Ndugu Wadogo Wa Afrika

KATIBA

ya Utawa wa Ndugu Wadogo wa Afrika

 

 

 

YALIYOMO

 

 

0. DIBAJI

 

1. KUISHI KIINJILI KAMA FAMILIA YA MUNGU

 

2. KUITIKIA WITO

 

3. KUMUONEA KIU MUNGU

 

4. KUZAA KWA KUPENDANA NA MUNGU TU

 

5. KUTUMIKIA NA KUFANYA KAZI

 

6. KUSHIKAMANA NA YESU FUKARA

 

7. KUISHI KIDUGU KATIKA JUMUIA

 

8. KUTII KWA UPENDO

 

9. KUWA MASHAHIDI WA KRISTO

 

 

 

 

 

0. DIBAJI

 

0.1.1. Yesu, Mwana pekee wa Mungu, alikuja duniani aokoe kila kabila la watu na kuongozana na kila mmoja katika safari ya maisha.

0.1.2. Alikuja kutuangazia utamaduni tulioachiwa na wazee, ili tuone unavyomuelekea yeye Adamu Mpya.

0.1.3. Alikuja kutukusanya tena kwa njia ya Roho wake wa upendo, anayetufanya familia ya Mungu Baba, jamaa ya wadogo wake walioshinda hofu na chuki kati yao, mfano wa Utatu mtakatifu, ushirika kamili katika tofauti za nafsi, ambapo lugha zote ziungane kutangazia maajabu aliyotutendea Mwenyezi Mungu.

 

0.2.1. Kwa upendo wake alitaka Afrika iwe bara lake la pili, ambapo asalimike utotoni na azidi kuwa Mwafrika kwa njia ya viungo vyake.

0.2.2. Kanisa la bara letu, baada ya kutendewa naye makuu na kustawishwa kwa juhudi na damu za wazee wetu katika imani, sasa linatakiwa kueneza wokovu hata miisho ya dunia, lisitosheke na kazi ya kukidhi mahitaji ya majimbo yake tu.

0.2.3. Kutuatana na Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatikano, Roho Mtakatifu katika Sinodi ya Kwanza ya Afrika ameliambia Kanisa hilo anavyolitaka lijionyeshe familia ya Mungu na kutangaza habari njema ya Yesu Kristo, aliye njia, ukweli na uzima kwa Mwafrika na kwa yeyote duniani.

0.2.4. Miaka ya elfu mbili, nafasi ya pekee ya kufikisha Injili kwa watu wote, ndiyo saa yake tena.

0.2.5. Ingawa Waafrika wengi wanazidi kuachwa nyuma kisiasa na kiuchumi, utamaduni wao wa uzima na mshikamano unahitajiwa haraka na ulimwengu wote.

 

0.3.1. Mtakatifu Fransisko wa Asizi alimshuhudia Kristo kwa upole na ushujaa mbele ya Waislamu wa bara letu, akitamani kumwaga damu yake kwa wasiomjua bado.

0.3.2. Mfano wake huo na karama aliyojaliwa, yenye sifa kuu mbili yaani udugu na udogo, vinafaa sana kuchangia utekelezaji wa maazimio ya Sinodi hiyo.

 

0.4.1. Tukizingatia hayo, sisi Ndugu Wadogo wa Afrika tunajisikia wito wa kutimiza karama hiyo katika mazingira halisi ya Waafrika, kwa kudumisha, kustawisha na kueneza tunu za utamaduni huo ambazo zinalingana na Injili.

0.4.2. Hivyo tunatumaini kuwa nguvu ya Mungu, inayojionyesha wazi katika udhaifu wa binadamu, itatutumia kwa ustawi wa Kanisa lote, ambao unategemea na kulenga utakatifu, yaani kushiriki kikamilifu uzima wa Mungu.

 

0.5.1. Utawa wetu wa Kifransisko wa kimisionari una makao makuu mjini Morogoro, ambapo askofu wa jimbo, mhashamu Telesphore Mkude, katika juhudi zake za kueneza Injili, ameuunda kama chama rasmi cha waamini kadiri ya kanuni 312 CIC.

0.5.2. Ni juu ya askofu wa jimbo hilo kuzidi kufanya utambuzi wa karama hiyo ili aweze kupendekeza utawa huo ukubaliwe kama aina mpya ya maisha yaliyowekwa wakfu, kadiri ya kanuni 605 CIC, au aufute kwa sababu nzito.

 

0.6.1. Mwenyewe amethibitisha katika hii itusaidie kumfuata kwa hakika Yesu na kutimiza matakwa ya Baba kwetu.

0.6.2. Tunaohusika nayo moja kwa moja ni sisi wanachama tuliojifunga kushika useja mtakatifu, ufukara na utiifu kwa kuishi Injili kijumuia katika jamaa za kiume na kike.

0.6.3. Ni wanachama halisi pia makleri wanajimbo na walei wanaume na wanawake, waseja na wenye ndoa, ambao kisha kupata malezi ya kufaa wanaishi ulimwenguni karibu na jumuia mojawapo ya namna hiyo, wakishirikiana nayo katika maisha ya kiroho na ya kitume: hao wanafuata kanuni na katiba za Utawa wa Kifransisko wa Ulimwenguni (S.F.O.) kama washiriki wengine wa Utawa huo wa Kipapa.

 

0.7.1. Katiba hii ina mambo yale tu ya karama na taratibu zetu ambayo hayatarajiwi kubadilika.

0.7.2. Hata hivyo tuzidi kuomba mwanga wa Mungu na kufaidi mang’amuzi yetu ili tuelewe vizuri zaidi anataka nini kwetu, kwa kuzingatia ufuasi wa Kristo kadiri ya Injili, hazina ya kiroho ya Kifransisko, malengo ya Kanisa na mahitaji ya ulimwengu, tukiweka daima mbele ustawi wa roho zetu na wokovu wa watu.

 

0.8.1. Askofu wa Morogoro anaweza kuthibitisha marekebisho ya katiba yaliyopitishwa na baraza pana kwa thuluthi mbili za kura, mradi yawe yanahitajika kweli ili tuendelee kujenga juu ya misingi ileile.

0.8.2. Haja hiyo isipokuwepo, afadhali yaachwe, kwa sababu mabadiliko yanadhoofisha sheria, na yale madogo yanachochea mengine makubwa, mpaka mfumo wa utawa unakuwa mwingine na kusababisha utasa wake.

 

0.9.1. Ili tuwe na heri kwa kutekeleza kikamilifu yale tuliyoonyeshwa, tujitahidi sura halisi ya utawa wetu ilingane na picha iliyochorwa katika katiba tuliyojaliwa na Mungu kwa njia ya Kanisa lake.

0.9.2. Mkutano mkuu unaweza kutoa kwa kiasi sheria ndogondogo zinazohusu jamaa nzima, na ambazo ziweze kurekebishwa nao inapotakiwa, mradi zilingane daima na kanuni na katiba.

0.9.3. Halmashauri kuu inaweza kutoa maagizo maalumu yanayohusu baadhi tu ya ndugu au jumuia, kadiri ya mahitaji yao na ya mazingira wanapoishi.

0.9.4. Lakini tutegemee uaminifu mnyenyekevu wa kila mmoja wetu kuliko wingi wa sheria na juhudi za watumishi na walinzi.

 

0.10.1. Ukitokea wasiwasi kuhusu utekelezaji wa sehemu ya katiba hii, halmashauri kuu iamue la kufanya, lakini baraza likikusanyika litoe maelezo rasmi kwa kibali cha askofu wa Morogoro.

 

0.11.1. Ni juu ya askofu wa jimbo husika kusamehe ndugu wasitekeleze sehemu fulani ya sheria zetu katika nafasi maalumu.

0.11.2. Ikiwepo sababu ya kutosha, watumishi na walinzi pia wanaweza kuwasamehe ndugu walio chini yao, wale waliopo kwa muda na hata jumuia nzima, isipokuwa katika yale yanayohusu miundo ya utawa wetu na kiini cha maisha yetu; tena, ikihitajika ruhusa ya kudumu, itolewe na mtumishi tu.

0.11.3. Aliyesamehewa ajitahidi zaidi katika mengine anayoyaweza, akijua urahisi wa ruhusa hizo unavyozima upesi hamu ya ukamilifu.

 

0.12.1. Hasa tujihadhari na kishawishi cha kuona sharti fulani la katiba hii, eti ni gumu mno, au kuacha kulitimiza kwa makusudi au kwa ulegevu.

0.12.2. Tuamini kuwa wokovu umetokana na upumbavu wa msalaba, halafu tung’amue jinsi mzigo wowote ulivyo mwepesi ukibebwa kwa ajili ya Yesu mpenzi ili kuungana naye.

 

 

 

1 . KUISHI KIINJILI KAMA FAMILIA YA MUNGU

 

1.1. YESU NA INJILI YAKE

 

1.1.1. Yesu wa Nazareti ndiye mfano kamili wa Mungu asiyeonekana, na ndiye anayetufumbulia kikamilifu ubinadamu wetu.

1.1.2. Injili takatifu, iliyo moyo wa Maandiko Matakatifu yote, inatufunulia matendo na maneno yake, na hivyo inatuelekeza njia pekee ya kumfikia Baba katika Roho Mtakatifu na ya kuwa watu waliokomaa anavyotutaka yeye.

1.1.3. Mzee wetu Fransisko wa Asizi tangu aanze kuongoka hakuwa kiziwi kwa ujumbe wa Injili, bali kwa kuushika sawasawa alikuja kufanana na Yesu kwa namna ya pekee.

1.1.4. Upendo wa Kristo uliotupata sisi pia, ndio asili ya maisha yetu yote ambayo tunalenga ukamilifu wa Injili yake, kwa kushika sio tu amri za Mungu, bali pia mashauri yanayotokana na mafundisho na mifano aliyotuachia, ili tumfuate kwa karibu iwezekanavyo huyo Mwanakondoo kokote aendako.

1.1.5. Tuzingatie hivyo Injili zaidi kuliko mapokeo ya kibinadamu, hata kama ni ya kitawa.

1.1.6. Kwa njia hiyo Roho Matakatifu atamfanya Yesu kuwa kiini cha maisha yetu na kuunda upya utamaduni wetu ndani mwake, kwa sifa na utukufu wa Mungu Baba.

 

 

1.2. VIUNGO VYA MWILI WA KRISTO

 

1.2.1. Kristo ameunganika kabisa na bibiarusi wake na kuishi ndani yake, kiasi kwamba kushikamana na Kanisa na kushikamana naye ni mamoja.

1.2.2. Tumtolee huyo Mama yetu maisha na moyo, maneno na matendo, muda na nguvu ili sikuzote tuishi na kufanya kazi ndani yake na kwa ajili yake, tukiamini tunaye Roho Mtakatifu kadiri tunavyolipenda Kanisa.

1.2.3. Tushirikiane na vyombo vyake mbalimbali katika kazi na hasa katika adhimisho la ekaristi, ili kuonyesha na kuimarisha umoja tulionao.

1.2.4. Tutegemeze pia miundo yake ya lazima kwa njia ya sadaka na michango mbalimbali, hasa kwa ajili ya mfuko wa pamoja kama umeanzishwa jimboni.

1.2.5. Sisi watawa ni zawadi ambayo Baba amelijalia Kanisa ili kuwakumbusha watoto wake undani wa miito yao maalumu, ambao kwa wote ni mmoja tu, yaani kuwa watakatifu katika mwenendo wao wote.

1.2.6. Kama vile sisi tunavyohitaji msaada wa waamini wenzetu, nao wanahitaji kuvutwa na sisi ambao tumekataa tamaa za ulimwengu, na kuweka pembeni hata tunu kadhaa za kidunia, ili kulenga moja kwa moja heri ya milele kwa kufuata njia aliyoielekeza Yesu katika hotuba ya mlimani.

1.2.7. Kwa mfano wa Maria wa Bethania, tumwage maisha yetu kama manukato ya miguu yake, ili Kanisa lote lijae harufu nzuri ambayo imchochee kila Mkristo kusikiliza upya Neno la uzima na kuchangia juhudi motomoto za familia yote ya Mungu katika kutangaza, kuadhimisha na kutekeleza Neno hilo.

1.2.8. Hivyo katika Mwili wa Kristo tutashika nafasi yetu hasa, yaani kuwa moyo wa maisha yake, wa utakatifu wake na wa utume wake.

 

 

1.3. MAKANISA MAALUMU

 

1.3.1. Kanisa Katoliki linaishi katika Makanisa maalumu ya Mashariki na ya Magharibi, yenye sura mbalimbali kadiri ya mazingira, historia na utamaduni wa watu wake.

1.3.2. Tuthamini utajiri huo wote na kuuzingatia hasa tunapohamia jimbo fulani ili karama yetu istawi humo kama mahali pake, na kulijenga kweli.

1.3.3. Popote pale tutekeleze kwa ushujaa karama yetu ya kinabii, tukitenda na kusema kwa niaba ya Mungu, bila ya kufuata mkondo au kutaka kuwapendeza watu; lakini kwa unyenyekevu pia, tukikubali waandamizi wa Mitume waifanyie utambuzi.

1.3.4. Tukiongozwa na imani tuwapende na kujali kazi zao tatu za kutufundisha, kututakasa na kutuchunga.

1.3.5. Tuwe tayari kushirikiana nao katika ziara rasmi wanazotufanyia kwa maendeleo ya utawa wetu ndani ya Kanisa.

1.3.6. Tuwaone mapadri wao kuwa ni kaka zetu katika Kristo na tupokee kwa shukrani huduma zao, hasa za maparoko wetu na za wale ambao askofu wa jimbo kwa kushauriana na watumishi amewateua kuwa washauri na waungamishi wetu utawa usipojitosheleza.

 

 

1.4 UMOJA WA KANISA

 

1.4.1. Umoja wa Mungu katika nafsi tatu ni asili, kielelezo na lengo la familia yake inayounganishwa na Roho wa upendo.

1.4.2. Ubora wa Kanisa unategemea mafungamano yetu watoto wake, yaani jinsi tunavyotunzana na kushikamana na kupendana, tunavyokaribishana na kujadiliana na kuaminiana.

1.4.3. Kwa ajili hiyo askofu wa Roma amekabidhiwa kundi lote la Kristo duniani, kusudi alichunge kwa upendo, na kuliimarisha katika imani liwe nguzo na msingi wa ukweli.

1.4.4. Kwa ahadi yetu tunawajibika kuwapenda na kuwatii kwa namna ya pekee yeye na Kanisa lake, tukijitahidi kujua na kutekeleza hati zote wanazozitoa.

1.4.5. Sisi tunaoshuhudia uzuri wa kuishi kidugu, tujenge madaraja kati ya makleri, walei, watawa na miundo yao pia, ili tufanye kwa nguvu ya umoja kazi ile kubwa ajabu tuliyoagizwa na Yesu.

1.4.6. Vilevile tujadiliane na kufahamiana, tushirikiane na hasa tusali na kutubu pamoja na ndugu zetu wa madhehebu mbalimbali, kusudi ushuhuda wetu kwa Kristo, amani yetu, uweze kuaminika hadi mafarakano yoyote yaishe kabisa.

 

 

1.5. TOBA YA KIFRANSISKO

 

1.5.1. Yesu Kristo akitangaza utawala wa Mungu aliwaita watu kuupokea kwa kufanya mapinduzi ndani mwao, wakianza kuwaza, kupima mambo na kupanga maisha kulingana na upendo wa Baba aliotufunulia.

1.5.2. Mwenyewe akamtuma mzee wetu Fransisko ili kwa mfumo wake alirekebishe Kanisa ambalo ni takatifu, lakini pia linahitaji siku zote utakaso na matengenezo, ili waamini wote watekeleze maishani sakramenti zilizowaweka wakfu.

1.5.3. Tuzingatie hazina ya kiroho ya mtakatifu huyo, kwa kuitimiza, kuilinda, kuichimba na kuikuza moja kwa moja, halafu kwa kuwashirikisha watu wowote ili wapate wokovu na utakatifu.

1.5.4. Ndani ya Kanisa jumuia zetu zijengeke kama mazingira ya toba juu ya msingi wa ubatizo unaowezesha maisha yote yawe Pasaka, tukizidi kufia dhambi ili kufufuka na Kristo kwenye uzima mpya.

1.5.5. Ingawa hatujui mwaliko wa Yesu wa kupoteza maisha yetu nyuma yake utatufikisha wapi, tusifadhaikie mambo ya hesko, ila tumuachie Mungu wa faraja zote na kusaidiana kidugu kubeba msalaba siku kwa siku.

1.5.6. Baada ya kufunga safari ya kuufikia upendo kamili, tushinde kishawishi cha kujipongeza kwa urahisi na kusimama katikati, tukijua kwamba tusiposonga mbele, tunarudi nyuma tu.

1.5.7. Kama alivyofanya mtakatifu Fransisko, kwa uongozi wa Roho na vipaji vyake, tuvue utu wa zamani na vilema vyake, tukamvae Kristo na maadili yake, hata kuchuma matunda ya Roho na kuonja heri za Yesu, malimbuko ya uzima wa milele.

 

 

1.6. MFUASI MKAMILIFU WA YESU

 

1.6.1. Vizazi vyote vinamshangilia Maria mwenye heri kwa jinsi alivyosadiki Neno la Mungu na alivyokubali kujiliwa na Roho Mtakatifu: hivyo amekuwa kielelezo cha namna ya kupokea neema na kujiweka wakfu kwa Mungu.

1.6.2. Vilevile, akishiriki toka mwanzo maisha yaliyofichika ya Mwanae, halafu akihudhuria matukio makuu ya utume wake, ametuonyesha namna ya kuungana naye, hasa kwa kuyaweka na kuyatafakari katika moyo safi yale yote yanayomhusu Yesu.

1.6.3. Maisha yetu ya kiroho, ya kijumuia na ya kitume yawe na tabia hiyo ya Maria hasa, ili tuweze kukua katika imani, tumaini na upendo tunavyofundishwa na Injili.

 

 

 

2. KUITIKIA WITO

 

2.1 NJIA YETU

 

2.1.1. Roho Mtakatifu anawaongoza watoto wa Mungu kumfuata Yesu kwa namna maalumu na kuunda ndani ya Kanisa familia za kiroho zenye karama za aina nyingi.

2.1.2. Kwa neema yake sisi tunawajibika katika familia ile iliyoanzishwa na mzee wetu Fransisko katika matawi mbalimbali, ili mataifa yote yazidi kushuhudia utakatifu wa Kiinjili unaopatikana kwa kufuata nyayo za Yesu fukara tena msulubiwa.

2.1.3. Ndiye kitabu kikuu ambamo Roho Mtakatifu anatufundisha maana na namna ya kuishi, kupenda na kuteseka, hata kupokea kwa amani matakwa ya Baba katika nafasi ngumu zaidi za maisha.

2.1.4. Kwa upendo wa pekee Mungu Baba anawavuta mfululizo wale anaowataka waache vyote wakaungane kabisa na Mwanae kiroho na kimaisha, hasa kwa njia ya utiifu, ufukara na useja mtakatifu, ambayo ni yake kabisa na ambayo yalimfaa sana ayashike duniani.

2.1.5. Kama vile upendo huo, mambo hayo pia yanahusu maumbile yetu mpaka ndani kabisa, tunapojisikia misukumo ya kujifanyia mipango, kumiliki vitu na kupendana kijinsia.

2.1.6. Sisi tuliojaliwa karama hiyo hatuwezi kuithamini vya kutosha, lakini tuipokee kwa shukrani na kumrudishia Mungu utu wetu wote ili uwezo wake uuzidishe kwa manufaa ya umati.

2.1.7. Hivyo tutawaelekeza watu kushinda tamaa za utawala, mali na anasa, ambazo zimo mioyoni mwa wote kutokana na dhambi ya asili, na ambazo zinawapeleka kwenye maangamizi.

 

 

2.2. MIITO

 

2.2.1. Maisha ya Bwana na agizo lake vinaonyesha kwamba toka mwanzo swala la miito mitakatifu ni la msingi kwa Kanisa, na kwamba sala ndiyo njia ya kulikabili kwa hakika kabisa.

2.2.2. Tushiriki katika kazi za Kanisa kwa ajili hiyo, tukiwafundisha hasa vijana waiombee miito, tukikaribisha na kuchambua wanaojisikia wito ili tuwatagemeze waitikie vizuri, tukionyesha kwa matendo ubora wa kuishi na Yesu na tukitambulisha karama yetu.

2.2.3. Kila wito ni mwaliko maalumu wa Mungu kwa mtu fulani ambao unaleta furaha na tumaini kwake na kwa jamaa, na kudai zifanyike juhudi mpya uweze kustawi kwa uaminifu wa wote.

2.2.4. Padri au shemasi asipokewe kabla mtumishi hajashauriana na askofu wake; aliyewahi kuwa mtawa au mseminari asipokewe pasipo taarifa ya mkuu wa shirika au gombera wa seminari husika.

2.2.5. Wafuatao hawawezi kabisa kupokewa: wenye umri chini ya miaka 18; wasiopata ubatizo, kipaimara na ekaristi; wasio ndani ya ushirika kamili wa Kanisa; wanaoingia utawani kwa kulazimishwa au kwa hofu kubwa au kwa udanganyifu; wanaopokewa na mtumishi kwa misingi hiyo; wenye madeni yanayowashinda; wenye mwenzi wa ndoa; wenye nadhiri za kitawa na wanashirika wa aina nyingine; waliowahi kuwa na ahadi ya daima katika jamaa yoyote ya utawa watu.

2.2.6. Ni lazima hatua za kuingizwa katika maisha yetu, ambazo ni utakaji, zoezi na uchipukizi, zifanyike chini ya walezi, ambao wawasaidie ndugu wapya kupata kwa taratibu ujuzi na mang’amuzi vinavyohitajika ili waendelee na safari ya kiroho kwa uhuru wa ndani ulio mkubwa zaidi na zaidi.

2.2.7. Kumrudisha nyumbani mtakaji na mwanazoezi asiyefaa ni juu ya mtumishi tu, ila kwa sababu nzito za haraka ni pia juu ya mlezi akiwa na kibali cha halmashauri ya jumuia husika.

 

 

2.3. MALEZI KWA JUMLA

 

2.3.1. Tangu mtu aingie utawani hadi kufa kwake anahitaji malezi ya Kifransisko kamili iwezekanavyo kuhusu utu, Ukristo, utawa na umisionari, ili asaidiwe kushiriki upendo wa Yesu hata msalabani kwa tumaini la kutimilika kabisa katika ufufuko.

2.3.2. Papo hapo malezi yanalenga kumfikisha kwenye ukomavu wa kibinadamu kama msingi ambao umwezeshe kujenga utawa, Kanisa na jamii.

2.3.3. Wakimtegemea Roho Mtakatifu, aliyetumwa kuwa mtendaji mkuu wa malezi, wahusika wote, yaani ndugu wenyewe waliopokea wito, baraza na halmashauri ya jamaa, walezi na viongozi wa kiroho, tena jumuia nzima, wawe na nia moja na moyo mmoja, wakishiriki vizuri kwa kuwajibika.

2.3.4. Wenyewe wajitahidi mfululizo kuitikia wito na kutumia vema misaada wanayopewa ili kulingana na Yesu, katika nafasi muhimu za maisha na katika zile za kawaida, katika utamu na ugumu wa kuishi pamoja na katika juhudi za kitume.

2.3.5. Ingawa maisha na malezi yetu yanategemea na kulenga moja kwa moja tuambatane naye kuliko kufuata mwongozo wenye vipengele vingi, hata hivyo baraza liandae mpango mzuri kwa kazi hiyo yote ambao utimilizwe na maandishi mengine maalumu kwa kila hatua na nyumba ya malezi.

2.3.6. Utekelezaji wake uhesabiwe na baraza kuwa ndio wajibu wake wa kwanza, hasa kwa kuwaandaa katika kila jamaa ndugu wa kutosha kwa kazi hiyo muhimu kama nini ya kuwalea na kuwafundisha wenzao.

2.3.7. Halmashauri ya jamaa inapowatuma ndugu kuanzisha jumuia katika nchi nyingine ihakikishe baadhi yao wafae kuwa walezi.

2.3.8. Wajue vizuri hasa njia ya Mungu ili kuweza kuwaongoza wale waliokabidhiwa na jamaa; halafu wasilemewe na kazi mbalimbali wasije wakashindwa kuwashughulikia ipasavyo.

2.3.9. Wawaonyeshe vizuizi vya wazi na vilivyofichika, haja ya kujikaza mfululizo, lakini hasa uzuri wa lengo na thamani ya karama inayofikisha huko.

2.3.10. Walau katika nyumba za utakaji, zoezi na uchipukizi, halmashauri ya jamaa iwateue pia wale wanaofaa zaidi kuwa vyombo vya Mungu kwa uongozi wa kiroho, kutokana na uzoefu wao wa kusikiliza Neno lake, kutumia vipaji vya Roho Mtakatifu na kufanya utambuzi.

2.3.11. Wanajumuia wengine wanapaswa kuwasaidia ndugu wapya kwa kuwapokea kwa upendo, kuwaombea na kuwatolea mifano bora.

 

 

2.4. UTAKAJI

 

2.4.1. Utakaji lengo lake ni kuziba mapengo ya malezi ya awali ya mtu ili wito wake uweze kueleweka, naye akiendelea nasi aifaidi hatua ya zoezi.

2.4.2. Mbali ya muda unaotumika pengine kufuata masomo kwenye shule na vyuo mbalimbali, mtakaji aishi katika jumuia zetu kati ya mwaka mmoja hadi mitatu.

2.4.3. Wakati huo ajichunguze na kuchunguzwa kuhusu ukomavu wa kibinadamu na wa Kikristo, yaani ushirikiano wa kidugu, bidii ya kufanya kazi, msimamo wa kijinsia na wa kimapenzi, imani halisi ya Kikatoliki, juhudi za kiroho na hamu ya kuokoa watu.

2.4.4. Baada ya kuvumbua maana ya utawa na aina zake, mtakaji aiombe kwa maandishi halmashauri ya jamaa husika aanze zoezi la kujipatia mpaka ndani sura hiyo.

 

 

2.5. ZOEZI

 

2.5.1. Katika mazingira ya imani, sala na kuhudumiana kidugu, wanazoezi wajifunze elimu ya upendo ili kuwa na msimamo uleule wa Yesu: kujikana kwa furaha na kuwa wanyenyekevu na wapole kwa wote na katika hali yoyote.

2.5.2. Wasaidiwe kufanya hivyo kwa mafundisho ya Kikristo na ya Kifransisko, na hasa kwa maongezi ya binafsi na mlezi, kusudi watambue wanavyopendwa jinsi walivyo, pamoja na wanavyoweza kukomaa.

2.5.3. Zoezi hilo linachukua miaka mitatu, ila kama pengine utahitajika mwaka wa nne uongezwe.

2.5.4. Mwaka wa pili mtumishi, kwa ombi la mlezi, anaweza kuwapeleka wanazoezi wakaishi kijumuia sehemu nyingine, au anaweza kuwaruhusu wauruke wakikusudia kuweka ahadi ya muda.

2.5.5. Kwa vyovyote katika hatua hiyo utiliwe mkazo juu ya kusali na kutafakari kama Yesu alivyofanya Nazareti alipojiandaa kujitoa kabisa kwa Baba ili kuondoa dhambi ya ulimwengu.

2.5.6. Miezi mitatu hivi kabla muda wa zoezi haujaisha, kila mmoja aiombe kwa maandishi halmashauri ya jamaa aweke ahadi kwa siku zote za maisha yake au kwa muda usiopungua mwaka.

2.5.7. Kisha kupata taarifa ya mlezi ikiwa ni pamoja na maoni ya jumuia, halmashauri hiyo ijadili ombi hilo na kulipigia kura za siri, ikizingatia kama kuweka ahadi kutamsaidia mwanazoezi kupenda zaidi au kutamuelemea.

2.5.8. Mwanazoezi akikubaliwa, kabla hajaweka ahadi ya muda amuachie mtu yeyote kusimamia na kufaidi mali zake binafsi, pia aandike wasia wake; baada ya hapo atahitaji sababu zinazoeleweka na ruhusa ya mlinzi ili kubadili alivyoviamua.

 

 

2.6. KUWEKA AHADI

 

2.6.1. Siku ya kuweka ahadi, mhusika awe ametimiza miaka 23 na kushauriana na ukoo wake walau kwa njia ya barua; kwa ahadi ya daima awe amepata kibali cha ndugu zake wanaohusika zaidi.

2.6.2. Wakati wa Misa atimilize ahadi za ubatizo kwa kujifunga hadharani kushika Injili kijumuia kadiri ya Kanuni na Maisha ya Ndugu wa Kiume na wa Kike wa Utawa Hasa wa Tatu wa Mtakatifu Fransisko, iliyokubaliwa na papa Yohane Paulo II, na kadiri ya katiba hii.

2.6.3. Ahadi hiyo kwa Mungu haimwajibishi aliyeiweka tu, bali pia jamaa iliyoipokea kwa niaba ya Kanisa, kuhusu kuyafikia malengo ya wito wake, hasa kwa kumpatia mazingira na malezi ya kufaa.

2.6.4. Kwa kuweka ahadi ya muda tunataka kufuata njia ya upendo kamili bila ya vipingamizi kusudi tuungane zaidi na Yesu ili azae matunda mengi ya utakatifu ndani mwetu; vilevile tuungane zaidi na Kanisa na umisionari wake kadiri ya wito wetu.

2.6.5. Ahadi ya muda inaweza kurudiwarudiwa bila ya mwisho: pia inaweza kuwa nafasi ya kukomaa ili baadaye tujitoe mpaka kufa.

2.6.6. Atakayeweka ahadi ya daima baada ya kuweka ile ya muda ili ajiaminishe kwa Mungu kama sadaka ya kuteketezwa kwa wokovu wa watu wote, ajiandae kwa miezi miwili ya kukusanya mawazo na kusali kama Mitume walivyojiandaa kumpokea Roho Mtakatifu awafanye mashahidi wa Kristo mpaka mwisho wa dunia.

2.6.7. Kwa ahadi ya daima tunaitikia kwa moyo usiogawanyika upendo wa Mungu Baba, kwa mfano wa Mwanae aliyependa upeo na kwa karama maalumu ya Roho Mtakatifu; tunawekwa wakfu kwa namna mpya na ya pekee kwa njia ya Kanisa; pia tunapokewa na utawa moja kwa moja kama familia yetu mpya, na kujitoa kikamilifu kwake, tayari kutumwa kokote duniani.

2.6.8. Kabla ya kuweka ahadi ya daima ndugu aandike hati ya kujinyima moja kwa moja mali yoyote, kwa kupanga namna ya kuwagawia maskini vyote alivyo navyo na vile vitakavyopatikana baadaye kwa kurithi; hati hiyo iwe na nguvu kuanzia siku ya kuweka ahadi hiyo.

2.6.9. Mtu ambaye alimaliza zoezi au kuweka ahadi ya muda, halafu akaacha vilivyo utawa, akiomba kwa maandishi kupokewa tena, halmashauri ya jamaa ikimkubalia impangie muda na masharti ya jaribio, ambalo likienda vizuri imkubalie kuweka ahadi ya muda, baadaye akipenda ile ya daima.

 

 

2.7. UCHIPUKIZI

 

2.7.1. Miaka mitatu inayofuata zoezi itumike kuendelezea malezi kuhusu Neno la Mungu na maisha ya kiroho, pamoja na ndugu kuzoea polepole kazi mbalimbali ndani na nje ya jumuia.

2.7.2. Hizo zipangwe na kutekelezwa hasa kwa manufaa yao, si kulingana na mahitaji ya sasa hivi ya jamaa au ya watu wa nje, wasije wakalemewa.

2.7.3. Mwelekeo wa sala na toba utawale hatua hiyo pia, ili wazidi kujitoa kwa upendo kadiri ya ahadi yao, na kujiandaa kukabili yale yote yatakayoweza kutokea maishani, hasa katika mazingira magumu.

2.7.4. Ihakikishwe kuwepo kwa nyakati maalumu za watawa chipukizi kukaa faraghani ili kusali, kutafakari na kuchimba mafundisho waliyoyapata.

 

 

2.8. MALEZI MAALUMU

 

2.8.1. Mungu ameunda utawa watu naye anaufanya upya siku kwa siku kwa kutuangazia tuyashike maisha ya Kiinjili ya Kifransisko, ambayo ni lengo kamili tena ni lazima liwe la kwanza kwa yeyote anayejiunga nasi.

2.8.2. Pamoja na hayo, ikiwa ndugu ameitwa kweli awe pia padri au shemasi au kutoa kuduma nyingine ya Kikanisa, mtumishi ampatie malezi yanayotakiwa awe mhudumu kadiri ya moyo wa Mungu, aliye tayari kumwakilisha Kristo kwa uaminifu na ukarimu; uamuzi wa mwisho ni juu ya askofu, lakini daraja inakusudiwa kutolewa kwa maisha na umisionari wa utawa wetu, sio kwa ajili ya jimbo lake tu.

2.8.3. Vilevile ikihitajika mmoja wetu akasome fani fulani, halmashauri ya jamaa imteue ndugu ambaye kwa ukomavu wake anatumainisha kwamba ataendelea kuwa kielelezo cha wito wetu.

2.8.4. Chini ya mlezi hao wote wakabili matatizo ya kipindi cha masomo, wakiangalia hasa yasidhuru roho ya ibada na sala, wala yasiwavimbishe, bali yawaongoze kumshiriki zaidi Mungu anayejifunua kwa wadogo, na yawaandae kuwahudumia watu vizuri zaidi.

 

 

2.9. MALEZI YA KUDUMU

 

2.9.1. Utawa unapaswa kuwasaidia ndugu wote kwa mwendo wake wa kila siku na pia kwa njia ya kozi, semina, mikutano na mang’amuzi mbalimbali ili wito wao wa Kifransisko ustawi mfululizo na utume wao ufae daima katika mabadiliko ya mazingira.

2.9.2. Kila mmoja wetu, kadiri ya uwezo na majukumu aliyonayo, awajibike kujiendeleza katika yale yanayomhusu, kwanzia maisha ya kiroho ambayo ni ufunguo wa malezi yote kwake na kwa wengine.

2.9.3. Tuamini kuwa Mungu Baba anailisha familia yake kwanza kwa Maandiko Matakatifu, ambamo anaongea nasi mfululizo ili kutuingiza katika ushirika naye na kutujulisha matakwa yake kwa maisha yetu.

2.9.4. Kila siku tushike mikononi Biblia takatifu, tukilenga kwa unyenyekevu kuielewa kulingana na imani ya Kanisa na mazingira yetu, ili tumfahamu Kristo ambaye ndiye Neno.

2.9.5. Halafu tupendelee kusoma maandishi ya Ualimu wa Kanisa, ya mababu wake, ya walimu wakuu wa maisha ya kiroho na habari za watakatifu, hasa Wafransisko, tukijitahidi kutekeleza.

2.9.6. Tushibe hayo kwa pamoja walau mchana au jioni tunapolisha miili yetu, isipokuwa kwenye Jumapili, sherehe na nafasi nyingine za kufaa.

2.9.7. Kwa mwanga huo wa Kiinjili Roho wa hekima atatuwezesha kutambua hali ya ulimwengu na dalili za nyakati zetu, kuchambua yanayotokana naye na yanayopingana naye, na kufurahia jinsi Baba anavyoongoza yote ili mabaya pia yaweze kuleta mema.

2.9.8. Tutatambua pia tukabili vipi matukio yoyote, kwa kumtumainia kama kwamba yote yanamtegemea yeye tu, na kwa kuwa kuwajibika kama kwamba yote yanatutegemea sisi.

2.9.9. Kwa ajili hiyo, vitabu na magazeti machache vyenye msimamo wa Kikatoliki kweli viwepo tayari kwa faida ya wote.

 

 

2.10. UAMINIFU

 

2.10.1. Kila mtawa wetu ana wajibu na haki ya kutimiza wito wake, na kushiriki katika maisha na utendaji wa jamaa na ngazi zake, kadiri ya katiba hii.

2.10.2. Adili la ibada na amri ya kwanza ya Mungu vinatudai tutekeleze yale tuliyomuahidia ili kumuonyesha heshima na upendo inavyotupasa.

2.10.3. Ili tutamani zaidi kufanya hivyo na kuwajibika kulingana na sheria ya moyoni, ambayo ni Roho Mtakatifu mwenyewe, kila siku tusome kwa pamoja sehemu ya katiba; halafu mara moja kwa mwezi turudie ahadi yetu baada ya kusoma kanuni nzima, onyo na laana vya mtakatifu Fransisko.

2.10.4. Tujiombee neema za kuzishika, tuzitafakari mara nyingi na kuziongelea katika mikutano yetu, ili zipenye zaidi na zaidi maisha ya kila mmoja na ya jumuia nzima na kutusaidia kulenga utakatifu na kufanya utume anavyotutaka Mungu.

2.10.5. Kwa uaminifu wake yeye hawezi kughairi kuhusu wito bora aliotujalia; vilevile sisi tuwe waaminifu kwake tukitegemea neema tusiyoweza kupungukiwa, mradi tukeshe na kusali pasipo kuchoka.

2.10.6. Kwa hakika kizo tupige mbio kwenye njia nyembamba ya uzima, ili kujinyakulia taji lisiloharibika, tukijua wengi wanaingia uwanjani bila ya kufanikiwa.

2.10.7. Tujihadhari na uvuguvugu ambao ni mwanzo wa uasi, tena tusifuate mitindo ya ulimwengu, bali tuzidi kujitoa kama sadaka hai, takatifu na ya kumpendeza Mungu.

2.10.8. Kanzu tunayoivaa usiku na mchana, na mtindo wetu wa kifukara kwa jumla, vimekusudiwa kutusaidia tudumu katika wito wetu, halafu kushtua na kufikirisha watu.

2.10.9. Hivyo tusivionee aibu ila tuangalie moyo wetu ulingane na sura ya nje kadiri inavyoonyesha unyenyekevu na usafi.

 

 

2.11. KUTENGANA NA UTAWA

 

2.11.1. Ndugu mwenye ahadi akiwa na shida anaweza kuomba kwa maandishi muda wa kujitenga na jamaa; baada ya mtumishi kuongea naye na kumpa nafasi ya kufikiri, halmashauri ya jamaa ikate shauri kwa upendo na busara, ambalo liandikwe katika rejesta na kuarifiwa kwa ndugu mhusika; hapo haki na wajibu vilivyotokana na ahadi yake vinasimamishwa, isipokuwa haruhusiwi kufunga ndoa; muda aliopangiwa ukiisha anaweza kuomba apokewe tena; asipoomba au asipokubaliwa, atoke moja kwa moja utawani inapoelezwa hapa chini.

2.11.2. Muda wa ahadi ukiisha, ndugu ana hiari ya kuacha utawa, na vilevile halmashauri inaweza kumkatalia asiirudie au asiweke ahadi ya daima zikiwepo sababu zenye msingi.

2.11.3. Mwenye ahadi ya daima ambaye kwa sababu nzito anataka kuacha utawa, kisha kushauriana na mtumishi wake, amuombe askofu wa jimbo anamoishi kitawa, ambaye anaweza kumruhusu kwa kuwasiliana na halmashauri ya jamaa.

2.11.4. Ndugu ambaye ameasi kabisa imani au amejitenga au ametengwa rasmi na ushirika kamili wa Kanisa au ametoroka utawani, amepoteza papohapo kazi alizokuwanazo utawani na haki zake kama mwanajumuia; mtumishi ajitahidi kumrudisha kwa kuwa anapaswa bado kutimiza ahadi yake; ikishindikana amtumie barua ya tahadhari kwamba ataondoshwa, ambayo isipoleta mafanikio baada ya mwezi mmoja halmashauri ya jamaa imuondoe rasmi; aliyeachishwa anaweza kumkimbilia askofu wa jimbo alimokuwa anaishi kitawa, na hivyo kusimamisha utekelezaji wa uamuzi huo, mradi asichelewe zaidi ya siku kumi baada ya kuarifiwa.

2.11.5. Kwa sababu nyingine nzito, wazi, zenye dhambi na thibitisho, zilizoorodheshwa katika sheria zetu ndogondogo, mtumishi afungue kesi mbele ya halmashauri yake, akimpa mhusika nafasi ya kujitetea, halafu awasilishe hati zote kwa askofu wa jimbo anamoishi kitawa ili aondoshwe.

2.11.6. Aliyetengana moja kwa moja na utawa kwa namna yoyote ile, hana tena wajibu na haki vilivyotokana na ahadi yake, wala hawezi kudai chochote kwa kazi alizozifanya utawani.

2.11.7. Upande wake jamaa iwajibike kutumia upendo na usawa kwa ndugu yeyote aliyeiacha, hasa kwa aliyekaa muda mrefu, ikimsaidia kukabili maisha na kuendelea katika safari ya kiroho.

 

 

2.12. BIKIRA MWAMINIFU

 

2.12.1. Kisha kumfuata Yesu mpaka Kalivari, Maria alituzaa kwa uchungu na kufanywa na Mwanae kuwa mama wa kila mmoja wetu, hasa wa wale aliowapenda zaidi.

2.12.2. Toka mwanzo wa kukaa utawani tumpokee upya kama mama tukimpenda na kumuiga, tukimfunulia siri za maisha yetu na kumuomba atulee kama alivyomlea Yesu.

2.12.3. Kwa hisani yake atatushirikisha upendo ule unaowezesha kumtolea Mwanae maisha yote bila ya kujitwalia tena hata chembe; kujiaminisha kwa Baba na kwa matakwa yake hata msalabani; halafu kufurahia maajabu anayotutendea kwa Roho Mtakatifu.

2.12.4. Furaha hiyo kudumu katika majaribu kutahakikisha ubora wa kuishi kwa ajili ya Mungu tu, kutavuta miito mingine, na kuuelekeza ulimwengu njia za kugeuka sura uwe ufalme wake.

 

 

 

3.KUMUONEA KIU MUNGU

 

3.1.MUUNGANO NA MUNGU

 

3.1.1. Kwa kuwa Yesu alidumu moja kwa moja katika muungano wake na Baba, aliingiza duniani ile ibada kamili katika Roho na ukweli inayompendeza.

3.1.2. Mwenyewe anaendelea kufanya hivyo kwa njia ya Kanisa lake, akitupelekea Roho Mtakatifu atusaidie sisi viungo vyake katika udhaifu wetu, na kutuongoza hata hali ya juu ya muungano na Mungu, kama alivyomjalia Fransisko, mtu aliyefanyika sala, ambaye alikuwa akimuona Mungu ndani ya vyote na vyote ndani ya Mungu.

3.1.3. Kwa kuwa tumeitwa kufuata nyayo zake, tuchague kile ambacho peke yake ni cha lazima: kumjua kweli Yesu anayetuvutia kumpenda na kumtangaza ulimwenguni kote, kwa kuwa ni mzuri kuliko wanadamu wote na hakuna mwingine aliyewahi kusema vema kama yeye.

3.1.4. Katika sala tuzingatie hasa alivyojishusha kwa ajili yetu, akikabili magumu yoyote hadi kilele cha maisha yake msalabani, ambapo upendo wa moyo wake safi ulifikia upeo, ufukara wake ulikuja kukosa yote kabisa, na utiifu wake ulijitoa mhanga.

3.1.5. Sala zetu zote zilingane na liturujia, zitokeze karama ya udugu na udogo, na kuzilisha roho zetu kwa mapokeo bora ya Kifransisko.

3.1.6. Tunasali kweli kama ndugu tukiwa roho moja na mojo mmoja: na kama wadogo tukishiriki hali ya wanaodhulumiwa na kumlilia Mungu usiku na mchana awapatie upesi haki zao.

3.1.7. Tuwaombee wenzetu wote, wazima na wafu, pasipo kubagua maadui, kwa kuwa nguvu ya sala ni upendo.

3.1.8. Tuwavute waamini kwenye maji hai ya sala ili maisha yao ya kiroho yastawi kweli, kwa kuwa anayesali ataokoka, lakini asiyesali atapotea kwa sababu anabaki pweke na unyonge wake.

 

 

3.2 LITURUJIA

 

3.2.1. Sala, ambayo ni pumzi ya roho zetu na ya jumuia pia, kiini chake kiwe liturujia, na hasa ekaristi, kwa kuwa ndimo kazi ya wokovu inamozidi kutendeka.

3.2.2. Upande wetu liturujia ni jibu la kijumuia kwa Mungu, kilele cha utendaji wa Kanisa na chemchemi ya uwezo wake wote.

3.2.3. Ukweli wa maneno hayo unategemea jinsi imani inavyozingatia mafumbo yanayoadhimishwa; pia unachangiwa na ubora wa ibada.

3.2.4. Mtindo mwepesi wa Kifransisko unaosisitiza upendo kuliko fahari za ibada, uendane daima na heshima inayodaiwa na kazi hiyo ya Kimungu.

3.2.5. Kwa kuwa liturujia ndiyo uwanja wa kwanza wa urekebisho na utamadunisho wa Kanisa, tutie maanani uzuri wa ishara zake mbalimbali, tukihusisha mwili na hisi zake; tufanye mabadiliko yale yanayokubalika na kutumia nafasi za kimya; tuimbe kwa moyo na sauti, tukipiga ala zetu za muziki za kuadhimishia ushindi wa uzima dhidi ya mauti.

3.2.6. Kila siku tushiriki kijumuia sadaka ya Misa au walau meza ya ekaristi, ambapo tujitoe kabisa kwa Yesu anayejitoa kwetu kwa upendo mnyenyekevu, ili tupate nguvu mpya za kumtumikia maishani.

3.2.7. Kwa ajili hiyo tujiandae kwa makini, halafu tukae tukimshukuru kwa muda usiopungua dakika ishirini, ili tuimarishe muungano wetu naye.

3.2.8. Zaidi tena, matunda tunayoweza kuchuma humo yanategemea usafi wa upendo wetu; basi, tuadhimishe kwa imani na unyofu sakramenti ya upatanisho kila baada ya wiki moja au mbili, ili kutengeneza upya roho na jumuia zetu.

3.2.9. Ili maisha yetu yote yawe wimbo wa kushangilia uzima mpya tuliojaliwa, mwendo wa kila siku wa jumuia zetu zote uongozwe na maadhimisho ya pamoja ya vipindi vyote vya Sala ya Kanisa vinavyompasa padri.

3.2.10. Tusali kila kipindi kwa wakati wake na kuamka usiku wa manane kwa Kipindi cha Masomo.

3.2.11. Tunatakiwa kusali kila mtu peke yake vipindi vile ambavyo tumeshindwa kuviadhimisha pamoja na ndugu zetu.

3.2.12. Hivyo tutakuwa mfano wa Kanisa ambalo linamsikiliza Mungu na kufanya ukumbusho wa fumbo la wokovu, likimsifu na kumuomba kwa umoja kwa ajili ya wote.

 

 

3.3. SALA YA MOYO

 

3.3.1. Katika kushiriki kabisa liturujia tujifunze kustawisha zaidi na zaidi uongofu wetu na sala ya moyo.

3.3.2. Tusali hivyo kwa pamoja kila siku, tukiwa na Yesu ekaristi ili tulingane na mawazo ya moyo wake.

3.3.3. Katika kuongea na Baba kama watoto tutamani kuwaka kwa upendo wake kuliko kuangaziwa tu maneno na matendo aliyojifunua kwetu.

3.3.4. Tumtegemee kama maskini Roho Mtakatifu na kujitahidi ili nafasi hizo zifanikiwe kabisa, lakini tukipatwa na majaribu yoyote tusikate tamaa, kwa sababu tunaamini kuwa tukidumu kwa uaminifu tunaupokea vilevile upendo wa milele unaotufinyanga kimyakimya.

3.3.5. Pengine, badala ya kunyamaza, tutamke kwa sauti yale yanayotutoka moyoni kumuelekea mpenzi wetu ambaye amekuwa kwetu hekima, uadilifu, utakatifu na ukombozi.

 

 

3.4. MATENDO YA TOBA

 

3.4.1. Ili tuwe watu wapya, wenye uhuru wa ndani na amani ya kweli katika kuungana na Mungu, ni lazima tujifahamu na kujitawala, kutambua jinsi dhambi zinavyomchukiza, kutubu kwa moyo na kuzaa matunda ya toba katika maisha ya kila siku.

3.4.2. Katika kupanga juhudi zetu, badala ya kujitafutia msalaba unaotupendeza, tuweke mbele kutekeleza amri ya upendo kwa wote, kuwajibika kadiri ya ahadi yetu, kufanya kazi kwa uaminifu, kupokea kwa furaha kamili matatizo ya maisha: usumbufu wa mazingira, ugonjwa na uzee, misiba na vishawishi, masikitiko yanayosababishwa na wenzetu, na hasa dhuluma kwa ajili ya Kristo.

3.4.3. Kwa kuwa ni lazima sisi watawa tujikaze kuliko waamini wengine, tena kwa pamoja, mbali ya kushika siku za toba walivyoagizwa hao pia, tufunge chakula mchana Kwaresima nzima; halafu kila Ijumaa ya mwaka tufunge chakula na kujinyima nyama na vingine vya gharama; isipokuwa siku za sherehe na Jumapili hatulazimiki.

3.4.4. Kwa njia hiyo aliyoifuata Kristo mwenyewe kisha kutumwa rasmi na Baba, akisukumwa na Roho Mtakatifu kushindana na Ibilisi, roho zetu zinakuwa wazi zaidi kwa Mungu na kwa jirani, na kupata nguvu za kushinda mwili, ulimwengu na shetani.

3.4.5. Ili tuwe daima na kiasi, tule vya kutosheleza mahitaji ya mwili tu, sio vya anasa na kunoga mno; nje ya vipindi vitatu vilivyopangwa kwenda mezani tusile wala tusinywe kinywaji isipokuwa maji.

3.4.6. Tukimkumbuka aliyekosa pa kupumzikia, tutumie kilalio kigumu hafifu, isipokuwa katika ugonjwa.

3.4.7. Ili kudumisha juhudi zetu tufanye kila siku malipizi ya hiari pia, kufuatana na shauri la kiongozi wa kiroho na pengine kwa ruhusa ya mlinzi.

3.4.8. Tuitunze afya tuliyojaliwa na Mungu ili tufanye kazi katika shamba lake; ila tusiihangaikie mno, kwa sababu tunapaswa kuzingatia kwanza mengine yaliyo muhimu zaidi na ya milele; na kwa sababu tunaamini mateso yakipokewa kwa upendo yanatuunganisha kabisa na Yesu katika kazi ya ukombozi na kuleta uzima tele.

3.4.9. Tujiandae kufa katika Bwana saa na namna atakazopenda, kama tendo la mwisho la toba yetu hapa duniani.

 

 

3.5 UTULIVU

 

3.5.1. Ili tumsikilize kwa makini Mungu kila anapopenda kusema nasi, na kuungana zaidi naye anayeishi ndani mwetu, tunahitaji tusivurugwe na lolote lile moyoni.

3.5.2. Kusudi makazi yetu yatusaidie kufikia hali hiyo ya ndani, tujitafutie mazingira ya utulivu halisi na kuyalinda kwa ushirikiano wa wote.

3.5.3. Kwetu tuseme kwa shida maalumu tu na kwa sauti ya chini, halafu tunyamaze kabisa katika vipindi na mahali mbalimbali kadiri ya sheria zetu ndogondogo, kwa kuwa hata upendo unatudai tusiwasumbue wanaohitaji kimya ili kusali, kusoma na kupumzika vizuri.

3.5.4. Tumkaribishe mgeni kwa ukarimu wote, tukimtumikia Yesu katika kila anayepiga hodi, lakini mapokezi hayo yasituhangaishe hadi kuzuia muungano wetu naye, taratibu za jumuia na utekelezaji wa wajibu.

3.5.5. Kwa kawaida mgeni asiingizwe ndani kabisa ya makazi yetu, isipokuwa aliyekubaliwa kufanya mafungo kwetu.

3.5.6. Tukwepe urafiki wenye maneno mengi mno; tusikae muda mrefu sebuleni, hasa jumuia inaposali; tusitoke nyumbani bila ya lazima na ya ruhusa ya mlinzi.

3.5.7. Mikutano ya jumuia itathmini na kulenga maendeleo ya maisha ya sala ili tusaidiane na kukomaa pamoja.

 

 

3.6. NAFASI ZA PEKEE

 

3.6.1. Kulingana na watu, wakati, mahali na kazi maalumu, kila jumuia ipange ratiba ya kila siku ambayo iidhinishwe na mtumishi, zikiwemo walau dakika 250 za sala za pamoja, halafu nafasi fulani huru kwa ndugu binafsi.

3.6.2. Mbali ya ratiba hiyo, zipangwe nyakati maalumu za kukaa na Bwana tu, ambazo kadiri tunavyoishi kati ya watu zinahitajika ili zisafishe na kuimarisha upendo wetu.

3.6.3. Walau tufanye mafungo ya siku moja kila mwezi, na mazoezi ya kiroho ya wiki moja kila mwaka; kwa kawaida tufanye hivyo kijumuia.

3.6.4. Miaka kumi hivi baada ya kuweka ahadi ya kwanza, kila ndugu aruhusiwe kutumia mwaka mzima katika mazoezi ya sala na toba tu, akiacha kazi maalumu na madaraka yoyote ndani na nje ya jumuia.

3.6.5. Katika safari ya kumuendea Mungu tuweze kupewa mida mingine mirefumirefu ya kukaa naye jangwani, kwa mfano baada ya miaka kadhaa ya kuishi sehemu fulani au kushika kazi fulani.

3.6.6. Katika bara la Afrika ulipoanza umonaki, tuheshimu sana maisha ya kuzama katika sala, ambayo yanadokeza kwa namna ya pekee uzima wa milele, Utatu mtakatifu utakapokuwa heri yetu kamili kabisa.

3.6.7. Kwa kuwa hata majimbo machanga yanahitaji mtindo huo wa maisha unaokamilisha Kanisa, tupokee kwa furaha miito ya namna hiyo ikijitokeza kati yetu kulingana hasa na kanuni iliyoandikwa na mtakatifu Fransisko kwa makazi ya upwekeni, au ile ya mtakatifu Klara.

3.6.8. Hasa bibiarusi kujifungia moja kwa moja mahali fulani ni njia maalumu ya kufia ulimwengu ili kukumbatiana na Bwana mpenzi kwa niaba ya watu wote na kuwavuta wamtafute kwa moyo wao wote.

 

 

3.7.BIKIRA WA KIMYA

 

3.7.1. Kwa nia ya kufanana na Bikira Maria, kielelezo cha wanasala, tutamani kutakaswa na kimya ili tuwe tayari kupokea Neno la Mungu na paji la Roho Mtakatifu kwa moyo usio na umimi.

3.7.2. Tufuate kwa bidii himizo la Kanisa la kustawisha ibada, hasa za liturujia, kwa Mama Maria.

3.7.3. Kila siku tusali kijumuia Malaika wa Bwana mara tatu na thuluthi ya rosari, au kufanya ibada nyingine ya Kimashariki.

3.7.4. Kutoka kwa Maria tutajifunza kuzingatia kwa imani na kutimiza maishani mafumbo ya Mwanae, hasa fumbo kuu la Pasaka, upendo wa Mungu ulipofurika ulimwenguni.

3.7.5. Tukiungana na Mama wa Yesu katika sala, kama walivyofanya Mitume kabla ya Pentekoste, tumuombe Roho Mtakatifu aufanye uso wa dunia uwe mpya, kuanzia mioyo yetu.

 

 

 

4. KUZAA KWA KUPENDANA NA MUNGU TU

 

4.1. KARAMA YA USEJA

 

4.1.1. Wakati ule maalumu ulipotimia, Yesu mwenyewe alikuja kufunua jinsi Baba anavyoupenda ubikira au useja uliotunzwa kwa ajili ya utawala wake, akampamba bibiarusi wake kwa karama hiyo ya Roho Mtakatifu ambayo inafanya upendo wake uonekane wazi na kustawi na kuzaa sana.

4.1.2. Usafi katika useja unatusaidia kuungana na Bwanaarusi pekee kwa kushiriki zaidi sala yake ya kudumu, maisha yake na Mitume na kazi yake ya wokovu, aliposhughulikia matakwa ya Baba bila ya kizuio chochote, akitangaza ukweli na haki pasipo hofu kwa familia yake, akiwapenda wote upeo, badala ya kujipendea na kuwapenda baadhi ya watu tu.

4.1.3. Kwa hiyo sio mzigo unaotulemea, bali ni fumbo la upendo na shauri la Kiinjili tulilojaliwa kulielewa na kulipokea kwa furaha na moyo mkuu kusudi litupenye mpaka moyoni tuje kufanana na Yesu kama ilivyomtokea mtakatifu Fransisko.

4.1.4. Katika kutoa ushuhuda huo wa pekee wa uzima wa milele na wa kuwa Mungu anatutosha kuanzia hapa duniani, tusijiamini kipumbavu bali tutegemee msaada wake pamoja na kufuata masharti na kukwepa hatari.

 

 

4.2. UPENDO WA MOJA KWA MOJA

 

4.2.1. Useja uliowekwa wakfu kwa Mungu ni hali bora kuliko ule usafi wa moyo unaowapasa wote; tena kwa uzuri unapita ndoa ya Kikristo, kama vile tumaini la ufufuko lilivyo kuu kuliko matazamio yoyote ya binadamu katika maisha haya.

4.2.2. Ukweli wake ni kuzidi kuchanganyikiwa na upendo wa Mungu na kung’amua kwa imani jinsi anavyotaka tumrudishie, tukishiriki kabisa maisha ya Yesu mpaka mwisho alipojitoa sadaka, yeye aliye mpenzi mkuu asiyependwa na watu.

4.2.3. Kwa vile unatokana na upendo wa pekee na kuelekea matendo ya upendo mkarimu usio na ubaguzi, useja mtakatifu unalishwa na upendo, hasa kwa kupokea sakramenti ipasavyo, kujenga jumuia kama familia bora, na kujiwekea malengo makubwa ya kitume.

4.2.4. Kwa kuwa unadai usafi kamili wa mwili na wa roho, pamoja na kujinyima upendo wa ndoa na uzazi wa kibinadamu, unamtaka mtu ajitahidi moja kwa moja kutekeleza tunu za jinsia yake kwa namna bora isiyotegemea mwili, ila kule kujitoa kwa upendo ambako ndiko ukuu wa binadamu.

4.2.5. Usipohuishwa na kukomazwa mfululizo, unaweza ukaharibika upesi kutokana na matatizo mapya ambayo yanazuka maishani katika hatua za mbele hata kufanya uaminifu kwa ahadi uwe mgumu, kama vile inavyotokea kwa watu wa ndoa ingawa wana sakramenti iliyowaunganisha.

4.2.6. Hapo mtu anabaki hana kitu: wala upendo, wala ukomavu, wala uzazi wa kiroho au wa kimwili.

 

 

4.3. TAHADHARI

 

4.3.1. Maisha yanaonekana ni vita vya kiroho visivyo na mwisho vya kudumishia uhuru tuliojaliwa, kwa kuwa ushindi wa Kristo hauzimi kabisa tabia yetu mbovu inayotokana na dhambi asili, wala hautuepushi na vishawishi vya ulimwengu na utamaduni unaotawaliwa na yule mwovu.

4.3.2. Hasa adili la useja, ambalo si la kawaida hapa duniani, ni lazima lilindwe na nidhamu ya hisi na ya moyo, na maisha magumu ya kujinyima hata vitu halali, pamoja na kuepukana na uvivu, utengano wowote na vilevile urafiki usiofaa.

4.3.3. Toka mwanzo tuuzuie moyo wetu usimuelekee mtu yeyote kwa namna ya pekee, wala usijidanganye kuhusu hiyo sumu tamu kwa visingizio vya kutaka kumpa au kupata toka kwake msaada wa kiroho, kwa sababu shetani akijipatia unywele wetu mmoja anaufanya upesi kuwa boriti.

4.3.4. Tusisahau onyo la Mungu kwamba kushirikiana na watu wa jinsia ya pili bila ya kuvutiwa visivyo na maumbile yao ni jambo gumu sawa na kutembea juu ya moto bila ya kuungua nyayo.

4.3.5. Katika utawa wetu, mafungamano kati ya waseja wa kiume na wale wa kike yawe madogo iwezekanavyo, yakifanyika tu kwa njia ya ndugu wenye maadili imara walioteuliwa na baraza.

4.3.6. Kwa kufuata mfano wa Yesu na uongozi wa Roho Mtakatifu, katika mafungamano yoyote tuoanishe adabu na uangalifu, wema na busara, upole na msimamo, uhuru na usafi, tusije tukachafua kwa kitambo cha udhaifu uzuri wa moyo ulioambatana kabisa na Bwana.

4.3.7. Katika nyumba zetu watu wowote wa jinsia ya pili waruhusiwe kuingia tu kwenye kikanisa, vyumba vya wageni, na sebule, ambayo iwe imetengenezwa kwa busara sana.

4.3.8. Pamoja na kuuheshimu mwili kama zawadi ya Baba, kiungo cha Kristo na hekalu la Roho Mtakatifu, tutunze safi macho na mawazo vilevile.

4.3.9. Tusikubali hata kidogo aibu za ulimwengu ziingie ndani au kati yetu kwa vyombo mbalimbali vya upashanaji habari, kama vile magazeti.

4.3.10. Tuepuke maneno yasiyowafaa watu waliojiweka wakfu kwa Mungu, na matendo yanayoweza kuwatilia wengine shaka juu ya usafi wa maisha yetu, tukizingatia pia mwongozo ambao pengine umetolewa na askofu kwa makleri na watawa wa jimbo lake.

4.3.11. Tuwaonyeshe wote jinsi usafi wa moyo unavyowezekana na unavyochangia ukomavu wa binadamu, kwa sababu jinsia haitakiwi kuchezewa wala kuabudiwa, bali inakusudiwa kuwa njia ya upendo yaani kujitoa kwa jirani na kumpokea kwa heshima.

 

 

4.4 BIKIRA, MKE NA MAMA

 

4.4.1 Roho Mtakatifu aliweza kumfanyia kazi Bikira safi bila ya kuzuiwa naye hata kidogo, akamjalia kujaa upendo na kumzaa Bwana wa uzima.

4.4.2. Tutamani sana usafi huo ili Roho amtunge Neno ndani mwetu pia, tukamlete kwa wenzetu kama Maria alivyowaletea akina Elisabeti.

4.4.3. Mwishoni, tutoe ushuhuda kuwa wale wote waliompitia Maria kwa unyenyekevu na tegemeo katika kuomba neema ya usafi, wameona maombezi yake yalivyo na uwezo.

 

 

 

5. KUTUMIKIA NA KUFANYA KAZI

 

5.1. NEEMA YA KAZI

 

5.1.1. Yesu kwanza alifanya kazi kwa mikono yake, halafu akahubiri Injili na kusaidia wenye shida.

5.1.2. Hivyo alishiriki utendaji wa milele wa Baba yake katika kuumba, kudumisha na kukomboa ulimwengu, tena alizitia heshima mpya kazi zote za binadamu.

5.1.3. Sisi tunaotamani kukaa naye milele, tujiandae kukutana naye kwa kuwa sasa watumishi wema na waaminifu kwake, kwa Kanisa, kwa utawa wetu na kwa wenzetu wote.

5.1.4. Tukizitumia kwa faida talanta tulizokabidhiwa na Bwana, kwa mfano wa mtakatifu Fransisko, tusali pasipo kikomo, tutangaze Injili, tusaidie wenye tabu na kufanya shughuli nyingine pasipo uvivu wowote.

5.1.5. Tukiamini kuwa kazi ni wajibu na haki ya kila mtu ili apate maisha anayostahili, tutoe mchango wetu ili wote wapate nafasi hiyo, halafu utekelezaji wake uheshimu na kukamilisha utu wao.

5.1.6. Hivyo kwa maisha ya kila siku tutaonyesha shukrani kwa Muumba wetu na kumfuata Mwanae aliyekuja si kutumikiwa, bali kutumikia hata kutoa uhai wake.

 

 

5.2. KUOKOA MUDA

 

5.2.1 Kisha kupata hakika ya kuwa Mungu ametuchagua tupende, tusifu na kutumikia tu, tumejitolea muda anaotujalia usiwe mali yetu tena, bali wa kwake na wa wenzetu.

5.2.2. Tujitahidi kutumia kila dakika ya maisha yetu kwa utukufu wake na kwa maendeleo kamili ya binadamu, kwa kuwa ni nafasi ya kutenda mema ambayo haitarudi.

5.2.3. Tukijua wokovu unatujia kwa nyakati maalumu kadiri ya mpango wa Mungu, tujitahidi kutambua kila wakati unatutaka tufanye nini.

5.2.4. Tuangalie tusizame katika kazi fulani, bali kuwe na uwiano mzuri kati ya mambo yote ya maisha yetu: sala na kazi za mikono, utume na malezi ya kudumu, halafu pumziko pia.

5.2.5. Tuchangie burudani fupi za kila siku wakati wa chakula au baada yake, na sherehe za kifukara zinazotupa nafasi ya kupumzika kirefu zaidi na kukaa na ndugu zetu.

 

 

5.3. UDUGU KATIKA KAZI

 

5.3.1. Tukizingatia jinsi Bwana Yesu alivyokuwa akiwatuma wanafunzi wake wawiliwawili, tuthamini faida ya kiroho na ya kitume inayotokana na utendaji wa kijumuia, na tupendelee kufanya kazi kwa vikundi.

5.3.2. Watumishi, walinzi na walezi ndio wenye madaraka ya karibu kuhusu kazi za ndugu zao.

5.3.3. Katika kuzichagua na kuzigawa washauriane na baadhi ya wenzao, wakizingatia wito wetu wa kitume, mahitaji ya Kanisa na ya watu, udogo wetu unaotuelekeza kufanya kazi duni, halafu ustadi na vipaji vya kila mmoja.

5.3.4. Mlinzi kabla hajawatuma ndugu wakafanye kazi nje ya utawa, ahakikishe kuwa wataweza kutimiza masharti yote ya maisha yetu, kama vile kuhudhuria kwa kawaida sala za jumuia.

5.3.5. Katika mikutano ya jumuia zetu tuarifiane kuhusu kazi tunazozifanya, ili wote tushiriki katika kazi za kila mmoja, naye aone kuwa anazifanya kwa niaba ya ndugu zake.

5.3.6. Tusishike shughuli yoyote nje ya jumuia bila ya ruhusa ya mlinzi, na hata tukiimudu sawasawa kazi fulani tangu siku nyingi, tuwe daima tayari kuiacha ili kuzifanya nyingine ambazo huenda tukaagizwa.

 

 

5.4. RIZIKI

 

5.4.1. Yesu ametuhimiza tumtegemee Baba wa mbinguni, ambaye hatatuacha tukose mahitaji yetu tukitafuta kwanza utawala wake na kushughulikia tabu za jirani.

5.4.2. Basi, tusijitafutie riziki kwa mafadhaiko na mahangaiko, yasije yakasonga kilichopandwa ndani mwetu yakatuzuia tusifanye utume na kazi nyingine ambazo hazituletei faida ya uchumi, lakini zinadaiwa na upendo.

5.4.3. Kadiri iwezekanavyo kila mmoja wetu afanye kazi za mikono, ambazo ni sehemu ya maisha yetu kwa kuwa zinatuwezesha kutimiza udogo kwa kushikamana na fukara wenzetu wanaopata hivyo riziki kwa ajili ya familia zao; pia zinatuwezesha kutoa mfano mwema, kusaidia wenye shida na kustawisha utu wetu.

5.4.4. Mapato na malipo ya kazi zetu yasipotutosha, tunaruhusiwa kupokea kwa shukrani misaada ya lazima, hasa kwa ajili ya malezi, tukijitahidi wote kuitumia vizuri, kuwashirikisha maskini na kutoa ripoti kadiri ya sheria za Kanisa.

 

 

5.5. MAISHA YA KIJAMII

 

5.5.1. Mwana wa Mungu kwa kutwaa mwili ameungana kimaisha na kila mtu, hasa fukara, na kumfanya binadamu kuwa njia ya kukutana naye.

5.5.2. Kanisa linapaswa kuwa la Kristo, katika Kristo na kwa ajili ya Kristo, kwa kuwa la watu, kati ya watu na kwa ajili ya watu.

5.5.3. Sisi pia tushikamane na mwenzetu yeyote na kushiriki katika maisha ya jamii kama majirani na raia wema, tukiwajibika kwa ustawi wao, lakini bila ya kushika mamlaka ya kiserikali wala kujiunga na vyama vya siasa au jeshi.

5.5.4. Kwa namna ya pekee sisi watawa wa watu wadogo tuwapendelee akina Lazaro walionyimwa nafasi duniani, ambao leo ni umati mkubwa.

5.5.5. Kwa kuwa hasa katika sura yao tunamtambua Yesu mteswa, na katika sura yake tunamtambua Baba wa mbinguni, hatuwezi kukubali sisi tujipatie mahitaji yote na kuwaacha hao katika hali duni kijamii, kiuchumi, kielimu na kisiasa.

5.5.6. Zaidi ya kuonja shida zao, tuwasaidie kupata kinga na matibabu, ufundi fulani, malezi kwa watoto wao na huduma nyingine ndogondogo, tukishirikiana na ndugu walei kadiri ya uwezo wetu.

5.5.7. Tudumishe na kustawisha tunu bora za utamaduni wetu ambazo zinawaandaa watu kupokea ujumbe wa Kristo na kujipatia maendeleo halisi.

5.5.8. Tutie maanani hasa mila zinazoonyesha furaha kwa mtoto kuzaliwa, heshima kwa uhai wa mtu, utunzaji wa mwenye shida, ujirani kwa mzee na aliye kufani, mshikamano na aliyefiwa, halafu tumaini la uzima wa milele kwa marehemu.

5.5.9. Kwa njia ya hisani yetu, Kanisa lionekane mama wa uzima na kuwasaidia wanadamu wote waishi kama jamaa ya Mungu, ishara na utangulizi wa ulimwengu ujao.

 

 

5.6. AMANI, HAKI NA UHAI

 

5.6.1. Tujitahidi kuwapatanisha watu ili tustahili kuitwa wana wa Mungu, na kujenga jamii juu ya msingi wa upendo.

5.6.2. Tukiwa watu wa amani, tuwaelekeze wote njia yake halisi, yaani kuongoka kwa kupokea huruma ya Baba, halafu kuwatolea wengine kwa kushinda ubaya kwa wema.

5.6.3. Kwa kuwa amani ni tunda la haki na la mshikamano katika maendeleo, tusipatane hata kidogo na aina yoyote ya dhuluma, ambayo daima inamlilia Mungu alipe kisasi.

5.6.4. Tumkimbilie yeye kwa sala na sadaka ili azuie jeshi la uovu, yaani watu wale ambao kwa visingizio mbalimbali wanapambana na utamaduni wa upendo na wa uzima, tena wanakanyaga heshima na haki za msingi za binadamu, kuanzia wale wasiozaliwa bado.

5.6.5. Tuwasaidie walei watafute utakatifu katika siasa, ambayo ni namna muhimu ya kutekeleza upendo, na wawajibike pamoja na watu wenye mapenzi mema ili kuleta maendeleo kwa wote.

5.6.6. Kwa kuwa bidii nyingi za namna hiyo zinakwamishwa na ushirikina, tusichoke kumtangaza Kristo ambaye amewashinda pepo wote na kutupatia Roho wa upendo ili tushikamane bila ya hofu.

5.6.7. Yeye tu, kwa njia ya Injili yake na ya Kanisa lake, anaweza kutatua matatizo ya ulimwengu ambayo ni makubwa kiasi cha kukatisha tamaa.

5.6.8. Tukimtegemea yeye na ahadi zake, tuwatumainishe watu wetu, na hasa vijana, kuhusu ukombozi kamili wa roho na mwili kwao na kwa wenzao.

5.6.9. Tuwatie moyo wa kusaidiana, kutetea haki zao na kuipatia nchi maendeleo halisi, ambayo yanategemea ukomavu wa binadamu na wa dhamiri yake kadiri ya tunu za dini, maadili na utamaduni, kuliko pesa, misaada, teknolojia na kasumba.

5.6.10. Wale ambao wananyanyaswa hata kuuawa wasiweze kusema kitu, tuwe sauti yao tukiamsha dhamiri za wote ili wamjali binadamu na kumpokea kama ndugu anayeleta baraka, wakimpenda na kushikamana naye hasa akiwa maskini.

5.6.11. Tupende kidugu viumbe vyote, ambavyo ni zawadi ya Mungu kwetu na bila ya maneno vinatangaza sifa zake, na tuwahimize wote kuhifadhi mazingira, la sivyo binadamu wenyewe watashindwa kuishi tena duniani.

 

 

5.7. HESHIMA YA WANAWAKE

 

5.7.1. Kwa mpango wa Mungu, maumbile ya wanawake yamewaandaa kuelewa maana ya upendo, yaani kujitoa kwa mwingine na kumpokea alivyo, kuvumilia mengi ili kumuachia nafasi akue, bila ya kujali sifa alizonazo.

5.7.2. Kumbe ubaguzi wa jinsia umezuia vipaji vyao visichangie kikamilifu ustawi wa jamii na wa familia ya Mungu.

5.7.3. Kufuatana na mfano wa Yesu, Mkombozi wa wote, tuungane na Kanisa katika azimio la kuwarudishia akina mama heshima na nafasi wanazostahili.

5.7.4. Tushughulikie malezi yao, tukijua kumuelimisha mwanamke ni kuwaelimisha watu wengi kwa njia yake.

 

 

5.8. MAMA WA HURUMA

 

5.8.1. Mafungamano yoyote yanahitaji hasa huruma, iliyo sifa bora ya Baba yetu wa mbinguni.

5.8.2. Maria anafanana naye zaidi kuliko nafsi zote za kibinadamu, kwa kuwa amefikia upeo wa upendo akiambatana naye katika maisha ya kila siku kijijini.

5.8.3. Wimbo wake unatuvutia kila siku kuwa waaminifu kwa Mungu na kushikamana na matarajio ya watu wadogo.

5.8.4. Kufuatana na mfano wake mzuri ajabu wa hisani, huruma na ukarimu, tujitahidi kuonja upendo wa Baba, na kuutangaza ulimwenguni na kuutekeleza vizuri kushinda akina mama.

5.8.5. Maria akiwa mwenyewe tangazo hai la huruma ya Mungu, alipokwenda tu kwa haraka kumtumikia jamaa yake, alifanya kitoto kichanga na mama yake wajazwe furaha ya Roho Mtakatifu.

5.8.6. Sisi pia tulete faraja kwa kutumia nafasi yoyote ya kuwasaidia kwa unyenyekevu wenye shida, kusudi uzuri wa Kimungu wa kuishi kwa upendo useme katika mioyo ya watu kabla midomo yetu haijamtangaza Kristo kuwa ndiye jibu la maswali yote juu ya maisha yao.

 

 

 

6. KUSHIKAMANA NA YESU FUKARA

 

6.1. HERI YA KWANZA

 

6.1.1. Mwenyezi Mungu aliwakabidhi wanadamu wote dunia na utajiri wake ili wajipatie kwa haki mahitaji yao na kusaidiana katika shida.

6.1.2. Toka mwanzo waliodhulumiwa na wenzao walipomlilia, yeye akawasikiliza, akiwatumia watu kuwakomboa na kuwatetea na hatimaye Mwanae wa pekee ashiriki moja kwa moja hali yao duni na kuwaelekeza njia ya wokovu.

6.1.3. Mzee wetu Fransisko naye alijifanya fukara mdogo kati ya wakoma na maskini kwa sababu ya kuwaonea huruma hao na kutiririka machozi akikumbuka Yesu mwenyewe alivyozaliwa pangoni na kulazwa horini, halafu alivyoteseka uchi msalabani.

6.1.4. Tukishikamana naye maskini hata leo, tutasikia njia na kiu ya haki, hata tushughulikie ukombozi wake na kusimama imara dhidi ya upotovu wa ulimwengu ambao kwa dai la kujiendeleza unakuja kuabudu mali na kumuangamiza binadamu.

6.1.5. Bidii hiyo italifanya Kanisa liwe kweli la watu maskini, wanaokusudiwa hasa kutangaziwa na kutangaza habari njema ya kuwa Mungu yu pamoja nao na pamoja na wale wanaowapenda.

6.1.6. Lenyewe linapaswa kufuata nyayo za Bwanaarusi wake hasa katika ufukara, ambao pamoja na upendo ndio utukufu wake na ushahidi wa kuwa linajiona chombo cha kazi ya Mungu kinachotegemea uweza wa Roho Mtakatifu tu.

6.1.7. Kadiri ya Injili ufukara ndio heri ya kwanza na ardhi bora inayostawisha maadili yote, maana unatushirikisha moyo na maisha ya Yesu vinavyotufunulia kikamilifu utakatifu wa Baba.

 

 

6.2. KUWA MASKINI WA ROHO

 

6.2.1 Ufukara wa Yesu unaonekana hasa katika kujitoa kabisa kwa watu na kumrudishia Baba yote aliyopewa naye, hata roho yake.

6.2.2. Tukiongozwa na Roho Mtakatifu nyuma yake, tumtamani Mungu tu na utukufu wake, na kumaliza umimi wetu kusudi tusiishi tena kwa ajili yetu wenyewe, bali Kristo awe anaishi ndani mwetu.

6.2.3. Kwa kujiona kuwa si kitu, tujifanye wadogo wa wote na kukaa chini yao hata wakituonea na kutudharau.

6.2.4. Tuchanganyikane na watu wa mwisho, tukikubali kujifunza kutoka kwao unyenyekevu na unyofu, udugu na ukarimu, subira na tunu nyingine.

6.2.5. Tuwe daima tayari kuwapokea wenzetu na kushirikishana nao mema yale yote ambayo Mungu ametukabidhi kwa faida ya wote.

6.2.6. Ndipo unapotokea ule ufukara mkuu kuhusu mali unaodhihirisha maisha yetu ya Kiinjili.

 

 

6.3. KUBANA MATUMIZI

 

6.3.1. Tukitegee masikio kilio cha maskini wanaoshindwa kushiba, tukitambua kuwa ni sauti ya Mungu anayetuita upya kushiriki kijumuia maisha yao magumu na kuotesha furaha na tumaini kwenye shida, badala ya kufanya moyo wetu kuwa mgumu na kuzoea tu kuona watu fukara kuliko sisi wakitamani makombo mlangoni.

6.3.2. Kadiri majirani wetu walivyo na mashaka tubane matumizi ili kuwashirikiska vitu vingi zaidi, yaani sio tu vile vya ziada, bali hata nguo ya pili na chakula chetu, na kila kitu tunachohitaji kwa kuishi, kwa sababu kutoa ni moyo, si utajiri.

6.3.3. Watu wakiwa na haja kuu, vitu vyote ni vya kwao pia, yaani vinatakiwa kuwatimizia: kutokana na haki hiyo ya fukara, kila mmoja wetu ajisikie huru wa kuwasaidia kulingana na utamaduni wa ukarimu walionao watu wetu, tusije tukawakwaza bure kwa kuwaacha hivihivi bila ya kuwajibika kwa ajili yao.

6.3.4. Kinyume chake, kwa matumizi yetu binafsi tunapaswa kuwa daima chini ya watumishi na walinzi.

6.3.5. Bila ya ruhusa yao tusiombe wala kutoa chochote kwa ndugu, marafiki na wengineo, kwa kuwa tumejinyima haki ya kuwa na mali yoyote.

6.3.6. Tusiwe watu wa kupenda umaskini mradi usitufanye tupungukiwe kitu, bali tumshukuru Mungu kila anapotujalia kuonja ukali wa ufukara kama anapotujalia kutimiza masharti mengine ya kitawa na majukumu ya kitume.

6.3.7. Kusudi ionekane wazi hazina yetu iko mbinguni, na ufukara wetu maana yake nini, tutumie vitu kwa kufuata kiwango cha chini, yaani kadiri ya lazima tu, si kadiri ya uwezo tulionao.

6.3.8. Kila ndugu anaruhusiwa kuwa na kanzu mbili au tatu, kamba, nguo ndogo za ndani, joho na makubadhi; akina dada wanavaa pia shela; hakuna mavazi mengine yanayokubalika, ila kwa ugonjwa; tena hayo yote yawe ya gharama ndogo na rangi hafifu.

6.3.9. Kabla hatujaomba ruhusa ya kutumia njia za mawasiliano na hasa kusafiri, tupime mbele ya Mungu sababu za kufanya hivyo, tukizingatia ufukara wetu na masharti mengine ya utawa.

6.3.10. Hata kijumuia haturuhusiwi kumiliki au kusimamia mashine za kusafiria, kunasia sauti au picha, kunakilia, kusafishia na vinginevyo vinavyokwenda kinyume cha ufukara mkuu tulioitiwa, kwa kuwa si vya lazima, tena pengine ni vya gharama.

6.3.11. Tujihadhari na kishawishi cha kulegeza ufukara huo, ambacho huenda kikatujia kwa njia ya watu wanaotupenda, lakini mawazo yao kama yale ya Petro si ya Mungu ila ya binadamu tu.

 

 

6.4 MFUKO

 

6.4.1 Kama vile Yesu na Mitume walivyokuwa wakipokea misaada na kuwa na mfuko maalumu uliokabidhiwa kwa mhasibu, Kanisa linatumia pesa na mali kwa ajili ya ibada, mahitaji ya wahudumu, utume, na vitendo vya huruma hasa kwa maskini.

6.4.2. Kwa malengo hayohayo jamaa na jumuia zetu pia zinaweza kutumia vitu na pesa, lakini kadiri vinavyohitajika tu, hata wote waone kuwa tumekombolewa kutoka tamaa ya mali, iliyo mzizi wa maovu yote.

6.4.3. Usimamizi wa pesa na vitu ufuate sheria za Kanisa na za utawa wetu, na kadiri iwezekanavyo ukabidhiwe kwa walei.

6.4.4. Halmashauri ya jamaa iwateue katika ngazi zote mhasibu stadi na washauri wake wawili ambao wote wafanye kazi hiyo chini ya mtumishi au mlinzi mhusika; katika jumuia isiyo na ndugu wengi, mlinzi mwenyewe anaweza kuwa mhasibu.

6.4.5. Kila baada ya miezi mitatu hao watoe ripoti kwa halmashauri ya ngazi ileile na kwa mtumishi; kila mwaka baraza litoe ripoti kwa askofu wa Morogoro; mtumishi wa jamaa atoe ripoti kwa mutano mkuu kila unapofanyika.

6.4.6. Baraza lipange kiwango ambacho watumishi na walinzi wanaruhusiwa kuingia deni, kutoa na kuuza vitu na kutumia pesa kwa mahitaji yasiyoingia katika kawaida ya huduma zao kwa ndugu waliokabidhiwa; juu ya kiwango hicho wanapaswa kuomba kibali cha halmashauri yao.

6.4.7. Malipo, zawadi na vitu vyovyote vinavyomfikia ndugu kwa namna yoyote, avitoe kwa mlinzi kwa manufaa ya jumuia nzima, ili tupate chakula, mavazi na mahitaji mengine kwa usawa kadiri ya ufukara wetu, bila ya kusahau maskini.

6.4.8. Matumizi yoyote ya pesa yanadai ndugu apate kwanza ruhusa ya mlinzi, halafu atoe ripoti kwake.

 

 

6.5. MAKAZI NA MAENEO

 

6.5.1. Makazi tunayoishi yawe madogo na kulingana kwa ufukara na yale ya maskini wanaotuzunguka, lakini yapendeze kwa usafi na utaratibu.

6.5.2. Mlinzi asijenge chochote kabla hajaruhusiwa na mtumishi pamoja na halmashauri yake, tusije tukapatwa na matatizo yale mazito yanayoelezwa na historia ya utawa.

6.5.3. Kadiri iwezekanavyo nyumba na maeneo tunavyovitumia viwe mali ja jimbo au ya wengine, tukikwepa ujanja wa kisheria na unafiki wowote katika utekelezaji wa neno hilo la msingi.

6.5.4. Tukilazimishwa kuhama, twende kwa furaha kumtumikia Mungu mahali pengine, badala ya kutetea haki ya kumiliki tuliyoamua kujinyima moja kwa moja.

 

 

6.6. KUWAJIBIKA KWA PAMOJA

 

6.6.1. Ufukara mtakatifu ni kama hazina tuliyokabidhiwa ili tuitunze kwa uangalifu na kuonyesha wazi kuwa si kujinyima tu, bali hasa ni sharti na tunda la kuwapenda wenye shida alivyotufundisha Yesu.

6.6.2. Katika mikutano ya ngazi zote tuhakikishe utekelezaji bora wa neno hilo kadiri ya mazingira, kwa kuwa kulegea katika ufukara mwisho wake ni uvuguvugu wa roho katika yote.

6.6.3. Watumishi na walinzi wawatangulie ndugu zao katika njia hiyo ili wawe na haki ya kuwahamasisha wote wawafuate.

6.6.4. Ndugu wakikiri udhaifu wao wafurahi kumkaribisha mtumishi akitembelea mara kwa mara kila chumba ili awasaidie kupunguza chochote cha ziada.

6.6.5. Kisha kusikia mkutano wa jumuia, mlinzi akague mara kwa mara vitu vyote ilivyonavyo, halafu akatoe vile vya ziada, tusije tukafanya dhambi kwa kujiwekea akiba vitu vinavyohitajiwa haraka na wengine.

 

 

6.7. MARIA FURAKA MNYENYEKEVU

 

6.7.1. Kati ya mambo yanayotupendeza zaidi katika maisha ya Yesu, mojawapo ni jinsi alivyoshika ufukara, akiwa ni Mwana wa Baba mwenye kuwakomboa maskini.

6.7.2. Hata katika hilo alitanguliwa na Mama yake, kielelezo cha ufukara wa Kiinjili na cha maadili yote yanayotokana nao, hasa unyenyekevu mpole na mnyofu, na uimara mtulivu na mkarimu kwenye mashaka ya maishani.

6.7.3. Wimbo wake wa furaha umekuwa shangilio la kudumu la wanyonge wote ambao wametambua wanavyopendelewa na Mungu na wanatarajia mapinduzi yake.

6.7.4. Tukilenga utakatifu kwa kufuata mifano ya Bikira Maria, tujitahidi kuwakaribia kwa huruma ya kimama wasulubiwa wa siku hizi, badala ya kupita haraka kwenda zetu tukiwaachia Wasamaria kujifanya majirani wa watu ambao wamevamiwa na kubaki hoi kabisa.

6.7.5. Tung’amue na kukiri wazi tunavyoshindwa kutimiza hata wajibu mkuu wa kuwapenda kama tunavyojipenda

6.7.6. Tuwahimize wote kurekebisha sana mitazamo na maisha yao ili wasisababishe Mwana na Maria azidi kuteswa katika wadogo wake, hasa wale wa bara la Afrika ambao ndio wa kwanza kushirikishwa naye msalaba wake kwa njia ya Simoni na Kirene.

 

 

 

7. KUISHI KIDUGU KATIKA JUMUIA

 

7.1. UMOJA

 

7.1.1. Yesu, mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi, alisali na kuonyesha njia ya upendo, akatoa uhai wake, akampeleka Roho wake ili wana wote wa Mungu waliotawanyika wawe kitu kimoja na Baba aliyemtuma.

7.1.2. Habari njema tunayoiamini na kuitangaza ni kwamba yeye ametufanya kuwa familia ya Mungu, yaani watoto wa Baba na ndugu kati yetu.

7.1.3. Katika mishipa yetu inazunguka damu ileile moja, yaani damu ya Yesu Kristo; nasi tuna uzima kwa roho ileile moja, yaani Roho wa upendo wa Mungu.

7.1.4. Kanisa linahamasisha watu waunde vyama vya kila aina, na mataifa yashirikiane, ili kustawisha utu wa kila mmoja na udugu kati ya wote, kadiri ya mpango wa Muumba.

7.1.5. Kwa namna ya pekee linapokea kwa shukrani karama ya maisha ya kijumuia ambayo inajitokeza ndani mwake na kulidhihirisha fumbo lake, yaani kuwa Kanisa hasa ni ushirika wa watu na Mungu na kati yao.

7.1.6. Mambo yote yaliyo maalumu ya utawa yanahusika nayo: usafi katika useja unatuwezesha kuwa wa kweli katika upendo wa kidugu, ufukara unatuongoza kushirikishana yote, utiifu unajenga umoja, tena sala inatukusanya mbele ya Mungu na utume unapata nguvu kwa ushuhuda wa pamoja.

7.1.7. Tukimpokea Kristo mshindi kati yetu, tufufue na kueneza ule udugu halisi tena mfurahivu ulioonekana wazi kati ya mtakatifu Fransisko na wenzake, na pia kati yao na viumbe vyote, kama matokeo ya kuungana na Utatu mtakatifu.

7.1.8. Kama wanafunzi wa Yesu wanaotambulikana mara, tuulenge daima umoja huo kwa upendo ule ambao mwenyewe ametushirikisha kutoka kwa Mungu na kwa hiyo una nguvu kuliko mauti.

7.1.9. Hivyo wote wavutiwe na uzuri wa mpango wake huo na kuona namna za kuutekeleza kwa kufungua tena njia za mawasiliano kati ya wale wasioelewana, mpaka upendo ujaze ulimwengu.

 

 

7.2. NEEMA YA UDUGU

 

7.2.1. Jumuia za Kikristo asili yake si mapenzi au mipango ya binadamu, bali ni upendo wa Mungu aliyewaita pamoja watu kadhaa, ili tofauti zozote kati yao zilete faida kwa kila mmojawao, na umoja wao ushinde matokeo ya dhambi asili, hata uonyeshe kwa namna fulani ule wa nafsi tatu za Kimungu.

7.2.2. Yesu aliwaita Mitume kwa jina washiriki maisha yake kama kundi moja ambalo liwe mbegu ya ushirika wake utakaokamilika mbinguni.

7.2.3. Mwenyewe anazidi kutukusanya kila siku ili aseme nasi na kutuunganisha naye na kati yetu katika ekaristi, ili tumfuate kwa umoja tunavyoelekezwa na karama aliyotujalia.

7.2.4. Tuko pamoja kwa jina lake, si kwa kuchaguana: basi tupokeane kwa shukrani kama zawadi za Bwana, tukijisikia familia moja na kuitana sote ndugu, tukijifanya kila mmoja mdogo wa mwenzie na kuungana katika malengo ya jumuia.

7.2.5. Kumega mkate wetu wa kila siku, kusali pamoja, kufuata mafundisho na maagizo ya wachungaji wa Kanisa na kushirikiana katika mambo yote kuonyeshe na kustawisha upendo tulionao sisi kwa sisi na ambao utatutegemeza katika magumu yote ya maisha yetu.

7.2.6. Kama Kristo alivyotuletea umoja kwa mateso yake, mapingamizi yanayotupata katika kuujenga tuyapokee kama nafasi za kuimarisha na kusafisha nia yetu ya kujitoa mhanga kwa wenzetu.

7.2.7. Kwa kujifanya chemchemi, kielelezo na kipimo cha upendo wetu, Yesu ametuhakikishia kuwa tumependwa upeo na kuwa tunaweza kupenda upeo: upendo huo unajenga jumuia siku kwa siku ukishinda udhaifu wetu.

 

 

7.3. MAISHA YA KIJUMUIA

 

7.3.1. Sisi kama jumuia ya kitawa si kundi la watu wanaojitafutia utakatifu wa binafsi, bali utakatifu na ukomavu wetu unategemea kabisa utekelezaji wa upendo katika maisha ya kijumuia.

7.3.2. Hiyo si kazi rahisi au ya muda mfupi, wala haikamiliki hapa duniani: lakini inawezekana daima kusonga mbele kwenye njia ya upatanisho na upendo.

7.3.3. Hivyo maisha ya kijumuia ni safari ya ukombozi wa kiroho, ni tendo kuu la toba yetu, ni shule tunapojifunza kuishi kidugu na watu wa nje pia.

7.3.4. Kwa ajili hiyo tustawishe adabu njema, ukarimu, unyofu, upole, ukunjufu na unyenyekevu.

7.3.5. Tujitahidi kuheshimiana na kuelewana, kusikilizana na kuaminiana, kushirikishana vipaji na madaraka, furaha na uchungu, mipango na matumaini.

7.3.6. Katika kila ngazi tufanikishe mikutano ya kidugu na kujadiliana ili kufahamiana zaidi, kuwaza na kupanga kwa pamoja, kukagua maisha yetu katika mazingira tunamoishi, yaani Kanisa na ulimwengu.

7.3.7. Tuarifiane juu ya maendeleo na matukio ya jumuia zetu mbalimbali, tukijua kuwasiliana ni njia ya kushirikiana.

7.3.8. Tusaidiane kila mmoja na mwenzie tukihisi na kushughulikia mahitaji ya ndugu yeyote upande wa roho na wa mwili, hasa akiwa mgonjwa, mkongwe au mwenye matatizo ya ndani.

7.3.9. Tusiwaonee kijicho ndugu waliojaliwa wingi wa neema na mafanikio, bali tumshukuru Mungu kwa kuwa utajiri anaomjalia mmoja ni hazina ya jumuia nzima.

7.3.10. Kadiri tunavyofaulu kudumu kwa umoja na furaha katika wito wetu, tukilinganisha tofauti za umri, kabila, elimu, tabia na mengineyo, tunashuhudia tayari kuwa utawala wa Mungu umefika.

 

 

7.4. NDUGU WA UKOO, MAREHEMU NA WATAKATIFU

 

7.4.1. Hata katika kuambatana na mpenzi wetu, anayeweza kutudai kuliko wote, tuwaheshimu waliotushirikisha uhai, na tutimize kama wana wema wajibu wetu kwao.

7.4.2. Ruhusa za kuwatembelea zitolewe na mtumishi kufuatana na sheria zetu ndogondogo na kwa kuzingatia hali yao, ahadi ya mwanao kuwa ya muda au ya daima, kipindi kilichopita baada ya safari ya mwisho na mengineyo.

7.4.3. Katika haja za pekee, kisha kusikiliza halmashauri yake, mtumishi awatolee misaada kwa niaba ya jamaa nzima, kwa kuwa tunawapenda wazazi wa kila ndugu kama wazazi wetu sote.

7.4.4. Ushirika wa kidugu unadumu hata baada ya kutembelewa na ndugu kifo: basi tumuombe Baba mwema awahurumie ndugu wa utawa na wa ukoo waliofariki dunia.

7.4.5. Tuwaheshimu kwa moyo wa ibada wazee wetu wa Kifransisko ambao wametangazwa na Kanisa kwamba wako kwa Mungu na wanatuombea.

 

 

7.5. MAMA WA KANISA

 

7.5.1. Jumuia ya Yerusalemu ilipoanza, Bikira Maria alichangia umoja kamili wa viungo vya Mwanae, akisali pamoja nao wajazwe paji la Roho Mtakatifu.

7.5.2. Kwa kusali na Maria, kumpenda kama watoto na kutamani kumuiga tutaunganika sisi kwa sisi kama ndugu wa tumbo moja, na kumtukuza pamoja Bwana kwa moyo wa shukrani, mshangao, unyenyekevu, tumaini na unabili, kama wa kwake.

7.5.3. Hapo jumuia zetu zote, zikiwa zimejaa furaha na Roho Mtakatifu zitakuwa tayari kutumiwa na Mwenyezi Mungu kwa kutenda maajabu yake.

 

 

 

8. KUTII KWA UPENDO

 

8.1 MATAKWA YA BABA

 

8.1.1. Yesu chakula chake kilikuwa ni kutimiza sikuzote matakwa ya Baba yake; upendo aliokuwanao kwake ulimzuia asitamani chochote zaidi kuliko hicho.

8.1.2. Ingawa ni Bwana aliishi miongoni mwa watu kama mtumishi wa wote, akiwatii wazee wake na kufundisha heshima kwa wenye mamlaka kwa kuwa inatoka kwa Mungu.

8.1.3. Kwa msaada wa Roho Mtakatifu akanywea kikombe cha mateso na kutii mpaka kufa, naam hata kufa msalabani, ili atimize kabisa kazi aliyoagizwa.

8.1.4. Kwa kufanya hivyo Mwana wa Mungu ametufumbulia kuwa hiari tuliyojaliwa ni safari ya kumtii Baba, na kwa njia hiyo kuchangia wokovu wa watu na kujipatia amani na uhuru wa kweli, ule wa watoto wa Mungu waliojaa upendo.

8.1.5. Mfuasi wake mdogo Fransisko akatuelekeza njia hiyohiyo ya kujikana ili kumwekea wakfu Mungu utashi wetu tusije tukaachana naye, sisi viumbe na watoto wake.

8.1.6. Dhidi ya umimi, ukaidi na utengano yanayomtawala binadamu, wanaojidai kuwa huru wa kufanya lolote linalowapendeza, tushuhudie heri ya umoja unaotokana na nia ya kutambua na kuitikia kwa pamoja wito wa Mungu kwetu kuhusu maisha ya kidugu na ya kitume.

8.1.7. Kama tulivyoahidi tunapaswa kumtii Baba na neno lake kwa kupitia wawakilishi wake katika Kanisa na katika utawa, walioshirikishwa mamlaka ya kufundisha, kutakasa na kuongoza kwa jina la Bwana.

8.1.8. Hivyo tuna hakika ya imani ya kumpendeza Mungu na kutumwa naye, badala ya kufuata mipango au matazamio yetu wenyewe, ambayo hata yakiwa mazuri namna gani, hayawezi kulingana na ya kwake, hasa kama ametuandalia msalaba ili utimilize upendo wetu.

 

 

8.2. UONGOZI WA ROHO MTAKATIFU

 

8.2.1 Roho yuleyule aliyemuongoza Yesu katika kumpendeza Baba, anajenga Mwili wake akiwagawia waamini kazi za huduma na karama nyingine na kuwaunganisha katika upendo.

8.2.2. Ndiye uhai na mhudumu mkuu wa utawa wetu pia, akifanya kazi kwa njia ya miundo na viongozi na moja kwa moja ndani ya kila ndugu.

8.2.3. Miundo yetu iwe midogo iwezekanavyo, yenye sura ya kifamilia, na hasa ifuate mvumo wa Roho, kwa faida ya kila mmoja na ya wote kwa jumla, kwa kuwa pasipo mwanga na nguvu zake katika kutimiza wajibu wa kidugu tunajichosha bure tu.

8.2.4. Vilevile kila mmoja wetu anapaswa daima kusikiliza na kufuata sauti yake, inayotufikia hasa kwa njia ya mikutano, watumishi na walinzi, ingawa mara nyingi anamfunulia aliye mdogo zaidi mambo yaliyo bora.

 

 

8.3. MIKUTANO

 

8.3.1. Kila mkutano wetu, katika ngazi mbalimbali, unahudhuriwa na Bwana kama alivyoahidi, tena unaonyesha udugu unaotuunganisha.

8.3.2. Katika hali ya imani na furaha washiriki wachange mang’amuzi mbalimbali na ufafanuzi wa haja maalumu zilizojitokeza, ili kutafuta njia zinazofaa kulingana na karama yetu sote.

8.3.3. Katika kupima kila jambo wakumbuke majukumu waliyonayo pia kwa ajili ya ndugu ambao pengine hawahudhurii, lakini wanahusika na kuwajibika hasa kwa sala.

8.3.4. Tusaidiane kuchunguza jinsi tunavyoshika Injili, kuchimba mada muhimu kwetu sote, kukabili maswala makuu ya maishani mwetu, halafu kukata mashauri kadiri ya sheria zetu, ikiwezekana kwa kauli moja, la sivyo kwa thuluthi mbili za kura, halafu kwa kutoa maelezo ili kurahisisha utekeIezaji wa wote.

8.3.5. Mamlaka ya juu katika kila jamaa inao mkutano mkuu, lakini ndani ya mipaka ya katiba hii.

8.3.6. Wenyewe uitishwe na mtumishi mapema kila baada ya miaka mitatu na kuhudhuriwa na ndugu ambao wasizidi ishirini lakini wawakilishe kweli jamaa nzima kadiri ya sheria zetu ndogondogo.

8.3.7. Mkutano mkuu upange ajenda zake, kisha kupata mapendekezo ya halmashauri kuu yaliyotokana na mchango wa ndugu wote.

8.3.8. Mkutano mkuu unaweza kuunda kanda zenye jumuia kadhaa, kuziunganisha, kuzirekebisha na kuzifuta ili ziwe daima hai katika Kanisa.

8.3.9. Mkutano wa jumuia uitishwe na mlinzi walau mara moja kwa mwezi, na kuhudhuriwa na ndugu wote wenye ahadi, isipokuwa kuhusu maswala ya malezi na mengineyo anaweza akawaalika wenye ahadi ya daima tu.

8.3.10. Ajenda za mkutano huo zipangwe na mlinzi kisha kupata mapendekezo ya wanajumuia.

 

 

8.4. HUDUMA KATIKA JAMAA

 

8.4.1. Mbali ya mikutano, utawa wetu una ndugu wenye madaraka katika jamaa na ngazi mbalimbali wanazoziwakilisha rasmi.

8.4.2. Ndugu hao, hasa watumishi, wakiishi katika nyumba iliyopangwa iwe makao yao, wanatakiwa kuímarisha ushirika wetu na Kanisa tena kati yetu, kumthibitisha kila mmoja katika wito wa Kiinjili wa Kifransisko, kutoa neno la mwisho katika kutambua matakwa ya Mungu na kustawisha ushuhuda wetu sote katíka jamii.

8.4.3. Kila mmojawao awe na washauri wawili ambao waishi naye na kushiriki katika madaraka yake kadiri ya sheria za utawa wetu.

8.4.4. Awe nao walau vikao vinne kwa mwaka, na kujali sana mchango wao.

8.4.5. Mmojawao awe kaimu wakati mtumishi au mlinzi asipokuwepo, ila asijihusishe na mambo yale ambayo huenda akajiwekea.

8.4.6. Mtumishi asishughulikie mambo ambayo yanampasa mlinzi, ila kwa salabu nzito.

8.4.7. Awaongoze watoto wa Mungu kwa upendo ule ambao Baba anao kwao, na kwa mifano mitakatifu ya maisha yake mwenyewe na ya jumuia anamoishí, ambamo ajitahidi ili Mungu atamaniwe na kupendwa kweli kuliko yote.

8.4.8. Asitende kama chifu, bali awasaidie kutii akiimarisha imani na kuheshimu utu wao, akiwasikiliza kwa moyo wa kimama.

8.4.9. Awasaidie ipasavyo wanayoyahitaji, hasa katika ugonjwa, akikumbuka atatakiwa kujieleza mbele ya Mungu kama ndugu fulani atapotea kwa sababu amemtendea kwa ulegevu au kumpa mfano wa kukatisha tamaa, au kumkosoa na kumuadhibu haraka na vikali mno.

8.4.10. Mbali ya kuwasiliana na jumuia zote alizokabidhiwa kwa njia ya barua, azitembelee rasmi walau mara moja kwa mwaka ili kuzistawisha kiroho na kiutume; halafu ampangie mlinzi muda wa kutoa ripoti juu ya utekelezaji wa maagizo aliyotoa.

8.4.11. Mtumishi kwa kibali cha halmashauri yake na kisha kuwasikia wanaohusika zaidi, anaweza kuweka jumuia mbili au zaidi chini ya ndugu mtunzaji ambaye azisimamie kwa karibu kwa niaba yake.

8.4.12. Kwa sababu maalumu, watumishi, watunzaji na walinzi wanaweza kumkabidhi ndugu fulani sehemu ya mamlaka yao ili ashughulike kwa niaba yao.

8.4.13. Hao wote, zaidi ya kuzitumikia jumuia zao, wawajibike kuhusu maisha na maendeleo ya jamaa nzima, wakikuza ushirikiano wa kiroho, kiutume na kiuchumi.

 

 

8.5. UCHAGUZI NA UTEUZI

 

8.5.1. Mkutano mkuu wa kila jamaa uchague mtumishi na washauri wake, ukiwakabidhi utekelezaji wa maagizo mbalimbali.

8.5.2. Kisha kuthibitishwa na askofu wa Morogoro, hao wachague katibu, walinzi na makamu wao, walezi na wengineo, afadhali kati ya wenye ahadi ya daima.

8.5.3. Wachaguliwe ndugu ambao wanathamini wito wetu, wanazingatia hali ya Kanisa na jamii, wako tayari kujadiliana na kushirikiana na wote.

8.5.4. Hao wote wanadumu miaka mitatu, halafu wanaweza kuchaguliwa tena mara mbili mfululizo katika kazi ileile; baada ya hapo wapumzike walau mwaka mmoja.

8.5.5. Katika uchaguzi wowote tuwe na nia njema na kufuata taratibu za Kanisa na za kwetu, pengine kisha kupata mapendekezo ya ndugu wengine; ziandikwe kumbukumbu zake ambazo zitunzwe katika masajili ya jamaa, pamoja na hati nyingine.

8.5.6. Tukiwa wadogo kweli, tusitamani kazi hizo wala tusizikatae kwa ukaidi, tukikubali kwa upendo matakwa ya Mungu kwetu na wajibu wa kutumikia wenzetu hata kwa kushika madaraka.

8.5.7. Katika kuzitekeleza tukumbuke daima wajibu wa kutunza siri.

8.5.8. Akiwa na sababu za haki, askofu wa Morogoro anaweza kumuondoa madarakani mtumishi, baada ya kuwasikiliza yeye na washauri wake.

8.5.9. Kwa manufaa ya jamaa, halmashauri kuu inaweza kumuondoa madarakani yeyote aliyechaguliwa nayo au kumhamisha kwingine.

8.5.10. Wadhifa wowote ukibaki wazi, pengo lizibwe na ndugu aliyechaguliwa na halmashauri kuu, ila wadhifa wa mtumishi ushikwe na mshauri mkuu wa kwanza, na wadhifa wa mshauri mkuu ushikwe na yule wa kwanza kati ya washauri wawíli wa akiba waliochaguliwa mapema na mkutano mkuu.

8.5.11. Hao wote walioziba pengo wadumu mpaka mkutano mkuu ujao, ambao ufanyike kama kawaida miaka mitatu baada ya ule uliotangulia.

8.5.12. Tunapotakiwa kujipanga kisheria, watangulie wenye ahadí ya daima kufuatana na tarehe ya kuiweka na ile ya kubatizwa, halafu ndugu wengine kufuatana na tarehe ya kuweka ahadi ya muda kwa mara ya kwanza na ile ya kubatizwa; nje ya liturujia wanaweza wakapewa nafasi ya pekee wenye madaraka utawani kadiri ya ngazi zao, lakini si kwa msingi wa daraja takatifu.

 

 

8.6. UMOJA WA UTAWA

 

8.6.1. Utawa wetu ni mmoja tu, ingawa tumegawanyika katika jamaa mbalimbali ambazo ushirikiano wake ufuate katiba hii na kuratibiwa na baraza linalokutanika mara moja kwa mwaka.

8.6.2. Katika baraza hilo kila jamaa, zikiwa ni pamoja na ile ya ulimwenguni, inawakilishwa na mtumishi pamoja na washauri wake; ila kwa kurekebisha katiba hii, na katika nafasi nyingine za pekee, waongezwe kwa kila jamaa ndugu watatu kati ya waliotangulia kuweka ahadi ya daima.

8.6.3. Baraza hilo halina mamlaka juu ya jamaa zenyewe, ila linasimamia hasa: malezi, ili kustawisha karama yetu; uundaji wa misheni mpya, ili kueneza Injili kwa mpango wa Kikanisa; halafu mgawanyo wa misaada ipatikanayo, ili kufanikisha shughuli hizo.

8.6.4. Ni juu ya baraza kukubali ombi la baadhi ya ndugu la kuanzisha jamaa mpya, na kuikataza jamaa fuIani isiendelee kupokea watakaji kuanza zoezi ikiwa imepatwa na uvuguvugu.

8.6.5. Ikíwa ndugu fulani ameshauriana na mtumishi wake na kuona ni vema ahamie jamaa nyingine ya utawa wetu aiombe halmashauri ya jamaa hiyo, ambayo ikimkubalia, kisha kupewa na mtumishi huyo taarifa zinazohitajika, impangie muda na masharti ya jaribio, ambalo likishindikana arudi katika jamaa ya awali.

8.6.6. Kwa sababu nzito askofu wa Morogoro anaweza kumteua mkurugenzi ambaye kwa niaba yake asimamie kwa muda utawa wote badala ya baraza, au jamaa mojawapo badala ya mtumishi.

 

 

8.7. JUMUIA ZA MAHALI

 

8.7.1. Jumuia zetu za mahaIi zina sura tofauti kwa kuwa ndipo mipango ya utawa wetu inapoitikia mahitaji ya Kanisa maalumu na watu wa utamaduni fulani, ndugu wakiwajibika siku kwa siku kutekeleza karama zao tofauti na kukomaa kwa umoja.

8.7.2. Kuunda jumuia ni juu ya halmashauri kuu, kisha kushauriana kwa wanabaraza, kuhakikisha mazingira yanafaa kwa maisha yetu na kupata kwa maandishi kibali cha askofu wa jimbo husika.

8.7.3. Kwa kawaida jumuia ziishi pembeni mwa vijiji, nazo ziwe na ndugu sita hadi kumi na wawili, ila monasteri na nyumba za malezi zinaweza kuwa na ndugu wengi zaidi wakihesabiwa wanaolelewa; kinyume chake makazi ya upwekeni yanaweza kuwa na ndugu watatu au wanne tu.

8.7.4. Mtumishi pamoja na halmashauri yake wajitahidi kuwapanga vizuri ndugu ili waishi Kiinjili kweli katika mazingira husika.

8.7.5. Wachague walinzi ambao wadumishe umoja na uaminifu wa wote, wakilinganisha hasa madai ya sala na ya utendaji.

8.7.6. Kwa faida ya maisha ya kidugu na ushuhuda wa Kikanisa, ikiwezekana kila jumuia inapoundwa ndugu zetu kadhaa wa ulimwenguni wahamie karibu nayo; makleri wanajimbo wafanye hivyo kwa ruhusa ya askofu wao.

8.7.7. Kínyume chake, jumuia mbalimbali za waliojiweka wakfu zisiishi kijiji kimoja, isipokuwa kwa lengo la kuboresha malezi au lingine muhimu.

8.7.8. Kisha kushauriana na askofu wa jimbo husika, jamaa moja inaweza kuhama nyumba au kuiachia jamaa nyingine, kadiri ya mipango ya baraza; hapo vitu vilivyopo nyumbani vigawiwe kidugu kati ya jamaa inayohama na jimbo, au kati ya jamaa hiyo na ile inayohamia.

8.7.9. Tufanye pia mipango ya kwenda kukaa kwa muda tu katika vijiji kimojakimoja, tukishika maisha yetu ya kijumuia, pamoja na kuwatembelea watu nyumbani kwao, na kuwakutanisha ili wasikilize Neno la Mungu na kushirikishana katika hali ya sala.

8.7.10. Baada ya kumaliza uchipukizi, ndugu wa kiume watakaopenda waruhusiwe kushika Kanuni ya Ndugu Wadogo iliyothibitishwa na papa Honori III, ili kufuata maisha yenyewe ya mtakatifu Fransisko yaliyoiga yale ya Mitume walipotumwa na Yesu safari ya kwanza.

8.7.11. Ili ndugu wa jamaa moja aweze kuishi kwa muda mrefu katika jumuia ya jamaa nyingine ya jinsia yake, anahitaji ruhusa ya watumishi wa pande zote mbili; ila ndugu yetu wa ulimwenguni inamtosha ruhusa ya mtumishi wa jamaa inayompokea.

8.7.12. Ndugu akitakiwa kuishi nje ya jumuia zetu kwa muda mrefu kwa sababu za afya au masomo, apangiwe na halmashauri ya jamaa ndugu wa kwenda naye na nyumba fulani ya kitawa; halafu aendelee kuwasiliana mara nyingi na mtumishi na ndugu wa jamaa yake kwa kuwa maisha ya kijumuia ni kiini cha wito na utume wetu.

 

 

8.8. BIKIRA MTIIFU

 

8.8.1. Aliposikia tu maneno ya malaika Gabrieli, Maria mnyenyekevu alipokea kwa moyo mkuu matakwa ya Mungu akijitoa mhanga kumtumikia katika nafsi na kazi za Yesu aliye mtumishi mtiifu.

8.8.2. Ili Mungu aweze kutimiza kazi aliyoianza ndani mwetu na kwa njia yetu, tujiachie kwa furaha mikononi mwa Baba, tukipokea yale yote anayotupa, tukimpa yale yote ambayo anatuondolea au kutuomba, tukikubali kwa imani tu atutumie anavyotaka, tukisikiliza na kutekeleza yale anayotuambia kwa njia ya viumbe vyake, hasa viongozi, tukimtolea akili na utashi, neema za kiroho na za kimaumbile katika kutimiza sawasawa yale tuliyoagizwa.

8.8.3. Kwa kurahisisha hayo, kila mmoja wetu aitikie upendo wa Mama Maria, akijiaminisha kwake kwa namna ya pekee ili asaidiwe naye kuwa sadaka ya upendo kwa Mungu na chombo cha amani yake kwa watu.

8.8.4. Hivyo kwa njia yake, Yesu ndiye atakayefikiri katika akili zetu, na kufanya kazi kwa mikono yetu, na kupenda kwa mioyo yetu.

8.8.5. Kutoka kwa Mama wa Kanisa tujifunze kufungamana na wenzetu kwa unyofu na upendo hata uhusiano kati yetu unapotakiwa kufuata sheria, kwa sababu upendo ndio utimilifu wa sheria.

 

 

 

9. KUWA MASHAHIDI WA KRISTO

 

9.1. UMISIONARI

 

9.1.1. Yesu aliwekwa wakfu kwa Roho Mtakatifu na nguvu akatangaze upendo wa Baba aliyemtuma; mwenyewe akajionyesha kuwa ni Habari Njema kwa watu wote kwa kuja kuwatafuta toka mbinguni na kutoa uhai wake kuwa fidia ya dhambi zao.

9.1.2. Kwa wokovu wa watu, ambao Mwana wa Mungu aliujali kiasi hicho, mzee wetu Fransisko alijisikia msukumo wa kuijaza Injili dunia nzima, akitamani kumwaga damu yake kama ushahidi bora wa ukweli na upendo.

9.1.3. Hivyo akaliamsha Kanisa litekeleze agizo la Kristo la kumshuhudia kwa wasiomjua ili ulimwengu wote ukisikiliza tangazo la wokovu uamini, ukiamini utumaini, ukitumaini upende.

9.1.4. Tunapofanya kazi hiyo, ambayo bado sana, papohapo inabidiisha na kukomaza imani yetu tunayotaka kuwashirikisha wengine, na inaimarisha umoja kati yetu.

9.1.5. Tuizingatie upeo ili makabila yale ambayo bado yampokee Mwokozi pekee, na kufurahia ukweli wote wa Mungu aliye Baba yetu mwema, na kuingizwa kwa maji na Roho Mtakatifu katika umoja wa familia yake yakiiletea utajiri wa tunu zao.

9.1.6. Hatuwezi kuwaongoa watu tusipotubu wenyewe kila siku, wala hatuwezi kuwa wamisionari tusipokubali kwa moyo maisha yetu yabadilike kwa kushikamana na watu tunaowatafuta, tukiingia kwa unyenyekevu katika utamaduni wao ili kuchochewa nao na kuumua kwa chachu ya Injili iliyokwishafanya kazi ndani mwetu.

9.1.7. Tukifungamana hivyo na watu wowote tutawasaidia pia kukaribiana, kuchanga mema yale mbalimbali waliyojaliwa, na kuunda utamaduni wa upendo.

9.1.8. Tutumie sana nyimbo na muziki, michezo na maigizo, michoro na mithali, hadithi na njia nyingine rahisi za kupashana habari ili tuwashirikishe wote hekima ya utamaduni uliostawishwa na imani ya Kikristo, ili ikoleze mioyo ya watu na miundo ya jamii.

9.1.9. Tukiitegemea hazi ya Roho Mtakatifu ndani ya wote, na kuziheshimu dhamiri zao, tujadiliane kwa wema na busara na wanaofuata dini za jadi, wanaojitahidi kumtii Mungu katika Uislamu, wanaomtafuta kwa moyo mnyofu, waliomsahau maishani na wengineo wowote, ili tuelewane nao mpaka ndani kama marafiki na kuongozana nao katika kumrudia aliyetuumba wote sawa.

9.1.10. Upendo wetu mpole mnyenyekevu katika kuwatolea ujumbe wa wokovu utawasaidia kuupokea kwa mikono miwili wakitambua kuwa ndio unaoshibisha kweli njaa ya roho zao.

9.1.11. Tuwaombee wamisionari wengine, tukifuata habari zao na kuwapokea kwa furaha wakifika kwetu.

9.1.12. Ingawa si wengi sana wanaojaliwa neema tukufu ya kumfia Yesu mwishoni mwa safari yao, ni lazima wote tuwe tayari kujitoa mhanga kwa ajili ya wenzetu na kumuungama Kristo mbele yao, tukifurahi kumfuata kwenye njia ya msalaba ambao wanafunzi wake halisi hawapungukiwi kamwe.

 

 

9.2. SALA NA UTUME

 

9.2.1 Sala ilimtegemeza Yesu daima, katika utume na katika mateso; ndiye kielelezo cha umoja unaohitajika maishani kati ya kuungana na Baba na kutenda mengi.

9.2.2. Kwa kuwa upendo ni mmoja tu, kumkazia macho Bwana kusipunguze juhudi zetu kwa ajili ya binadamu walio mfano wake, bali kumjua Mungu mpaka ndani na kupokea upendo wake kutusukume kuwashirikisha wengine mang’amuzi hayo, yaliyo utajiri wetu pekee, na chemchemi ya furaha tusiyoweza kunyang’anywa.

9.2.3. Tujitahidi kuwa wanasala hodari katika umisionari na wamisionari hodari katika sala, tukitunza muda wa kuongea na Mungu kwa niaba ya watu, na tukitumia vizuri muda wa kuwashughulikia watu kwa ajili ya Mungu.

9.2.4. Mchanganuo huo mzuri utaziwezesha juhudi zetu katika sala na toba kutakasa na kustawisha utume hata ukiwa mgumu namna gani; hapo utume utailetea sala bidii mpya; isipotokea hivyo maana yake tumekwama kiroho na kiutume.

9.2.5. Mara kwa mara tumrudie katika sala yule aliyetutuma ili tupime pamoja naye kazi yetu, tukijikumbusha tulivyo vyombo vyake vya udongo tu, na tukimshukuru kwa yale anayoyatenda kwa njia yetu.

 

 

9.3. NENO LA UZIMA

 

9.3.1. Kama vile Yesu alivyokuwa hachoki kuwatolea watu Injili, wakiwa mmoja mmoja au katika umati, sisi sote tutumie sawasawa kila nafasi ya kuieneza, tukijua wokovu unatokana na imani, nayo imani inatokana na kusikiliza ujumbe.

9.3.2. Hakuna jina lingine la kulishuhudia au neno lingine la kulitangaza, ila Yesu aliye Neno la uzima, kwa kuwa aliupokea uzima wa Baba akaja kutushirikisha uzima huo kwa njia ya Roho Mtakatifu na sakramenti za Kanisa.

9.3.3. Upendo wake unatusukuma kumtangaza hasa kwa wasio Wakristo, kwa sababu wote wana haja na haki ya kumjua yeye aliye kiini na lengo la viumbe vyote: hakuna huduma nyingine muhimu zaidi.

9.3.4. Tuwasaidie wote kukutana naye kweli na kumkimbilia katika shida, ili watambue kuwa ndiye anayewaokoa na kuwapenda, anayewajalia mvua na uhai, watoto, afya na maendeleo, na ndiye anayewakomboa kutoka dhuluma na utumwa wowote.

9.3.5. Tuna deni hilo kwao: ole wetu tusipowapasha habari njema katika mazingira yao ili waambatane kweli na Yesu na Injili yake kwa imani, kwa sakramenti na kwa matendo!

9.3.6.Katika ibada za Jumapili, mafundisho ya kuandalia sakramenti mbalimbali, na vipindi vya dini shuleni, tuwazoeshe waamini kuelewa Maandiko Matakatifu na imani ya Kanisa tangu utotoni kabisa, na tuwahimize kujitolea mapema katika utume.

9.3.7. Imani ionyeshwe daima kuwa ni zawadi ya Mungu inayotakiwa kuenezwa, kuadhimishwa na hasa kutekelezwa kwa pamoja katika familia, parokia, jumuia na vyama mbalimbali, kwa kuwa uzima wa milele tulioahidiwa unayatia maanani maisha ya hapa duniani, na kutudai tuitikie sasa wito wa kuwa wana wa Mungu kwa kuongozwa na upendo kwa Baba na kwa ndugu wote.

9.3.8. Shukrani na furaha tulizonazo kwa kuumbwa zinatutuma kumshirikiska kila mtu hata aheshimu, alinde, apende na kutumikia uhai wa mwenzake yeyote, na ashike amri nyingine za Mungu ambazo kwa pamoja zinatuhakikishia uzima.

9.3.9. Tuwajulishe wote vilema na maadili, adhabu na utukufu wa milele, kusudi mbele ya Yesu msulubiwa watambue kwa unyofu uovu wa dhambi na njia ya wokovu.

9.3.10. Tuwe tayari kushirikiana na wenye mitambo ya vyombo vya upashanaji habari, vinavyotengeneza kwa kiasi kikubwa utamaduni wa umati, na tuwaelekeze watu kuvitumia kwa faida, si kwa kujiangamiza.

 

 

9.4. USHUHUDA WA UTAKATIFU

 

9.4.1. Tunaishi kwa nguvu ya Neno, tunafurahia uwepo wake ndani mwetu, tunasafiri pamoja naye na kushiriki utume wake alioufanya kwa kujishusha moja kwa moja badala ya kutegemea uwezo wake tu.

9.4.2. Juhudi zetu za kumzingatia daima Yesu na mifano aliyotuachia ili tufuate nyayo zake, zinatuelekeza kufanya shughuli ambazo hazihitaji vifaa vingi na uwezo wa kibinadamu, bali pamoja na bidii zinadai hasa imani kuwa anayeeneza kweli Injili ni Roho Mtakatifu.

9.4.3. Tufuate kwa makini uongozi wake ili atulinganishe na yule tunayetaka kumshuhudia, kusudi ndani mwetu, katika jumuia na katika Kanisa, watu wamuone na kumpenda Yesu na kushangaa maajabu anayoyatenda katika udhaifu wetu, sisi watumishi wa bure.

9.4.4. Tuwaonyeshe hasa upendo mkubwa wa kidugu, tukijua binadamu wanawaamini mashahidi kuliko walimu, na kuzingatia matendo kuliko maneno, na kuguswa wakiona namna bora ya kuwapokea na juhudi kwa ajili ya maskini, wadogo na wenye shida.

9.4.5. Tusisahau kuwa wito wa umisionari unatokana na ule wa utakatifu, kwa sababu msingi na sharti la kazi ya wokovu, na kipimo cha utekelezaji wake si utendaji mwingi, bali ni upendo.

9.4.6. Kadiri tunavyoupokea upendo wa Baba na kumrudishia kwa uaminifu alivyofanya Mwana hadi msalabani, tuwe na hakika ya kuwashirikisha watu uzima wa Utatu mtakatifu kwa uweza wa Roho, hata tusipoona mafanikio yoyote.

 

 

9.5. HUDUMA MBALIMBALI

9.5.1. Tufanye juu chini ili jumuia ndogondogo za Kikristo ziwe hai, kwa kuwa ndipo watu wanapojifunza kutekeleza upendo kwa wote, na kuishi kama familia ya Mungu, wakimtii Baba, wakimfuata Mwana na kuungana katika Roho.

9.5.2. Upande mwingine, Kanisa litastawi hivyo ikiwa tu familia za Kikristo zitakuwa kweli vikanisa vya nyumbani, shule za Injili, patakatifu pa uzima na misingi imara ya jamii.

9.5.3. Kwa mfano wa familia takatifu iliyokimbilia bara letu, tuwasaidie baba, mama na watoto kukuza upendo kati yao na tunu nyingine zinazofanya maisha kuwa zawadi ambayo tunaipokea na kuwashirikisha wengine.

9.5.4. Tuadhimishe vizuri sakramenti ili zituwezeshe sisi na wenzetu kuzikabili hatua na hali mbalimbali za maisha pamoja na Bwana msulubiwa na mfufuka.

9.5.5. Ndugu makleri waheshimu sana daraja yao ambayo imewafanya kitu kimoja na makleri wote, na kuweka wokovu wa watu hasa mikononi mwao; watimize kazi yao kitakatifu, kwa ukarimu na kulingana na karama yetu ya Kifransisko.

9.5.6. Ndugu wanaowajibika katika vitendo vya huruma ya kiroho na ya kimwili, washiriki zaidi katika uchungaji wa Kanisa kwa kuwaelekeza watu kwenye imani na sakramenti zake.

9.5.7. Ndugu wale ambao hawawezi kutenda kazi za kitume au wamejifunga kusali tu, kadiri wanavyoishi kwa ajili ya Baba, walivyonaswa na upendo wa Yesu na wanavyoongozwa na Roho Mtakatifu, wanachanga umisionari wetu kwa njia bora isiyoelezeka.

9.5.8. Hivyo kwa njia mbalimbali kila jumuia yetu itaeneza katika mazingira yake uzima wa Kristo mfufuka.

 

9.6. MPANGO WA KIKANISA

 

9.6.1. Kwa moyo uleule wa Yesu na wa Mama Kanisa wa kutaka wokovu umfikie kila mtu, tuangalie tusilemewe na miundo yetu, wala tusimezwe na ile ya majimbo, bali tuwe wepesi wa kwenda kokote duniani ili umati wa watu hoi kama kondoo wasio na mchungaji utambue tena huruma ya Yesu.

9.6.2. Tuwaombe wale wanaoratibu umisionari wa Kanisa watutume hasa kushika nafasi ngumu, kati ya watu fukara wa bara letu au wenye asili ya Kiafrika, waliosahaulika zaidi au waliolazimika kuhama nchi yao, ili tuwasaidie tunavyoweza mpaka watakapopata uchungaji wa kawaida.

9.6.3. Tuchochee moyo wa kimisionari hata katika Makanisa machanga, na kushiriki kikamilifu katika kuandaa na kutekeleza mipango ya askofu na ya paroko, jinsi inavyotufaa sisi ndugu wadogo, bila ya kudai malipo, kwa ushirikiano mzuri na waamini wenzetu, tukishika nafasi yetu maalumu na kuwasaidia washike vema nafasi zao mbalimbali.

9.6.4. Katika mkataba ambao inatubidi tuufanye na mkuu wa kila jimbo tunamokwenda kuishi, izingatiwe kuwa huduma yoyote ambayo tuitoe inatakiwa kulingana na karama maalumu tuliyokubaliwa, kwa sababu ustawi wa Kanisa unategemea hasa vipaji vile mbalimbali ambavyo Roho anawagawia waamini, hao wakivipokea na kushirikishana kwa mikono miwili.

 

 

9.7. NYOTA YA KUONGOZA KWA KRISTO

 

9.7.1. Bikira Maria ni mfano bora wa ule upendo wa kimama ambao wawe nao wanaoshiriki katika Kanisa kazi ya kuzaa upya watu na kutunza uzima wao wa Kimungu.

9.7.2. Tukiwa mitume pamoja na Maria, tuwe pia mitume wake, tukimtoa kama zawadi kwa watu wapate kumjua na kumpenda na kuongozwa naye kwa Mwanae.

9.7.3. Maana roho ya ibada kwa Bikira mwenye heri, chini ya ile kwa Mkombozi, inafaa sana kuunda imani na mwenendo wa Kikristo, kwa kuwa Maria ni muhtasari wa mafundisho ya Yesu na picha yake inayotuvutia kutamani ukamilifu wa maadili yake yote, hasa upendo.

LINKS:

 

WIMBO WA TAIFA

Mungu Ibariki Afrika

Wabariki viongozi wake

Hekima, umoja na amani

Hizi ni ngao zetu

Afrika na watu wake. 

CHORUS:    

Ibariki, Afrika

Ibariki, Afrika

Tubariki, watoto wa Afrika

Kiroka: un gruppo di famiglia al termine degli esercizi spirituali annuali 2003. - Kiroka: picha ya pamoja mwishoni mwa mazoezi ya kiroho ya mwaka 2003. - Kiroka: a picture all together at the end of the spiritual exercises of the year 2003.