mwaka 1855). Hivyo kila yalipotaka kuinuka, mashirika yalikumbwa na matatizo mapya. Hatimaye yalijikuta mali zake zimepungua sana, na wanashirika vilevile, lakini waliobaki wametakaswa kiasi kikubwa.

Kwa jumla, si wengi sana waliofurahia hatua za serikali kuwaondoa utawani, ingawa katika nchi nyingi walipewa pensheni. Kati yao mapadri walifanya kazi ya kichungaji jimboni, na baadhi wakawa Maaskofu; mabradha walitoa huduma katika sakristia au hospitali, ila wengine walirudi kwa ndugu zao. Idara ya Papa kwa Watawa ilitoa miongozo kuhusu hali yao na uhusiano na shirika, ikiwahimiza daima waishi kijumuia kadiri iwezekanavyo. Ndizo juhudi za Watumishi wakuu pia, ingawa waliona ugumu wa kuzitekeleza. Mang’amuzi ya maisha ya nje, yasiyo na hakika kiuchumi, yaliwasaidia watawa kuelewa watu wa kawaida, ambao si wakulima hasa kama zamani, bali umati wa wafanyakazi wenye kudhulumiwa na ubepari katika nchi za viwanda. Wakiishi ulimwenguni hasa Ndugu Wadogo waliacha usomi wao na tabia nyingine za tabaka la juu walizokuwanazo, wakajenga uhusiano mpya na watu na kuwajibika kuwasaidia hata kijamii. Miaka ya kukaa nje ya konventi ndiyo miaka ambapo mashirika mengi ya huduma yalianzishwa na watawa hao.

 

1.3.2. UKARABATI (1869-1962)

 

Maisha ya kitawa yalipoanza kuruhusiwa tena, waliojitahidi kufufua mashirika yao hawakufikiria kutekeleza karama asili katika mazingira mapya, bali kukarabati tu kilichobaki cha karne iliyopita. Waliridhika kujiona wanashangiliwa bado na watu wema wengi, bila ya kujali jamii inavyozidi kusogea mbali na tunu zao. Hivyo katika malezi wakasisitiza mambo yaleyale ya zamani hasa katika nchi (k.mf. Italia) ambapo miaka ya utawa kuzuiwa haikuwa mingi. Ndugu Wadogo waliweza kupata kwa urahisi miito ya kibradha, ila si ya kipadri, kwa kuwa wengi hawakuwa na elimu au ilikuwa tofauti na ile iliyodaiwa na Kanisa. Tena, waliokuwa wamesoma waliona wazi mbele yao njia za kufanikiwa ulimwenguni, na hawakuweza kufuata mitindo ya malezi ya kitawa iliyokuwa ileile ya zamani, yenye kusawazisha mno watu wenye vipawa tofauti. Basi, miito ikatafutwa kati ya watoto wa familia bora za wakulima wasioweza kuwasomesha: kwao ilikuwa heshima kuwa na mtoto padri mtawa. Ndivyo zilivyoanza (1869) seminari za kiserafi ambazo, baada ya kupingwa na watawa wazee, zikaja kuenea haraka na kuhimizwa rasmi katika matawi yote. Hapo muundo mzima wa malezi ukaja kubadilika, kwa kupatikana madarasa ya vijana wa kuongozana kuanzia umri wa miaka 11-12 hadi upadri, wakipata malezi yote utawani na hivyo kufyonza desturi, misimamo, mitazamo na matarajio ya shirika. Hawakukosekana watawa maarufu waliopinga malezi ambayo pengine haikuwa na maana tena wala ukweli na unyofu wa Kifransisko, ikitaka kusawazisha wote katika mitindo ya nje, na kugeuza vijana kuwa wanasesere wanaotenda lolote kwa kuongozwa. Hata hivyo seminari hizo ndogo zikawa mbinu kuu kwa karibu miaka mia.

Jubilei ya miaka 700 tangu azaliwe Mt. Fransisko (1882) iliadhimishwa kwa unyonge, lakini Leo XIII (1878-1903) alitoa hati iliyohimiza kufufua miundo ya Kifransisko, hasa Utawa III, dhidi ya ubinafsi unaotawala dunia. Miaka miwili baadaye Wakapuchini wakaadhimisha mkutano mkuu muhimu sana, uliochukua hatua mbalimbali na kumchagua Mtumishi mkuu bora aliyeongoza miaka 24 kwa mafanikio makubwa katika yote, k.mf. wanashirika wakiongezeka kutoka 7,896 hadi 10,083. Mwaka 1889 Wafransiskani pia, baada ya kuongozwa miaka 20 na Mriformati bora, wakafaulu kufanya mkutano mkuu uliotunga katiba kwa shirika lote, jambo lililokusudiwa bure tangu mwaka 1517; hata hivyo Wariformati walidai ruhusa ya kufuata pia sheria zao maalumu. Mwaka 1895 Leo XIII aliupendekezea mkutano mkuu muungano wa matawi OFM uwe agenda kuu, na Kardinali akaeleza namna ya kuyaunganisha. Waoservanti wote wakakubali, Warekoleti vilevile kwa sharti la kutunza ufukara kwa uangalifu, kumbe Wariformati na Pekupeku walio wengi wakakataa; jumla ya kura ikawa 77 ndiyo na 31 hapana. Basi kamati ikaandaa katiba mpya iliyothibitishwa mwaka 1897, halafu Leo XIII akatangaza rasmi muungano kamili wa matawi yote chini ya Mtumishi mkuu tu, ambao uonekane wazi hata kwa nje (kanzu ya mtindo mmoja badala ya ainaaina na rangi ya kahawia badala ya zile tofauti za awali: nyeusi, ya kijivu, ya zambarau na ya baharia). Akaagiza kanda zisizokubali wasiweze kupokea wanovisi tena, na watawa binafsi wasiokubali wapangiwe nyumba maalumu ambapo wakae wao tu, bila ya kuchanganyikana na walioungana. Hata hivyo muungano haukufanikiwa vizuri; Wahispania walikubali katiba lakini wakaendelea kujiongoza kitaifa hadi 1932; hasa majaribio ya kuunganisha katika kanda moja Wafransiskani wa matawi mbalimbali yalisababisha ushindani mwingi hadi juzijuzi. Hatimaye Wakonventuali pia walianza tena kufanya mikutano mikuu (1891); mwaka 1904 wakamchagua Mtumishi mkuu kutoka kanda ya Marekani, iliyoanzishwa 1872: hatua hiyo ilionyesha wazi mwelekeo mpya wa kimataifa.

Jubilei ya miaka 700 tangu shirika lianze (1909), iliadhimishwa kwa fahari zaidi, kutokana na hali ya kutumainisha ya matawi yote. Ila lilizuka suala la uhalisi wa shina na uongozi kuhusiana na Mt. Fransisko. Hapo Mt. Pius X (1903-1914) akatamka kwamba, “Watumishi wakuu wa familia tatu za Kifransisko wako sawa kwa heshima na mamlaka walizonazo, nao watazamwe sawia kama makamu na waandamizi halisi wa Mt. Fransisko, kila mmoja katika familia yake... Mashirika matatu ya familia ya Ndugu Wadogo ni kama matawi matatu ya mti uleule, ambao mzizi na shina lake ni Mt. Fransisko, na viungo vyake ni Ndugu Wadogo kwa haki kamili na sawia”.

Vita vikuu vya kwanza (1914-1918) na Mkusanyo wa Sheria za Kanisa (1917) havikuleta mabadiliko makubwa utawani. Jubilei ya kifo cha mwanzilishi (1926) ilichochea Wafransisko wote; hali ilikuwa tofauti na karne iliyopita, kwa sababu ya kujitolea sana hata kijamii, jambo lililowafanya waheshimiwe upya na Waprotestanti na waasi wa dini pia. Hata hivyo katika nchi chache dhuluma zikawajia tena: kwanza Mexico (1926-1932), halafu Hispania (1936-1939), walipouawa Ndugu Wadogo 320 na Wafransisko wengine 88. Baadaye vikazuka vita vikuu vya pili (1939-1945) vilivyoharibu sana hasa Ulaya ya Kati na kanda zake.

Lakini mabaya zaidi yakafuata Ulaya Mashariki ukiwa chini ya Ukomunisti ambao, pamoja na kueneza mafundisho ya wakanadini na kupotosha maadili, pengine ulifuta mashirika yote, pengine uliyawekea vizuio vingi. Kumbe Magharibi tunu nyingi zikaja kufifia kadiri uchumi ulivyostawi na kuleta anasa. Watawa wote na Kanisa zima wakajiuliza upya kuhusu maana ya uwepo wao katika ulimwengu wa kisasa. Majibu yakawa tofauti, na vizazi vikabishana: katika hali hiyo M.H. Yohane XXIII (1958-1963) aliitisha Mtaguso II wa Vatikani (1962-1965).

Ingawa kesi za kutangazia watakatifu zinachukua kwa kawaida miaka mingi, baadhi ya ndugu wa kipindi hicho wameshafikia hatua hiyo. Kuna Wafransiskani wanane waliofia dini China (1900): Maaskofu Gregori Grassi, Francesco Fogolla na Antonino Fantosati, halafu mapadri Elia Facchini, Teodoriko Balat, Giuseppe Maria Gambero na Cesidio Giacomantonio, hatimaye bradha Andrea Bauer. Wakapuchini wako watatu: bradha Konrado wa Parzham (+1894), bawabu; halafu mapadri Leopoldo Mandich (+1942) na Pio wa Pietrelcina (+1968), mashujaa wa kitubio. Mkonventuali ni mmoja, Maksimiliani Maria Kolbe (+1941), shahidi wa upendo katika makambi ya maangamizi ya Wanazi. Wenye heri wako 50, wengi wao wakiwa wafiadini.

 

1.3.3. CHANGAMOTO YA MTAGUSO II WA VATIKANI (1962-2005)

 

Mtaguso huo ulisisitiza kweli za kudumu na kuelekeza namna ya kukabili kichungaji ulimwengu wa kisasa. Kwa ajili hiyo watawa pia walidaiwa kujirekebisha upya, hasa kiroho. Ndugu Wadogo, sawa na watawa wote, walipaswa kurekebisha katiba zao pia kwa kutoa wote maoni yao, kufanya mikutano mikuu na majaribio mbalimbali. Kazi hiyo ilichukua miaka mingi kuliko ilivyotarajiwa, kwa kufikiria upya vipengele vyote vya maisha ya Kifransisko. Kwa mara ya kwanza mabadiliko ya katiba yaliwekwa mikononi mwa wanashirika, kwa kujali wingi si ubora wao, basi, iliwezekana kufuta harakaharaka mambo yaliyowashinda wengi, bila ya kujali kama yanafaa bado au la. Halafu wasiwasi uliokuwepo kabla ya Mtaguso ulilipuka na kusababisha wengi wapotewe na dira hata katika imani na maadili. Matokeo yake wengi waliacha utawa na upadri. Wengine walibaki pasipo msimamo, kwa kuona mengi ya zamani yamebadilishwa na mapya ni ya muda (yamekubaliwa kwa majaribio). Ratiba ya sala ilipunguzwa sana, kama si kuachwa kabisa. Utafiti uliofanywa na uongozi wa Wakapuchini ulionyesha kwamba wanashirika walio wengi wasingeshauri kijana kujiunga nao. Ndiyo sababu, pamoja na miito kujitokeza kwa nadra Ulaya, idadi ya Ndugu Wadogo ikapungua haraka tangu mwaka 1963 (OFM) na 1964 (OFMCap); kumbe Wakonventuali walipungua haraka kati ya 1968 na 1975, halafu wakaanza kuongezeka polepole sana.

Wengine wasioridhika na mabadiliko hayo, baada ya kunyimwa na Watumishi wao uhuru waliotaka kwa kufuata maisha ya kijumuia ya Kifransisko zaidi, wakaamua kuanzisha matawi mapya. Wakapuchini kadhaa (wakifuatwa na Wafransiskani pia) wakaanzisha Ndugu Wadogo Wapya huko Italia (1972) na Ndugu Wadogo Wamisionari huko Brazili (1973). Akielewa nia yao njema katika hali ya fujo iliyotanda, Paulo VI (1963-1978) aliwakubalia wabaki na nadhiri zao kuu baada ya kuacha shirika walipoziweka. Wakapuchini wengine wa Italia walianzisha Ndugu wa Mt. Fransisko (1983), na wa Marekani Wafransisko wa Upyaisho (1987). Hatimaye Wakonventuali kadhaa wa Italia na Filipino wakaanzisha Wafransisko wa Imakulata (1990) kwa ruhusa ya pekee ya Yohane Paulo II (1978-2005) iliyowafanya mara moja kuwa shirika la Kipapa. Huko na huko kuna makundi mengine madogo, na akina dada wanaoyafuata kwa kushika vilevile kanuni ya Utawa I. Juhudi za kuyaunganisha zimeshindikana kwa kuwa yana sura tofauti. Kwa jumla mashirika hayo hayakuongezeka sana. Hata hivyo uwepo wake umekuwa changamoto kwa matawi makubwa ambayo yakaanza kujirudi kidogo, baada ya kupungukiwa na wengi wasiokuwa na msimamo pamoja na kutambua matokeo ya majaribio yaliyofanywa; shida ni kwamba kujirekebisha baada ya kulegea sana si rahisi, hasa kama kazi hiyo inahusu idadi kubwa ya watu.

Polepole karama ya mwanzilishi na ya kila tawi ikaja kuzingatiwa tena kwa furaha, badala ya kujali masuala ya miundo tu. Mambo mengi yaliyosahauliwa kwa karne kadhaa yakaja kuonekana muhimu hasa leo, kama vile roho ya kanuni (udugu na udogo) kuliko mtazamo wa kisheria uliotawala matamko ya Mapapa wa zamani; au usawa wa watawa wote bila ya tabaka; au uwajibikaji wa kila mmoja katika uendeshaji wa jumuia, kanda na shirika; au umuhimu wa mikutano, kuanzia ngazi ya nyumba (ambapo ulikuwa umebaki kwa Wakonventuali tu). Wakati huohuo mabishano kati ya matawi yakapungua sana kwa njia ya ushirikiano wa kidugu mkubwa zaidi na zaidi katika ngazi zote. Hatimaye katiba zikaja kuthibitishwa na Kanisa kulingana na toleo la pili la Mkusanyo wa Sheria zake kwa Walatini (1983). Utulivu upande huo umeleta msimamo mkubwa zaidi kwa viongozi na kwa wanashirika jumla: kinadharia njia imeeleweka; sasa kazi ni kuifuata hadi mwisho.

Baada ya Ukomunisti kuanguka (1989) matawi yote yamejitahidi kujiimarisha Ulaya Mashariki walipopata tena nafasi ya kuhubiri na kupokea miito, ambayo huko ni mingi. Mungu anazidi kuongoza historia yetu.

 

1.3.4. UTUME (1762-2005)

 

Kati ya 1762 na 1889 dhuluma zilifyeka idadi ya Wafransisko kwa asilimia 82.1 na kufuta kabisa kanda nyingi (Ufaransa zote 32!) na kuziacha nyingine hoi. Hata hivyo, kanda chache zilistawi, kwa kuwa mawazo ya uhuru kwa wananchi yalikomesha dhuluma za kidini pale zilipokuwepo toka muda mrefu sana, hasa Irelandi na Uingereza. Kwa namna ya pekee mashirika yakaja kustawi Amerika Kaskazini walipohamia watawa wengi.

Baada ya dhuluma hizo kwisha, kadiri Ndugu Wadogo walivyorudi kupenya maisha halisi ya Kanisa na ya jamii, walielewa ni tofauti sana na yalivyokuwa kabla ya dhoruba. Iliwabidi kutumia ubunifu wa Kifransisko kuitikia mahitaji mapya ya watu kwa utendaji usiozimika, ingawa ukatokea mgongano kati ya taratibu za maisha ya kijumuia na madai ya utume huo.

Mahubiri yaliendelea kuwa njia kuu ya utume, sio tu katika wiki za uamsho, maandalizi ya sherehe na mafungo, bali pia kwa njia ya vyombo vya upashanaji habari: baada ya magazeti (la kwanza lilianzishwa na Wakapuchini wa Ufaransa mwaka 1861; kufikia mwaka 1919 yalikuwa 164 tayari, halafu yakazidi tena), Ndugu Wadogo walifanya kazi katika redio na televisheni au kuzimiliki wenyewe. Katika nusu ya kwanza ya karne ya XX utume wa maungamo ulishika nafasi kubwa hata kwa Wakapuchini, ambao toka mwanzo hadi mwaka 1847 walikuwa wakizuiwa na katiba wasifanye kazi hiyo.

Nusu ya pili ya karne ya XIX na nusu ya kwanza ya karne ya XX juhudi za Ndugu Wadogo zilizaa vyama vingi vya kitume. Kati ya vile vilivyoenea zaidi tukumbuke kile cha Mashujaa wa Imakulata (1917) cha Mt. Maximiliani Maria Kolbe, na kile cha Makundi ya Sala cha Mt. Pio wa Pietrelcina. Baadaye Ndugu Wadogo wengi wakaja kupendelea matapo mapya ya kiroho, yaliyoanzishwa na walei, wakajihusisha nayo kuliko walivyojihusisha na shirika lao, hata kusababisha swali: je, kwao ni muhimu zaidi kuwa wanashirika au kufuata tapo fulani?

Utume wa kijamii ulipata sura nyingi kulingana na mahitaji ya watu wadogo: huduma za huruma, mshikamano wa kutumia kiasi (katika kunywa), upatikanaji wa kazi na vitendeakazi, vyuo kwa mabubu-viziwi, benki, utume kwa wazururaji, kwa watu wa kuhamahama, na kwa wahamiaji wa nchi zilizoendelea, huduma hospitalini n.k.

Baada ya vita vikuu vya pili, na hasa mara baada ya Mtaguso, karama maalumu iliposahauliwa ili kujali zaidi upadri wa mtawa, mashirika yalikimbilia utume wa mapadri wanajimbo kwa kupokea parokia nyingi. Kumbe yalipokumbuka tena karama ya kitawa yakaona ugumu wa kupunguza utume wa aina hiyo (kurudisha parokia kwa jimbo lililopungukiwa mapadri). Hivyo, pamoja na uhaba wa miito yakajikuta yanalemewa yasiweze kutua mzigo waliojitwisha.

Upande wa umisionari, katika karne ya XIX ukoloni wa Wazungu, waliokuja kutawala maeneo makubwa duniani kote, ulifungua njia na milango kwa uenezaji wa imani. Kanisa lilichangamkia tena kazi hiyo kuanzia Ufaransa, na kufanya mipango mingi ya ushirikiano na wamisionari, hata kuanzisha miundo ya kimataifa ambayo yakaja kuwekwa moja kwa moja chini ya Papa, na vilevile mashirika mbalimbali ya kimisionari tu. Ndugu Wadogo walipoanza kuinuka baada ya dhoruba wakakuta juhudi hizo zimeshaenea hata zikaja kufikia kilele chake kati ya vita vikuu. Basi matawi yote matatu yakajitosa katika kazi hiyo, tena kwa upana na mpango kuliko zamani. Kufikia mwaka 1934 Wafransiskani walishika nafasi ya kwanza kati ya mashirika yote kwa wingi wa wamisionari (3,600). Pigo kubwa lililowapata ni kufukuzwa wageni wote 550 waliokuwepo China katika majimbo 29 ya kwao (1949). Wakapuchini wamisionari waliokuwa 377 mwaka 1890, wakaongezeka hadi kuwa 1,562 mwaka 1975, wengi wao Afrika, India na Indonesia.

Hivyo kanda za Amerika ya Kilatini zikastawi (ndugu 1,600 wa mwaka 1905 wakawa 4,700 mwaka 1975); zikaanzishwa nyinginyingi Asia, na chache Afrika na Australia. Basi, kama inavyotokea kwa Kanisa lote, asilimia ya Wazungu shirikani inazidi kupungua, kumbe ndugu wa kontinenti nyingine wanaongezeka. Kwa mfano, kati ya Wakapuchini mwaka 1997 asilimia 15 walikuwa Amerika ya Kilatini, 14 Asia-Australia na 10 Afrika.

Takwimu ni kama ifuatavyo:

 

Matawi

Mwaka 1762 hivi

Mwaka 1889 hivi

Mwaka 1964 hivi

Mwaka 2005

   (Waoservanti)

39,900

6,200

 

 

   (Pekupeku)

7,000

900

 

 

   (Wariformati)

19,000

5,700

 

 

   (Warekoleti)

11,000

1,600

 

 

OFM jumla

76,900

14,400

27,100

15,794

Wakonventuali

21,000

1,500

4,800

4,595

Wakapuchini

34,000

7,600

15,800

11,229

Waimakulata

 

 

 

282

Jumla kuu

131,900

23,500

47,700

31,902

 

Upande wa elimu, kulingana na sheria za Kanisa, mipango ya masomo imebadilika, miaka ya falsafa na teolojia kwa ajili ya upadri imeongezeka, mbali ya seminari ndogo kuna vituo vingi wanaposoma pamoja watawa wa mashirika mbalimbali na pengine waseminari wa majimbo, kila tawi limeunda kituo kikuu cha malezi ya juu huko Roma, ambapo kuna vyuo vikuu vya Wakonventuali (Seraphicum) na OFM (Antonianum), na digrii kati ya wanashirika zimeenea.

 

2. UTAWA WA PILI

 

2.1. MCHE MDOGO ULIVYOSTAWI (1212-1517)

 

2.1.1. MWANZO NA UENEZI (1212-1300)

 

Mt. Klara, aliyejiita “mche mdogo wa Mt. Fransisko”, ndiye jiwe la msingi la Utawa II ulioleta karama ileile ya Ndugu Wadogo kwa wanawake na kwa kujifungia faraghani. Ndizo nguzo mbili za utawa huo.

Binti huyo wa ukoo bora alizaliwa Asizi (1193). Kisha kuvutiwa na mifano ya Mt. Fransisko, na kusikiliza mahubiri na mashauri yake, akaamua kujiweka wakfu kwa Kristo katika ufukara mkuu. Basi, akatoroka nyumbani usiku (1212) akamuendea Mt. Fransisko huko Porsyunkula ambapo alinyolewa naye na kuvikwa kanzu, kamba na shela nyeusi. Kesho yake asubuhi akapelekwa kwa masista Wabenedikto, na baada ya wiki mbili kwenye monasteri yao nyingine, alipofikiwa na mdogo wake (Mt. Anyesi) ambaye pia alipaswa kukabili upinzani mkali wa ukoo wao. Mt. Fransisko alipomaliza kuandaa jengo la Mt. Damiano, wakahamia huko kushika maisha ya ndani, wakaongezeka haraka. Miaka 40 baadaye Mt. Klara akaja kuandika kwamba mwanzo ulikuwa mgumu na walidharauliwa sana. Mwaka huohuo (au ule uliofuata) mwanzilishi, alipoona walivyovumilia yote, aliwaandikia kwa ufupi “mtindo wa maisha”. Wakati huo aliwaomba wamsaidie kutambua kama Mungu anataka yeye na Ndugu Wadogo waishi upwekeni tu au wafanye utume pia. Jibu likawa kwamba wakahubiri; lakini Mt. Klara na wenzake watawafuata kiroho tu kwa sala na sadaka, wakichangia urekebisho wa Kanisa bila ya kutoka nje ya kiota chao.

Baada ya Mtaguso IV wa Laterano (1215) kukataza kanuni mpya iliwabidi wapokee mojawapo ya zamani ili wakubaliwe na Kanisa kama watawa. Basi wakaichagua ile ya Mt. Benedikto, wakiifuata katika mambo kadhaa kadiri yalivyopatana na mtindo wao mpya, bila ya nia ya kuwa Wabenedikto. Hapo ilimpasa Mt. Klara kuitwa abesi, jina alilolikubali tu kwa kumtii mwanzilishi, ingawa akaendelea kujiita “mtumishi wa Kristo na wa akina dada fukara”. Hasa Mt. Klara hakutosheka na uhalali wa monasteri yake mbele ya Kanisa, bali kwa njia ya Mt.Fransisko aliomba akapewa na Inosenti III “fadhili ya ufukara” (1216), yaani ruhusa ya kuishi bila ya mali hata kijumuia, kama jambo la msingi katika wito wake wa “kuishi kadiri ya ukamilifu wa Injili takatifu”, kwa kuungana na Kristo fukara kama bibiarusi fukara.

Kardinali Ugolino, akiona monasteri za namna hiyo zinavyoongezeka huko na huko, alizitungia katiba (1219) iliyopitishwa na Honori III (1216-1227) ambayo ikawa msingi wa kanuni zote zilizoandikwa baadaye kwa Utawa II. Lengo lake lilikuwa kukinga monasteri hizo dhidi ya upinzani na kuzipa mtindo wa kimonaki zaidi bila ya kuondoa usahili wake maalumu, ziwe muundo mpya wa aina moja chini ya Kanisa la Roma moja kwa moja. Katika juhudi zake za kurekebisha umonaki alielekeza hata monasteri kadhaa za zamani zifuate mtindo wa Mt. Damiano. Desturi kali alizoziagiza humo hazikumtisha Mt. Klara, ambaye alijishinda tayari na kujitesa kwa ushujaa mkubwa (katika kula, kuvaa, kulala n.k.) mpaka akakatazwa asizidishe. Wala hakuogopa ukali wa ugo ulioagiwa na katiba hiyo, ili kutunza mazingira ya sala. Wasiwasi wake ulihusu ufukara mkuu akiona hautajwi na katiba hiyo. Mwanzoni Ugolino alitaka msimamo huo udumu katika monasteri kadhaa, ila alipochaguliwa kuwa Papa akaanza kuzipatia mali nyinginyingi, labda kisha kung’amua matatizo yaliyojitokeza. Lakini Mt. Klara hakukubali kabisa akamuomba amtibitishie “fadhili ya ufukara” akakubaliwa (1228), lakini si kwa monasteri zote.

Suala lingine lililojitokeza mapema, halafu likaendelea kusababisha migogoro, ni nani awajibike kuwasaidia Waklara upande wa roho na upande wa riziki. Mt. Fransisko alipokuwa Mashariki, nd. Filipo Longo aliteuliwa msimamizi wao, lakini mwanzilishi aliporudi uteuzi huo ukafutwa, masista wakasimamiwa tena na wasio Wafransisko, mpaka Gregori IX alipowalazimisha Ndugu Wadogo kuwajibika (1221).

Mt. Klara alipoona wito wake wa Kiinjili upo hatarini upande wa sheria, kwa kuwa kanuni na katiba hazikuwa za Kifransisko, akaanza kuomba aweze kuahidi kushika kanuni ya Ndugu Wadogo badala ya ile ya Mt. Benedikto. Mwaka 1234 akaja kumuunga mkono Mt. Agnesi wa Praha, binti mfalme ambaye alikataa kuolewa na mfalme mkuu Federiko II wa Ujerumani akaanzisha monasteri yake iliyokubaliwa “fadhili ya ufukara”. Alitunga kanuni mpya kwa kuchanganya “mtindo wa maisha” alioandika Mt. Fransisko na katiba ya Ugolino, akamuomba Gregori IX, halafu Inosenti IV waithibitishe, lakini akakataliwa. Kumbe Inosenti IV akathibitisha katiba ya Ugolino (1245) na kusisitiza ifuatwe kanuni ya Mt. Benedikto kwa sababu ina sifa nyingi. Wakati huohuo alijaribu kusuluhisha mgogoro wa uhusiano kati ya Ndugu Wadogo na Waklara. Mt. Klara alikuwa akiendelea kudai kwa nguvu msaada wa kiroho wa ndugu hao kulingana na ahadi ya mwanzilishi. Kumbe Mtumishi mkuu Kreshensi wa Iesi aliomba shirika liondolewe mzigo liliobebeshwa na Gregori IX, yaani himizo la kuanzisha konventi ndogo karibu na kila monasteri ya Waklara. Basi, Inosenti IV aliamua Waklara wawe chini ya uongozi na mamlaka ya Ndugu Wadogo, akapendekeza masista waunganishwe na Utawa I. Lakini shirika likazidi kuona litalemewa na wingi wa monasteri.

Mwaka 1247 Inosenti IV akatunga katiba mpya badala ya ile ya Ugolino iliyokwishaenea katika monasteri zote za Kifransisko, ikitumika pengine pamoja na desturi maalumu za mahali. Katiba hiyo ilifanya kanuni ya Ndugu Wadogo kuwa msingi wa sheria za Waklara bila ya kuwadai waishike katika yote, ila katika utiifu, utovu wa mali na useja mtakatifu. Katiba hiyo ilimuondolea Kardinali mlinzi mamlaka juu ya Waklara, ambao wakawekwa moja kwa moja chini ya viongozi wa Utawa I. Kwa katiba hiyo Waklara wakaja kutambulikana Wafransisko kisheria, lakini ndani mlikuwa na pigo kubwa kwa Mt. Klara, yaani iliandikwa wazi kuwa monasteri zao zinaruhusiwa kuwa na mali za kujitegemea. Ndiyo sababu monasteri chache tu zikaipokea katiba hiyo. Vilevile Ndugu Wadogo wakazidi kulalamika hadi Kardinali mlinzi akajitwalia polepole mamlaka yao na hatimaye (1250) aliwaandikia wasithubutu kujiingiza katika uongozi wa Waklara. Hivyo kwa muda mfupi katiba hiyo ikashindikana pande zote.

Mt. Klara, mgonjwa toka siku nyingi, alipoona kifo kinamkaribia, aliandika wasia wake ambamo alimuiga Mt. Fransisko katika kukumbusha asili ya wito wake na wa jamaa yake, na kutamka kwa msisitizo mkubwa nia imara ya kufuata ufukara mkuu “aliouahidi kwa Mungu na kwa Mt. Fransisko” pamoja na kuhimiza sana umoja wa dada zake. Lakini pia, upande wa sheria, aliona haja ya kutunga upya “mtindo wa maisha” kwa kulinganisha kanuni ya Ndugu Wadogo na masharti ya maisha ya ndani tu. Humo aliingiza pia maandishi mawili mafupi ya Mt. Fransisko kwao, kuhusu ufukara mkuu na kuhusu ahadi ya kwamba yeye na Ndugu Wadogo watawahudumia Waklara sawa na wenzao wa kiume. Upande wake Mt. Klara aliahidi kuwatii waandamizi wa mwanzilishi. Kiini cha huo “mtindo wa maisha” kinasisitiza kwa nguvu nia ya kuishi bila ya mali yoyote, isipokuwa monasteri na bustani. Jambo lingine linalokazwa ni udugu: humo neno “dada” linapatikana mara 66! Udugu huo unatimizwa siku kwa siku chini ya “abesi na mama” kwa umoja wa mioyo pasipo ubaguzi wowote (tofauti pekee ni kati ya wanaojua na wasiojua kusoma kuhusu Sala ya Kanisa). Hata dada “wa nje” (yaani “wanaohudumia nje ya monasteri” bila ya kubanwa na ugo) washiriki maisha ya jumuia sawa na wenzao. Hao ni kundi maalumu la mtindo wa Kiklara, linalohitajika kadiri wenzao wanavyojifungia ndani: ni “akina Marta” kwa “akina Maria” kadiri Mt. Fransisko alivyowapangia Ndugu Wadogo wanaoishi upwekeni. Udugu huo unajitokeza hata katika mikutano, ambayo inatakiwa kufanyika kila wiki kwa mchango wa wote, kupanga shughuli za maana na kuteua watakaoshika nyadhifa mbalimbali. Abesi mwenyewe, ingawa anachaguliwa kwa maisha yake yote, kadiri ya mapokeo ya kimonaki, anaweza kubadilishwa dada zake wakiona hawezi kutimiza vizuri kazi zake. Uhusiano na Utawa I unasisitizwa tena kwa kudai msimamizi wa monasteri awe daima Ndugu Mdogo, pamoja na kuomba Utawa huo uipatie monasteri mapadri 2 na mabradha 2 kwa huduma za kiroho na za kimwili.

Huo “mtindo wa maisha” ukakubaliwa na Kardinali mlinzi (1252) halafu na Inosenti IV (1253). Mt. Klara akapewa hati yake kitandani akaibusu; siku mbili baadaye akafa akiishika mikononi, wakihudhuria nd. Leo, nd. Angelo na nd. Ginepro wenzi wa Mt. Fransisko; pia alijaliwa faraja za Bikira Maria na wanawake watakatifu kadhaa. Mazishi yalihudhuriwa na Papa, Makardinali, Maaskofu na wengineo. Inosenti IV alitaka ziimbwe sala za watakatifu mabikira badala ya zile za wafu, ila akakubali shauri la Kardinali mlinzi la kufuata taratibu zilizopangwa kabla mtu hajatangazwa mtakatifu. Miaka miwili baadaye, Kardinali huyo akiwa amepewa Upapa kwa jina la Aleksanda IV (1245-1261), akamtangaza rasmi kuwa mtakatifu (1255). Mwaka 1260 masalia yake yakahamishiwa mjini Asizi katika kanisa lililojengwa kwa heshima yake.

Pamoja na kanuni na wasia, Mt. Klara ametuachia walau barua nne (kwa Mt. Agnes wa Praha). Maandishi hayo ndiyo chemchemi ya kwanza ambamo tuchote utajiri wa roho yake na wa utu wake. Hasa ya mwisho inatuonyesha alivyogeuka ndani ya Yesu kwa kuzidi kumkazia macho kama kioo chake na kujifunza toka kwake hasa ufukara, unyenyekevu na upendo wa ajabu, vilivyong’aa katika hatua mbalimbali za maisha yake kuanzia Bethlehemu hadi Kalivari. Mt. Klara alimfikia Mungu kwa kumfuata Yesu kama bibiarusi mwaminifu katika hatua hizo za maisha yake halisi, kama alivyoelekezwa na Mt. Fransisko, kadiri ya karama yake mpya katika kumtazama Yesu na kuelewa Injili.

Katika karne ya XIII monasteri chache ziliipokea kanuni ya Mt. Klara iliyothibitishwa kwa ajili ya nyumba asili tu. Kumbe monasteri kadhaa zikaja kupokea kanuni maalumu ambayo M.H. Izabela (+1270), dada wa Mt. Ludoviko IX mfalme wa Ufaransa, aliiandika akakubaliwa na Aleksanda IV kwa monasteri yake ya Longchamp (1259). Kanuni hiyo iliweka Waklara chini ya Ndugu Wadogo na kukubali mali na mapato ya mara kwa mara.

Mwaka 1263 mkutano mkuu wa Ndugu Wadogo ulizidi kukataa wajibu wa kuwahudumia Waklara. Akiwa Mtumishi mkuu, Mt. Bonaventura alijaribu kusuluhisha kwa kusema huduma za kiroho kwa dada hao zinatokana na upendo, lakini si wajibu ambao waudai kwa haki; pia zitegemee uamuzi wa Kardinali mlinzi. Kumbe mwaka huohuo Urbani IV (1261-1264) alipitisha kanuni mpya ili kustawisha nidhamu na. umoja ikidai monasteri hizo zote ziitwe Utawa wa Mtakatifu Klara (O.S.C.), kama ilivyoelekea kufanyika baada ya kutangazwa mtakatifu. Kanuni mpya ilifuata kidogo ile ya Klara, na zaidi katiba ya Inosenti IV, ikibana sana masista katika vipengele vingi. Zaidi ya hayo ilipanga mali (mashamba na kodi zake) kuwa tegemeo la kawaida la uchumi wa monasteri. Hatimaye iliwaondolea Watumishi wajibu wa kuwahudumia Waklara. Kanuni hiyo ikakataliwa na monasteri bora na baadhi ya Ndugu Wadogo. Hivyo ukatokea mgawanyiko unaodumu hadi leo kati ya Waklara wanaofuata kanuni ya Mt. Klara (inayoitwa ya I) na wale wanaofuata kanuni ya Urbani IV (Waurbani au wa kanuni ya II), na kufanana na Wakonventuali (ambao pia wamekubali kuwa na mali kishirika). Kanuni nyingine zikaachwa kabla ya karne kwisha. Kwanza ilienezwa sana ile ya Urbani, lakini ile ya mt Klara ikabaki huko na huko ikiendelea kuathiri sana historia yote ya Waklara kwa kukumbusha tunu asili na kuchochea marekebisho mengi kuliko yale ya Ndugu Wadogo, kutokana na urahisi wa kubadili hali ya monasteri moja kuliko ya shirika kubwa iliyotawanyika sehemu mbalimbali.

Tofauti hizo hazikuzuia uenezi wa monasteri usiende kasi ajabu, kulingana na uenezi wa Utawa I Ulaya na hata ng’ambo ya Bahari ya Kati. Kila monasteri ilijitegemea kikamilifu; kilichowaunganisha ni hakika ya kutokana na moto ule uliowashwa na Mt. Klara, uhusiano wa kiroho na Ndugu Wadogo na mamlaka ya Kardinali mlinzi. Kwa kawaida monasteri zilikuwa na masista wengi sana. Miito mingi ilitokea kati ya koo maarufu na za kifalme pia, hasa Urbani IV alipodai kila mtakaji alete “mahari” monasterini, sheria ambayo ilienea kote. Karne ya kwanza ilizaa watakatifu 4 (Klara na Agnes wa Asizi, Agnes wa Praha na Kinga wa Hungaria) na wenye heri 6 katika nchi mbalimbali, hasa kutoka koo za kifalme. Halikukosekana taji la ushahidi wa imani na wa ubikira (Waklara wote wa Tripoli mwaka 1289, na wote 70 wa Tolemais mwaka 1291).

Takwimu ni kama ifuatavyo:

 

 

Mwaka 1253

Mwaka 1300

Waklara

 

Zaidi ya 15,000

Monasteri

111

413

   Italia + visiwa

68

196

   Hispania + Ureno

21

57

   Ufaransa

14

68

   Ujerumani + Ulaya Mashariki

8

46

   Mashariki + Korasia

 

23

   Uingereza + Irelandii

 

23

 

2.1.2. ULEGEVU (1300-1400)

 

Karne ya XIV ilileta ulegevu katika Utawa II, kama tulivyoona kwa ule wa kwanza, hasa kutokana na wingi wa masista na wa mali. Walipokewa kwa urahisi wanawake wasiofaa lakini wenye kuleta mahari kubwa, ambao waliingiza monasteri watumishi wao binafsi, hata kuleta anasa, pengine kwa idhini ya Papa. Uovu ulizidi wakati wa farakano la Magharibi na fujo iliyofuata. Hata hivyo si monasteri zote zilipatwa kwa pamoja, kutokana na kila moja kujitegemea. Hazikukosekana pia juhudi za kurudisha nidhamu zilizofanywa na wasimamizi wa Utawa I – ambao Bonifas VIII (1295-1303) aliurudishia wajibu wa kuwahudumia Waklara (1296) – na Makardinali walinzi na Mapapa wenyewe. Kati yao ni muhimu hasa Benedikto XII (1334-1342), aliyekuwa mmonaki wa Citeaux, ambaye aliwapa Ndugu Wadogo katiba (1336) ambayo sura yake mojawapo inahusu Waklara tu. Katiba yake ilibadili sura ya monasteri. Kwanza ilipanga idadi ya juu ya masista katika kila monasteri; pili ilisisitiza ugo wa Kipapa, taratibu za pamoja kwa wote, usimamizi mzuri wa mali, katazo la pesa za binafsi na la dhuluma dhidi ya monasteri; tatu alilazimisha hata dada waliohudumia nje ya ugo wabaki ndani na hivyo wakaja kuwa tabaka la chini masista, wakiwatumikia wenzao bila ya kuwa na sauti mikutanoni (ilikuwa hivyo kwa Wabenedikto, lakini ni kinyume cha udugu alioutaka Mt. Klara); nne kwa huduma hizo za nje waliruhusiwa wanawake wasekulari wa kufaa; tano vilikatazwa vyumba vya binafsi.

Jambo lingine lililokuja kubadilishwa ni muda wa uongozi wa abesi, kwa kuzingatia kwamba urefu wake unaweza ukafaa wakati wa juhudi, lakini unaweza ukasababisha uharibifu wa kudumu ulegevu ukiingia. Mtindo wa maisha wa Mt. Klara hausemi abesi adumu muda gani, ila unafuata kanuni ya Mt. Fransisko ukisema asipofaa tena aondolewe, halafu achaguliwe mwingine. Lakini utekelezaji wake haukuwa rahisi. Hivyo Inosenti VII (1404-1406) aliagiza (1405) abesi achaguliwe kila baada ya miaka 10; baadaye muda ukapunguzwa tena hadi miaka 3. Lakini sheria hizo hazikufuatwa popote, hivyo baadhi ya monasteri zikaendelea kumchagua abesi hadi atakapokufa.

Pamoja na juhudi hizo na nyingine za kurekebisha hali, historia ya watawa inaonyesha kwamba nidhamu ya kuzalimishwa inaweza ikasidia kiasi, lakini haiwezi kuleta hali mpya, kwa kuwa uhai unatoka ndani ya watawa wenyewe kwa kazi ya Roho Mtakatifu. Si suala la miundo, bali la roho. Hata katika ulegevu wa karne ya XIV mtindo wa maisha wa Mt. Klara ulivutia: kwa mfano malkia Sancha wa Napoli (+1345), alipojifanya Mklara hakukubali kuingia monasteri ya fahari ya Mt. Klara mjini, bali alianzisha nyingine ndogo fukara kwa kuita wamonaki toka Asizi na kushika kanuni ya I. Huko na huko Ufaransa ilitokea vilevile. Katika karne hiyo walipatikana wenye heri 3.

Takwimu ni kama ifuatavyo:

 

 

Mwaka 1300

Mwaka 1385

Waklara

Zaidi ya 15,000

Zaidi ya 15,000

Monasteri

413

404

   Italia + visiwa

196

245

   Hispania + Ureno

57

51

   Ufaransa

68

39

   Ujerumani + Ulaya Mashariki

46

50

   Mashariki + Korasia

23

11

   Uingereza + Irelandii

23

8

 

2.1.3. MAREKEBISHO KUANZA (1400-1517)

 

Karne ya XV hadi ya XVIII ziliona monasteri za Waklara kuhuishwa tena, kufuatana na marekebisho ya Ndugu Wadogo (kama ilivyotokea kwa wanawake wa mashirika mengine), halafu na Mtaguso wa Trento na maagizo ya Mapapa, lakini pia kutokana na karama yenyewe ya Mt. Klara iliyojitokeza wazi katika kanuni yake. Toka mwanzo utawa wake haukuwa tu muundo mpya wa kimonaki, bali mfumo mpya wa maisha ya Kiinjili, ambao unadai kufuatwa, la sivyo monasteri hazitatulia, kama vile Ndugu Wadogo.

Mwanzoni mwa karne ya XV ulitokea urekebisho mkubwa kwa njia ya Mt. Koleta Boylet (+1447) wa Corbie (Ufaransa). Baada ya kujifungia ndani amevaa mavazi ya Wafransisko Wasekulari, alitokewa mara kadhaa na Mt. Fransisko na kuhimizwa arekebishe utawa wake. Basi, akatoka (1406) akaenda kwa Papa wa Avignon (bila ya kutambua kwamba ni wa bandia) akaweka mikononi mwake nadhiri ya kushika mtindo wa maisha wa Mt. Klara, akafanywa naye abesi na mrekebishaji wa utawa wote wa Mt.Fransisko (I-II-III), kutokana na karama yake wazi ya kurekebisha Kanisa kuanzia monasteri na miundo mingine ya Kifransisko. Kwa neema ya Mungu na kwa msaada wa wakuu wa dunia akaanza kutembelea Ufaransa na Benelux ili kueneza chachu ya Kiinjili, hasa ufukara. Upande wa Waklara alirekebisha au kuanzisha monasteri 22 kufuatana na kanuni ya I aliyoomba nakala yake halisi kwa monasteri mama ya Asizi. Mwenyewe aliiongezea katiba iliyopitishwa na Mtumishi mkuu (1432) halafu ikathibitishwa na Pius II (1458-1464). Humo alikataza mahari za masista, mali yoyote na mapato ya hakika kwa monasteri, kodi na ghala za kutosha muda mrefu, kila kitu cha thamani au kisicho cha lazima, majengo yasiyo duni. Aliagiza wote wafanye kazi ili kupata riziki, bila ya kuagiza watu wa nje kwa kazi wanazoweza kuzifanya wenyewe. Kwa udogo, alikataza baraka kuu kwa abesi na ibada ya kuweka wakfu mabikira. Hata hivyo alisisitiza usafi na masomo na kupunguza masharti ya ugo. Kwa ajili ya upendo wa kidugu alifuta matabaka, aliagiza vipindi vya burudani (maongezi), alisisitiza mikutano ya kila wiki, alionyesha tena kuwa wadhifa wowote ni utumishi tu. Ingawa alikubali vipengele kadhaa vya kanuni ya Urbani IV vilivyopata kuwa vya kawaida, kwa jumla alirudia vizuri karama ya Mt. Klara. Kama yeye alitaka mafungamano imara na Utawa I, monasteri zote zikiwa chini ya Ndugu Wadogo, na wanne kati yao wakiwa tayari kuihudumia kila mojawapo. Kwa sababu hiyo, kama tulivyokwishaona, watawa kadhaa wa kiume waliingia katika juhudi zake za urekebisho (Ndugu Wadogo Wakoleta).

Waoservanti mwanzoni walikataa kuwahudumia Waklara, lakini polepole wakalazimishwa na Kanisa kwa ombi la monasteri zilizorekebishwa. Hapo urekebisho wa kina ukapamba kwa juhudi za wamonaki bora, kama Mt. Katerina wa Bologna (+1463), M.H. Antonia wa Firenze (+1472), Mt. Eustokia Calafato (+1485) na M.H. Batista Varano (+1524) huko Italia, na wengineo Ufaransa na Hispania. Wote walishikilia kanuni ya I sio tu kwa Waurbani, bali pia kwa monasteri nyingi za Utawa III na hata nyingine zisizokuwa za Kifransisko! Si zote zilikubali kwa ridhaa yao urekebisho. Kumbe Waoservanti walijaribu kuueneza kote, hata kwa mabavu, mpaka walifikia hatua ya kutumia nguvu za kijeshi kupitia serikali! Kati ya wote aliyejitahidi zaidi ni Mt.Yohane wa Capestrano, ambaye alitaka pia kuunganisha monasteri zote chini ya Waoservanti, lakini akashindana na msimamo wa mt Koleta aliyetaka kubaki chini ya Mtumishi mkuu na kudumisha uhusiano na Wakonventuali. Mt.Yohane akaandika (1445) ufafanuzi wa kanuni ya Mt. Klara akiorodhesha amri mia na zaidi, jambo lililowashangaza sana Waklara, hata mwaka uliofuata ulitolewa ufafanuzi mwingine juu ya maana ya amri hizo, halafu Eugeni IV (1431-1447) akatamka kwamba chache tu zinawabana masista kiasi cha kutenda dhambi wakizivunja (1447). Mwenyewe aliweka chini ya Waoservanti monasteri zote zilizorekebishwa, hata zikifuata kanuni ya II, akiziacha nyingine chini ya Mtumishi mkuu. Kwa maana sera ya Kanisa haikuwa kulazimisha monasteri kufuata kanuni ya I, ila kuzirekebisha kwa kufuata sawasawa sheria za kila mojawapo; pengine waliokataa urekebisho iliwabidi wahame. Mwishoni mwa karne ya XV Waklara wa urekebisho wakawa wengi kuliko wasiorekebishwa. Sehemu nyingine monasteri za hawa wa mwisho zilikuwa na hali mbaya kweli. Hatimaye baadhi ya zile zilizokataa urekebisho zilibadili kanuni na kufuata ile ya Mt.Benedikto. Jambo lingine lisilopendeza lilikuwa kuona Waoservanti na Wakonventuali wakishindania monasteri za dada zao.

Kati ya marekebisho hayo, Wakoleta wamedumisha hadi leo umoja fulani kati ya baadhi ya monasteri zao. Vilevile Waklara Pekupeku walioanzishwa na Marina wa Villaseca (Hispania) aliyeruhusiwa (1490) kurekebisha monasteri yake ya Utawa III kwa kufuata kikamilifu kanuni ya I, na kupokea Waurbani wasirudie unovisi. Makundi mengine yamepoteza umaalumu wao: kwa mfano Dada Fukara Waklareno ambao Sisto IV aliwaweka (1473) chini ya Mtumishi mkuu kumpitia makamu wake Mklareno.

Inosenti VIII (1484-1492) alimruhusu (1489) mt Beatriche wa Silva Meneses (+1490) aunde monasteri ya Kibenedikto aina ya Citeaux kwa heshima ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi Asili (Imaculata Concepcion). Baada ya mwanzilishi kufariki, Aleksanda VI akawaruhusu hao masista Wakonsesioni wafuate kanuni ya Mt.Klara na kuunda monasteri nyingine, halafu Julius II (1503-1513) akawapatia kanuni mpya (1511) ambayo inafanana nayo, lakini inaruhusu mali ya monasteri na kulegeza mfungo. Hata hivyo wakaachwa chini ya Ndugu Wadogo wakapewa fadhili zote za Waklara (1520). Ndiyo sababu wanaorodheshwa pamoja na Utawa II. Hao wakastawi sana Ulaya na Amerika hadi leo.

Tofauti zaidi ni Utawa wa Bikira Maria (Waanunsyata) ulioanzishwa na malkia Mt. Yoana wa Valois (+1505) kwa heshima ya Maria Mpashwa Habari. Tawi hilo halifuati kanuni ya Kifransisko, lakini toka mwanzo liko chini ya Waoservanti na linashiriki fadhili za Waklara: ndiyo sababu linaorodheshwa pamoja nao.

Katika kipindi hicho ni vigumu sana kutoa takwimu za idadi ya masista. Kati yao, mbali ya watakatifu 5 waliotajwa, walipatikana wenye heri 7.

 

 

2.2. MAREKEBISHO KUENDELEA (1517-1762)

 

Baada ya utengano wa Ndugu Wadogo (1517) monasteri zilizo nyingi ziliwekwa chini ya Waoservanti, hata zile za Wakoleta (nyingine tena zikaongezwa baadaye, k.mf. zile zote za Hispania na Ureno mwaka 1566). Kama kawaida mzigo huo ulilalamikiwa na mkutano mkuu (1532); hivyo ikakatazwa monasteri nyingine zisipokewe chini ya OFM pasipo ruhusa ya mkutano, na hasa wahusika washughulikie mahitaji ya kiroho tu ya Waklara. Baada ya Mtaguso wa Trento kutoa maagizo kuhusu watawa wanawake (1563) yaliyochangia marekebisho ya sheria na hasa juhudi kwa maisha magumu, mkutano mkuu wa OFM ulitunga sheria muhimu kwa utekelezaji wake ukifuta wadhifa wa ndugu msimamizi wa Waklara na kuwaweka moja kwa moja chini ya Watumishi wa kanda (1565). Lakini Waoservanti walipojaribu kusawazisha mno, kwa kudai monasteri zote ziwe na mali (ilivyoruhusiwa na Mtaguso) wakapatwa na matatizo makubwa, hasa kwa sababu Wakoleta hawakukubali kuacha ufukara mkuu, na kuja kulingana na Waurbani wenye kutegemea mali zao.

Urekebisho wa Ndugu Wadogo Wakapuchini ulisababisha mapema tawi jipya la Waklara linalodumu hadi leo. Mwanzilishi ni Maria Lorenza Llonc (+1542) mjane Mhispania aliyeishi Napoli (Italia) na kuhudumia wagonjwa pamoja na jumuia ya wanawake Wafransisko wasekulari aliyoianzisha. Wakapuchini walipohamia hospitali yake (1529), akawakabidhi uongozi wa jumuia hiyo. Kati ya 1533 na 1538 wakaongozwa na Mt. Gaetano wa Thiene aliyewaelekeza kwenye maisha ya sala tu na kuwatafutia idhini ya kuishi kimonaki kwa kufuata kanuni ya Mt. Klara (1535). Baadaye akawakabidhi tena Wakapuchini, kwa kuwa karama yao iliathiri sana monasteri hiyo na roho yake, na ndivyo alivyotaka mwanzilishi. Paulo III (1534-1549) akathibitisha hayo na nia yao ya kushika kikamilifu kanuni (1538). Kwa ajili hiyo mwanzilishi aliikamilisha katiba ya Mt. Koleta kwa kutumia ile ya Wakapuchini. Sifa ya monasteri ikaenea haraka na kusababisha kabla ya 1600 zianzishwe 17 nyingine Italia (Mt. Karolo Boromeo aliunda tatu katika jimbo lake). Ila Wakapuchini wanaume wakakataa katakata kuzisimamia, isipokuwa mbili. Hata hivyo dada zao wakaendelea kuomba msaada huo kwa kuwapitia Maaskofu na wafalme, mpaka Mapapa wakalazimisha hao wanaume kuhudumia walau kiroho monasteri fulanifulani. Hata nje ya Italia wakaenea haraka: Hispania (1588), Ufaransa (1603), Ureno(1625), Mexico(1665) ambayo ikawa nchi walipoongezeka zaidi hadi leo, Peruu (1713), Gwatemala (1725), Chile (1727) n.k.

Hata marekebisho mengine ya Utawa I yalijaribu bure kukataa huduma kwa Waklara, hasa Wariformati waliojitahidi sana ili Mapapa wawaweke wote chini ya Maaskofu. Hatimaye wakalazimika kuwahudumia Waklara. Masista wa Utawa II na III waliokuwa chini ya Warekoleti wakaja kutumia jina hilo pia.

Marekebisho mengine ya Waklara yalifanyika katika karne ya XVII, hasa Italia. Kati yake ule wa Wakaapweke wa Mt. Petro wa Alkantara, ulioanzishwa na Kardinali Mkapuchini na kuthibitishwa na Klementi X (1670-1676), ndio tawi gumu kuliko yote yaliyowahi kuwepo. Masista hao waliishi kila mmoja peke yake kama Wakartusi na kujitahidi kumuiga Mt. Petro wa Alkantara katika yote, lakini hawakuenea sana.

Katika karne ya XVII na XVIII hata Waurbani wakapata marekebisho yao hasa upande wa ufukara, Ufaransa na Italia.

Waklara waliorekebishwa walitoa mifano bora ya kutetea imani na ubikira wakati wa uenezi wa Kiprotestanti na vita vya dini vilivyofuata. Upungufu uliosababishwa na mambo hayo Ulaya Kaskazini ulifidiwa kabisa sio tu katika nchi zilizobaki kuwa za Kikatoliki, bali hata Amerika na Asia. Wakonsesioni walifika Mexico mwaka 1540. Waklara wakafungua monasteri yao ya kwanza ya Amerika huko Hispaniola mwaka 1551. Monasteri nyingine zikaanzishwa karne hiyohiyo Peruu, Ekwado, Kolombia, Chile, Gwatemala na Brazili. Katika karne ya XVII Waklara wakaenea Filipino (1621) na China (1633). Katika karne ya XVIII ongezeko liliendelea ingawa kasi yake ilipungua. Takwimu ni kama ifuatavyo:

 

 

Mwaka 1587

Mwaka 1680

Waklara tu

28,000

38,000

Monasteri zao

618

973

   Hispania + Ureno

277

394

   Italia + visiwa

199

248

   Ufaransa

91

182

   Ulaya ya Kati

46

128

   Amerika

5

21

Monasteri za Wakonsesioni

76

90

Monasteri za Waanunsyata

9

40

 

Kati yao wote anang’aa hasa Mt. Veronika Giuliani (+1727) aliyejaa karama na njozi tangu utotoni, alivyosimulia kwa utiifu na unyofu katika shajara yenye kurasa 22,000. Wako pia wenye heri 4.

 

 

2.3. KARNE ZA MWISHO (1762-2005)

 

Kama ilivyowatokea Ndugu Wadogo, Waklara pia walishambuliwa na siasa mpya za serikali, kuanzia Austria na nchi zote zilizokuwa chini yake (1782-1783), monasteri zote zilipofutwa. Uamuzi huohuo ulichukuliwa Ufaransa (1792); miaka 2 baadaye M.H. Yosefina Leroux akauawa kwa kosa la kuanza tena kuishi kijumuia), halafu Ubelgiji, Italia, Ujerumani na Hispania. Katika nchi hiyo ya mwisho monasteri nyingi zikaendelea hata baada ya sheria nyingine kudai zifutwe; pengine ilitumika mbinu ya kukubali kutoa huduma fulani (k.mf. shule) Lakini katika nchi nyingine monasteri nyingi zikaisha, hasa Ureno ambapo zilikwisha zote kufuatana na sheria ya mwaka 1834.

Tangu miaka ya kwanza ya karne ya XIX monasteri zikaundwa tena Ufaransa na Ubelgiji, pamoja na kuanzishwa mashirika mengi ya Kifransisko. Mojawapo ni tunda la Maria Klara Bouillevaux (+1871) aliyelianzisha Paris (1854), likifuata kanuni ya Utawa Hasa III na katiba maalumu, yenye jambo la pekee la kuabudu ekaristi saa zote. Mwaka 1912 monasteri zake zote zikapokea kanuni ya Urbani IV na kujiita Waklara Fukara wa Kuabudu Mfululizo, halafu Wafransisko wa Sakramenti Kuu. Walienea sana na kudumisha uhusiano na Wakapuchini. Hata katika nchi nyingine monasteri mpya ziliundwa na nyingine zilifunguliwa tena. Baadhi ziligeuka kuwa mashirika ya kitume, bila ya kuacha kanuni ya Kiklara.

Katika karne ya XX uenezi ukaendelea hasa katika nchi za Amerika na za misheni. Baada ya Mkusanyo wa Sheria za Kanisa idara ya Papa kwa Watawa iliagiza itungwe katiba moja kwa Waklara wote, isipokuwa Wakapuchini. Kazi hiyo ilifanywa polepole na OFM kwa kupokea mapendekezo ya maabesi pia, ikapitishwa (1930), lakini si kwa Wakoleta. Kwa Waklara Wakapuchini katiba ilitungwa na wenzao wa kiume na kupitishwa mapema zaidi (1927). Waurbani pia wakaja kukubaliwa katiba maalumu (1973). Juhudi hizo za kuimarisha umoja zilichangiwa sana na Pius XII (1939-1958) alipohimiza mashirikisho ya monasteri pamoja na kulegeza masharti ya ugo (1950) kwa lengo la kuziondoa katika hali ya ukiwa, kuzisaidia upande wa malezi na kuruhusu pengine uhamisho. Kazi hiyo ilianza Ufaransa (1953) na kuendelezwa na Mtaguso II wa Vatikani hivi kwamba mwaka 1975 kulikuwa na mashirikisho 43 (1 chini ya Wakonventuali, 7 ya Wakapuchini na 35 ya OFM). Ni mafanikio makubwa tukizingatia ugumu wa kushinda desturi za siku nyingi na tofauti za kila aina. Uhusiano kati ya monasteri na kati ya hizo na Wafransisko wengine umeongezeka na kuinua ujuzi wa kidini na wa hali na mahitaji ya Kanisa na ya ulimwengu. Mtaguso uliagiza pia matabaka kati ya masista yafutwe; hivyo Waklara wakarudia mpango wa mwanzilishi kuhusu udugu, pamoja na kuzidi kuchimba karama yake kwa jumla. Katika uchangamfu huo mpya monasteri nyingi zikapokea kanuni ya I badala ya ile ya II. Hivyo mnamo mwaka 1975 kati ya monasteri za Waklara, 660 hivi zilikuwa zinafuata kanuni ya I na 150 hivi ile ya II. Hata sinodi ya Maaskofu kuhusu watawa (1994) ikajadili sana masuala ya wamonaki na kuhimiza tena mashirikisho yaimarishwe na ugo urekebishwe hasa kwa faida ya malezi.

Baada ya ongezeko la nusu ya kwanza ya karne ya XX, uhaba wa miito Ulaya umerudisha nyuma ustawi wa monasteri nyingi. Takwimu ya uenezi ni kama ifuatavyo:

 

 

Mwaka 1907

Mwaka 1980

Mwaka 2005

Waklara tu

11,000

17,000

12,593

Monasteri zao

561

824

930

   Hispania + Ureno

185

289

 

   Italia

157

144

 

   Amerika

40

172

 

   Ulaya ya Kati

53

78

 

   Asia + Afrika + Australia

 

60

 

   Ufaransa

43

52

 

Monasteri za Wakonsesioni

88

153

157

Monasteri za Waanunsyata

6

4

8

 

Kuhusu matawi, mwaka 2005 takwimu zilikuwa hivi:

 

 

Watawa

Monasteri

Waklara wa kawaida

7,662

569

Waklara Wakoleta

681

57

Waklara Waurbani

1,122

86

Waklara Wakapuchini

2,246

162

Wakapuchini wa Sakramenti Kuu

295

22

Waklara wa Kuabudu Mfululizo

587

34

Jumla ya Waklara

12,593

930

Wakonsesioni

2,019

157

Waanunsyata

96

8

 

Waklara wafiadini wengine 6 wa karne ya XX, hasa Wahispania, wameshatangazwa wenye heri. Mklara maarufu zaidi wa milenia mpya ni sr. Maria Anjelika wa Kupashwa Habari ambaye, karibu na monasteri yake ya kuabudu ekaristi mfululizo, ameanzisha (1981) mtandao wa Kikatoliki mkubwa kuliko yote ya Amerika (EWTN)!

 

 

 

 

3. UTAWA WA TATU

 

 

3.1. ASILI NA USTAWI WA UTAWA WA TOBA (1209-1517)

 

3.1.1. MTAKATIFU FRANSISKO KATIKA TAPO LA TOBA (hadi mwaka 1226)

 

Tangu mwanzo Kanisa liliona kufanya dhambi na toba si jambo la binafsi tu, bali linaathiri wengine pia. Ndiyo sababu liliwadai waamini malipizi ili kuwapa msamaha wa Mungu, na waliopaswa kuyafanya waliandikishwa katika orodha rasmi ya Watubu (Ordo Poenitentium). Kitubio cha siri kiliposhika nafasi ya utaratibu huo, wengi walijiamulia kufanya malipizi ya hadhara hata kwa dhambi za wengine wakajulikana kama Watubu. Toba ni neno la msingi katika historia ya Kanisa. Maana yake asili ni kujitoa kabisa kwa Mungu na kuishi kadiri ya Injili, lakini Wakristo wa karne za kati waliona inadai sana huzuni na fidia kwa dhambi za binafsi na za ulimwengu. Mtubu, akiwa peke yake au pamoja na wengine, alitarajiwa kuacha kazi zilizotazamwa ni kinyume cha Injili (k.mf. biashara na uaskari), kujitenga na jamii ili kufungamana zaidi na Mungu kwa maisha ya sala na tafakuri, kuhiji, kufunga, kujinyima, kutoa sadaka na kujitesa kwa wokovu wake na wa wote. Wengi kati yao walikuwa wanawake, hasa wa koo bora, kama mama wa Mt. Klara.

Tapo la toba liliwahusu walei, ambao baadhi yao wakawa baadaye watawa na hata makleri, tunavyoona kati ya Wahumiliati waliostawi kidogo tu kabla ya Mt. Fransisko. Wakati huo walei walihesabiwa kama ngazi ya chini (ya tatu) baada ya makleri na watawa. Uenezi wa Watubu ukasababisha wapewe na sheria hadhi ya pekee, kwa kuwahesabu kama kundi maalumu kati ya walei na watawa, na kuwapa haki na fadhili kadhaa za watawa. Watubu walikuwa walei, lakini wa pekee kutokana na azimio lao (propositum) lililowadai zaidi katika mengi. Kwanza walikuwa wanashika usafi kamili, lakini kuanzia karne ya XII baadhi yao wenye ndoa waliahidi tu kujinyima ndoa ya pili (wakifiwa) na hata tendo la ndoa siku za kufunga chakula na za kupokea sakramenti.

Mambo ya namna hiyo yanasomwa katika maisha ya Mt. Fransisko, kwa jinsi alivyoathiriwa na roho hiyo. Ndiyo sababu alipozungumzia maisha yake mapya alitumia neno “toba”, na jina asili la kundi lake lilikuwa “Watubu wa Asizi”. Baadaye ukubwa wa karama yake ulimfanya ajitokeze kama kiongozi wa tapo hilo, kwa kuwa namna yake ya kuelewa Injili iliathiri Watubu wengi walioanza kumfuata. Nd. Thoma wa Celano aliandika (1229) kwamba, “kwa uvuvio wa Mungu, watu wengi, maarufu kwa wadogo, makleri kwa walei, walimkaribia mtakatifu Fransisko wakijitolea kuishi chini ya uongozi wake na ualimu wake. Hao wote aliwashirikisha maji tele ya neema za mbinguni ambayo yalibubujika toka rohoni mwake na kustawisha maua ya maadili katika shamba la mioyo yao. Wanaume kwa wanawake walifuata mifano yake, kanuni yake na mafundisho yake; hivyo tunapaswa kumtangaza kwa haki mtendaji asiye na kifani wa hali mpya ya Kanisa na wa ushindi wa majeshi matatu ya wateule. Aliwapa wote mwongozo wa maisha na kadiri ya hali ya kila mmoja alielekeza kwa unyofu njia ya wokovu”. Hayo yalianza kutokea muda mfupi baada ya kukubaliwa na Inosenti III, alipohubiri huko na huko (1211).

Kesi ya pekee ni ile ya kijiji cha Greccio, aliposhangaa kuona kilivyojaa Watubu wengi kuliko wale wa miji mikubwa. “Mara nyingi, ndugu walipoimba Masifu ya Jioni, kama walivyofanya sehemu nyingine nyingi, watu wa kijiji hicho, wakubwa kwa wadogo, walitoka nje ya nyumba zao na kusimama barabarani na kuwaitikia ndugu kwa sauti kubwa, Asifiwe Bwana Mungu wetu!” (Simulizi la Perugia).

Tangu zamani baadhi ya walei walikusanyika kuishi kando ya monasteri ili kufaidika nazo kiroho na kiuchumi. Baadhi yao waliweza kujifunga kwa namna mbalimbali waishi kwa useja, au kwa uadilifu, au kwa utiifu au kwa kufuata kanuni maalumu. Ikawa vilevile kwa Wakanoni, aina mpya za watawa. Mageuzi ya jamii yalipozidi kuvuta watu mijini ili wafanye kazi tofauti na kilimo, walei wengi waliona mashirika ya Ombaomba yanalingana zaidi na mahitaji yao ya kiroho, wakayafuata kama Watubu. Bila ya kuacha kazi zao mpya wala ndoa wakaanza kuvaa nguo ya kitawa ya shirika husika (walau joho), nyeusi kwa Wadominiko, ya kijivu kwa Wafransisko. Hata kabla Mt. Fransisko hajafa, walikuwepo Watubu, hasa wanawake, walioamua kuishi pamoja ili kushika vizuri zaidi azimio lao; k.mf. mwaka 1213 kulikuwa na jumuia ya kike huko Padua.

Mt. Fransisko, akiwajibika kwa watu hao, aliwaandikia aina ya kanuni katika Barua kwa Waamini (1215), alimojumlisha mahubiri yake kwa waliotamani kushika toba nyumbani kwao. Katika toleo la pili la barua hiyo (1221) akaongeza mawaidha na miongozo akitanguliza dibaji iliyo nzito kiteolojia na kiroho.

Chini ya Inosenti III, na zaidi chini ya Honori III, hasa kwa juhudi za Kardinali Ugolino, Kanisa lilikusudia kulipa tapo la toba umoja na muundo fulani, pamoja na kulikinga dhidi ya uzushi. Hivyo lilitunga kanuni maalumu (1221) kwa kuchota mengi katika Azimio la Wahumiliati lililokubaliwa mwaka 1201. Kanuni hiyo mpya iliitwa Kumbukumbu ya Azimio (Memoriale Propositi) ikarekebishwa 1228. Hiyo ni sheria hasa yenye namba 39. Ya kwanza inahusu uduni wa mavazi; halafu kuna katazo la kuhudhuria karamu, tamasha na michezo; agizo la kufunga chakula mara moja au mbili kwa wiki; la kusali Masifu kama makleri au Baba Yetu kadhaa; la kupokea ekaristi Noeli, Pasaka na Pentekoste; la kulipa zaka; la kutotumia silaha na kutokula kiapo kwa kawaida; la kufanya familia nzima iishi Kikristo; la kukutana mara moja kwa mwezi kwa Misa, mafundisho na mchango kwa ndugu na wengineo wenye shida; la mtumishi kutembelea ndugu wagonjwa kila wiki; la kushiriki mazishi ya ndugu na kuwaombea; la kuandika wasia mapema ili kuzuia ugomvi; la kupatana kidugu; la kuungama kila mwezi. Kati ya masharti ya kumpokea ndugu mpya, lipo la kutokuwa na madeni, uadui na uzushi; pia mwanamke awe na ruhusa ya mume. Baada ya mwaka wa jaribio, anayefaa aweke ahadi kwa maisha yote asiweze kuacha jamaa tena isipokuwa kwa kuingia shirikani. Pia kuna taratibu za kusamehe na za kufukuza ndugu. Hatimaye kuna maelezo ya kuwa kuvunja kanuni si dhambi, ingawa kunastahili adhabu. Kwa jumla hakuna mambo ya pekee ya Kifransisko.

 

3.1.2. UENEZI (1227-1300)

 

Ugolino, kisha kuchaguliwa awe Papa Gregori IX, aliwaandikia Maaskofu wa Italia (1227) juu ya aina mbili za Watubu: wale wa kawaida walioishi nyumbani kwao, na wale walioishi upwekeni kwa mfano wa watawa halisi: ndio msingi wa tofauti kati ya OFS na TOR iliyoratibiwa baadaye. Mwenyewe aliandika pia (1238) kwamba Mt. Fransisko alianzisha aina tatu za utawa: “ule wa Ndugu Wadogo, ule wa Akina Dada wa Ugo na ule wa Watubu”.

Jambo linalodhihirisha umuhimu wa Ufransisko ni uenezi wa aina hiyo ya tatu katika Ulaya ya karne ya XIII, unaothibitishwa na hati nyingi zilizotolewa na Mapapa ili kuitetea. Ingawa hatuwezi kujua idadi yao, walienea haraka nje ya Italia, hasa Ujerumani, Ufaransa, Uswisi, Ubelgiji, Uholanzi na Hispania. Kwa njia hiyo ujumbe wa Injili wa upendo na amani ulipenya maisha ya familia, kazi na mazingira yote ya kila siku, ukiunganisha watawala na raia, wakubwa na wadogo, wasomi na mafundi wa kila aina. Hao Ndugu wa Toba walijisikia viungo si vya chama cha kitume kama vingine vingi, bali vya utawa wa kimataifa, wenye sura na haki za pekee. Kilichowapa nguvu ni fadhili walizopewa na Mapapa: zile zilizotolewa zamani kwa Watubu wote ziliongezewa kwa Wafransisko wa sehemu mbalimbali. Muhimu hasa ni ile ya kutopaswa kuapa uaminifu kwa mtawala, uliodai mtu awe tayari kwenda vitani; halafu ile ya kutopaswa kushika serikalini wadhifa usiolingana na hali ya kitawa; tena ile ya kutumia mali yao bila ya kuingiliwa (hasa kwa lengo la kumudu hospitali na huduma nyingine); hatimaye ile ya kutoweza kuhukumiwa na mahakama ya serikali, ila na ile ya Kanisa tu. Mt. Selestini V alifikia hatua ya kuwapa Watubu wa L’Aquila fadhili ya kutolipa kodi! Bila ya shaka viongozi wa nchi walipinga vikali fadhili hizo zilizodhoofisha mamlaka yao, wakasumbua sana jamaa za toba. Kwa Kanisa ilikuwa njia ya kupunguza nguvu za mfalme mkuu wa Ujerumani dhidi ya Papa, lakini ilisaidia pia kupunguza vita vya wenyewe kwa wenyewe huko Italia.

Ndugu wa Toba walikuwa chini ya mamlaka ya Askofu wa jimbo, aliyetakiwa kusimamia maendeleo yao na kuwatetea mbele ya serikali. Lakini Maaskofu pia walipinga vikali fadhili nyingine muhimu, yaani ile ya kutobanwa na katazo la kushiriki ibada likitolewa na Askofu dhidi ya Wakristo wa eneo fulani.

Upinzani huo wote, ukijumlishwa na ule uliowapata Ndugu Wadogo, unaeleza kwa nini hao walisimamisha mara kadhaa huduma kwa Watubu (k.mf. 1232-1247, halafu 1257-1284). Sababu nyingine ilikuwa kutotaka kulemewa nazo. Hasa nd. Elia na Mt. Bonaventura walizikataa katakata. Hivyo kwa kiasi kikubwa Watubu walijiongoza na kujieneza. Mkutano wa jamaa, chini ya mkaguzi toka nje, ulikuwa na mamlaka ya juu katika kuamua, kuchagua, kufukuza. Polepole jamaa zikafungamana. Zamani za Mt. Bonaventura zilikuwa zimeshaunda kanda zikiongozwa na Mtumishi wa kanda; zilikuwa na mikutano mikuu pia zilizokusanya wajumbe wa kanda nyingi, kabla ya mwisho wa karne ya XIII.

Pamoja na hayo, jumuia za Watubu walioishi nyumba moja ziliongezeka haraka. Tuna hakika ya kuwepo kwa jumuia hizo nje ya Italia pia: Ujerumani (1228), Korasia (1250), Ureno (1285) na Ufaransa (1287). Kulingana na maelekeo mawili ya Mt. Fransisko (moja la toba, sala na upweke, lingine la ushuhuda wa Kiinjili kati ya watu), jumuia hizo zilikazania ama muungano na Mungu ama huduma kwa wenye shida. Toka mwanzo wakaapweke wengi walijiunga na Utawa wa Toba, baadhi yao wakiwa na wafuasi. Jumuia kubwa zaidi zilikuwa zile za kutolea huduma fulani, hasa kutunza wagonjwa.

Katika hali hiyo Nikola IV, Papa Mfransisko, alitoa (1289) kanuni mpya kwa Watubu wote, wa kiume na wa kike, wa wakati huo na wa wakati ujao, akiwaweka chini ya Ndugu Wadogo kama “wakaguzi na washauri” wao, kwa kumuona Mt. Fransisko kama “mwanzilishi wa Utawa wa Toba” (tamko ambalo si sahihi kihistoria). Kanuni hiyo haikubadili sana sheria za Memoriale, ila ilizipanga vizuri zaidi kulingana na zile za kitawa. Ina sura 20 zenye jumla ya namba 60, ambamo 1-13 zinahusu mapokezi na ustawi; 14-42 namna ya kuishi; 42-60 maisha ya kidugu na uongozi. Kanuni hiyo iliweza kuchangia ustawi wa Watubu, lakini ilipingwa mapema na mashirika mengine yenye watu wa namna hiyo (k.mf. mwaka 1285 Wadominiko walikuwa wameamua kushughulikia Watubu waliofuata karama yao, hivyo wakaendelea mpaka walipokubaliwa kanuni maalumu mwaka 1405, baada ya mfumo wao kumzaa Mt. Katerina wa Siena). Shida nyingine iliyojitokeza ni kwamba kanuni ya Nikola IV haikuzungumzia walioishi kijumuia: hiyo ilizidi kuwaletea matatizo mpaka walipopewa kanuni tofauti (1521).

Kwa kuwa kanuni hiyo ilikuwa ya tatu kwa Wafransisko (baada ya ile ya Ndugu Wadogo na ile ya Waklara), Utawa wa Toba ulianza kuitwa Utawa III (Tertius Ordo) na washiriki wake wakaitwa Watersyari (wa tatu). Kumbe kabla ya hapo Tertius Ordo ilimaanisha kundi la tatu la waamini, yaani walei, waliopangwa baada ya makleri na watawa. Wazo la toba pia lilibadilika, na tapo lake likamezwa na Utawa III wa mashirika mbalimbali. Watersyari waliweza wakaishi ama nyumbani kwao, ama kijumuia, ama upwekeni (pengine kwa kutunza patakatifu fulani au kwa kujifungia mahali, k.mf. ndani ya mnara wa ngome ya mji); waliweza wakaishi katika ndoa au kuahidi useja n.k.

Kati yao, waliotangazwa watakatifu wanaweza wakafikia 4, mbali na wenyeheri 8. Idadi kamili haieleweki kwa sababu mwanzoni taratibu za kujiunga na Utawa huo hazikuwa wazi bado. Wa hakika zaidi ni mtakatifu Margerita wa Cortona (+1297) ambaye, baada ya kuacha maisha ya dhambi, alishika toba kali na kukusanya jumuia ya wafuasi. Somo wa Utawa III ni Mt. Elizabeti wa Hungaria (+1231), kwanza malkia aliyemtambua na kumtumikia Yesu katika wenye shida, halafu mwanzilishi wa jumuia, pamoja na Mt. Ludoviko IX (+1270), mfalme bora kabisa.

 

3.1.3. WATERSYARI KUZIDI KUTOFAUTIANA (1300-1517)

 

Wakarmeli walipoanza kuelekeza Watersyari wao kuweka nadhiri ya useja (kuna ushahidi wa mwaka 1283), desturi hiyo ikaenea haraka: mwaka 1307 mwanamume Mfransisko aliweka nadhiri tatu kufuatana na kanuni ya Nikola IV ingawa hiyo haitaji kabisa nadhiri. Kadiri Watersyari walivyozidi kujilinganisha na wanadhiri, yalizuka maswali juu yao: mbona kanuni haisemi juu ya kuishi pamoja? Mbona wanaweka nadhiri kama si watawa? Mbona wanawake wanaoishi kijumuia hawashiki ugo? Mbona wengine wanaweka nadhiri halafu wanaendelea kuishi kwao? Je, ni watawa? Majibu yakapatikana polepole, mpaka wakabainishwa Wasekulari (yaani ndugu wa ulimwenguni) na Waregulari (watawa hasa).

Zaidi ya hayo, tangu zamani tapo lolote la walei lililokazia Injili lilishukiwa kuwa na uzushi. Basi, mwanzoni mwa karne ya XIV Utawa III wa Kifransisko (TOF) ulijaribiwa sana, kutokana na matatizo ya Ndugu Wadogo, waliotaka kushindana na Papa, na yale ya makundi ambayo yalifanana na TOF yakaja kukatazwa na Mtaguso wa Vienne (1312). Ingawa laana hiyo haikuipata TOF, kwa kuwa Klementi V aliwahi kuagiza utafiti halafu akathibitisha tena kanuni yake (1308), Maaskofu wakaendelea kuwa na shaka na kusababisha dhuluma dhidi ya Watersyari. Isitoshe, makundi mengi yaliyokatazwa yaliamua kujiunga na TOF ili kuendelea kihalali. Jumuia ziliweza kuwa na ndugu 3 hadi 40. Maisha ya pamoja hayakuwa na lazima ya ndugu kushirikishana mali. Baadhi yao waliendelea kuwa na mali binafsi kama Wasekulari, ingawa baadhi walichanga kila kitu kama watawa hasa. Kazi zao zilikuwa za ufundi (kushona, kuhariri, kutengeneza hostie na mishumaa n.k.), za malezi (kufundisha watoto), za uuguzi (nyumbani kwa wagonjwa au hospitalini) pamoja na kuwakeshea mahututi na maiti. Riziki zilipatikana kwa kazi hizo, lakini pia (hasa kwa wanawake) kwa kuombaomba mlango kwa mlango.

Muundo wa jumuia ulikuwa sawa na ule wa Wasekulari, yaani kila moja ilikuwa chini ya Askofu, pamoja na mkaguzi au mshauri toka Utawa I, halafu ilikuwa na uongozi wa ndani (Mtumishi na halmashauri yake). Muundo huo ukaja kubadilishwa na baadhi ya jumuia mwishoni mwa karne ya XIV, kutokana na ongezeko kubwa la jumuia hizo za kiume na za kike. Pengine moja ilizaa nyingine ambayo ikabaki chini ya ile mama. Pia ulihitajika ulinganifu mkubwa zaidi wa taratibu (kanzu, ugo n.k.) kati ya jumuia za jimbo au kanda moja. Kwa kibali cha Askofu na cha Mtumishi wa Ndugu Wadogo, shirika jipya la namna hiyo liliweza kuwa na mkutano mkuu na kumchagua Mkuu wake. Kila shirika lilikuwa na mkaguzi toka shirika lingine. Jaribio la kwanza lilifanywa na Alfonsi Pecha aliyetaka kuunganisha wakaapweke wote wa Italia ya Kati na Kusini (1373) asifaulu. Kumbe walifanikiwa Watersyari wa Utrecht (Uholanzi, 1401), Ubelgiji wa Kiholanzi (1413), Koln (Ujerumani, 1427), Hispania (1442), Ubelgiji wa Kifaransa (1443), Italia (1447), Irelandi (1456), Marburg (Ujerumani, 1467), Ureno (1470), Korasia (1473) n.k. Wengine waliruhusiwa kuweka nadhiri kuu ya useja (1401) au zote tatu (1413). Yalijipatia kibali ingawa upinzani uliendelea kwa kuwa masuala yao hayakuwa bayana kinadharia. Hata hivyo hayakuwa mashirika ya kimataifa, yanayotarajia kuenea popote, bali ya kijimbo au ya kikanda. Kwa kuwa hayakuwa ya kitawa rasmi, yaliweza kuunganisha jumuia za kiume na za kike chini ya Mkuu mmoja; hapo kulikuwa na Mtumishi wa kike pia kwa jumuia za kike. Mashirika hayo yalitoa huduma zilizopangwa vizuri kadiri ya katiba yake. Mwaka 1439 lile la Ubelgiji wa Kiholanzi lilikuwa na konventi 70 na ndugu 3,000 hivi, wa kiume na wa kike, wote wakivaa kanzu ya kijivu.

Elekeo la kitawa la mashirika hayo lilikuwa wazi, hivyo si ajabu kwamba yalizidi kujilinganisha na wanadhiri. Hata Waoservanti walichangia sana, hasa Italia: kuanzia mwaka 1380 nd. Paolucho Trinci alijipatia ruhusa kadhaa, mojawapo ile ya kupokea Wasekulari (1384), halafu ile ya kuanzisha monasteri kwa ajili ya wale wa kike huko Foligno (1388). Tangu mwaka 1397 hadi 1435 monasteri hiyo ikaja kuongozwa na M.H. Anjelina wa Marsciano aliyefaulu kuzianzisha 16 nyingine: ndio mwanzo wa shirika la kike (1428) lililofanana sana na yale ya kisasa. Lilikuwa na Mtumishi mkuu ambaye alichaguliwa na Watumishi wa kila monasteri na kuwa na mamlaka ya kuzitembelea zote. Halikuwa na ugo wala nadhiri, isipokuwa ya utiifu. Kazi kuu ya wanashirika ilikuwa kulea wasichana. Anjelina alipofariki, Eugeni IV alikuza mamlaka ya Mtumishi mkuu, lakini uamuzi huo ulipingwa na Watumishi wa monasteri na Waoservanti. Halafu ongezeko la nyumba hata nje ya Italia lilidai safari nyingi za Mtumishi mkuu na za wengine, nazo zikasababisha vurugu. Basi, Pius II alifuta wadhifa wa Mtumishi mkuu (1461), hivyo shirika likapotewa na sura yake na umoja wake. Waoservanti walipozidi kudai Watersyari hao wote washike ugo wa Kipapa, wengine wakakubali (Watersyari wa ugo, ambao baadhi yao wakaja kuwa Waklara), ila wengine wakajitenga na Waoservanti ili kuendelea na utume. Ingawa Sisto IV alitaka Watersyari wote wa kike wakae chini ya Ndugu Wadogo (1471), wengine walijiweka chini ya Maaskofu, wengine chini ya TOR au chini ya Waamadei wasibanwe na ugo.

Kwa kweli Waoservanti walishughulikia sana Utawa III na kuustawisha upya. Katikati ya karne ya XV Mt. Antonino wa Firenze, Mdominiko, alishuhudia kwamba, “Watersyari Wadominiko ni wachache sehemu hizi, tena wa kiume ni mmojammoja tu; kumbe chini ya kanuni na kanzu ya Utawa III wa Mt. Fransisko wako wengi wa kiume na wa kike. Wengine kama wakaapweke, wengi kama wauguzi wa hospitali, wengine wameunda shirika”. Ili kupunguza upinzani, Martino V (1417-1431) alikuwa ameweka Wasekulari wote chini ya Watumishi wa Ndugu Wadogo (1428), ambao tu waliruhusiwa kupokea watakaji, kufundisha, kukagua na kukosoa. Pengine waandamizi wake wakawa na msimamo tofauti na kuwarudishia mamlaka Wasekulari wenyewe. Mt. Yohane wa Capestrano aliwashughulikia na kuwatetea kwa namna ya pekee, akikusudia kuratibu na kuunganisha jumuia zote za Watersyari zisizo na sura maalumu kisheria ili azihusishe na urekebisho wa watawa na wa Kanisa lote. Alipokubaliwa na Eugeni IV kwa sauti tu (1436) ifutwe hati ya Yohane XXII iliyokataza jumuia zote za Watersyari, akawatangazia haraka, ikaanza mikutano ya kanda na mikutano mikuu. Kwa miaka 10 Watersyari wakaapweke wa Italia waliunganika wote. Lakini wengine walipendelea kujitegemea zaidi, na wengine walikataa kujilinganisha kabisa na watawa na kuweka nadhiri (walivyodai hasa Waklareno, waliojitenga na OFM na kukimbilia Utawa III). Basi, Nikola V baada ya miaka miwili alifuta kabisa ruhusa aliyoitoa mwaka 1447, akisema, “Wanaopenda maisha magumu zaidi wanao tayari Utawa ulioanzishwa na Mt. Fransisko mwenyewe”.

Lakini mwaka 1457 Watersyari wa Lombardia walikubaliwa tena kuwa na Mkuu wa kwao, halafu wakaenea katika mikoa mingine ya Italia, wakakubaliwa (1467) fadhili zote walizopewa wenzao wa shirika la Hispania, zikiwa ni pamoja na ile ya kuweka nadhiri kuu tatu. Mwaka 1472 mkutano mkuu ulitunga kanuni mpya. Mwaka 1476 walikuwa na kanda kadhaa tayari. Hatimaye Sisto IV alitamka rasmi (1480) kuwa nadhiri za Watersyari wa kiume na wa kike zilizowekwa kwa fahari zihesabiwe kuwa kuu kisheria. Tamko hilo likathibitishwa (1517) na Leo X aliyekanusha kuwa hivyo pia kwa nadhiri ya useja ya wanaoishi nyumbani kwao, ingawa aliwakubalia fadhili kadhaa. Hata kuhusu ugo kwa wanawake, uliobaki kuwatofautisha na wamonaki, ilitamkwa (1487) kuwa ni wa hiari.

Pia baadhi ya Watersyari waliishi utawani kwa Ndugu Wadogo ili wawatumikie kwa hiari pasipo malipo wala nia ya kuwa watawa hasa, ingawa waliweza wakashiriki maisha ya jumuia chini ya mlinzi, wakiweka nadhiri ya utiifu na useja. Ni kwamba katika karne ya XIII Utawa I ulipojali mno ukleri na kuzuia ongezeko la mabradha pamoja na kudharau kazi za mikono, ulikuja kuhitaji maboi (wanazungumziwa na hati za Kanisa kuanzia mwaka 1248). Katiba ya OFM (1260) ilikataza wasiongozane na Ndugu Wadogo ili kuwashikia pesa na kuzitumia kwa niaba yao; ila iliruhusu watoe baadhi ya huduma konventini, mradi wasilale huko. Baadaye ndugu maarufu waliruhusiwa kuwa na boi binafsi (katiba ya 1316 n.k.). Mwishoni mwa karne ya XV maboi walianza kufikiriwa washirikishwe kwa kiasi fulani maisha ya kitawa: kwanza wafuate vizuri dini, halafu wajiunge na Utawa III na kuvikwa kanzu fulani, mradi ionekane wazi ni tofauti na ile ya Ndugu Wadogo.

Hasa katika karne ya XIV, matunda ya Utawa III ni mengi na ya kila aina: malkia na mapadri, watu wa ndoa na waseja, wakulima na mafundi, waanzilishi wa mashirika na mashujaa wa huruma, wakaapweke, wafiadini n.k. Mbali na watakatifu ambao hatuna hakika kama walijiunga na Utawa III, kuna Elzeario wa Sabran (+1323), aliyeishi na mke wake (M.H. Delfina) kwa usafi kamili, malkia Elizabeti wa Ureno (+1336), aliyemaliza maisha yake katika jumuia ya Utawa III, Konrado Confalonieri (+1351) aliyeishi miaka mingi upwekeni, na malkia Birgita wa Sweden (+1373), somo wa Ulaya. Kati ya wenye heri 23 wakumbukwe hasa Anjela wa Foligno (+1309), anayeitwa “mwalimu wa wanateolojia” kwa ubora wa maandishi yake juu ya mang’amuzi ya kiroho, na Raimundo Lull, mwandishi, mwanzilishi wa seminari ya kimisionari na hatimaye mfiadini kwa mikono ya Waislamu (+1316). Umisionari wa Utawa III ulijitokeza kwa namna ya pekee kati ya Waregulari wa Ureno, waliosindikiza wapelelezi wa nchi yao katika safari za hatari pia, kama vile Kongo na Angola. Mmojawao akasoma Misa mbele ya mfalme wa Kongo (1491) akambatiza (1495). Lakini utume wa Watersyari ulijitokeza zaidi katika mazingira ya kawaida ya walei wa Ulaya, na katika huduma mbalimbali walizozianzisha: hospitali, wokovu wa makahaba, uombaji wa msaada kwa ajili ya maskini, ghala za kugawia chakula bure, mafunzo kwa watoto fukara na kwa wanaosomea upadri n.k.

 

 

3.2. KANUNI TOFAUTI KWA WASEKULARI NA WAREGULARI (1517-1762)

 

3.2.1. WAREGULARI KUKOMAA KAMA WATAWA HASA (1517-1762)

 

Mtaguso wa V wa Laterano ulitofautisha (1516) aina nne za Watersyari: wanaoishi pamoja, wanaume wanaoishi katika konventi za Utawa I, wanawake wanaoishi nyumbani kwa nadhiri ya useja, na Wasekulari. Kwa msingi huo M.H. Gabrieli Maria alitunga (1517) kanuni sahili kwa Waregulari ambayo ikaja kukubaliwa na Leo X, halafu na Julius III, ikaendelea kufuatwa na konventi nyingi za Ufaransa. Lakini nyingi zaidi zilikubali ile ya Leo X iliyokusudiwa (1521) kuleta umoja na usawa kati ya Waregulari, ikiwafanya watawa hasa na kuwatenganisha na Wasekulari, walioendelea kufuata kanuni ya Nikola IV hadi mwaka 1884. Katika sura zake 10, kanuni hiyo mpya ilidai nadhiri za Waregulari wote ziwe tatu tena kuu, ingawa iliiachia kila konventi ya kike kuamua kuhusu ugo kama haijaushika, kusudi utume kwa wagonjwa na wasichana usizuiwe. Hata hivyo haikupokewa na Waregulari wote, na ilipingwa vikali hasa Ulaya Kaskazini. Sababu mojawapo ni kwamba ilitaka konventi zote za kiume na za kike ziwe chini ya Ndugu Wadogo, zikibaki na Mkubwa wa nyumba tu, bila ya Watumishi wakuu wa mashirika. Uamuzi huo ulitokana na juhudi za Waoservanti za kuzuia uwepo wa shirika lingine la Kifransisko lenye uongozi unaolingana na ule wa Utawa I. Basi, mashirika yaliyokwishakubaliwa yakaendelea kufuata kanuni ya Nikola IV pamoja na katiba zao. Lakini mapambano hayo yalidumu muda mfupi tu, kwa kuwa uenezi wa Uprotestanti ulifuta mapema karibu jumuia zote za Ujerumani na Uholanzi.

Hapo katikati shirika la Waregulari wa Hispania, kisha kushindana sana na Ndugu Wadogo waliodai kulikagua, lilikubaliwa na Paulo III kanuni mpya (1547) kwa Watersyari wote wa Hispania, Ureno na makoloni yake. Kanuni hiyo, tofauti sana na ile ya Leo X, ilikuwa na sehemu kuu tatu: ya kwanza kwa Watersyari wa kiume walioishi pamoja kwa nadhiri; ya pili kwa wale wa kike wenye nadhiri walioishi pamoja bila ya ugo; ya tatu kwa Wasekulari, pamoja na wakaapweke na mabikira walioishi makwao. Jambo la pekee zaidi, lilikuwa kuwaweka wote chini ya Mtumishi mkuu wa Waregulari wa kiume (aliyetakiwa kuwa padri): hivyo hao walifikia kulingana na Utawa I. Nje ya Ufransisko jambo kama hilo halijatokea hata leo: kuwepo Utawa III wenye masista na Wasekulari chini yake! Halafu Waregulari wa Italia pia wakakubaliwa katiba na uhuru kamili kwa kanda zao.

Baada ya hapo juhudi za urekebisho zilizofuatana na Mtaguso wa Trento zilidai masista wote washike ugo ili kukwepa makwazo. Mt. Pius V kwanza alidai (1566) masista wote wa shirika lolote wabanwe daima na ugo wa Kipapa, hata kama hawajawahi kuwa nao; wenye nadhiri ndogo (ambazo wakati huo hazikuwa na nguvu za kisheria) wahimizwe kuweka zile kuu na hivyo kukubali ugo, la sivyo wakatazwe wasipokee tena miito waje kwisha. Haikuwa rahisi kutekeleza agizo hilo, pia kwa sababu ya umuhimu wa huduma ambazo walikuwa wanazitoa na ambazo hazikupatana na ugo. Matokeo, baadhi ya jumuia zikawa monasteri za Waklara, lakini nyingine zikaendelea huru katika nchi zote na katika mashirika karibu yote. Halafu, akiona maisha yao hayana toba na nidhamu za kutosha, ingawa Kardinali mlinzi alijitahidi, aliwaweka wote, wanaume kwa wanawake, chini ya Waoservanti (1567-1568). Hatimaye alifuta jumuia zote zenye nadhiri ndogo akakataza zisianzishwe tena (1568): hata agizo hilo likashindikana, lakini yote yalikuwa changamoto zifanyike juhudi za urekebisho. Hapo kwa wanaume wa Ufaransa kanda 7 zilikuja kushika maisha yaliyofanana sana na yale ya marekebisho ya Utawa I: kuishi mbali na watu, kuamka usiku wa manane kwa sala, kufanya malipizi makali na kutembea peku. Kwa wanawake pia mkazo ulikuwa kufuata mfano wa Wakapuchini au marekebisho mengine, pamoja na kushika ugo na nadhiri kuu, hasa Uswisi, Ujerumani, Ubelgiji, Ufaransa. Hata hivyo wakaendelea kushika kanuni ya TOR na pengine kufundisha.

TOR ya Italia ilijipatia tena uhuru (1586) kwa kanda zake 11 chini ya Mtumishi mkuu; polepole Waregulari wa nchi nyingine ama walijiunga nayo katika karne ya XVII, ama wakakoma kwa kumezwa na OFM au kwa kudhulumiwa na serikali. Mwaka 1700 wanaume wa TOR jumla walikuwa 3,991 katika konventi 217 na kanda 20, takwimu ambayo haikubadilika sana katika nusu ya kwanza ya karne ya XVIII. Upande wa wanawake haiwezekani kukadiria idadi yao. Pamoja na hayo, yalianzishwa mashirika mapya ya kiume Hispania, Ufaransa na hata Gwatemala kwa ajili ya huduma mbalimbali. Watakatifu waliopatikana wakati huo ni Yasinta Mariscotti (+1640), aliyeongoka baada ya kuishi miaka 15 utawani kwa ulegevu, Petro wa Betancur (+1667), aliyeweka msingi wa shirika la Ndugu Wabethlehemu, na Maria Kreshensya Hoess (+1744), aliyeabudu sana Roho Mtakatifu, mbali ya mwenye heri Mjapani aliyefia dini kwao.

 

3.2.2. WASEKULARI KUZIDI KUENEA (1517-1762)

 

Upande wa Wasekulari, karne ya XVI iliwarudisha nyuma Italia (watu waliporudia sanaa za kipagani) na Ulaya Kaskazini (ulipoenea Uprotestanti), kumbe iliwastawisha katika nchi zilizoongoza kisiasa na kidini (Hispania na Ureno) pamoja na makoloni yake huko Ulaya na ng’ambo (hasa Amerika na Filipino: mwaka 1586 nchi hizo zilikuwa na Wasekulari zaidi ya 100,000!). Wahispania (hata wafalme, majemadari, Maaskofu) walikuja kumheshimu sana Mt. Fransisko na kutamani waitwe wanae na kuzikwa wamevaa kanzu yake. Uenezi ulileta pia ulegevu katika maisha yote ya toba, hata uduni wa kanzu uliachwa, halafu badala yake vitambaa viwili kifuani na mgongoni hadi kwenye kamba kiunoni vikaruhusiwa kuvaliwa chini ya nguo yoyote, hata ya fahari.

Katika umati huo kuna watakatifu pia, kuanzia Mt. Ajela Merichi (+1540) aliyeanzisha kikosi cha Mt. Ursula kwa roho ya Kifransisko na chini ya kanuni ya Utawa III, ambacho muda mrefu baadaye kikageuka kuwa shirika la kitawa. Wengine ni Gaetano wa Thiene (+1547), Ignas wa Loyola (+1556), Filipo Neri (+1595) na Kamilo wa Lellis (+1614), waanzilishi wa mashirika yasiyo ya Kifransisko, ambao ni vigumu kusema walichota nini katika Utawa III. Walio wengi ni wafiadini 17 wa Japani waliochanganya damu yao na ile ya wamisionari wa Utawa I waliowashirikisha Injili kwa roho ya Kifransisko (+1597): Paulo Suzuki, Gabrieli wa Ize, Yohane Kinuya, Thomas Danki, Fransisko wa Meako, Thomas Kozaki, Yohakim Sakakibara, Bonaventura wa Meako, Leo Karasuma, Mathias wa Miyako, Antoni wa Nagasaki, Ludoviko Ibaraki, Paulo Ibaraki, Mikaeli Kozaki, Petro Sukejiro, Kosma Takeya na Fransisko Adauctus.

Katika karne ya XVII uenezi uliendelea katika nchi hizo na pia Austria, halafu Ufaransa, hasa Ndugu Wadogo wa matawi mbalimbali walipoamua kuwajibika zaidi upande huo wakaanza kushindana kati yao tena na TOR. Mapapa, wakijua umuhimu wa Utawa III katika kuzuia uzushi, walichangia uenezi huo kwa kuupatia rehema na fadhili za pekee. Kwa ajili ya Wasekulari vilitungwa pia vitabu vingi vya sala na maelezo ya kanuni, pamoja na kukaza maisha ya kiroho (tafakuri, mafungo ya kiroho, sakramenti) na huduma kwa wenye shida. Hata hivyo hali ya jumla ilizidi kudidimia, na OFS ilionekana kulingana na chama chochote cha kumheshimu mtakatifu fulani, kuadhimisha sherehe yake n.k. Lakini mambo kama hayo hayapiti bure yasiathiri roho za watu na jamii nzima, hasa yanapogusa umati (mwaka 1689 Madrid ilikuwa na Wasekulari 25,000!). Vilevile miundo ya huduma iliyoanzishwa na Wafransisko hao iliendelea hata katika matatizo mengi, hivi kwamba mingine ipo hadi leo.

Tunda bora ni Maria Ana wa Yesu wa Paredes (+1645), Mfransisko wa kwanza wa Amerika kutangazwa na Kanisa kuwa ni mtakatifu. Wengine waliojiunga na OFS au kuvaa kamba yake ni wat. Fransisko wa Sales (+1622), Yoana Fransiska wa Chantal (+1641) na Yosefu Kalasanzi (+1648). Kundi kubwa zaidi ni lile la wenye heri 30, hasa wafiadini wa Japani tena.

Kwa Watersyari walioishi utawani kwa Ndugu Wadogo katikati ya karne ya XVII ulipangwa umri wa chini (miaka 20) na malezi ya miaka 3 chini ya padri. Baadaye tena hali yao ikafafanuliwa kikamilifu na katiba, hasa ya OFM (iliyokuwa na Watersyari wengi zaidi konventini).

 

 

3.3. WASEKULARI NA WAREGULARI NYAKATI ZETU (1762-2005)

 

3.3.1. WAREGULARI KUDHULUMIWA HALAFU KUONGEZEKA AJABU (1762-2005)

 

Kwa Utawa III pia miaka ya mwisho ya karne ya XVIII na sehemu kubwa ya ile iliyofuata ilikuwa kipindi kigumu cha majaribu, kutokana na dhuluma za serikali nyingi. Falsafa ya waasi wa dini na utaifa wa wafalme na Maaskofu wa nchi kadhaa vilielekeza hata kumwaga damu za wengi, hasa baada ya mapinduzi ya Kifaransa kuenea Ulaya karibu nzima.

Ilianza Jamhuri ya Venezia (1767) kwa kufuta kanda moja ya TOR. Akafuata malkia wa Austria na Hungaria, aliyekataza (1776) OFS isipokee tena watakaji. Mtoto wake akafuta Utawa III kwa namna zake zote (1782). Ufaransa ukafuta miundo yote ya kidini (1790), ikiwa ni pamoja na Utawa III, na kutaifisha mali yake. Baadhi ya Watersyari kwa uaminifu wao walifungwa hata kuuawa. Hispania (1812) na Ureno (1834) pamoja na Brazili mashirika yote yakafutwa, ingawa jamaa za OFS zikaendelea. Hata Italia jamaa hizo ziliondolewa hadhi yao mbele ya sheria (1861-1866), lakini zikaendelea kama vyama vya hiari.

TOR ni kati ya mashirika yaliyopigwa zaidi, hata karibu kutoweka: kwa miaka 30 hivi kanda nyingi zilikwisha; katika mikutano mikuu iliyofanyika tena kuanzia mwaka 1824 waliweza kuhudhuria tu ndugu toka mikoa 3 ya Italia na pengine toka Korasia.

Dhuluma hizo zilipiga sio tu miundo na mali, bali pia mfumo wa maisha, kwa kudai watawa wawe na faida kwa jamii, si mzigo kwake. Katika mazingira hayo yakaja kuanzishwa mashirika mengi ajabu, hasa ya wanawake: karne ya XIX ndiyo iliyozaa mashirika mengi kuliko nyingine zote. Kati yake, asilimia kubwa ni ya Kifransisko (siku hizi yapo 22 ya wanaume na zaidi ya 400 ya wanawake, yanayojumlisha watawa 120,000 hivi, mbali ya monasteri 61 zenye masista 900!). Si rahisi kuandika historia ya mashirika hayo yote. Kwa kifupi, mengine yalitokana na monasteri za Waklara waliolazimika kushika utume fulani ili waruhusiwe kuendelea kuishi kijumuia (baadhi yake wanafuata bado kanuni ya Utawa II kwa namna yao). Mengine yalitokana na Wasekulari walioanza kuishi pamoja. Mengine yalianzishwa tu kutokana na elekeo la kila jimbo kutaka liwe na shirika lake, hivi kwamba Askofu (au hata paroko) alijitahidi kujianzishia jipya au kutenga tawi na nyumba asili; katika hilo pengine hali ya siasa na ya jamii ilichangia, pamoja na hamu ya kujitegemea. Ustawi huo ulitokea wakati uleule wa mashirika ya zamani kufifia: tena watawa hao, waliofukuzwa na serikali kutoka konventi zao, ndio walioanzisha mashirika mengi kulingana na mahitaji ya watu katika ulimwengu mpya wa kibepari. K.mf. M.H. Honorati Kazminski (+1916), padri Mkapuchini aliyeanzisha mashirika 27 tofauti (kati yake 17 bado yapo), na Askofu Mkapuchini Luis Amigò (+1934), aliyeanzisha mashirika mawili makubwa (la kiume na la kike) yaliyokwishapata wenye heri 22 wafiadini.

Kwa kawaida ni mashirika ya nadhiri ndogo, au yasiyo na nadhiri, yanayotoa huduma maalumu upande wa umisionari, huruma kwa maskini, ustawi wa jamii, malezi, tiba n.k. Kwa sababu ya kutoweka nadhiri kuu, wanashirika hawakuhesabiwa kama watawa, wala wale wa kike hawakubanwa na ugo. Walifuata katiba zao maalumu chini ya viongozi wao. Waliotaka kuwa Wafransisko walijiunga binafsi na OFS. Kanisa, baada ya kutamka (1887-1893) kwamba mtawa hawezi kuwa Mtersyari pia, na baada ya kutambua (1900) mashirika hayo kuwa ya kitawa liliamua (1901) shirika la mchepuo fulani wa kiroho lisianzishwe pasipo fungamano na Utawa I wa mchepuo huo. Hapo watawa wote wa mashirika hayo wakahesabiwa kuwa Watersyari jumla, bila ya kujiunga binafsi na Utawa III. Mashirika mengi ya Kifransisko yalifungamana kiroho na OFM (1905 n.k.) na OFMCap (1906 n.k.).

TOR ilipoomba ruhusa ya kuwa na mashirika ya Watersyari chini yake, ilikubaliwa baada ya miaka 5, halafu ikaondolewa. Ugumu wa suala hilo ni kwamba TOR yenyewe ni Utawa III: inawezaje kujilinganisha na Utawa I? Lakini Benedikto XV (1914-1922), baada ya kuona TOR inameza mashirika madogo ya Watersyari, aliiruhusu tena (1921) akipendekeza mashirika yote ya kiume na ya kike ya Utawa III wa Kifransisko yaungane nayo. Kwa ajili hiyo aliilinganisha TOR na matawi matatu ya Utawa I: tangu hapo familia ya Kifransisko ikahesabiwa kuwa na Wakuu 4.

Kufuatana na Mkusanyo wa Sheria za Kanisa, Pius XI (1922-1939) alitoa kanuni mpya (1927) iliyotungwa kwa ushirikiano wa Wakuu 4 wa familia ya Kifransisko iwe kanuni pekee kwa mashirika ya Utawa III, yakiwa ni pamoja na TOR yenyewe iliyokuwa imeikataa ile ya mwaka 1521. Ingawa juhudi ya kuyaunganisha yote chini ya TOR ikashindikana kwa sababu karibu yote yalipendelea kujitegemea, kuanzia mwaka 1950 ilifanyika mikutano mingi ya pamoja na kuzidisha ushirikiano hasa kwa ajili ya kutunga kanuni nyingine kufuatana na maelekezo ya Mtaguso II wa Vatikani. Kanuni hiyo iliyothibitishwa (1982) na Yohane Paulo II ni ya Kifransisko kuliko zile zote zilizotangulia. Hatimaye likaanzishwa (1985) Baraza la Kimataifa la Kifransisko (IFC-TOR) linaloshirikisha mpaka sasa ¾ za mashirika yote ya Utawa III.

Ushirikiano mpya wa Utawa III na ule I uliimarishwa kwa kuunda (1995) Baraza la Familia ya Kifransisko, linalojumlisha Wakuu wa OFM, OFMConv, OFMCap, TOR, IFC-TOR na OFS. Utawa II hauna mwakilishi, kutokana na muundo wake wa monasteri zenye ugo. Baraza la Familia ya Kifransisko linawakilishwa katika Umoja wa Mataifa kwa njia ya asasi isiyo ya kiserikali inayoitwa Franciscans International.

Watersyari Waregulari 40 wa kipindi hicho wameshatangazwa wenyeheri, k.mf. Maria wa Mateso (+1904) aliyeanzisha shirika kubwa la Wafransisko Wamisionari wa Maria (wako 7,712 katika nchi 76), ambao 7 kati yao ni watakatifu waliofia dini China (+1900): Maria Ermelina wa Yesu, Maria wa Amani, Maria Klara Nanetti, Maria wa Mt. Natalia, Maria wa Mt. Yusto, Maria Amandina wa Moyo Mtakatifu na Maria Adolfina Dierk. Muda mrefu kabla yao alistawi Maria Fransiska wa Madonda Matano (+1791), aliyestahimili mateso mengi, na baada yao Mt. Alberto Chmieliwski (+1916), aliyeanzisha mashirika mawili (la kiume na la kike) huko Polandi.

 

3.3.2.   WASEKULARI KUFIKIA KILELE CHA USTAWI WAO (1762-2005)

 

Kuna mambo mbalimbali yaliyochangia ustawi mpya wa Utawa III katika matawi yake kuanzia mwisho wa karne ya XIX: kikomo cha dhuluma za serikali katika nchi nyingi, hali mpya ya Utawa I, mvuto mkubwa wa mtakatifu Fransisko kwa wenye elimu na uenezi wa roho ya Kifransisko kupitia magazeti. Ndiyo sababu Utawa III ulianzishwa hata kati ya Waanglikana na Waprotestanti! Kwa miaka 115 mfululizo (1848-1963) Mapapa wote walikuwa wa OFS (kuanzia M.H. Pius IX hadi M.H. Yohane XXIII) wakahamasisha Maaskofu na wengineo kueneza Utawa huo, hasa Leo XIII aliyetoa kanuni mpya (1884) yenye sura tatu na namba 24 jumla. Pamoja na kufupisha ile ya zamani ilirahisisha mengi iweze kuwafaa Wakristo wote, ikiwadai tu wavae skapulari ndogo na kamba, kupata malezi ya mwaka mmoja kabla ya kutoa ahadi, kuvaa na kuishi pasipo makuu, kukwepa tamasha za kilimwengu, kuwa na kiasi mezani, kuungama na kupokea kila mwezi, kusali Zaburi au walau Baba Yetu, Salamu Maria na Atukuzwe mara 12 kwa siku, kuandika mapema wasia, kujitafiti dhamiri kila siku, kushiriki Misa kila siku ikiwezekana, kuhudhuria mkutano kila mwezi, kuchangia gharama za Utawa na misaada kwa maskini, kukaguliwa na Ndugu Wadogo kila mwaka.

Kwa juhudi hizo, na hasa kwa makongamano mengi makubwa, OFS ilionekana mshikamano wa kidugu wa kimataifa mbadala wa Ukomunisti uliotangaza chuki kwa mabepari. Lakini wengine waliogopa elekeo hilo la kijamii. Basi, Mt. Pius X aliweka Wasekulari chini zaidi ya Ndugu Wadogo na kudai wawajibike katika siasa binafsi, si kwa pamoja. Hivyo OFS ikarudi kutazamwa kama shule ya kiroho tu, ikachapishiwa vitabu vingi, hasa juu ya masharti yake, namna za kusali na kujinyima, kujipatia fadhili na rehema n.k. Mkusanyo wa Sheria za Kanisa ulipanga aina zote za Utawa III katika nafasi ya kwanza kati ya vyama vya waamini, na kueleza kuwa lengo lake ni ukamilifu wa Kikristo kadiri ya maisha ya ulimwenguni kwa kufuata kanuni maalumu iliyokubaliwa na Papa na chini ya uongozi na roho ya Utawa I unaohusika.

Kwa hamasa za Mapapa, wengi walijiunga na OFS (mwaka 1934 walikaribia kuwa 4,000,000!) lakini muda mfupi kabla ya vita vikuu vya pili walianza kupungua kutokana na matapo mengine ya kiroho kuanzishwa na kuhamasishwa na Mapapa, hasa Aksyo Katoliki; pia kwa sababu wingi si hoja, yaani ongezeko lao lilisababisha ulegevu fulani hata kusawazisha OFS na chama chochote. Kabla na hasa baada ya Mtaguso II wa Vatikani ilitokea misukosuko na maswali mengi. Ili kuyakabili, ilifanyika mikutano mingi ya matawi yake mbalimbali (1950 n.k.) na kuzidisha ushirikiano kati yake (pia na Utawa III wa michepuo mingine) hata ikatolewa (1957) katiba moja kwa Wasekulari wa matawi yote ya Kifransisko. Miaka hiyohiyo lilianzishwa kundi la Vijana Wafransisko. Halafu ikaanzishwa halmashauri ya kimataifa ya OFS yote (1973) na Paulo VI akathibitisha (1978) kanuni mpya ya OFS kulingana na maelekezo ya Mtaguso huo. Ina sura tatu na namba 26 jumla kuhusu asili ya OFS na kanuni yake (1-3), mtindo wa maisha (4-19) na taratibu zake (19-26). Ni kama mwongozo wa maisha ya Kiinjili unaomkazia Yesu Kristo kwa kuwa Injili si nadharia, bali ni mwenyewe (namba 12 kati ya 26 zinamzungumzia wazi). Haina tena maagizo ya kinaganaga kuhusu toba, ambayo yaliachwa kwa katiba mpya (1990) iliyounganisha moja kwa moja matawi yote yaliyokuwa chini ya Wakuu 4 wa familia ya Kifransisko. Mwaka huo Wasekulari walikuwa 508,619, wengi wao wakiwa Meksiko na Italia. Hapo katikati toleo la pili la Mkusanyo wa Sheria za Kanisa lilitaja Utawa III peke yake kati ya vyama vya waamini, kutokana na heshima uliyopewa na mapokeo. Jambo jipya ni kwamba sasa mashirika yoyote yanaweza kuanzisha aina ya Utawa III, hata yale ya kike.

Kuhusu Wasekulari kuishi katika nyumba za Ndugu Wadogo, mtazamo baada ya Mtaguso II wa Vatikani ukawa tofauti: Ndugu Wadogo wanapaswa kutumikia, si kutumikiwa na Wasekulari; watu wakiishi konventini kwa kufanya kazi fulani, basi walipwe kadiri ya sheria za nchi. Hivyo idadi yao ikazidi kupungua haraka: kwa OFM mwaka 1968 walikuwa 536, mwaka 1994 wakabaki 155 tu.

Kati ya Wasekulari wa hakika wa karne hizi za mwisho tunakuta wenye heri 11 na watakatifu Yosefu Benedikto Cottolengo (+1842), Vinchensya Gerosa (+1847), Vinchensyo Pallotti (+1850), Emilia wa Vialar (+1856), Yohane Maria Vianney (+1859), Maria Yosefa Rossello (+1880), Yohane Bosco (+1888), Pius X (+1914) na Fransiska Saverio Cabrini (+1917), wengi wao wakiwa waanzilishi wa mashirika yasiyo ya Kifransisko. Pia kuna watakatifu 11 wa China waliofia dini (+1900): Yohane Zhang Huan, Patrick Dong Bodi, Yohane Wang Rui, Filipo Zhang Zhihe, Yohane Zhang Jinggwang, Thomas Shen Jihe, Simoni Chen Ximan, Petro Zhang Banniu, Fransisko Zhang Rong, Mathias Feng De na Petro Wu Anpeng.

 

Jedwali la matunda bora ya familia ya Kifransisko ni kama ifuatavyo:

 

 

Wenyeheri

Watakatifu

Jumla

Utawa I

181

85

266

Utawa II

27

10

37

Utawa III - Waregulari

45

15

60

Utawa III - Wasekulari

69

55

124

Waliovaa kamba

0

4

4

Jumla

322

169

491

 

Kati yao, 280 ni wafiadini, 3 mapapa, 14 maaskofu, 4 walimu wa Kanisa.