Ndugu Wadogo Wa Afrika

SAFARI YA MALEZI

ya Utawa wa Ndugu Wadogo wa Afrika

 

 

 

YALIYOMO

 

 

0. UTANGULIZI

 

1. KUSHIKA INJILI

 

2. KUENEZA INJILI

 

3. WATENDAJI

 

4. UTU NA UKRISTO

 

5. HATUA ZA KUINGIZWA

 

6. MALEZI YA KUDUMU

 

7. HATIMA: MAMA MARIA

 

 

 

 

 

0.    UTANGULIZI

 

0.1.           AINA ZA UFUASI

 

Yesu, Mwana wa Baba, ndiye ukombozi na ukamilifu wetu.

Kadiri ya matakwa ya Baba na kwa msukumo ya Roho Mtakatifu, kila wakati wanapatikana waamini ambao wanamfuata Yesu na kushuhudia fumbo lake kwa namna mbalimbali, hasa: walei kwa kuratibu malimwengu, wenye daraja kwa kutoa huduma walizokabidhiwa mitume, na wanaoshika mashauri ya Kiinjili kwa kufanana zaidi na Yesu safi, fukara na mtiifu ili wote watambue kuwa kweli yu pamoja nasi hata mwisho wa dunia.

 

 

0.2.           KARAMA YETU

 

Mungu Baba ametujalia tuanzishe chama cha kimisionari chenye jamaa mbalimbali ndani yake, ambamo tufuate nyayo za Mwanae katika kujishusha mfululizo ili kutumikia kwa upendo hata kufa msalabani.

Sisi sote wanachama tuishi kati ya watu wa nyakati zetu tukiwa na msimamo huohuo aliokuwanao yeye, ingawa kila mmojawetu kadiri ya hali maalumu aliyonayo ndani ya Kanisa, kama mlei, kleri au mshikamashauri ya Kiinjili.

Tarajio la chama ni kujaliwa kwa wingi mashahidi wa imani ambao wamelishwa sana Injili hata waweze kuishi kama ndugu wadogo wa wote, tena kwa namna bora zaidi na zaidi, katika mazingira mbalimbali watakayopangiwa.

 

 

0.3.           SAFARI HII

 

Kwa ajili hiyo yanahitajika malezi ambayo yafuate maelekezo ya Kanisa na kulingana na karama yetu maalumu, tusiisawazishe na miito mingine tusije tukamzimisha Roho Mtakatifu na kulidhoofisha taifa la Mungu.

Malezi hayana mwisho kamwe: ingawa kuna hatua za kupigwa, ni mtiririko mmoja tu wa ustawishaji wa maadili n.k.

Ulinganifu wa malezi ya Kiroho, ya kitume, ya kielimu na ya kiufundi utusaidie tangu tunuie kukomaa ndani ya Kristo mpaka tukutane naye moja kwa moja kwa kupokea ndugu kifo.

 

 

0.4.           MIONGOZO MAALUMU

 

Mpango huu unakusudiwa kuonyesha wazi namna ya kuchochea karama yetu.

Upande mmoja utuonyeshe namna ya kuitekeleza katika hatua mbalimbali za maisha hadi kufikia utakatifu.

Upande mwingine utuonyeshe namna ya kuishirikisha kikamilifu kwa vizazi vijavyo viweze kuitimiza katika utamaduni wowote, kwa kuwa Ufransisko unafaa kuutakasa na kuuboresha kila utamaduni kwa chumvi na chachu ya Injili, bila ya kukwama katika wowote ule.

Lakini malezi hayawezi kupangwa jumla tu, pasipo kuzingatia wahusika ni wepi na wanaishi wapi: kwa hiyo mpango huu utimilizwe na halmashauri kuu kwa kila jamaa, hatua na nyumba.

Miongozo yake hiyo iwe sahili, mifupi na wazi, ilingane na mpango huu halafu ipitiwe kwa marekebisho kila baada ya miaka mitatu.

 

 

 

 

1. KUSHIKA INJILI

 

1.1.           UTATU NA UTAWA

 

Karama yoyote ya kitawa inaongoza kwa Baba, ikitia hamu ya kutimiza matakwa yake yote: humo utiifu unazaa uhuru wa kweli, useja mtakatifu unatokeza jinsi moyo usivyoweza kutosheka na upendo wa viumbe, na ufukara unachochea njaa ya haki aliyoahidi kuishibisha.

Halafu inaongoza kwa Mwana, ikirahisisha ushirika wa ndani naye, katika kuwatumikia kwa bidii Mungu na watu, na katika kusali na kuteseka ili kueneza ufalme.

Hatimaye inaongoza kwa Roho Mtakatifu, ikiandaa kujiachia kwake na kutegemezwa naye katika maisha ya Kiroho, ushirika wa kidugu na utume.

 

 

1.2.           KARAMA ZA KITAWA

 

Namna mbalimbali za kuishi kitawa zinatokana na karama maalumu ambazo waanzilishi walijaliwa na ambazo wafuasi wao wakashirikishwa ili wazitekeleze, wazitunze, wazichimbe na kuziendeleza mfululizo kulingana na ustawi wa Mwili wote wa Kristo.

Kanisa linataka kila utawa ustawi kadiri ya karama hai na bunifu ya mwanzilishi, kufuatana na mapokeo yake maalumu ya Kiroho, ya kijumuia na ya kitume.

Hivyo sio tu kwamba tuna historia tukufu ya kuikumbuka na kuisimulia, bali pia tunayo nyingine ya kuitimiza bado ili katika milenia mpya ulimwengu uliokabidhiwa mikononi mwetu binadamu uwe na imani na upendo, haki na amani zaidi, uwe kama utangulizi wa ulimwengu ujao.

Roho anatusukuma tukafanye makuu, hivyo tuitazame kesho kwa tumaini.

 

 

1.3.           UTAWA NA NYAKATI ZETU

 

Tumeitwa tutambue na kuhudumia mpango wa Mungu kwa ajili ya watu, ambao unatangazwa na Maandiko Matakatifu na kujitokeza katika maisha yao.

Kwa hiyo tuwe tayari kuchochewa na Neno la Mungu na ishara za nyakati, tukiunganisha daima upya wa Kiroho na ari ya kitume, ambavyo cha kwanza kinawezesha cha pili.

Tumshiriki Mungu ili kukabili changamoto za nyakati zetu, tukiamini ya kuwa Roho anaweza kutoa majibu ya kufaa hata kwa zile ngumu zaidi.

Mbele ya changamoto kuu tatu za ulimwengu tuonyeshe jinsi mashauri ya Kiinjili yanavyotustawisha kwa kutuelekeza moja kwa moja kwa Mungu aliye Wema mkuu, badala ya kufuata mielekeo ya kibinadamu iliyoathiriwa na dhambi.

Hasa siku hizi wanahitajika watakatifu ambao watumainishe wale waliokata tamaa kuhusu maisha na maana yake: ubora wa utawa unaweza kuwatuliza wale wanaoona kiu ya tunu halisi.

 

 

1.4.           USEJA MTAKATIFU NA UTAMADUNI WA ANASA

 

Changamoto ya kwanza ni utamaduni wa anasa unaoona jinsia ni mchezo tu usio na masharti: matokeo ni maovu ya kila aina yanayoathiri kinafsi na kiuchumi jamii, familia na watu mmojammoja, kuanzia watoto.

Itikio la maisha ya wakfu ni kuishi useja mtakatifu kwa furaha, na hivyo kushuhudia uwezo wa Mungu unaofanya kazi katika udhaifu wa binadamu hata akampenda yeye kuliko yote na kumpenda yeyote kwa uhuru wa wanae.

Ushuhuda huo unahitajiwa na wote kadiri wanavyoshindwa kuuelewa, ili wajifunze kuwa wa kweli katika mafungamano.

Mapendo yao ya kibinadamu yanapewa kielelezo cha yale safi ya mtawa ambaye anachota katika Mungu-Upendo: kwa kuzama katika fumbo la Utatu anajisikia apende wote pasipo mipaka na kwa kujitawala.

Hakika, usafi unaukomboa moyo kwa namna ya pekee na kuzidi kuuwasha upendo kwa Mungu na kwa watu wote.

Mchango mmojawapo mkubwa wa mtawa ni kuonyesha kwa maisha yake uwezekano wa kujitoa kwa wengine na kushiriki furaha na huzuni zao kwa uaminifu na udumifu, pasipo vitendo vya jinsia wala misimamo ya utawala na ubaguzi.

Pia utawa unamaanisha na kuelekea moja kwa moja uzima wa milele, hasa kwa njia ya useja unaotugeuza tayari kwa ajili ya ulimwengu ule ambapo watu hawaoi wala hawaolewi.

 

 

1.5.           KUZINGATIA TUNU NA GHARAMA YAKE

 

Kwa kuwa useja huo unadai usafi kamili na kuyahusu sana maelekeo yetu ya dhati, wanazoezi wasiuahidi wala wasikubalike kabla ya kujaribu vya kutosha na kufikia ukomavu wa kufaa upande wa nafsi na wa hisi za moyo.

Watambue kwamba elekeo la umimi tulilonalo linataka tutie maanani mno mapendo ya kibinadamu, na kumtumia mwenzetu kama njia ya kujipata heri fulani.

Lakini wasiangalishwe tu kuhusu hatari zinazowakabili, bali walelewe kukumbatia useja kwa ajili ya ufalme wa Mungu, kama tunu kwa ustawi wao na wa Kanisa.

 

 

1.6.           MALEZI YA USEJA

 

Malezi ya useja mtakatifu yajitahidi:

- kuchochea furaha na shukrani kwa upendo ule ambao kila mmoja ametazamwa na kuteuliwa na Yesu;

- kuangazia matunda ya moyo usiogawanyika, yaani uzazi mwingi wa Kiroho hasa katika utume;

- kuhimiza adhimisho la upatanisho, uongozi wa Kiroho na upendo halisi katika jumuia;

- kujenga hali ya kuaminiana kati ya walelewa na mlezi, ambaye awe tayari kusikiliza yoyote kwa upendo ili aangaze na kutegemeza;

- kumsaidia kila mmoja akubali mang'amuzi yake mabaya ya zamani kwa kutambua udhaifu, kujinyenyekeza na kukesha;

- kumshukuru Mungu tu na kuzuia kiburi cha kujipongeza kwa usafi, usije ukazua ugumu wa moyo;

- kufundisha juu ya jinsia mbili upande wa mwili, nafsi na roho;

- kueleza maana ya mwili na namna ya kutunza afya yake;

- kuelekeza kujitawala upande wa ashiki na wa moyo, na vilevile upande wa ulafi na ulevi;

- kuwa waangalifu katika kutumia vyombo vya upashanaji habari na katika mafungamano na watu (busara inawadai watumishi, walinzi na walezi pia wachukue hatua za kufaa).

 

 

1.7.           UFUKARA NA UTAMADUNI WA FEDHA

 

Changamoto ya pili inatokana na ulimwengu kuabudu pesa na mali, kwa kutoelewa maana yake kwa maisha, wala kufuata kiasi kinachofaa, wala kujali mahitaji na mateso ya wanyonge, wala kuhifadhi mazingira kwa ajili ya wajukuu wetu.

Hivyo leo ufukara unatawala maisha ya watu wengi na ya nchi nyingi kwa sababu ulimwengu unaendeshwa namna inayozidisha hali ya njaa, ujinga, maradhi, kukosa kazi, kunyimwa haki za msingi, ukoloni mamboleo, rushwa n.k.

Itikio la maisha ya wakfu ni ufukara wa Kiinjili ambao upendo unahimiza kupokea mlio wa wenye mashaka katika matatizo, mateso na matarajio yao ili kuwasaidia wakabili maisha kwa mshikamano wa wote.

 

 

1.8.           YESU NA UFUKARA

 

Asili ya ufukara huo wa Kiinjili ni kutafakari alivyoishi Yesu fukara msulubiwa; udhihirisho wake ni kushika maisha ya kawaida ya watu wadogo kuhusu chakula, mavazi na nyumba, na kukwepa uwezo wowote wa kutawala wengine kisiasa, kijamii, kiuchumi, kielimu na kidini.

Moyo wa maskini tu ulioamua kumfuata Yesu hivyo unaweza kushikamana na watu usiambatane na vitu.

Jumuia ndogo za kitawa katika mazingira duni zinatokeza ule upendeleo wa Kiinjili kwa fukara, unaotufanya sio tu tuwashughulikie, bali tuishi pamoja nao, tena sawa nao kadiri inavyofaa kulingana na hali halisi na mahitaji ya kila mmojawetu, hasa akiwa bado katika hatua za kuingizwa.

Upendeleo huo unatokana na upendo ambao Yesu aliuishi, hivi kwamba kila mfuasi wake anapaswa kuwa nao, hasa sisi tunaomfuata kwa karibu zaidi katika maisha ya wakfu, ambayo ni ya kifukara na ya kuwatetea fukara.

Mshikamano nao ndio msimamo unaotufanya ndugu wadogo, ni mhuri wa Ukristo halisi, kichocheo cha wongofu, tendo la kitume na thibitisho la ujio wa ufalme wa Mungu, ambapo fukara wanahubiriwa na kuhubiri Injili.

Zaidi ya hayo ufukara wenyewe ni tunu iliyotangazwa na maisha yote ya Yesu kama heri ya kwanza na ushuhuda wa kuwa Mungu ndio utajiri pekee wa moyo.

 

 

1.9.            MALEZI YA UFUKARA

 

Malezi ya ufukara yakazie maisha ya Yesu aliyejifanya maskini kwa ajili yetu.

Halafu yahimize:

- kuwa na unyenyekevu;

- kuishi kwa imani kama wana wa Baba wa mbinguni anayejua mahitaji yetu na kututunza siku kwa siku;

- kuwajibika katika kazi;

- kujali vitu vinavyopatikana jumuiani;

- kutaka vyote viwe kweli vya wote ili kila mmoja apate anavyohitaji;

- kutumia fedha na vitu kwa usimamizi wa viongozi;

- kubana matumizi iwezekanavyo, bila ya kufuata uwezo uliopo wala ruhusa tu;

- kuwa tayari kukosa vitu mbalimbali;

- kujiepusha na vitu ambavyo watu wadogo hawawezi kujipatia, ili kuishi ufukara kwa ukweli zaidi;

- kujinyima kwa hiari hata vitu halali.

Pia yazingatie:

- historia ya kila ndugu kabla ya kupata wito (wengine walijitegemea na kupata vingi, kumbe wengine walikuwa na hali ngumu kuliko ile ya jumuia);

- hali ya sasa ya familia yake na matarajio iliyonayo juu ya mwanae;

- mafundisho ya Kanisa kuhusu jamii, kwa kuwa ufukara wetu haulengi maendeleo ya roho tu.

 

 

1.10.       UTIIFU NA UTAMADUNI WA UHURU USIO NA MASHARTI

 

Changamoto ya tatu inatokana na mtazamo ambao unadai hiari ya mtu isibanwe sana na maadili, na hivyo unasababisha kwa wingi ubinafsi, dhuluma, ukatili n.k.

Itikio la kufaa ni utiifu wa kitawa unaoonyesha kwamba kutimiza matakwa ya Mungu kunatukamilisha kwa kukuza ukweli wetu kama viumbe tunaomtegemea kabisa Muumba, na kama watoto wapenzi tunaotafuta na kutekeleza kwa pamoja yale yote yanayompendeza Baba.

Umoja huo wa jumuia ni ishara kubwa ya jinsi ya kushinda ugomvi na utengano, na ni hakika ya kufuata njia tuliyopangiwa.

Katika malezi na maisha ya kila siku, chama kinatusaidia tupate msimamo wa kudumu, kwa mafundisho ya hakika kuhusu kufikia ukamilifu, kwa ushirika wa kidugu katika kumfuata Yesu na kwa utiifu unaoimarisha hiari yetu katika kuitikia wito.

 

 

1.11.       KUSHIRIKI UTIIFU WA YESU

 

Shauri hilo, tunalolipokea kwa upendo ili kumfuata Yesu aliyetii hata kufa msalabani, linatuelekeza tuweke matakwa yetu chini ya yale ya wakili wa Mungu, yaani mlinzi, mtumishi, askofu na hasa Baba Mtakatifu.

Utiifu huo hautudhalilishi bali unastawisha uhuru wetu kama wana wa Mungu wanaoendeleza ule wa Yesu kwa wokovu wa ulimwengu.

Nidhamu utawani isishikwe tu ili kulinda maisha ya kijumuia na upendo, bali kama sharti la kujijengea tabia ya kujitawala, kukomaa n.k.

Hivyo itekelezwe namna inayostawisha utayari wa kutii si kwa hofu, bali kwa kufuata dhamiri na maadili.

Polepole ndugu wazoee kutumia vema hiari yao katika kujifanyia mipango na kutenda kwa uelewano na watu wa ndani na wa nje ya jumuia, hasa viongozi.

Mtumishi au mlinzi anayejadiliana na ndugu zake anawasaidia kutii kwa uwajibikaji, mradi hatimaye awe tayari kutoa uamuzi na kuagiza la kufanya kwa niaba ya Mungu.

Katika majadiliano hayo tuzuie mawazo ya kibinadamu mno yasijiingize upande wa kiongozi wala wa ndugu wala kati yao, bali wote tulenge tu matakwa ya Mungu yafanyike.

 

 

1.12.       MALEZI YA UTIIFU

 

Katika malezi ya utiifu tukumbuke kwamba:

- ni lazima kwanza tutambue na kutambuliwa hadhi yetu kama watu na watoto wa Mungu ili tutii kibinadamu, si kwa unyonge;

- tunapaswa kuvuka toka yale yanayotupendeza sisi hadi yale yanayompendeza Mungu, ambayo yanajitokeza kwa namna ya pekee kwa njia ya wachungaji wa Kanisa na ya kanuni na katiba walizotuthibitishia;

- ushuhuda wetu kama watawa watiifu una uzito kuliko nadharia tunayowafundisha walelewa, ingawa hao wanatakiwa kufuata njia nyofu bila ya kukwazwa na mifano yetu mibaya.

 

 

1.13.       USHUHUDA WA JUMUIA

 

Kwa kuwa tendo la kuweka ahadi linatuingiza katika chama kwa haki na wajibu vinavyoelezwa na katiba, tunapaswa kuishi kidugu katika jumuia yake mojawapo kama mahali ambapo upendo, ukichota nguvu katika sala, uongoze maisha yote na kuzaa heri.

Hivyo uanachama unatuwezesha kumpatia Yesu ushuhuda wa hadhara na wa pamoja, mradi maisha yetu yawe ishara ya ufalme wa Mungu na tangazo hai la Injili.

Kwa ushuhuda huo wa jumuia zilizojaa furaha na Roho Mtakatifu, ambapo ubinafsi unashindwa na uwajibikaji kwa ajili ya wengine, ambapo madonda yanaponywa na msamaha, na ambapo karama inaongoza uaminifu wa wote katika wito na utume, ndivyo Kanisa linavyojitambulisha kama sakramenti ya umoja na Mungu na kati ya watu, na kuonyesha matunda ya amri mpya aliyotuachia Bwana.

Pamoja na hayo, Kanisa linataka kuonekana wazi ulimwenguni hata kwa njia ya kanzu zetu.

 

 

1.14.       KATIKA USHIRIKA WA KANISA

 

Maisha ya Wakristo wa kwanza huko Yerusalemu ndiyo kielelezo ambacho Kanisa lilikizingatia kila lilipojaribu kuchochea ari ya mwanzoni na kuendelea Kiinjili safari yake.

Kwa mfano wao tuzidi kuchanga na waamini wote neema na juhudi ili sura ya Kanisa ipendeze, nalo likabili kwa nguvu ya umoja changamoto za nyakati zetu.

Basi, tusimbane Roho katika chama chetu, lakini tusaidie wengine kufaidika na karama yetu.

Sisi watawa tunaitwa kuwa wataalamu wa ushirika, mashahidi na wajenzi wa ule umoja ulio lengo la mpango wa Mungu: tuwe hivyo kutokana na tamko letu la kushika mashauri ya Kiinjili ambayo yanakomboa ari ya upendo isiwe na kizuio chochote; tena kutokana na mang'amuzi yetu ya kila siku katika kuishi, kusali na kufanya kazi kama jumuia ya Kikanisa.

Kwa namna ya pekee ushirika wa Kanisa unatudai utiifu wa akili na moyo kwa maaskofu, ambao utekelezwe mbele ya watu wote, hasa tukishughulikia katekesi, ufundishaji, uandishi na upashanaji habari.

Msimamo wetu watawa kuhusu jambo hilo ni muhimu kwa sababu tuna nafasi maalumu katika Kanisa na katika kushiriki utume wa maaskofu.

 

 

1.15.       WANDANI WA MUNGU

 

Ili tujaliwe kuwa kweli manabii, yaani kusema na wote kwa niaba ya Mungu, kwanza ni lazima tuwe wandani wake, wasikivu kwa Neno lake katika nafasi yoyote ya maisha, wenye utambuzi wa Kiroho na kupenda ukweli.

Basi, tuzidi kumuelekea Mungu, tukitafuta uso wake, tukiachana na mitazamo isiyolingana na ufunuo wake, halafu kubadili mwenendo wetu pia.

Tukiwa wanafunzi wa Neno linalotolewa na Kanisa, tunakua kumuelekea Kristo katika yote hata tufikie kimo cha utimilifu wake, tukizidi kujifunza fumbo la wokovu, kumuabudu Baba katika Roho na Ukweli, na kutekeleza ukweli kwa upendo.

 

 

1.16.       TOBA YA KUDUMU

 

Ili tuwe mashahidi halisi wa Kristo duniani kote, kwanza tunapaswa kuhakikisha tumeitwa na Mungu na kumtolea nafsi yetu pamoja na yote tuliyonayo, hasa yale yanayotuzuia tusimuitikie kikamilifu.

Wito wetu wa toba ya kudumu unataka turekebishe mfululizo uhusiano wetu na Mungu, na watu na ulimwengu ili Mungu atawale moja kwa moja maisha yetu.

Kwa ajili hiyo tukiri kwa moyo udhaifu, ujinga na uovu wetu, halafu tupambane navyo kwa roho na kwa mwili pia, tukifuata kwa uaminifu kanuni, katiba, ratiba na mbinu za kufanya juhudi.

 

 

1.17.       MAISHA YA KIROHO

 

Daima maisha ya Kiroho yawe na nafasi ya kwanza katika malezi yetu ili chama kiwe hasa shule ya Injili.

Ukarimu kwa fukara, uzazi wa kitume, mvutio kwa miito na vinginevyo vinategemea ustawi huo wa ndugu mmojammoja na wa jumuia nzima katika kuishi ndani ya Kristo kadiri ya Roho Mtakatifu kwa utukufu wa Baba.

Tunafanya safari hiyo ya uaminifu mkubwa zaidi na zaidi kwa Mungu Baba tukiongozwa na Roho anayetulinganisha na Yesu katika ushirika kamili wa Kanisa.

Safari hiyo inadai wongofu wetu wa binafsi na wa kijumuia usikome kamwe, bali uzidi kukamilika kwa kulipokea Neno la Mungu mpaka ndani ya moyo wetu na ya utendaji wetu, na kwa kuupokea uvuvio wa Roho Mtakatifu kadiri tulivyojaliwa na Baba, aliye asili na lengo la maisha yoyote.

 

 

1.18.       NENO LA MUNGU

 

Neno la Mungu ndilo chemchemi ya kwanza ya maisha ya Kikristo: linachochea uhusiano wa dhati na Mungu aliye hai na utekelezaji wa matakwa yake yenye kuleta wokovu na utakatifu.

Ndiyo sababu toka mwanzo watawa waliheshimu usomaji wake wa Kiroho, hata hekima ikaangaza maisha yao.

Uzoefu na Neno uliwapa mwanga unaohitajika kwa utambuzi, wasilingane na mitindo ya ulimwengu.

Kwa mfano wa mwanzilishi wetu, tuitafakari hasa Injili ili kuzingatia matendo na maneno ya Yesu, Maria na mitume.

Kutafakari Neno na mafumbo ya Kristo kunaleta ari katika sala na utume; pia kutumia muda wetu miguuni pake ndio namna wazi ya kumtangaza Yesu kuwa ni Bwana wetu na kuwa yu hai kati yetu.

 

 

1.19.       USHIRIKISHANO JUU YA INJILI

 

Kwa kuwa maisha yetu ni ya Kiinjili hasa, tutie maanani ushirikishano wa mawazo na mang'amuzi kuhusu Injili.

Kuitafakari kijumuia kuna thamani kubwa kwa kutufanya tuchange kwa furaha utajiri tuliochota humo ili tukue pamoja na kusaidiana kidugu katika maisha ya Kiroho.

Tena, ushirikishano juu ya Neno unalisha imani na tumaini, kuheshimiana na kuaminiana, kupatana na kushikamana katika sala.

Halafu zoezi hilo linatusaidia kulieneza kati ya viungo vingine vya taifa la Mungu.

Tutafute namna za kuwafanya wote wajifunze kushirikishana kwa unyofu.

Vilevile ugumu wa mtu fulani kushirikisha ulio na mzizi wa kisaikolojia usiwe kisingizio cha kutomjali, bali wote wapokee toka kwake pia yale anayotaka kuyatoa kwa maneno na matendo.

 

 

1.20.       LITURUJIA

 

Tuwe na hakika ya kuwa jumuia inajengwa na liturujia, hasa ekaristi na upatanisho.

Maajabu hayo ya Mungu yanasababisha sifa, shukrani, furaha, umoja wa mioyo, nguvu za kukabili matatizo ya kila siku na kutegemezana katika imani.

Yesu anazidi kutuita pamoja kila siku hasa katika ekaristi ili aseme nasi na kutuunganisha naye na kati yetu: ndio moyo wa maisha ya Kanisa na ya utawa vilevile.

Ekaristi inafungamana na juhudi za wongofu zinazokamilika katika kupokea mara nyingi upatanisho, ili tuwe wazi na waaminifu katika uhusiano na Mungu.

 

 

1.21.       EKARISTI

 

Sisi tuliomfanya Yesu awe maana pekee ya maisha yetu, tunavutwa kutamani tuzidi kumshiriki kwa njia ya sakramenti inayomfanya awepo kati yetu, ya sadaka anayojitoa kwa upendo kwetu, na ya meza anayotulisha safarini.

Kwa njia hiyo tunaitwa kuishi fumbo la Pasaka tukiungana naye katika kujitoa kwa Baba kwa nguvu ya Roho.

Tumuabudu mara nyingi na kwa muda mrefu katika ekaristi ili tufurahie na kutamani zaidi zawadi hiyo.

Hata tusipoweza kuhudhuria Misa kila siku, kiini cha maisha yetu kiwe ni fumbo hilo la Bwana kuwepo hai ndani ya jumuia.

Katika kulea roho ya kijumuia tuanze daima hapo, kwa kuwa ekaristi ikiadhimishwa au kuabudiwa na kuliwa ndipo umoja wa mioyo unapojengwa.

 

 

1.22.       SALA YA JUMUIA

 

Pamoja na ekaristi, Sala ya Kanisa inatokeza wito wetu wa kuinua daima mioyo kwa Mungu ili kumtolea sifa na maombezi.

Adhimisho lake linahuisha mfululizo sala yetu kwa kutuletea Neno kadiri ya mzunguko wa mwaka wa liturujia na linatufanya tujisikie washiriki wa taifa la Mungu.

Sala ni zawadi ya Mungu inayotupasa tuipokee na kuistawisha kwa bidii, mafunzo na uaminifu.

Hasa walelewa waongozwe kuthamini zaidi na zaidi nafasi za sala ya jumuia zinazoongoza mwendo wa siku zetu, ili wazitumie zote kwa bidii walau kuanzia zoezi, wakidumu katika uchipukizi na baadaye.

Kila ndugu apate ujuzi wa kitaaluma, wa Kiroho na wa kichungaji kuhusu Maandiko na liturujia utakaomwezesha kulishwa navyo na kuwasaidia waamini wengine wavumbue hazina hizo na kufaidika nazo.

Ili jumuia itimize wajibu wa kulea katika sala, ndugu wote watoe mchango wao kwa kujenga mazingira yanayofaa, kwa kujiandaa, kuwahi na kusali vizuri.

 

 

1.23.       SALA NA KIMYA

 

Sala ieleweke kuwa ni muda wa kukaa na Mungu aweze kufanya kazi ndani mwetu na kuenea katika maisha yetu, akitufariji na kutuongoza kati ya uchovu na mawazo ya kila aina, kusudi hatimaye tuwe wake tu.

Sala ya pamoja inazaa kadiri inavyoshikamana na ile ya binafsi: toka mwanzo wa malezi yetu tusisitize umuhimu wa kuhusiana kwa dhati na Baba, wa kuongea na Bwanaarusi na rafiki moyo kwa moyo, wa kuchimba yaliyoadhimishwa katika Roho Mtakatifu, na wa kutunza kimya cha ndani na cha nje kama nafasi ya Roho na Ukweli kutuhuisha kabisa.

Kusikia na kuitikia wito wa utakatifu kunadai kimya hicho ambacho kimejaa uwepo wa Mungu tu, na kinatuwezesha kuelewa anapotaka na anavyotaka kusema nasi.

Hivyo tuzoee mapema kimya na upweke: upweke wa hiari unaelekeza kwenye kimya cha ndani, nacho kinadai kimya cha nje.

Tufurahi kuwaruhusu ndugu waliokwishaonyesha ukomavu fulani katika maisha ya kijumuia waweze kujipatia nafasi zaidi za upweke na sala.

Nyumba zetu ziwe tayari kupokea watu kwa ukarimu, hasa kwa sala, lakini bila ya kuvuruga hali ya kimya, nafasi ya faragha na mengine ya kitawa.

 

 

1.24.       SALA NA KUMSHIRIKI YESU

 

Tukipanda mlima wa sala pamoja na Yesu, kama walivyofanya Petro, Yakobo na Yohane, tunafunuliwa fumbo lake katika utukufu wa Utatu na katika ushirika wa watakatifu, tukatamani kukaa naye moja kwa moja; pia tunaandaliwa kushuka naye kati ya watu tukabili shughuli za kila siku na kushiriki msalaba wake bila ya kukwaza nao.

Daima watu wa sala ndio waliofanya makuu, kwa kuelewa na kutekeleza vizuri matakwa ya Mungu.

Sala inakusudiwa kutuathiri hata kila wazo, neno na tendo letu, katika nafasi muhimu na za kawaida vilevile, lionyeshe tunavyofanana na Yesu katika kujitoa mhanga.

Ushirika naye utuongoze kujiunga na kila jambo ambalo mwenyewe aliunganika nalo kwa dhati: na Baba aliyemtuma ulimwenguni, na Roho aliyemsukuma maishani, na Kanisa alilojitoa kwa ajili yake, na binadamu wote, hasa wenye hali ngumu zaidi ambazo alipenda kuzishiriki kama kaka yao.

Tusichoke kuhimizana ili wakati wa shughuli tudumishe ile roho ya sala inayotakiwa iwe lengo la malimwengu yote, hivi kwamba siku nzima na kazi zake mbalimbali zigeuke kuwa nafasi za kuungana na Bwana.

Maisha hayo ya ndani yanaleta furaha ya Kifransisko ambayo ni nguvu ya kushinda mabaya na kuzidi kujitoa maisha yote.

 

 

1.25.       MALEZI YA SALA

 

Katika malezi ya sala tuelekeze:

- kuunda moyo safi unapoweza kung'aa uzuri wa Mungu;

- kutambua daima uwepo wa Mungu na matakwa yake;

- kustawisha uwezo wa kuyashangaa maajabu yake katika uumbaji na ukombozi;

- kuzoea kusikiliza Neno la Mungu na kutumia sala za Biblia ili kumuonja Mungu na kuingia katika historia ya wokovu;

- kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Kanisa kadiri ya mwaka wa liturujia ili kuishi mafumbo makuu ya ukombozi;

- kufuata vema ratiba ili kudumisha sala hata isipojibubujikia;

- kuwa na moyo mpana ambao unasali na kuishi ukishiriki furaha na huzuni za wote;

- kujua jinsi watu mbalimbali wa zamani na wa siku hizi walivyong'amua fumbo la Mungu;

- kumpenda kitoto Mama wa Mungu aliyekingiwa dhambi asili.

 

 

1.26.       UDUGU

 

Mang'amuzi ya dhati ya Mungu kuwa ni Baba yalimuongoza mzee wetu Fransisko kutambua na kuishi upya udugu wake na watu wote, hasa na wale aliojaliwa na Baba awe nao njia moja.

Tukishiriki karama yake, tuwapokee na kuwapenda wenzetu kama zawadi ya Bwana.

Tumetumwa kushuhudia udugu wa Kikristo kwa kuwaona wote kuwa ni wana wa Mungu tayari, au walau wanaitwa wawe hivyo, na kwa kujitoa kwa upendo kwa kila mmojawao, hasa wale wa mwisho.

Jina la chama lina uzito mkubwa na linadai tuwe:

- wadogo wa Yesu, wenye uhusiano wa dhati naye, aliye kaka wa wengi;

- ndugu sisi kwa sisi kwa kupendana na kufanya kazi pamoja;

- ndugu wadogo wa kila mmoja kusudi tustawishe udugu ndani ya Kanisa na ya jamii, tukishuhudia upendo wa Kristo kwa wote na kuwakumbusha ukweli huu wa msingi: "Nyinyi nyote ni ndugu".

 

 

1.27.       KUIMARISHA UDUGU

 

Ili tuhifadhi na kuimarisha maisha ya kidugu kadiri ya Injili:

- tujiite na kuwazoesha wote watuite "ndugu";

- tunapoeleza karama yetu ili kuchochea miito na kuingiza utawani, tuyakazie mambo makuu ya maisha hayo (kuishi kijumuia, kuwa wadogo wa wote n.k.) kuliko kazi au hadhi fulani (upadri n.k.);

- kwa kuwa wito wetu kimsingi ni uleule, malezi ya utakaji na zoezi yalingane kwa wote; baadaye tu ndugu wapewe nafasi ya kujiendeleza kadiri ya uwezo wao na ya udogo wetu;

- tutoe huduma za kutufaa zaidi kama wadogo (kutangaza Neno, kufundisha sala, kutekeleza matendo ya huruma, kufanya kazi za mikono n.k.);

- tuwe watu wa haki na amani, tukiwasaidia wote kuunda dhamiri zao kuhusu tunu hizo;

- tuchangie pia maendeleo halisi ya jamii kuendana na Injili na katiba yetu ili tuwe watu wa Mungu wasio mbali na mashaka ya maisha ya watu.

 

 

1.28.       UPENDO WA KRISTO

 

Kristo katika fumbo la Pasaka ndiye kielelezo cha kudumu cha namna ya kujenga umoja, tena ndiye chemchemi na kipimo cha upendo unaohitajika.

Ili tufaulu kuishi kidugu ni lazima Roho wake atuwezeshe kupendana kama Yesu alivyopenda.

Akiwa ni upendo wake uliomiminwa mioyoni mwetu, anatusukuma tupende wote kwa kubeba udhaifu wao na matatizo yao hata kujitoa mhanga kwa ajili yao.

Hasa kuishi na ndugu ambao hawajisikii vizuri, na hivyo wanasababisha uchungu kwa wenzao na kuvuruga maisha ya jumuia, ni fursa ya kukomaa kiutu na Kikristo.

Safari hiyo ya ukombozi wa moyo inadai tujikane ili tumpokee mwingine alivyo, pamoja na tofauti na mipaka yake, sifa na kasoro vilevile, kuanzia yule aliyepewa uongozi, tusije tukamdai mno.

Moyo huo tu, ambao unatokana na upendo na kulenga ustawi wa upendo ndani mwetu na mwa wenzetu, utatuwezesha kutegemezana, kukosoana, kujishtaki hadharani, kukagua na kupanga maisha kwa pamoja n.k.: namna hizo zote tuzing'amue kuanzia utakaji.

Ikiwa ndugu atajisikia anapokewa alivyo, hapo tu ataondoa kinga zake na hofu zinazomfunga akapokea ukosoaji na shauri na kukua vema.

 

 

1.29.       JUMUIA NA UKOSEFU

 

Kwa kuwa maisha na malezi yetu yana elekeo la kidugu, kumuingiza mtu katika utamu na ugumu wa kuishi pamoja kunafanyika katika jumuia.

Wengi wanavutiwa nayo, lakini kudumu ndani yake katika hali halisi ya maisha kunaweza kukawa mzigo mzito: mtu wa kawaida, akipenda umoja, hataki kuugharimia mwenyewe kwa kuwajibika.

Kwa hiyo toka mwanzo tujulishe kwamba maisha ya jumuia yanadai sadaka, lakini kujiangamiza kwa ajili ya wenzetu ndiyo njia ya wokovu: Injili inataka watu ambao, sawa na chembe ya ngano, wanajua kujifia ili udugu ustawi.

Hivyo jumuia inakuwa shule tunapojifunza kumpenda kweli Mungu kwa kuwapenda ndugu aliowaweka karibu nasi, na binadamu wote, hasa wanaohitaji zaidi huruma ya Mungu na mshikamano wa kidugu.

Jumuia kamili haipatikani duniani, ambapo Kanisa lenyewe, pamoja na miundo na utakatifu wake, linajengwa juu ya udhaifu wa binadamu.

Hata hivyo kwa msaada wa Mungu tunaweza daima kuongoka na kujenga kwa pamoja jumuia juu ya msamaha na upendo.

Umoja tunaoulenga unategemea upatanisho: kwa hiyo utovu wetu wa ukamilifu usitukatishe tamaa, mradi tushike upya kila siku njia tuliyoelekezwa na Neno.

 

 

1.30.       NJIA ZA UMOJA

 

Umoja halisi ni zawadi ya Mungu kwa wanaosikiliza Injili na kuishika.

Ili tupendane kama watoto wa Baba mmoja:

- tukuze hali ya kifamilia, ya furaha na ya unyofu kati yetu;

- tuzidi kuaminiana, kuelewana, kuthaminiana;

- tuelezane shida zetu;

- tuimarishane wakati wa taabu na wa kuvunjika moyo;

- tupendane bila ya masharti;

- tutumikiane kwa ukarimu;

- tutiiane kwa upendo;

- tusihukumiane;

- tuzoee kuvumilia na kusamehe sabini mara saba;

- tukosoane kidugu tukilenga daima wongofu;

- tupambane na ugeugeu wetu na misukosuko ya kujianzia;

- tuachane na chochote kinachoweza kuvuruga maisha ya kidugu;

- tushirikishane kila kitu.

Pasipo juhudi hizo, umoja haupatikani.

 

 

1.31.       FUMBO LA JUMUIA

 

Ushuhuda wa kidugu unadhoofishwa na shughuli nyingi mno zikituzuia tusishiriki kwa kawaida sala za pamoja, maisha ya jumuia na huduma za nyumbani.

Basi, ratiba ya kila siku isipangwe kwa kujali utendaji wa kitume kuliko maisha ya kidugu, bali jumuia ijipatie muda wote unaohitajika ili kuboresha maisha hayo yasiwe ya kuhangaika hata kujichosha bure.

Tuelewe mapema kuwa ushirika wa kidugu sio tu njia ya kufanya vizuri kazi yetu, bali ni mahali pa kung'amua uwepo wa Yesu hai kati yetu, tena pa kuushuhudia Utatu, yaani Baba anayetaka kuwafanya watu wote kuwa familia moja, Mwana aliyekusanya waliotawanyika, na Roho anayewaunganisha katika upendo.

Umoja hautegemei raha ya kulingana kwa mawazo, kwa tabia na kwa machaguo, bali wito wa Bwana aliyetuweka wakfu namna moja ili tuishi pamoja na kufanya utume mmoja.

Hasa mfano wa jumuia za kimataifa unaweza ukasaidia makabila mbalimbali kushirikiana, kutajirishana na kurekebishana.

Lakini umoja kati ya watu tofauti si rahisi: unadai nia imara upande wa wote, na utambuzi upande wa viongozi na walezi.

Juhudi za kuwatii kwa imani, za kupokeana wenyewe kwa wenyewe na za kutatua matatizo katika jumuia mchanganyiko zinadhihirisha kwamba tuko pamoja kwa jina la Bwana.

Kumbe tungetaka kuchaguana tungepunguza: utayari wetu wa kutumwa kokote, ukweli wa kwamba umoja unamtegemea Roho Mtakatifu, na hivyo hata ushuhuda wa udugu.

 

 

1.32.       JUMUIA NA NDUGU BINAFSI

 

Jumuia ndiyo mahali tunapovuka kila siku toka "mimi" hadi "sisi", tukiishi na kutenda kidugu kwa utajiri wa vipawa mbalimbali.

Kwa ajili hiyo:

- tushukuru pamoja kwa zawadi ya wito na utume uleule tuliyojaliwa ambayo inazidi tofauti yoyote iliyopo kati yetu;

- tuishangae hekima ya Mungu aliyotufanya tuwe zawadi kila mmoja kwa wenzake;

- tumsifu kwa kile ambacho kila ndugu anashirikisha;

- tuvumilie mwendo wa polepole wa walio dhaifu, bila ya kuchelewesha ustawi wa wenye neema na bidii nyingi zaidi;

- tuchangie utume wa chama kadiri ya vipawa tulivyojaliwa kwa faida ya wote;

- tumuone mtawa akitumwa kuwa ni mjumbe wetu;

- tumsaidie kujiendeleza na kuchangia tathmini ya maisha na kazi ya jumuia.

 

 

1.33.       KUJIKANA NA UKOMAVU

 

Tulenge uwiano mzuri kati ya kumjali mtu na kujali ustawi wa pamoja, mahitaji ya binafsi na yale ya jumuja, karama ya mtu na mpango wa kitume wa chama.

Tusivumilie maelekeo tofauti mno ambayo yanavuruga chama na kuhatarisha umoja: wingi wa karama za wanachama usisababishe ushindani, bali ushirikishano kati ya ndugu na ndugu, tena kati ya ndugu na jamaa nzima.

Katika kupima ukweli wa karama ya mlelewa tuzingatie hasa anavyokubali masharti ya maisha ya kidugu, kwa kujikana na kutii.

Tunamshiriki Yesu hasa tunapojifunza kutii kwa mateso.

Hiyo ni sehemu ya lazima ya udugu na utekelezaji wa upendo katika kuwatumikia wenzetu kwa kuwatolea yale yote tuliyonayo hata nafsi yetu yenyewe.

Tuelewe mapema kwamba kuweka pembeni vipawa na maelekeo ya binafsi kwa manufaa ya jumuia ni dalili ya ukomavu wa kiutu na wa Kiroho.

 

 

1.34.       FURAHA

 

Jumuia yenye furaha ni neema toka juu kwa ndugu wanaoiomba na kupokeana.

Kama vile amani na umoja, kufurahia maisha hata yakiwa magumu ni ishara ya ufalme wa Mungu, kwa kuwa ni tunda la kujifia na kupokea paji la Roho Mtakatifu.

Furaha hiyo ya Pasaka ni ushuhuda mzuri wa kuwa utawa ni wa Kiinjili kweli, ni hatima ya safari ngumu inayozeweshwa na sala, ni tegemezo la kudumu kwa wanajumuia na kivutio kikubwa kwa miito mipya.

Kumbe jumuia isiyo na furaha inaelekea kuzimika, kwa kuwa wanajumuia watashawishika mapema wakaitafute kwingine.

Kwa hiyo, tujihadhari na ari chungu na tabia ya kujiulizauliza mfululizo kuhusu wito wetu na hali ya kesho.

Kumbe kumtegemea Roho Mtakatifu, kujipatia nafasi za kutulia binafsi na kijumuia, kufurahi na wenzetu, kuangalia shida zao, kukabili kesho kwa tarajio la kukutana na Bwana daima na kwa vyovyote: hayo yote yanalisha amani na furaha kwa ndani na kutia nguvu katika utume.

 

 

1.35.       KUITIKIA WITO KWA UMOJA

 

Sisi tunastawi kwa kuitikia wito wa Mungu Baba ambaye anatuvuta kwa karama maalumu ya Roho Mtakatifu tulingane na Yesu kwa kutekeleza Injili yake namna fulani pamoja na wenzetu.

Tuone wito wetu kama namna bora ya kuishi, kama neema inayoyatia maisha yote ukweli, wema na uzuri, ili tujisikie na hakika kuhusu sura yetu, tusihitaji kutegemezwategemezwa na watu, wala kujitafutia faraja mbalimbali.

Hivyo tutaimarisha umoja wetu kwa kuwaona tunaoitikia nao wito mmoja kuwa ndio wa kwanza kustahili udugu na urafiki wetu.

Kupenda wito ni kupenda Kanisa na chama kama familia yetu halisi.

 

 

1.36.            UDOGO

 

Mzee wetu Fransisko hakujifanya mtawala wa ulimwengu, bali ndugu mdogo wa viumbe vyote akiimba sifa za Mungu kwa niaba yao na kwa ajili yao; pia alivitumia ili kuishi, lakini bila ya kuzidhisha wala kujilimbikizia.

Udogo huo ndio sifa kuu ya pili ya karama yetu, ambayo inatutia na kutudai msimamo wa kujishusha daima mbele ya Mungu na ya watu, tukimfuata Yesu katika ufukara na unyenyekevu na kushiriki hali ya watu wa mwisho, tukiishi duniani kama wakimbizi na wapitanjia tu na kwenda ulimwenguni kwa upole, amani, utaratibu, upendevu, unyofu na utiifu.

Neno kuu la utekelezaji wake ni kujikania mali na sifa, hata zile za Kiroho.

Mtakatifu Fransisko aliongoka kwa kutumikia wakoma akataka wanaoingia utawa wake waanze na kazi hiyo: basi, kila ndugu azoeshwe kufanya kazi kati ya watu na kwa ajili yao, kupendelea zile zinazopatana zaidi na udugu na udogo wetu, na hasa kufungamana na maskini na wenye dhiki.

Udogo unadai tena tujifunze kujitolea katika huduma za nyumbani, kama vile upishi na matunzo ya mazingira.

Hatuwezi kusisitiza vya kutosha umuhimu wa mchango wa ndugu wanaotoa huduma hizo, wakitunza hali ya kimya na makini, usahili na furaha, na hivyo kufanya jumuia zetu ziwe na sura ya Kifransisko kweli.

Kwa misimamo hiyo na kwa vitendo hivyo, ndivyo udugu wetu katika udogo unavyojengwa siku hadi siku.

Hata uwajibikaji katika sala na mafunzo ni sehemu mojawapo ya kazi, kwa kuwa ni sharti la kuhudumia vizuri chama, Kanisa na jamii.

 

 

1.37.       KAZI

 

Kadiri ya sheria asili ya binadamu tunatakiwa kufanya kazi ya mikono au nyingine yoyote kiasi cha kustahili chakula.

Walelewa wazoee kufanya kazi kweli ili kutekeleza udugu, kuimarisha umoja, kushirikisha vipawa vyao, kustawisha uwajibikaji, kukomaa kiutu na kuaminika kiwito.

Kufuatana na mfano wa Yesu na maonyo ya mzee wetu Fransisko, wazoee kufanya kazi kwa roho ya sala, kwa kuziona ni nafasi muhimu za kukutana na Mungu katika kuchangia uumbaji na ukombozi.

Si njia za kujipatia riziki tu, bali utekelezaji wa maisha ya Kiroho na ya kitume, kwa namna ya pekee kwetu tuliowekwa wakfu pamoja na maisha yetu yote.

Kumbe utamaduni wa teknolojia unapima vyote na wote kwa kuzingatia wanavyoleta faida: wanaoufuata wanaweza wakaona inafaa tutumie tofauti maisha yetu kwa kulenga zaidi maendeleo ya kijamii.

Lakini upendo unatuhakikishia kwamba kuungana na Yesu kwa kushiriki maisha na utume wake, ndiyo shukrani furahivu ambayo tunaitikia mwaliko wake, ndiyo njia ya kuzaa matunda, hivyo ndiyo faida pekee.

 

 

1.38.       USHIRIKIANO WA MIITO MBALIMBALI

 

Mtaguso umeangaza jinsi miito mbalimbali ndani ya Kanisa inavyokamilishana na kumshuhudia kwa pamoja Bwana mfufuka katika kila hali na mahali.

Ushirikiano kati ya waamini ni kielelezo cha ushirika wa Kanisa na unastawisha nguvu za kitume.

Hasa tunu maalumu za walei (kuhisi sana maisha ya ulimwengu, utamaduni, elimu, siasa, uchumi n.k.) na zile za watawa (juhudi za pekee katika kumfuata Kristo, kuelekea sala na uzima wa milele n.k.) zikikutana bila ya kuchanganyikana zinaweza zikaleta faida kwa wote.

Mabadilishano hayo yanatakiwa kuwa ya dhati zaidi kwetu, ambako walei na makleri wanajimbo wanaitwa kushiriki kwa namna yao karama na umisionari wa chama, kufuata safari ya malezi ya Kifransisko, na kuhusiana kwa msingi wa usawa.

Ili walei waweze kushiriki utajiri wa utawa na kuchangia sala na utume wake, kama wanachama wa ulimwenguni au wakiishi kwa muda jumuiani, wanahitaji malezi maalumu na kutimiza masharti fulani.

Vilevile wanajumuia wanaweza wakatumwa na mtumishi kushiriki kazi kadhaa za wasekulari, hasa huduma kwa maskini wa kila aina, mradi wadumishe yaliyo maalumu ya maisha ya kitawa.

Tuwe wazi pia kwa ndugu wa matawi mengine ya familia ya Kifransisko, tukisali pamoja na kushirikiana katika utume ili kutiana moyo na kutajirishana.

Wanachama na viongozi wao wawe macho kuhusu ndugu kujiunga na mifumo mingine ya Kiroho na ya kitume asije akasogea mbali na karama na masharti ya chama chetu.

 

 

1.39.       VISHAWISHI

 

Tutambue na kushinda vishawishi vinavyoweza vikaonekana vyema, kumbe sivyo; kwa mfano:

- malezi yetu ya Kiroho ya ndani zaidi yanaweza yakatufanya tujisikie bora kuliko waamini wenzetu;

- haja ya ujuzi kwa ajili ya ufanisi wa kazi inaweza ikageuka imani potovu ya kuwa huo unatutegemea sisi binadamu kuliko Mungu;

- haja halisi ya kujua jamii ya leo na changamoto zake inaweza ikapunguza ari ya Kiroho na ya kitume au kukatisha tamaa;

- hamu ya kuwakaribia watu wa leo inaweza ikatufanya tuige mitindo ya ulimwengu;

- kushiriki matarajio ya taifa na kuzingatia utamaduni wetu kunaweza kukatufanya tushikilie utaifa au desturi zinazohitaji kutakaswa na Injili.

 

 

 

 

2. KUENEZA INJILI

 

2.1.           USHIRIKA WA KIMISIONARI

 

Kanisa limejaa Utatu, hivyo nalo ni ushirika; ushirika huo unadumishwa na mitume na waandamizi wao chini ya mamlaka ya Petro, iliyo msingi wa kudumu wa umoja wa waamini wote.

Hilo taifa lenye asili katika ushirika wa Utatu limetia mizizi katika historia ya binadamu hivi kwamba haliwezi kuanzishwa tena na mtu yeyote.

Ni taifa ambalo linachota Neno la Mungu katika Maandiko, mapokeo na ualimu wake kwa pamoja na linalenga umoja kamili wa madhehebu yote.

Ni taifa ambalo linajitambua kuwa ni fumbo lenyewe la Mungu linaloshirikishwa kwa watu wa jana, leo na daima; hivyo haliwezi kueleweka kibinadamu (k.mf. kijamii au kisiasa) kwa sababu uhai wake halisi unafikiwa na imani tu.

Hatimaye ni taifa la kimisionari lisiloridhika kubaki kundi dogo, bali linatamani kuihubiri Injili kwa viumbe vyote hata ulimwengu mzima uungane katika kukiri kwamba jina la Yesu tu unaleta wokovu.

 

 

2.2.           UMISIONARI WETU

 

Tukiishi Injili kwa unyofu na furaha, Roho anatusukuma tushiriki kazi ya Kanisa, nalo linatutuma ulimwenguni tumwakilishe Bwana katika kuokoa watu na kueneza amani yake kwa njia ya ushuhuda wa maisha, utekelezaji wa upendo na tangazo wazi la Neno.

Hauwezekaniki utawa usio na karama na lengo maalumu, wala utawa wa kimisionari usiolenga utakatifu kwa njia ya utume wake.

Umisionari unahusu maumbile ya utawa wetu kiasi kwamba maisha yote ya kitawa yanatakiwa kujaa roho ya kimisionari, kama vile utendaji wetu wote unavyopaswa kuhuishwa na roho ya kitawa.

Tunawekwa wakfu upya kwa Mungu kwa ajili ya umisionari wa Kanisa: katika tendo hilo vinaingia kazi ya Mungu, itikio la ndugu na upokeaji na utoleaji wa Kanisa.

Hivyo maisha yetu ya Kiinjili, kadiri yalivyochochewa na Roho Mtakatifu na yalivyokubaliwa na Kanisa, yanalenga utume pia: lakini tukumbuke daima kuwa huo unadai tumshuhudie Yesu kama watu ambao tunafyonza uzima wake, sio tu tutoe huduma kadhaa.

Kila ndugu ajisikie zaidi na zaidi mwenezainjili kwa kuungana na Yesu na kupata ari yake: hapo wito wa kitume, baada ya kuanza kutekelezwa, utazidi kukomaa.

Pia aungane na Kanisa lote: katika ujuzi wake hai wa Injili na katika hamu yake kama bibiarusi ya kutunza safi imani kwa Bwanaarusi, pia katika hamu yake kama mama na mwalimu ya kueneza imani hiyo kulingana na utamaduni, umri na hali yoyote ya watu.

Alingane hasa na Kanisa maalumu anamoishi, akielewa na kushiriki juhudi za jimbo na za parokia.

 

 

2.3.           IMANI

 

Habari Njema inawaalika wanaume na wanawake wote kuongoka na kusadiki: wito huo wa Yesu unazidi kusikika kwa njia ya Kanisa, jumuia ya wafuasi wake inayopokeza imani sahihi.

Imani hiyo:

- ni kukutana mwenyewe na Yesu, kumuongokea na kugeuka kuwa mwanafunzi wake, kama ilivyotokea kwa mitume;

- inadai mapinduzi kamili kuanzia moyo, kwa kuwajibika moja kwa moja kuwaza kama yeye, kupima mambo kama yeye na kuishi kama yeye;

- ni kama kuzaliwa upya: halafu mtoto mchanga anatarajiwa kukua polepole awe mtu mzima aliyekomaa hadi utimilifu wa Kristo;

- ni zawadi inayotarajiwa kustawi kwa wongofu wa kudumu katika Kanisa.

 

 

2.4.           HATUA ZA IMANI NA WONGOFU

 

Katika maendeleo hayo ya imani na wongofu kuna hatua muhimu kadhaa:

- kuvutiwa na Injili, ingawa mtu hajaamua kuipokea;

- kuitafiti: mvuto wa kwanza unahitaji muda uwe uamuzi imara;

- kuongoka kwa kuambatana na Yesu: juu ya msingi huo yanajengwa maisha yote ya Kikristo;

- kupokea katekesi: aliyeamua kumfuata Yesu anatamani kumjua ili alingane naye, kuelewa fumbo lake, ufalme alioutangaza, masharti na mashauri yake, na njia yote aliyotuelekeza: ujuzi huo wa imani unahimiza safari ya Kiroho;

- kubadili mitazamo na mienendo kwa changamoto na sadaka lakini pia kwa furaha nyingi;

- kuungama imani hadharani kwa namna hai inayozaa matunda;

- kuelekea ukamilifu ili kutimiza hamu ya Kristo ya kutuona tumefanana na Baba wa mbinguni: mwamini, akizidi kusukumwa na Roho Mtakatifu na kusaidiwa na malezi ya imani, akilishwa na sakramenti, sala na utekelezaji wa upendo, anajitahidi kuitikia wito wa utakatifu wa wabatizwa wote.

 

 

2.5.           KUHAKIKISHA MSINGI KWANZA

 

Katika utekelezaji wa utume si rahisi kutofautisha hatua za kwenda na kukaribisha, kutangaza na kulea, kuita na kuingiza.

Pengine anayejitokeza kutaka katekesi na sakramenti, au hata kuingia utawani, anahitaji bado kupashwa habari njema na kuongoka kweli.

Kumbe, bila ya msimamo katika imani, katekesi haiwezi kutimiza kazi yake ya kulea, wala sakramenti haziwezi kuzaa matunda maishani.

Halafu uchungaji wowote pasipo katekesi ya awali unakosa msingi na kubaki wa wasiwasi: tatizo lolote linaweza likaangusha jengo lote.

Malezi hayo ya msingi, ambayo kiini chake ni zile hakika kuu za ungamo la imani na zile tunu kuu za Injili, yanalisha mizizi ya maisha ya Kiroho pamoja na kuingiza katika jumuia ya Kikanisa ambayo inakiri, inaadhimisha na kushuhudia imani kimatendo, na ambamo mwamini anaweza kupokea lishe ngumu zaidi inayotolewa kila siku.

 

 

2.6.           KATEKESI

 

Imani iliyosababishwa na neema na kushughulikiwa na Kanisa inatakiwa kukomaa.

Ustawi wa dhati wa Kanisa na wa kila mmoja ndani yake unategemea sana malezi kamili na ya mpango ya imani.

Katekesi bora inayohudumia ustawi huo ni kumuingiza mtu kwa utaratibu katika ufunuo wote wa Mungu, ambao unatunzwa katika kumbukumbu ya Kanisa na katika Maandiko na kukabidhiwa kwa namna hai toka kizazi hadi kizazi ili kuhimiza ungamo la imani wazi na lenye matunda maishani.

Kwa kuwa katekesi inahusiana sana na liturujia na maisha, tunapoitoa tuzingatie sawasawa mafundisho, adhimisho lake na utekelezaji wake.

Mtu mzima ajisikie anatajirishwa na Neno la Mungu, ageuke mpaka ndani na kuwajibika kadiri ya ubatizo asimkaribie tu Yesu, bali aishi moja kwa moja katika ushirika naye kama tawi ndani ya mzabibu.

Atambue kwamba upendo wa Mungu unataka kuenea katika nafsi yake yote, asiwe tena mali yake binafsi, bali Kristo aishi ndani mwake.

Kwa hiyo anatakiwa kutoa itikio la upendo la kujitoa moja kwa moja, kwa kujikana na kukubali misalaba ya kila aina ili aungane na Kristo kwa dhati na kutimiliza yaliyopungua katika mateso yake kwa ajili ya Kanisa; hatimaye akubali kupoteza maisha yake na hata uhai wake ili kumpata yeye milele.

 

 

2.7.           MIKAZO YETU

 

Kwamba katekesi ni sehemu ya msingi ya malezi yoyote ya Kikristo si kizuio kwa malengo ya chama na kwa utekelezaji wa karama yetu, kwa kuwa tunaweza kuiwekea katekesi mikazo maalumu, mradi tusipotoshe maumbile yake.

Kulea roho ya Kifransisko ni mwendelezo halali wa malezi ya msingi yanayotarajiwa kutolewa kwa Wakristo wote.

Basi, mafundisho yetu yamfanye Yesu kuwa kiini chake, ambacho kinaunda na kuangaza mengine yote, kama alivyo kiini cha mpango wote wa Baba katika kuumba, kukomboa na kutakasa ulimwengu kwa upendo mkuu.

Tumtambulishe katika maisha yake halisi hadi Pasaka, kwa kuwa ndiye ukweli, yaani utimilifu wa ufunuo wa Mungu.

Kwa ajili hiyo tuzitegemee daima Injili, zilizo moyo wa Maandiko yote, kwa sababu ndizo shuhuda kuu juu ya maisha na mafundisho ya Neno aliyefanyika mwili.

Tuingize katika kusoma Maandiko kulingana na Roho anayehuisha Kanisa ambalo daima linalitazama Neno hilo hai kwa imani, linalisikiliza kwa ibada, linalitunza kwa uangalifu na kulifafanua kwa uaminifu.

Tusichoke kuteka katika Mapokeo na Maandiko Matakatifu ambayo kwa pamoja ndiyo amana takatifu iliyokabidhiwa kwa familia ya Mungu ili ichote humo mfululizo mapya na ya kale.

 

 

2.8.           YESU, NENO

 

Walioanza kumfuata Yesu wanahitaji mfululizo kulishwa Neno la Mungu ili wakue katika maisha yao ya Kikristo.

Neno ndiye Yesu ambaye, bila ya kuacha kuwa Neno wa milele wa Baba, anajitokeza katika sura nyenyekevu ya maneno ya kibinadamu.

Huduma ya Neno inapokeza ufunuo wa Mungu kwa kutumia maneno ya binadamu; lakini inahusu daima matendo, yaani yale ambayo Mungu aliyatenda zamani na bado anayatenda hasa katika liturujia na katika maisha ya watakatifu.

Tujulishe kwa mpango ujumbe wa Kikristo kwa kuzingatia yote kupitia nyakati tatu za historia ya wokovu (Agano la Kale, maisha ya Yesu na historia ya Kanisa) na sehemu kuu nne za ujumbe wenyewe (Kanuni ya Imani, liturujia, maadili na sala), ambazo zote zinatokana na chemchemi moja, yaani fumbo la Kristo.

Kwa njia ya huduma hiyo Roho Mtakatifu anaendeleza majadiliano ya wokovu kati ya Mungu na binadamu: yeye tu anafanya Injili iwe hai ndani ya Kanisa na kwa kulipitia hilo isikike kweli ulimwenguni.

 

 

2.9.           BIBLIA NA KATEKISIMU YA KANISA KATOLIKI

 

Maandiko yanatakiwa kushika nafasi ya kwanza katika huduma ya Neno: mafundisho yetu yahusiane nayo daima na kupenywa kabisa na mawazo, maelekeo na misimamo ya Biblia, hasa Injili.

Matunda ya huduma hiyo yanategemea kuyasoma Maandiko kwa akili na moyo wa Kanisa, yaani kwa mwanga wa Mapokeo, ambapo Katekisimu ya Kanisa Katoliki inashika nafasi muhimu.

Ingawa kitendeakazi hicho peke yake hakitoshi, wala hakipo juu ya Neno la Mungu, kinalihudumia ili lipokezwe kwa ukweli na usafi.

Basi, Maandiko Matakatifu na Katekisimu ya Kanisa Katoliki vinatakiwa kuongoza malezi yote ya imani ya nyakati zetu, vikichangia katekesi ya Biblia na mafundisho mengine vilevile, kila kimoja kwa namna yake na kwa mamlaka yake maalumu: Maandiko yakiwa ni Neno la Mungu lililoandikwa kwa uvuvio wa Roho Mtakatifu, na Katekisimu hiyo ikiwa ni tokeo muhimu la kisasa la Mapokeo hai ya Kanisa na kanuni ya hakika kwa ufundishaji wa imani kwa watu wa leo.

Maandiko yawe mada kuu na roho yenyewe ya malezi yote, na Katekisimu ya Kanisa Katoliki rejeo kuu la mafundisho.

Tuviamini vyote viwili ili kupokea na kupokeza Neno kwa namna hai na yenye maana.

 

 

2.10.       KATEKISIMU YA MAJIMBO NA UTAMADUNISHO

 

Katekisimu ya Kanisa Katoliki imetolewa kwa waamini wote na kwa wanaopenda kujua imani na maadili yake.

Halafu imekusudiwa kuhamasisha na kusaidia utungaji wa katekisimu mpya za majimbo ambazo zizingatie zaidi lugha na hali mbalimbali za walengwa, bila ya kuvuruga umoja wa mafundisho ya Kikatoliki.

Tutumie pia katekisimu hizo zilizothibitishwa na askofu wa jimbo au na baraza la maaskofu kusudi Injili imuelee kila mmoja hata aione kweli ni habari njema kwake na nguvu yake ifanye kazi mpaka moyoni mwa utamaduni wowote.

Tukumbuke kuwa utamadunisho hautoki juu, bali unachipuka na kukua kutoka shina, yaani unaanzia kwa watu na ni kazi ya Kanisa mahalia; kwa hiyo tujali mapokeo yake na kutamadunisha kwa busara na hekima, tukielimisha kwanza na kutekeleza hatua kwa hatua.

Lengo liwe kuleta mwamko wa kiroho kama ule aliouleta mzee wetu Fransisko.

 

 

2.11.       TANGAZO NA MANG'AMUZI

 

Kushirikisha imani ni tukio la neema linalofanyika Neno la Mungu likikutana na mang'amuzi ya mtu na kumuonyesha maana ya matukio (ya Biblia, ya liturujia, ya maisha ya Kanisa na ya maisha ya kawaida) kadiri ya ufunuo.

Tunaweza kuanza na tangazo la habari njema halafu kuona namna ya kulipokea maishani, au kuanza na maisha yalivyo, yaani hali na maswala ya watu, halafu kuyaangaza kwa Neno.

Njia zote mbili zinafaa zikitumika vizuri kwa kujali imani na akili, yaani fumbo la neema na mang'amuzi ya binadamu.

Mang'amuzi hayo yatathminiwe mfululizo kwa makini, kwa kuwa:

- yanasababisha ndani ya mtu mivuto, maswali, matumaini, mafadhaiko, mawazo na maamuzi ambayo yote yanaungana katika hamu ya kubadili maisha;

- yanasaidia kuelewa ujumbe wa Kristo, tunavyoona alipoyatumia ili kudokeza mambo ya juu, na alipoelekeza msimamo wa kufaa mbele ya hayo;

- yakitumiwa na imani, ni mahali ambapo Mungu anamfikia binadamu na kumuokoa.

Malezi yamsaidie ndugu kuchambua mang'amuzi yake ya msingi na kuyapima kwa Injili ili aishi upya.

Kwa ajili hiyo, kabla hajaweka ahadi asipelekwe mbali mno na mazingira ya utamaduni wake, ili ajitahidi na kusaidiwa kuuelewa zaidi (pamoja na namna za kufikiri, kusema, kutenda na kukabili maisha, hekima, desturi, ishara, lugha, fasihi, sanaa n.k.).

Akipambanua kwa mwanga wa Injili tunu alizozirithi ataweza kutathmini utamaduni wowote wa watu atakaotakiwa kuwasiliana nao baadaye.

Walezi wa utakaji na zoezi wasipotokea katika mazingira hayohayo, waelewe utamaduni wa mlelewa na kuwapenda watu wake.

 

 

2.12.       IMANI NA MAISHA

 

Uhusiano wa Injili na mang'amuzi ya msikilizaji si swala la mbinu tu, bali unatokana na kiini cha imani: Neno alipojifanya mtu alitwaa ubinadamu wetu wote isipokuwa dhambi.

Akiwa mfano kamili wa Mungu asiyeonekana, ni pia mtu kamili kuliko wote, ndiye kielelezo cha utu, hivi kwamba mwenyewe tu anatuangazia fumbo la ubinadamu wetu tuweze kujielewa kweli pamoja na wito wetu wa ajabu.

Malezi yetu yanapokea kwake sheria ya uaminifu kwa Mungu na kwa binadamu kwa pamoja.

Kwa vile imani haitenganiki na maisha, bali inayaangazia yote, tulee kwa kulinganisha vizuri ya kibinadamu na ya Kimungu, tukisisitiza ukweli na uhuru kadiri ya Injili, uundaji wa dhamiri, ukomavu kwa ajili ya upendo, utambuzi wa wito na uwajibikaji.

Yesu aliishi kibinadamu kwa ukamilifu wote, akifanya kazi kwa mikono ya kibinadamu, akiwaza kwa akili ya kibinadamu, akitenda kwa utashi wa kibinadamu na kupenda kwa moyo wa kibinadamu; hivyo anatuwezesha tuishi hayo yote ndani yake, naye ayaishi ndani mwetu.

Kwa njia ya umoja huo imani inamfundisha mwanafunzi afikiri, atende na kupenda kama Mwalimu wake, na akimshiriki hivyo ang'amue uhai mpya unaomwezesha kuishi upya.

Kwa sababu hiyo tumkazie Yesu na kuangaza kwa Injili mang'amuzi ya walelewa binafsi na ya jamii ili tuchochee hamu ya kujirekebisha kimaisha.

 

 

2.13.       KUZINGATIA WASIKILIZAJI

 

Kulingana na nafasi tunayopokeza Neno la Mungu, tulitoe kwa namna maalumu, kwa kuzingatia tofauti za wasikilizaji upande wa utamaduni, umri, ukomavu wa Kiroho, hali katika jamii na Kanisa, maswala, matazamio na mahitaji ya ndani, lakini bila ya kusahau umoja wao wa msingi na ukweli wao kama binadamu kadiri ulivyofunuliwa na Mungu.

Tusiridhike kuitumia Injili kwa kupamba tu utamaduni, yaani kama nyongeza isiyo ya lazima, bali tuipendekeze kwa namna hai na ya dhati hata ipenye mizizi yenyewe ya utamaduni.

Kwa ajili hiyo:

- tutambue katika utamaduni wa watu tunu halisi ambazo zinalingana na Injili au walau ziko tayari kuipokea;

- tutakase yaliyoathiriwa na uovu, ujinga na udhaifu wa binadamu;

- tuchochee watu kukomaa kwa ndani na kumuongokea Mungu kabisa;

- tuhakikishe imani isipokewe kinadharia tu, bali iguse mioyo na kubadili mienendo hata isababishe maisha motomoto ambayo yanahuishwa na upendo na kuzaa matunda ya utakatifu.

 

 

2.14.       DINI SHULENI

 

Vipindi vya dini vinavyotolewa shuleni vieleweke kuwa vinatofautiana na kukamilishana na katekesi.

Kilicho maalumu cha vipindi hivyo ni kuchimba elimu ya dini kuhusiana na masomo mengine ili kuchangia ujuzi mzima wa mtu kuhusu asili ya ulimwengu, maana ya historia, msingi wa maadili, nafasi ya dini katika elimu na utamaduni, lengo la binadamu na uhusiano wake na viumbe vingine.

Somo la dini shuleni linaingiza Injili kama chachu katika juhudi za mpango kwa ajili ya elimu, ili itegemeze, ichochee, istawishe na kukamilisha fani zote na kupenya mawazo yote ya wanafunzi.

Kwa msingi huo linatakiwa kulingana na masomo mengine kwa hadhi, madai na usahihi, na kujadiliana nayo ili kumjenga mtu pande zote kwa umoja wa ndani.

 

 

2.15.       KUKARIRI

 

Katekesi inashirikisha kumbukumbu ya Kanisa, hivyo toka mwanzo kutumia kumbukumbu ya mtu ni sehemu ya lazima ya malezi ya imani, kwa kuwa imani na ibada hazichipuki katika jangwa la malezi yasiyotumia kumbukumbu.

Ili kukwepa hatari ya kukariri kimashine tu, kazi ya kushika kwa moyo inatakiwa kuhusiana na njia nyingine za kujifunza, kama vile maitikio ya kujianzia, majadiliano, kimya, tafakuri na maandishi.

Maneno muhimu zaidi ya Biblia, dogma, liturujia na sala ya Kikristo na ya Kifransisko yakaririwe pamoja na kueleweka kwa ndani na kushikwa kwa dhati: kwa hiyo yatolewe kama muhtasari baada ya ufafanuzi ili kudumisha umoja wa Kanisa katika mafundisho na lugha yake.

 

 

2.16.       MWANGA WA HABARI NJEMA

 

Tuwatangazie wasikilizaji Habari Njema kwa namna inayowafanya waone jinsi inavyotimiliza maumbile na matazamio yao na inavyoshibisha kiu ya moyo wao.

Katekesi ya Biblia iwasaidie kuelewa maisha ya leo kwa mwanga wa mang'amuzi ya taifa la Israeli, ya Yesu Kristo na ya Kanisa.

Katekesi ya Kanuni ya Imani iwaonyeshe jinsi mafundisho makuu ya ufunuo (uumbaji, dhambi asili, umwilisho, Pasaka, Pentekoste na vikomo vyetu) yanavyoangaza utu wetu.

Katekesi ya maadili ikiwaelekeza upendo kamili iwaonyeshe pia msingi wake katika maadili ya kibinadamu.

Katekesi ya liturujia iwakumbushe mang'amuzi yanayodokezwa na ishara na ibada zenye asili katika utamaduni wa Kiyahudi na wa wazee wetu katika Ukristo.

 

 

2.17.       TULEE KUJADILIANA

 

Mbele ya wingi wa dini na madhehebu tutoe malezi ya Kiinjili kwa namna inayofaa wahusika wajisikie furaha ya kuwa watoto wa Mungu na wa Kanisa, wawe na msimamo katika imani na waweze kujadiliana na yeyote kuhusu dini, wakitambua yasiyo ya kweli lakini pia wakifurahia chembe za ukweli ambazo katika dini hizo ni kama maandalizi ya Injili.

Tulee kwa uangalifu wa pekee kujali ukweli, haki na heshima kuhusu dini ya Kiyahudi, kwa kuwa Kanisa linahusiana sana na taifa la Israeli, lililokuwa la kwanza kusikiliza Neno la Mungu: pande hizo mbili zinafungamana zisiweze kujifanya hazifahamiani.

Tuimarishe misingi ya imani na kuchochea wongofu wa kudumu; tuchimbe ukweli na tunu za Kikristo dhidi ya vipingamizi mbalimbali vya kinadharia na vya kimaisha; tutambulishe kiini cha Injili na utekelezaji wake wa kila siku; hatimaye tuhamasishe umisionari kwa ushuhuda wa maisha, kwa ushirikiano na majadiliano, na kwa tangazo wazi la jina la Yesu.

 

 

2.18.       EKUMENI

 

Kila jumuia ya Kikristo inasukumwa na Roho Mtakatifu kujenga umoja; basi, malezi yoyote ya imani, hasa utawani, yanatakiwa kuwa na mtazamo wa kiekumeni:

- yalishe hamu halisi ya umoja, hasa kwa kupenda Maandiko;

- yafafanue kweli za imani, zinazotunzwa na Kanisa Katoliki, kwa kujali mpangilio wa umuhimu wake;

- yaonyeshe umoja uliopo tayari kati ya Wakristo wowote, pamoja na hatua za kuchukua ili kuyamaliza mafarakano, hasa kukazania wongofu na sala kusudi Roho abomoe kuta zote;

- hatimaye yaandae kuishi na ndugu wa madhehebu mengine kwa kuheshimu dhamiri yao bila ya kupotewa na sura halisi ya Kikatoliki.

 

 

2.19.       IBADA ZA WATU WADOGO

 

Katika Kanisa Katoliki zinapatikana namna maalumu za kuishi kidini ambazo zimejaa ari, nia safi na kiu ya Mungu kiasi ambacho watu sahili na maskini tu wanaweza kuwa nazo.

Hizo zinaweza kuwafanya:

- wahisi sana sifa za Mungu (k.mf. maongozi yake na uwepo wake wenye upendo);

- watimize kwa urahisi maadili kadhaa (k.mf. uvumilivu, kutoambatana na malimwengu, utayari wa kutumikia);

- wajitoe mhanga hadi ushujaa katika kuungama imani.

Hata hivyo imani hiyo inaweza ikahitaji kutakaswa na kuimarishwa isije ikapatwa na udanganyifu, ukali wa msimamo,na ushirikina wala kuchanganyikana na dini nyingine.

Kumbe ikiongozwa kwa hekima na utajiri wa katekesi inaweza kuleta umati wa watu wadogo wakutane kikamilifu na Mungu kwa njia ya Yesu Kristo: basi tufanye kazi hiyo hata kwa wenye wito wanaoonyesha kuwa na mwelekeo huo.

 

 

2.20.       MALENGO NA MBINU

 

Moyo wetu uzidi kupanuka na kutusukuma tufanye juu chini kwa wokovu wa watu.

Kila ndugu, pamoja na kutoa ushuhuda kwa matendo yake yote, anapaswa kuwa mwalimu wa imani.

Tangazo wazi la jina la Yesu ndilo kipaumbele cha kudumu cha umisionari ili watu waongoke kwa kuambatana naye na Injili yake.

Humohumo mna nafasi kwa utamadunisho na majadiliano na dini nyingine: changamoto hizo zikabiliwe kama wito wa kushirikiana na Roho Mtakatifu aliyetangulia kufanya kazi ndani ya watu wowote wa mazingira yoyote.

Kwa ajili hiyo turekebishe malengo na mbinu za utume kadiri ya mabadiliko ya mazingira; tujiandae kwa makini, tufanye utambuzi wa busara, tusipotoshe karama ya chama na tushikilie imani sahihi, uadilifu na ushirika na Kanisa lote.

Tukabili utamaduni wa wenzetu kwa msimamo wa kujikana na kutumikia kama Yesu, tukifuata nyayo alizoziacha Mungu katika historia ya watu binafsi na ya mataifa yao.

Utafiti huo unaweza kutuletea faida sisi wenyewe, kwa kuwa tunu tunazozivumbua zinatufanya tuelewe upya mapokeo ya Kikristo na ya Kifransisko.

 

 

2.21.       MALEZI YA KITUME

 

Utume wowote unapungukiwa nguvu ikiwa wanaoufanya wanakosa utakatifu, halafu vipawa, ujuzi na mang'amuzi.

Mipango, mbinu na vitendeakazi visipotumiwa na watu wenye sifa hizo havitoshi.

Kwa hiyo baraza lihakikishe malezi ya kitume kwa wote, katika hatua za kuingizwa na katika malezi ya kudumu.

Malezi hayo yana pande nyingi, lakini wa msingi zaidi unamhusu ndugu mwenyewe kama mtu, mwamini na mtume kulingana na karama alizojaliwa kama kleri, mtawa au mlei wa Kifransisko.

Utume wa kisasa unahitaji ndugu wanaoweza kuunganisha usahihi wa imani na ubora wa matendo, maswala ya Kikanisa na ya kijamii.

Lengo liwe kukomaza wamisionari kwa mazingira halisi ya leo, wenye sura ya ndani ya Kikristo, ya Kikanisa na ya Kifransisko ambao wanaweza:

- kutangaza jina la Yesu na Pasaka yake;

- kujulisha maisha yake katika mtiririko wa historia ya wokovu:

- kufafanua fumbo lake kama Mwana wa Mungu aliyejifanya mtu, tena mtumishi mtiifu hata kufa, naam, hata kufa msalabani;

- kushirikisha ujumbe wa Injili yake kwa urahisi, usahihi na nguvu;

- kuelekeza watu hatua kwa hatua katika kumfuata kwa imani;

- kusaidia kuungana naye zaidi na zaidi kwa njia ya sakramenti.

Mtazamo huo unaomkazia macho Yesu uathiri moja kwa moja nafsi na utume wa ndugu.

 

 

2.22.       UTUME NA WATU

 

Aandaliwe kurahisisha ustawi wa imani ya watu, bila ya kusahau kuwa imani si tunda la kazi yake, kwa kuwa Mungu tu anaipanda mioyoni.

Ajue vema: ujumbe anaokusudiwa kuueneza, wale anaotumwa kwao pamoja na mazingira yao, na namna ya kupasha ujumbe kwa unyofu katika mafungamano na majadiliano, kwa utulivu wa mitazamo kuhusu maisha, kwa uwezo wa kufariji na kutumainisha, na kwa nia safi ya kuongoza kwa niaba ya Yesu.

Amvutie yeye mioyo ya watu kwa kuzingatia heshima na uelewano; kwa kuwakaribia wenye shida; kwa kuwahurumia wakosefu na dhaifu; kwa kuamini uwezekano wa neema kuongoa watu; kwa kujitoa sadaka kwa ajili yao.

Utume unatarajiwa kustawisha upendo alionao kwa watu anaowashughulikia; upendo huo sio tu ule wa mwalimu kwa mwanafunzi wake, bali wa mzazi kwa mtoto wake: Bwana anataka kila mhubiri wa Injili na mjenzi wa Kanisa awe na upendo wa namna hiyo.

Vilevile imani aliyonayo inakusudiwa kukuzwa na utume wake: tunafundisha imani kwa kujifunza kwanza wenyewe, na tunapoishirikisha inaongezeka ndani mwetu.

 

 

2.23.       UTUME WAKATI WA KUINGIZWA UTAWANI

 

Kulingana na elekeo letu maalumu tulee hatua kwa hatua, kuanzia utakaji, kuwahudumia na kuwahubiria maskini.

Ni juu ya mlezi kuhakikisha kwamba kila ndugu, kadiri ya mahitaji na ya uwezo wake, apate mang'amuzi mbalimbali na ya kutosha kuhusu utume wetu, aufanye pamoja na wengine chini ya ndugu aliyekomaa zaidi na kwa namna ambayo idumishe jumuia, akikabili shida za mazingira bila ya kumezwa nayo.

Kwa msaada na mwongozo wa mlezi aelewe mapema masharti ya utume bora na kutambua jinsi karama yake inavyoweza kuchangia utume wa chama bila ya kuuvuruga, kwa kuoanisha kila siku maisha ya kijumuia na utume, yaani hali ya mfuasi anayeishi pamoja na Yesu na kundi lake dogo, na hali ya mtume anayepelekwa naye ashiriki kazi yake ya ukombozi.

Pia mbinu zinazotumika katika malezi ni za msingi kwa utume, kwa sababu ni vigumu kwa ndugu kubuni mitindo ambayo hajazoeshwa.

Halafu mwenyewe ajipatie namna yake ya kufanya utume akilinganisha misingi ya kazi hiyo na nafsi yake.

 

 

2.24.       MALEZI NA UTAMADUNISHO

 

Injili na karama ya Kifransisko vitaumua utamaduni wa watu (taifa, kabila na vikundi maalumu, k.mf. wasomi, wanafunzi, wafanyakazi, vijana, walalahoi) vikifaulu kuwasisimua na kuyakidhi mahitaji ya utu wao.

Hivyo inatubidi tuwajue vizuri ili kutamadunisha ujumbe wa wokovu uwaelee.

Lakini hatuwezi kuwa tangazo hai la Habari Njema kwa watu tukirudi nyuma upande wa imani na kujilinganisha na ulimwengu badala ya kuuangaza Kiinjili.

Basi, tuonyeshe kimaisha muungano safi wa imani na tunu za utamaduni, na kupinga mapotovu yanayoenea pasipo kuchujwa.

Tunapaswa kuwa waangalifu na kuchambua, kwa kuwa mema na mabaya, ambayo yanaathiri kila wakati na mahali na kujitokeza katika miundo ya jamii, yanapiga hodi katika maisha ya wote, hata ndani ya Kanisa na ya utawa.

 

 

2.25.       VYOMBO VYA UPASHANAJI HABARI

 

Tuwe makini kuhusu ujanja wa kikoloni wa wale wanaotumia vyombo vya mawasiliano ili kupotosha watu na kuwatawala kwa kujifaidisha.

Katika hatua za kuingizwa tueleze vyombo vya habari vinavyoweza kutuathiri sana, tuelekeze juu ya ukweli na uadilifu wa ujumbe wake, na kuzoesha msimamo safi katika matumizi ya kiasi tusije tukadhuriwa navyo.

Zaidi ya hayo, tusisambaratike katika kufuatafuata mfululizo habari za kila aina, kama kwamba kujua hali halisi ya Kanisa na ya ulimwengu kunategemea wingi wa habari.

Kinyume chake, tuwajibike kutambua yaliyo muhimu katika mwanga wa Mungu na tuyalete mbele yake katika sala.

Vilevile tuwaongoze watu wote wasizame katika malimwengu kwa mvuto wa vyombo hivyo, bali watambue ubatili mtupu wa mambo yapitayo na umuhimu wa jambo lile ambalo peke yake ni la lazima.

Tufuate katiba kuhusu vyombo vya habari: sharti hilo litatusaidia kutunza usafi wa moyo na roho ya sala, yaani kumuona Mungu katika vyote na yote.

Mawasiliano ya mlelewa na watu wa nje (kwa barua n.k.) yaratibiwe na mlezi, ili kuepa urafiki usiofaa au unaotawanya mawazo tu.

 

 

2.26.       MALEZI YA KIDARAJA

 

Kuhusu kusomea upadri au ushemasi, karama yetu ya kidugu inadai malezi yawe sawa kwao na kwa wenzao wote hadi kuweka ahadi.

Baada ya hapo malezi ya wale wanaojiandaa kupata daraja au huduma fulani yafuate sheria za Kanisa na za chama, bila ya kuweka pembeni masharti ya maisha ya kitawa tuliyoahidi, wala pengine madai ya uchipukizi.

Kozi maalumu za kusomea daraja zifuatwe kama sehemu ya mpango mpana zaidi unaohusisha malengo ya utawa wetu.

Kipaumbele katika masomo ya kidaraja ni kuchimba na kutafakari Maandiko Matakatifu na mafundisho halisi ya Kikatoliki hadi yawapenye kabisa, pamoja na kujifunza kupima vizuri dhana za teolojia ambazo hazijatathminiwa na Ualimu wa Kanisa.

Kwa ajili hiyo uzingatiwe hasa mfano na urithi wa mtakatifu Thoma wa Akwino na wa walimu wa Kanisa wa Kifransisko.

 

 

2.27.       MALEZI YA KICHUNGAJI

 

Ingawa malezi hayo yote yanalenga kazi ya kumuingiza mtu wa leo katika maisha ya Kanisa, yanahitajika malezi maalumu ya kichungaji ambayo yalingane na karama ya chama, na kuendana na utekelezaji wa huduma na daraja ambazo wanateolojia wanakabidhiwa moja baada ya nyingine.

Wanaolenga kuwa mapadri waandaliwe kwa kozi maalumu kutoa sakramenti ya upatanisho na uongozi wa Kiroho.

Kwa msaada wa padri mlezi na kadiri ya mtindo wa maisha yetu, wajitahidi hasa kulingana na Mchungaji Mwema katika kutamani wokovu wa watu na kujitoa kabisa kwa ajili hiyo.

Wachochee upendo huo kwa kuishi Kiroho kwa dhati, kusoma kwa bidii na kushiriki katika maisha ya Kanisa.

Mwishoni mwa masomo yote, wakati wanapotekeleza ushemasi katika uchungaji, wasaidiwe kusanisi yale yote waliyojifunza ili waone kwa umoja fumbo la Kristo.

Mtumishi kabla hajamuomba askofu wa jimbo ampe ndugu daraja takatifu ya ushemasi au ya upadri, awe na thibitisho la maandishi la mlezi kuhusu sifa zinazohitajika kisheria, pamoja na kibali cha halmashauri yake.

 

 

2.28.       MTAWA MWENYE DARAJA

 

Miaka mitatu inayofuata upadirisho ndugu wapangwe wanapoweza kujiendeleza kiteolojia na kichungaji.

Halmashauri kuu iwapangie walau vipindi kadhaa, hasa vya kichungaji, na semina moja kwa mwaka.

Mang'amuzi yanaonyesha kuwa katika mapadri watawa daraja takatifu inazaa zaidi kwa sababu mashauri ya Kiinjili waliyoyashika yanadai na kusaidia muungano wa ndani na Bwana.

Katika maisha yao upadri na utawa vinaunganika kwa dhati na kukamilishana katika kutimiza fumbo lote la Kristo.

Kanisa maalumu ndilo nafasi ambamo wito wowote unatekelezwa Kiroho na kitume: kila mmojawetu ajitahidi kustawi katika jimbo lolote kama mahali pake, bila ya kupoteza mwelekeo wa kimataifa wa chama chetu na wa taifa lote la Mungu.

Zaidi tena padri au shemasi ni msaidizi wa kundi la maaskofu kwa kushiriki utume wao chini ya mmojawao: basi ajisikie nyumbani katika jimbo lolote.

Malezi ya ndugu wanaotarajia kupewa daraja yazingatie watakavyopaswa kuingia katika kundi la makleri mara wa jimbo hili, mara wa jimbo hili.

Ndugu padri au shemasi akishiriki uchungaji pamoja na wenzake wanajimbo, anapaswa kuonekana wazi kimatendo kuwa ni mmisionari mtawa, tena wa Kifransisko.

Kwa ajili hiyo, anayejiandaa kupewa daraja na aliyekwishaipata vilevile azingatie masharti yafuatayo ili kulinganisha pande zote (utawa, umisionari na daraja) za wito wake ulio mmoja tu (kuwa padri au shemasi mmisionari wa Kifransisko):

- awe anaelewa kuwa daraja inahusu muundo na uongozi wa Kanisa, na kuwa utawa, hata ukidai utume, unahusu uhai na utakatifu wa Kanisa;

- kwa maisha ya Kiroho achote hasa katika chemchemi za Kifransisko na kuchochea ndani mwake karama ya chama ambayo ni zawadi ya Mungu kwa Kanisa;

- maisha yake yalingane na ushuhuda na mafundisho ya mwanzilishi;

- atekeleze kanuni na katiba alizoahidi;

- aishi katika jumuia hivi kwamba ushirika wa kidugu uwe ndio mwanzo na mwisho wa utume wake;

- awe tayari sikuzote kupelekwa na mtumishi akahudumie jimbo lolote.

 

 

2.29.            UMOJA WA NDANI MWETU

 

Katika utume wowote tukumbuke tunavyopaswa kuwa hasa viongozi wa Kiroho, jambo linalodai tustawishe paji lililo bora yaani Roho Mtakatifu.

Kwa njia yake tunamiminiwa upendo, ambao unaongoza na kuhuisha utekelezaji wa mashauri ya Kiinjili na utume vilevile.

Kwa kuwa yeye ni Roho wa umoja hata ndani mwetu, hatutakiwi kugawanyika kati ya maisha ya kitawa na utendaji wake.

Kwa ajili hiyo katika nafasi yoyote tudumu katika maisha yaliyofichika pamoja na Kristo ndani ya Mungu, tukimtafuta na kumpenda kuliko yote yeye aliyetangulia kutupenda: ndimo unamobubujika upendo kwa jirani, unaojitosa kwa ujenzi wa Kanisa, wokovu wa ulimwengu na ustawi wa jamii.

Basi, kumpenda na kumhudumia jirani kusitutenganishe na Mungu, bali huduma hizo zitokane kweli na upendo wa Kikristo ziwe ibada kwa Mungu.

Tufanye juu chini ili kuunganisha hivyo maisha ya Kiroho na utendaji, kusudi kazi tunazomfanyia Bwana zitufikishe kwake, aliye chemchemi na lengo la utendaji wowote.

Tujifunze mapema jinsi sala ilivyo moyo wa utume, na jinsi utume unavyotakiwa kuchochea sala, halafu kila mmojawetu atathmini mfululizo kama utendaji wake unatokana na muungano wake na Mungu, unaudumisha na kuuimarisha au la.

 

 

2.30.       UTUME NA JUMUIA

 

Utendaji wetu utokane vilevile na maisha ya pamoja na moyo wa kijumuia, na ueneze udugu kwa maneno na matendo.

Ushirika wetu wenyewe ni utume tayari, kwa kuwa ndio ishara kuu ya wafuasi wa Bwana inayofanya ulimwengu usadiki.

Utawa utazaa matunda kadiri yalivyo bora maisha yake ya kidugu; kadiri hiyohiyo watawa watadumu katika wito na hivyo watakuwa ishara ya uaminifu wa Mungu kwetu itakayotegemeza uaminifu mgumu wa Wakristo wa ulimwenguni kwake.

Maisha ya kijumuia yana thamani hasa mishenini kwa kuwa yanawaonyesha wasio Wakristo upya wa dini yetu, yaani upendo: kumbe ndiko utekelezaji wake unapopambana na matatizo mengi zaidi na unakodai juhudi za pekee ili kuyatatua.

Utiifu kwa matakwa ya Mungu yaliyodhihirishwa na watumishi na walinzi ndio njia ya kujipatia umoja maishani.

 

 

 

 

3. WATENDAJI

 

3.1.     BABA

 

Wokovu wetu binadamu, ulio lengo la milele la mpango wa Mungu, ni tunda la malezi yake ya ajabu katika historia yetu yote.

Katika Maandiko anajifananisha na baba, mwalimu na mzee mwenye hekima ambaye anampokea mtu alivyo, anamkomboa katika vifungo vya uovu na kumvuta kwake kwa vifungo vya upendo, akimfanya akue hatua kwa hatua kuelekea ukomavu wa mwana huru na mtiifu.

Ili kufikia lengo hilo anatumia majaribu, tuzo na adhabu.

Akijilinganisha na nyakati na hali mbalimbali za watu anaowalea, anawageuzia matukio ya maisha yawe mafundisho ya hekima ambayo yakabidhiwe toka kizazi hata kizazi.

 

 

3.2.           MWANA

 

Wakati ulipotimia Baba alimtuma Mwanae aendeleze malezi hayo ya Kimungu kwa kutumia mbinu zote za mawasiliano kati ya watu, kama vile semi, mifano, kimya, ishara na matendo.

Yesu aligusa wote kwa jinsi:

- alivyotangaza ufalme wa Mungu kama habari njema ya ukweli;

- alivyowapokea watu, hasa maskini, wadogo na wakosefu kama wapenzi wa Baba;

- alivyowapenda wote kwa hisani na nguvu ili kuwakomboa;

- alivyowahimiza kuishi kwa imani, tumaini na upendo usio na mipaka.

Hivyo alifunua Mungu na binadamu walivyo, akiokoa na kuongoza, akisema na kusukuma, akikosoa na kusamehe.

Aliwalea kwa makini hasa wanafunzi aliotaka wawe wajumbe wake:

- alijitambulisha kwao kama mwalimu pekee, mwenye utambuzi na ubunifu, akiwafundisha kwa maisha yake yote; na papo hapo kama rafiki mvumilivu na mwaminifu akiwajulisha yote aliyoyasikia kwa Baba;

- aliwachochea kwa maswali ya kufaa;

- aliwafafanulia kwa ndani zaidi yale alioutangazia umati;

- aliwaingiza katika sala yake;

- aliwapeleka kufanya mazoezi ya kitume;

- aliwapitisha kwenye majaribu;

- aliwatabiria yatakayowapata;

- hatimaye aliwaahidia Roho wa Baba ambaye atawaongoza kwenye ukweli wote na kuwategemeza katika nafasi ngumu.

Yesu Emanueli yupo bado pamoja nasi, akija kwetu kila siku tuongozane safarini mpaka aje kwa utukufu.

 

 

3.3.     ROHO WA BWANA

 

Mzee wetu Fransisko tangu aongoke, pamoja na kuzingatia ishara yoyote ya matakwa ya Baba ili ayatimize, imara katika nia ya kufuata upeo Injili ya Mwanae, alizidi kutambua na kushangaa kazi ya Roho Mtakatifu ndani mwake mwenyewe na katika utawa wake, akishirikiana naye kwa unyenyekevu na usikivu.

Akiwa mtu wa Roho, aliita "Roho wa Bwana" uwepo huo wa Mungu katika maisha yetu, ambao unakuwa hakika na upendo katika maisha ya imani tupu, na unatuchochea tushuhudie na kutangaza Injili.

Malezi na maisha yote ya Kifransisko yanategemea kuwa wazi daima kwa Roho Mtakatifu, anayefanya kazi ndani ya moyo hadi matunda yaonekane kwa nje, katika ulinganifu wa mwamini na Yesu kwa utukufu wa Baba.

 

 

3.4.            UPAMBANUZI WA ROHO

 

Yeye ni Roho wa ukweli ambaye anafundisha, anakumbusha na kuongoza hadi ukweli wote; ni mpako unaowezesha kupima, kuchagua na kuonja; ni mtetezi na mfariji ambaye anasaidia udhaifu wetu, akitutegemeza na kutufanya wana wa Mungu; ni mtendaji asiyeonekana wa malezi na wa utakatifu ambaye anadai tuwe macho kutambua na kufuata sauti yake kwa kuweka pembeni mivuto ya ubinadamu na ya shetani.

Utambuzi huo ni tunda la kujizoesha mfululizo:

- kupokea matakwa ya Baba ili kuambatana naye kabisa;

- kujichunguza ili kuanza upya kila siku kadiri ya Injili;

- kusoma ishara za nyakati, mahitaji ya Kanisa na tunu za watu;

- kusali, kutafakari na kujadiliana;

- kuwa na busara, unyofu na uhuru wa ndani;

- kutojiamini mno, bali kuwajali wengine, kuelewa mitazamo yao, kusikiliza lawama zao na kujirekebisha mapema panapotakiwa.

- kutambua Roho anavyotenda na kusema kwa njia ya watu aliowakabidhi huduma na karama nyingine, tukiwa tayari kushauriwa na kuelekezwa hasa katika uongozi wa Kiroho, kwa kuwa si rahisi mtu kukomaa peke yake.

 

 

3.5.            KANISA

 

Tangu mwanzo Kanisa, kama sakramenti ya Kristo, limeshiriki katika malezi hayo likipata kwake neema za juu, mvuto wa kudumu na mfano wa hakika kwa kazi hiyo yote.

Karne hadi karne limejipatia hazina kubwa ya mang'amuzi: ushuhuda wa watakatifu, aina mbalimbali za maisha ya Kiroho, hatua za malezi, utajiri wa mafundisho n.k.: hayo yamekuwa urithi wetu hasa kupitia mapokeo ya Kifransisko.

Kanisa ni mama na mlezi wetu halisi, linaloendeleza utume wa Bwana Yesu kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.

Kwa mfano wa Bikira Maria linatunza moyoni hazina ya imani, halafu linaitangaza na kuiadhimisha na kuitekeleza.

Hivyo linashirikisha imani linayoishi, tumaini lililojawa nalo na upendo lililonao ili viumue maisha ya wapokeaji, nao wavitajirishe kwa tunu za utu na utamaduni wao.

Tustawishe mapema tabia ya kuambatana daima na Kanisa na viongozi wake.

Ndani yake, kwenye meza ya Neno la Mungu na ya Mwili wa Kristo, tunapata mkate wa uzima ambao ulishe maisha yetu yaliyowekwa wakfu kuanzia ubatizo; kwa sakramenti ya kitubio tunayopata mara kwa mara tunajaliwa huruma ya Mungu na kupatanishwa na jumuia ya waamini tuliyoijeruhi kwa dhambi: hivyo liturujia ni kilele kinacholengwa na jumuia yoyote ya Kikristo, na chemchemi ya nguvu yake ya Kiinjili.

 

 

3.6.            KULEA KIKANISA

 

Kwa kuwa malezi ya Kikristo ni tendo la Kikanisa hasa, wanaoyashughulikia wawe daima waaminifu kwa Kristo na kwa Kanisa vilevile, wakishikilia ufunuo ulivyotufikia: tunaipokea Injili kwa Kanisa na kuielewa kwa msaada wa mapokeo yake na wa ufafanuzi rasmi wa ualimu wake.

Hasa malezi ya kitawa yanatakiwa kufanywa katika ushirika wa Kanisa, kwa kuwa watawa ni watoto wake kwa namna ya pekee.

Tuliojitoa kabisa kwa Mungu tunahusiana sana na fumbo la Kanisa, maisha yake na utakatifu wake, na tunasukumwa na mashauri ya Kiinjili tutende kwa moyo usiogawanyika kwa ustawi wa Mwili wote wa Kristo.

Ndiyo sababu katika sadaka ya Misa siku ya ahadi ya daima tunawekwa wakfu upya kwa Mungu kwa ajili ya umisionari wa Kanisa: katika tendo hilo vinaingia kazi ya Mungu, itikio la ndugu na upokeaji na utoleaji wa Kanisa.

 

 

3.7.           ASKOFU

 

Daima kutangaza, kuadhimisha na kutekeleza Injili kunafanyika katika Kanisa maalumu (jimbo), yaani jumuia ya wanafunzi wa Kristo inayoishi katika mazingira fulani ikitimiza sifa zote za Kanisa lililo moja, takatifu, katoliki na la mitume.

Mtaguso wa Pili wa Vatikano umesisitiza nafasi ya askofu katika maisha yote ya Kanisa, kuanzia malezi ya imani anayoyatoa kwa karama ya ukweli.

Kama mwalimu halisi wa ukweli wa Kimungu na wa Kikatoliki, ufundishaji wa imani jimboni ni juu yake.

Vilevile kama mlezi wa ukamilifu kwa wanajimbo ana jukumu la kuwaelekeza wote wamfuate Yesu, na kwa namna ya pekee waliojaliwa karama ya kumfuata kwa karibu zaidi.

Hivyo anapaswa kukesha juu ya safari yetu watawa kuelekea utakatifu ili alinde uaminifu wetu kwa wito huo maalumu.

Huduma hiyo ya askofu haitakiwi kugongana na ile ya viongozi wa utawa, kwa kuwa yeye anapaswa kutumia mamlaka yake kwa kuheshimu ya kwao, nao wamewekwa kuongoza katika maisha ya Kiinjili jamaa nzima au jumuia yake mojawapo, kwa kulingana daima na maaskofu.

Chama chetu pia kina taratibu zake na mamlaka yake kwa ustawi wa maisha ya kitawa, lakini hizo zinapaswa kutekelezwa katika ushirika wa Kanisa, zikilindwa na kudumishwa na askofu.

Chama chetu kama shule ya ukamilifu na njia ya utakatifu ni mali ya Kanisa; kwa hiyo ustawi wa taifa lote la Mungu unamdai askofu awajibike sio tu kuhusu utendaji wetu, bali kimsingi zaidi kuhusu utakatifu wetu na usahihi wa imani yetu.

Basi, askofu wa jimbo tunamoishi ajulishwe na mtumishi safari yetu ya malezi aweze kujihusisha ipasavyo.

 

 

3.8.           JUMUIA ZA KIKRISTO

 

Ushirika, ambao ni tunda la Roho Mtakatifu na kiini kinachounda Kanisa la kimataifa na kila Kanisa maalumu katika umoja, unatekelezwa katika jumuia za namna nyingi, ambamo Wakristo wanazaliwa katika imani, wanalelewa na kuishi: familia, parokia, mashirika, vyama, jumuia ndogondogo, shule za Kikatoliki.

Jumuia yoyote ya Kikristo ni asili, mahali na lengo la malezi ya imani: tangazo la Injili linaanza daima katika jumuia likimuita kila ndugu kuongoka na kumfuata Kristo; ndiyo inayowapokea wanaotaka kumjua zaidi na kuishi upya; ndiyo inayowasindikiza kimama ikiwashirikisha mang'amuzi yake.

Kimsingi, malezi ya imani ni yaleyale daima, ila aina ya jumuia yanapofanyika inayatofautisha.

Jumuia ya Kikristo inaundwa na kujitokeza hasa katika parokia kwa kuwa ndiyo mahali penyewe pa huduma ya Neno na maadhimisho mbalimbali na ndipo tofauti zote za kibinadamu na za karama zinapoyeyushwa na upendo ili kuunda umoja.

Kwa hiyo:

- toka mwanzo wa malezi ya kitawa tusisitize kujisikia wanaparokia;

- tusilee bila ya uhusiano na parokia;

- tuwe wepesi kushiriki maisha yake chini ya paroko;

- tuchangie kuifanya iwe familia inayovutia, ambapo Wakristo wote wajitambue kama ndugu.

 

 

3.9.           CHAMA NA VIONGOZI WAKE

 

Ndani ya Kanisa, malezi yetu ni jukumu la chama kizima, nacho kinayachangia hasa kadiri kinavyoishi kulingana na karama, bila ya kupatwa na uvuguvugu katika mienendo na mitazamo ya jumla na ya wanachama binafsi.

Ni kwamba ustawi wa mtu katika hatua zote unategemea sana mazingira yake.

Ni hivyo hasa upande wa imani kwa kuwa tunakutana na Yesu hai katika jumuia.

Kila mmojawetu anamuitikia akifungamana na wengine walioitwa namna ileile kusudi tuishi kwa umoja.

Basi, maisha bora ya pamoja yatazamwe kuwa mazingira ya lazima ya malezi yetu, hasa ya awali.

Jumuia ambayo kweli inatokana na imani, inajitahidi kutekeleza Injili na kuwa ishara ya upendo kati ya watu, inasali na kufanya kazi, inashirikisha na kutumikia kwa ari ya kitume: ndiyo shule ya kufaa kwa vizazi vipya.

Wanaolelewa wanahitaji kukuta humo ari ya Kiroho na ya kitume ambayo iwavute kumfuata Kristo kwa nguvu zao zote.

Jumuia zote za malezi zishike sana kanuni, katiba na ratiba: ndilo jambo ambalo linalea zaidi na kustawisha wito.

 

 

3.10.       JUMUIA YA KITAWA

 

Jumuia inaundwa siku kwa siku chini ya Roho Mtakatifu, ikikubali kupimwa na kuongozwa na Neno la Mungu, kutakaswa na kitubio, kujengwa na ekaristi, kuhuishwa na maadhimisho ya mwaka wa liturujia.

Halafu umoja wake unastawi tukisaidiana kwa ukarimu na kushirikishana mema ya Kiroho na ya kimwili.

Mafungamano kati yetu yawe na unyofu na tumaini, yakitegemea hasa imani na upendo.

Kila ndugu ajisikie anapokewa kama zawadi ya Bwana na anasaidiwa na hali ya kifamilia kutambua vipawa vyake na kustawi kwa kuitikia wito kwa bidii kubwa zaidi na zaidi.

Jumuia bora inajitambulisha kwa jinsi inavyoshughulikia malezi, ikiyaweka mbele kuliko kazi za nje, na inavyomwezesha kila mmojawetu kukua katika uaminifu kwa karama ya chama.

Basi, tuwe tumekubaliana kweli kuhusu malengo yetu, mipango ya malezi na mbinu zake; halafu mara kwa mara tutathmini malezi na maisha yetu kwa jumla.

 

 

3.11.       WALELEWA

 

Jumuia haitoi tu kwa walelewa, bali inapokea pia toka kwao: wanaojiunga wanailetea utajiri wao wa kibinadamu na wa kidini, hivi kwamba jumuia inakua na kustawi.

Malezi yenyewe hayakomazi tu walelewa, bali jumuia pia.

Kila mmoja ajitambue mlelewa na mlezi sawia na kuwajibika kukua si kwa ajili yake mwenyewe tu, bali kwa manufaa ya jamaa yote, akitekeleza karama yetu na kushirikiana na watumishi, walinzi na walezi.

Jumuia zetu ni jinsi tunavyoziunda: ili ziweze kutulea, zinadai kwanza tuzipende, tuzistawishe na kuzitumikia.

Jumuia ya Yesu na mitume wake iwe lengo letu na onyo kwetu ili tujenge jumuia kwa bidii na unyenyekevu, bila ya kukata tamaa wala kusahau ubinadamu wetu ulivyo.

 

 

3.12.       WALEZI

 

Malezi ni ushirikiano wa upendo hasa kati ya wawili: Mungu akiwa daima wa kwanza, mwamini aliyeitwa naye ana jukumu la kumuitikia, akitegemea kuwa Mungu atakamilisha alichokusudia.

Hisi ya wajibu huo na ya uwezekano huo inamsukuma mtu atafute kwa unyenyekevu mwanga na njia, iwe ni moja kwa moja toka kwa Mwenyezi Mungu, au kupitia maelekezo na misaada ya kidugu ya waliokomaa zaidi ambao Bwana anawaweka karibu naye ili wamsaidie kutambua na kufuata uongozi wa Mungu katika safari yake ya maisha.

Wenyewe ni washiriki tu wa kazi anayoifanya Mungu ndani ya kila mmoja, kwa sababu hakuna kiumbe kinachoweza kushika nafasi ya uhusiano hai wa moyo wa Baba na moyo wa mwanae wa kambo.

Mungu tu anaweza kumuita, naye tu anamwezesha kuishi Kikristo, akimuunda kwa njia ya Roho awe na msimamo uleule wa Mwanae mpenzi.

Kuitikia kwa hiari ni kukubali yale yote yatakayotokana na jibu la ndiyo, ambalo si la kinadharia bali la kimaisha.

Basi, kwa vile hali za maisha hazirudii kamwe, na upendo, wito na utendaji wa Mungu ni mpya daima, mtu anaalikwa mfululizo kumuitikia upya.

Safari yake inafanana na ile ya taifa la Israeli toka Misri, jangwani hadi nchi ya ahadi; pia inakumbusha mabadiliko ya polepole ya wanafunzi wa Yesu wenye mioyo mizito ya kuamini.

 

 

3.13.       USHIRIKIANO KATIKA MALEZI

 

Malezi ni kazi kubwa na ya msingi kwa ustawi wa Kanisa na chama ambayo haiwezi kufanywa na mlezi binafsi, bali inadai ushirikiano wa wote ili tuyakamilishe iwezekanavyo.

Mtumishi na mlinzi wana majukumu maalumu kama wastawishaji wa ndugu mmojammoja na kijumuia ili wakomae pande zote (teolojia, roho, utume, utu, elimu na ufundi) juu ya msingi wa Kristo kadiri ya karama yetu.

Ingawa mlelewa ndiye wa kwanza kuwa na jukumu kuhusu wito wake, hawezi kulitimiza nje ya mapokeo ya chama, ambayo mlezi ndiye shahidi na mwelekezaji wake rasmi.

Yeye ametumwa na chama ili kwa niaba yake, kwa uaminifu kwa karama yetu maalumu, na kwa ushirikiano na wahusika wengine, awasaidie walelewa kushika maisha yetu kwa msimamo wa dhati utokanao na imani.

Kwa kazi hiyo nyeti sana tuandae ndugu ambao, pamoja na kujua vizuri na kukubali imani na maadili katoliki, wawe na sifa za kufaa kama vile:

- hekima itokanayo na usikilizaji wa dhati wa Neno la Mungu;

- upendo kwa liturujia na ujuzi wa nafasi yake katika malezi;

- mang'amuzi ya sala;

- uwezo wa kushirikisha karama yetu kama tunu kwa siku hizi;

- tumaini imara kwa Mungu kuhusu kesho ya ulimwengu, ya Kanisa na ya chama;

- utulivu wa ndani na mapendo halisi kwa wale aliokabidhiwa;

- kipawa cha kupokea na kuelewa watu;

- nia ya kujitoa ahudumie kila mmoja, sio kikundi tu;

- uhusiano mzuri na jumuia;

- elimu inayohitajika na hamu ya kujiendeleza.

 

 

3.14.       UMUHIMU WA KAZI YA MLEZI

 

Katika hatua yoyote, karama aliyojaliwa mlezi, uimara wake katika imani na ushuhuda safi wa maisha yake, ndivyo roho ya mbinu zozote kwa kuwa ndivyo vinavyoweza kuhakikisha matumizi ya kufaa ya maandishi na vitendeakazi vingine.

Mlezi ni mshenga kati ya walelewa na fumbo la Mungu, kati yao wenyewe kwa wenyewe, na kati yao na jumuia.

Maneno na maisha yake yawasaidie kutamani, kupokea na kuchimba ujumbe wa Kristo.

Ajue sana njia ya Mungu hata aweze kuielekeza kwa wengine, akiwaonyesha vizuio lakini hasa uzuri na thamani ya karama inayowezesha kumfuata Yesu kwa karibu zaidi.

Ustahimilivu na tumaini yawe maadili yake maalumu, akikumbuka kwamba ustawi wa roho ni tunda la neema ya Mungu na la hiari ya mhusika, hivyo ategemee hasa kazi ya Roho Mtakatifu na sala, toka mwanzo hadi mavuno yatakapopatikana.

Atambue vema lengo la kazi yake, kwa kuwa katika malezi malengo ni muhimu; mojawapo, tena kuu, ni kuwafikisha ndugu kwenye uwiano wa maadili yote.

Awahimize watekeleze mambo yote ya kanuni na katiba zetu bila ya kukwazwa na ruhusa ambazo wengine wanaweza wakapewa kwa udhaifu wao; kinyume chake wajitahidi kufidia kwa niaba yao.

 

 

3.15.       MALEZI NA MOYO WA MTU

 

Malezi yamguse mtu mpaka ndani, kwa kuchochea dhamiri yake awajibike kujipatia tunu za Kiinjili na za Kifransisko pamoja na kushika taratibu anazoelekezwa, akiamini anachofanya kwa msukumo wa Roho Mtakatifu, badala ya kuiga tu au kulazimishwa.

Kwa ajili hiyo walezi waoanishe malezi ya kundi zima na ya kila mmoja, kwa kujali muda uliopangwa jumla kwa kila hatua na hasa muda anaohitaji mtu maalumu kadiri ya mwendo wake.

Kwa kuwa kiwango cha elimu na cha ukomavu cha walelewa ni tofauti, wazingatie kwa makini mahitaji ya kila mmoja ili wawahudumie kwa hisani na uaminifu.

Wawe karibu nao sana, daima tayari kwao, kwa moyo unaojali maswala yao na ni mwepesi kuhisi mambo wanavyoyaona wao.

Halafu:

- walete mwanga;

- watoe maelekezo;

- wasahihishe mitazamo;

- wakosoe kwa busara, imara na upendo;

- wasaidie kuchagua yanayofaa na kujibandua inavyotakiwa;

- wachochee maswali, juhudi na mabadiliko wakati wa wasiwasi, udhaifu na ulegevu;

- waratibu mipango;

- watambue pamoja na walelewa vipawa vyao na kuwahimiza wavitumie vizuri hivyo na muda waliojaliwa;

- wawalishe kadiri ya hatua waliyofikia;

- wapime pamoja nao maendeleo yao na jinsi wanavyotimiza masharti ya hatua hiyo.

 

 

3.16.       USINDIKIZAJI WA BINAFSI

 

Watumie hekima ya Roho na ujuzi wa kibinadamu katika kufanya utambuzi wa wito na kumlea mtu awe huru.

Njia kuu ni uhusiano mzuri na mlelewa na maongezi ya mara kwa mara naye: usindikizaji wa binafsi unaonekana kidogo na kudai sana, lakini ni muhimu kuliko kazi nyingine na miundo ya malezi.

Ni kumsikiliza kwa moyo wazi na kumpokea alivyo, anapojitahidi kujitambua na kujifunua, aweze kujithamini zaidi jinsi alivyo pamoja na anavyoitwa kuwa.

Kwa mfano wa Yesu na wanafunzi wake, fungamano la mlezi na mlelewa ni la lazima daima kwa kuwa linagusa kuliko mafundisho ya hadhara.

Walezi waunde mazingira yanayosaidia kuwa wazi, kuaminiana na kuwasiliana kwa unyofu na uhuru, la sivyo hawataweza kutimiza kazi hiyo kwa urahisi.

Hata hivyo wasisikilize maungamo ya wale wanaowalea wasipowaomba wenyewe.

 

 

3.17.       MUUNGAMISHI NA KIONGOZI WA KIROHO

 

Pamoja na hayo waheshimu nafasi ya padri muungamishi (yule wa kawaida ateuliwe na askofu wa jimbo husika) na ya kiongozi wa Kiroho (halmashauri imteue mmoja kwa kila nyumba ya malezi).

Pia wahakikishe kwamba wanazoezi na watawa chipukizi wanafuata kweli uongozi wa Kiroho.

Ni lazima katika chama tuwe na watawa wenye uwezo wa kuwasaidia wenzetu upande huo: kwa kuwa ndio wanaopenda zaidi maisha yetu na wameng'amua shida zake maalumu pamoja na namna za kuzikabili.

Kazi yao inategemea maendeleo ya yule anayeongozwa, lakini kwa jumla jukumu lao hasa ni kutambua kazi ya Mungu ndani yake, kumlisha maneno ya imani, kumuelekeza katika utekelezaji wa maadili na sala, kumsindikiza katika njia ya Bwana na kutathmini safari aliyokwishafanya, bila ya kuishia katika saikolojia, kwa kuwa mbinu za kibinadamu haziwezi kushika nafasi ya zile za Kiroho.

Ndugu akijifunua kwa unyenyekevu na unyofu anaweza kupata mwanga wa hakika katika kuelekea ukamilifu wa Injili, anavyohitaji hasa katika hatua za kuingizwa na nyinginezo za pekee.

 

 

3.18.       USHIRIKIANO

 

Chini ya mtumishi uongozi wa walelewa ni juu ya mlezi wao tu: asitingwe na shughuli yoyote inayoweza ikamzuia asifanye kikamilifu ile ya malezi; akiwa na wasaidizi, wawajibike chini yake na kumsaidia kufanya utambuzi wa miito halisi.

Katika kundi la walezi kazi ni tofauti lakini zina lengo moja; hivyo kila mmojawao atambue nafasi yake na mipaka yake pamoja na kuheshimu kazi za wenzake.

Wote watende kwa umoja hata wakishughulikia hatua mbalimbali.

Kwa ajili hiyo mara moja kwa mwaka mchochezi wa malezi ya kudumu, mlezi wa machipukizi, wa wanazoezi na wa watakaji watathmini kwa pamoja malengo na utekelezaji wake ili kulinganisha kazi zao kufuatana na mpango huu.

Wakiitwa kutoa huduma ya mafundisho, sakramenti au uongozi wa Kiroho mapadri, watawa au walei wa nje ya chama, wasaidiwe kuelewa karama yetu maalumu na kuistawisha kwa kushirikiana na kuheshimiana na mlezi katika kazi zao tofauti.

Walelewa wakitumwa kupata mafunzo katika vituo yisivyo vya chama, watumishi na walezi wawe macho ili mafunzo hayo yachangie malezi yetu bila ya kuyavuruga.

 

 

3.19.       WAZEE WETU NA WATU WA NJE

 

Biblia na utamaduni wetu vinamuona mzee kama mlezi asili kwa kujawa na hekima, uchaji wa Mungu na mang'amuzi.

Jumuia na walezi wamsaidie ndugu mzee kuutumia utajiri wake huo kwa ustawi wa chama: mabadilishano kati ya ndugu wa marika mbalimbali yatawafaa wote, hasa vijana.

Mafungamano na watu wa nje pia, hasa maskini, yanaweza yakachochea karama ya kitawa na kuwa njia ya malezi.

Watu wadogo wanatufundisha tuwe kweli ndugu wasio na makuu, washiriki wa hali yao na washirikishaji wa yale yote tuliyojaliwa, wasikilizaji wa dhati wa watu, hali na matukio.

Inapowezekana familia ya mlelewa ipewe nafasi ya kujua chama chetu, maana ya utawa na namna inavyoweza kushiriki katika malezi na utambuzi wa wito wa mtoto wao.

Upande wetu, kama Wafransisko, tunapaswa kudhihirisha tunavyojisikia ndugu hasa kwao, ingawa jamaa ya kitawa ndiyo familia yetu mpya.

 

 

3.20.       MAKLERI, WATAWA NA WALEI KUCHANGIA MALEZI

 

Makleri, watawa na walei wachangie kwa pamoja malezi yetu ili yatolewe kikamilifu iwezekanavyo: ikikosekana aina mojawapo ya waamini kati ya hizo, malezi yanapungukiwa kiasi cha utajiri wake.

Mchango maalumu wa padri unatokana na sakramenti ya kudumu ya daraja inayomlinganisha na Kristo Kichwa ili aunde jumuia kwa kuratibu na kuimarisha huduma na karama nyingine za waamini wote.

Mang'amuzi ni kwamba ubora wa malezi unategemea sana uwepo na utendaji wa padri, hasa katika kitubio na uongozi wa Kiroho.

Pia ahamasishe wote wawajibike kwa pamoja na kuheshimu waliopewa rasmi kazi ya kulea; aelekeze mafundisho na malezi kwa jumla yatolewe vizuri kulingana na mipango ya Kanisa; ahusianishe malezi na liturujia, hasa anapoadhimisha ekaristi.

Mchango maalumu wa mtawa unatokana na mashauri ya Kiinjili anayoyashika ambayo amewekwa wakfu upya na kufanywa ishara hai ya uzima wa milele.

Kwa kuwa hiyo ni zawadi ya Mungu kwa Kanisa lote, yeye anaitwa kutoa katekesi kwa namna ya pekee, na kila shirika linatakiwa kujitahidi iwezekanavyo katika kazi hiyo.

Karama ya mwanzilishi ina uzito mkubwa kidini, kijamii na kimalezi, hivyo isiwekwe pembeni katika utume wa wafuasi wake, bali watoe ujumbe uleule wa Kanisa kwa mikazo maalumu; historia inaonyesha uhai ulioletwa na karama hiyo.

Basi hayo yaliyo kweli kuhusu utume kwa watu wa nje, ni kweli zaidi kuhusu malezi ya wanaojiunga na utawa: ni lazima hayo yatolewe kadiri ya karama yetu maalumu, hasa na sisi tuliyonayo.

Hatimaye, mchango wa mlei una sifa maalumu inayotokana na hali yake ya kuishi ulimwenguni kabisa akipokeza Injili kwa kuzingatia sana utekelezaji wake katika maisha ya kila siku ya watu wa kawaida.

 

 

 

 

4. UTU NA UKRISTO

 

4.1.            MALEZI YA KIBINADAMU

 

Milenia mpya inapoanza tutazame kwa huzuni ya kimama umati mkubwa wa wanaume na wanawake, watoto na wazee wanaokosewa haki na heshima wanazostahili.

Dhuluma za kila siku zinamfanya kila mmojawao awe maskini sio tu upande wa uchumi, bali pia upande wa elimu, maadili na dini.

Kumbe watu wote, wa kabila, hali, umri na jinsia yoyote, kutokana na hadhi yao kama binadamu, wana haki ya kupata malezi yanayolingana na matarajio, vipawa na utamaduni wa kila mmoja.

Malezi hayo yanatakiwa kuwaelekeza wafungamane kidugu na watu wowote ili kuchangia maendeleo ya jamii katika umoja na amani, na hasa wawe tayari kuipokea Habari Njema ili walifikie lengo kuu la kuishi na Mungu milele.

 

 

4.2.            MALEZI YA KIKRISTO

 

Vilevile wabatizwa wote, kutokana na hadhi yao kama wana wa Mungu, wana haja na haki ya kupewa na mama Kanisa malezi ya Kikristo ili wakomae Kiroho.

Imani waliyojaliwa kwa mfumo wake inatakiwa kujulikana, kuadhimishwa, kutekelezwa na kugeuka sala, tena si kibinafsi tu, bali katika jumuia ya Kikristo na kwa kuelekea utume ulimwenguni.

Tunapofanya kazi hizo tuzingatie hali ya ardhi, yaani mambo yanayoweza kuchangia au kuzuia mavuno moyoni mwa mtu, ili apokee mbegu vizuri iwezekanavyo na hatimaye azae sana kwa utukufu wa Baba.

Tukumbuke daima kwamba kila mmoja ni mtu wa pekee, anaishi katika hali maalumu na kuathiriwa na malezi, jamii, utamaduni na dini, ajue asijue.

Kwa mfano, tofauti kati ya maisha ya vijijini na ya mijini inasababisha athari mbalimbali.

Mara nyingi vijijini kuna ufukara, hofu na ushirikina, lakini pia usahili, tumaini, mshikamano, imani kwa Mungu na uaminifu kwa mapokeo.

Kumbe hali za wanaozidi kumiminika mijini ni za kila aina, kuanzia utajiri mkubwa hadi unyonge mkubwa zaidi: huko kuna upweke, uchovu, kishawishi cha kutowajibika na urahisi wa mabadiliko.

 

 

4.3.            DALILI ZA NYAKATI

 

Tukifundishwa na Neno la Mungu kutambua katika malimwengu dalili za uwepo wa Mungu na za mpango wake, tukiri kwamba tumejaliwa kuishi katika hatua mpya ya historia: mabadiliko ya haraka zaidi na zaidi yanaathiri mtu binafsi na jamii, namna ya kuwaza na kutenda.

Hivyo tunahitaji kuliko zamani kukabili na kuchambua maelekeo mapya na matokeo yake, tukizingatia hakika tatu: utendaji wa Mungu anayeshirikisha wema wake, uwezo wa dhambi wa kumfunga na kumpoteza binadamu, nguvu za uzima mpya uliotokana na ufufuko wa Kristo.

Sayansi na teknolojia zinazidi kuathiri watu wote hata upande wa dini na maadili, pia kwa sababu wengi hawatambui mipaka yake na hatari zake, hivyo wanameza bila ya wasiwasi matunda yake pamoja na sumu yake.

Papohapo katika utandawazi utamaduni wa kigeni unatuvamia kwa nguvu na kuvuruga urithi wa tunu zetu pamoja na uwiano wa aina za watu; wengi wanafuata kasumba wakidhani zitawasaidia kukabili maisha.

Tuwaonyeshe namna ya kujipatia tunu halisi kutoka pande zote, pamoja na kuchuja yale yanayozuia ustawi wa mtu mzima (roho na mwili) na wa watu wote; tukifanya hivyo waweze kutambua kwamba hatuwaondolei yanayowafaa, bali tunawafaidisha.

 

 

4.4.            VIJANA

 

Hasa vijana ni changamoto kubwa kwa kuwa wanawahi zaidi kuathiriwa; mageuzi ya harakaharaka katika jamii, mivuto ya ulimwengu, maendeleo duni ya nchi zetu, utovu wa ajira unaowachelewesha wasichukue majukumu ya utu uzima: hayo yote yanachangia kuwafanya wawe na matazamio makubwa, na papohapo wakate tamaa na kujisikia wametupwa.

Utamaduni wa anasa unawadanganya watamani vitu wasivyoweza kujipatia kwa njia halali; hivyo wanashawishika kufuata njia mbovu wasijali matokeo yake.

Kutokana na vikwazo vingi, upande wa maadili giza ni nene zaidi: dhambi na neema hazieleweki, wala uzito wake.

Kwa jumla, misingi ya ukweli si imara kwao, hivyo wanashindwa kujielewa, kujieleza na kujiwekea malengo.

Kwa wengine maendeleo yao katika elimudunia hayalingani na yale ya ukomavu wao katika utu; wengi hawakupitia familia imara; wanajifunza kupitia picha lakini wanasoma kidogo mno mambo ya maana; hawana mtazamo wa kihistoria, ni kana kwamba ulimwengu unaanza leo tu.

Uenezi wa vikundi vya kidini unachochea maswali mengi kuhusu imani, na kuwafanya watamani kujua zaidi dini, lakini bila ya hakika tulivu ya imani inayohitajika.

Kwa kutotegemezwa kiroho na kiadili na familia na parokia, wengi wanasogea mbali na Kanisa, wakilitazama kibinadamu tu kama muundo, si kama fumbo la imani.

Basi, tujenge mapema msimamo wa dhati wa ushirika na Kanisa lote, hasa na askofu wa Roma, na wa usikilizaji na utekelezaji wa mafundisho yake, bila ya kuishia katika Biblia tu.

 

 

4.5.            VIJANA NA MIITO

 

Kutokana na hayo yote ni vigumu kuhudumia miito yao, kuwachambua na kuwalea.

Wajitambue au la, wengine wanakimbilia utawa ili kujiepusha na mabaya ya ulimwengu (ukimwi n.k.); wengine wanatafuta tu maisha, yaani maendeleo na hakika kwa kesho.

Hivyo inatubidi tunyoshe motisha zao na kuwaelekeza njia pekee ya ukomavu: kuaminika, kujikana, kujitoa kwa ukarimu na udumifu, kufurahi katika Bwana na hasa kupenda kama yeye.

Juhudi yoyote ya kuboresha jamii inawatumainia vijana, nao ndio tumaini la Kanisa pia: lenyewe lina mengi ya kuwaambia, nao wana mengi ya kuliambia.

Ingawa wanapatikana watu wazima wanaojisikia wito wa kitawa, walio wengi wana umri kati ya miaka 18 na 25.

Moyo wao unatamani udugu, urafiki, mshikamano, amani na haki; wanatarajia kuona ulimwengu bora zaidi, usio na ubaguzi, vita, njaa, ujinga, dhuluma.

Baadhi wanaishi Kikristo tayari na kuwajibika katika utume; wengi wao wanatafuta maana ya maisha: wanahisi sana mambo ya dini, lakini wanahitaji bado kutangaziwa Habari Njema.

Basi, tunapaswa kuwatolea ushuhuda wetu kwa ari na ubunifu, hata wakutane na Kristo kwa namna hai ambayo iwabadili kwa ndani wakaanze maisha mapya ya kujitoa, wakiwajibika kustawisha jamii na kuhubiri Injili.

Tutatue kwa busara tatizo la lugha (mitazamo, miguso, mitindo na misamiati) kati ya vijana na Kanisa, ili kuwatafsiria ujumbe wa Yesu na wa Kanisa uweze kujitokeza kwa namna mpya katika utamaduni wao bila ya upotovu.

Katika kufanya kazi hiyo tusiogope kutumia pia misamiati maalumu ya mapokeo ya imani, mradi tuifafanue na kuonyesha umuhimu wake kimaisha, kwamba ni habari iliyo njema kwao na kwa jamii nzima.

 

 

4.6.            HABARI NJEMA KWA VIJANA

 

Kiini cha Injili kwa vijana kiwe wito wa Yesu kwa kijana tajiri, ambao upendekezwe kwa wanaotaka kujiunga nasi na kwa vijana wote, kama alivyofanya Yohane Paulo II katika barua aliyowaandikia tarehe 31-3-1985.

Katika ukurasa huo kijana anamuelekea Yesu, naye anamfunulia utajiri wake wa pekee na kumualika awajibike kuutumia kwa faida ya wote, hasa walio maskini, akiwa na hakika ya kuwa ndiyo njia ya kutajirika kweli kwa kuishi kama yeye.

Kila mmoja atambue mapema kwamba namna za kumfuata Yesu ni nyingi, kwa kuwa Roho wake anavuma anakotaka: maisha ya Kikristo na ya Kifransisko yana matawi ya kila aina ambayo katika majira yoyote ya historia ya Kanisa yanafyonza rutuba ya Injili na kuzaa sana.

Katika ushirika wa Kanisa na wa chama chetu, hali za maisha ni mbalimbali lakini zinafungamana na kukamilishana, kwa kuwa wito wa msingi ni sawa kwa wote, yaani kwamba tuishi kitakatifu kadiri ya hadhi yetu kama wana wa Mungu.

Utume wa miito lengo lake si kudumisha chama, bali kuhudumia karama hizo mbalimbali ili mpango wa Mungu juu ya kila mmoja utekelezwe.

Ndani ya Kanisa sisi pia tuwajibike kuchochea, kupokea, kusindikiza na kulea wanaojisikia wito, tukitegemea hasa sala na ushuhuda wa maisha bora ya mtu binafsi na ya jumuia.

 

 

4.7.            NYUMBA YA MAPOKEZI

 

Ingawa chama chote kinapaswa kufanya kazi hiyo, tuwe na nyumba maalumu ambapo, kwa msaada wa ndugu kadhaa na kwa njia za kufaa, wenye wito waimarike katika imani, wajifunze kusali, kuishi kijumuia na kulihudumia Kanisa, waweze kutambua namna wanavyoitwa kumfuata Kristo.

Waishi hapo hadi mwaka mmoja wakiwajibika katika sala na kazi na kufundishwa yafuatayo: Wito, Agano la Kale, Agano Jipya, Katekisimu Ndogo, Maisha ya Mtakatifu Fransisko.

Ili mgeni alifikie lengo hilo tumsaidie:

- ajifahamu na kujipokea alivyo, pamoja na vipawa na kasoro zake;

- achanganyikiwe na Yesu ili ajiunge naye katika kutimiza matakwa ya Baba kwa nguvu ya Roho Mtakatifu;

- atambue wajibu wake kama mbatizwa, yaani mtoto wa Mungu na wa Kanisa;

- atamani kuitikia mlio wa fukara;

- apange Kikristo tunu ambazo ziongoze maisha yake;

- apambanue kilichomleta kwetu;

- aelewe maisha yetu ili kutambua kama ndiyo yanayomfaa.

 

 

4.8.     WATU WAZIMA

 

Malezi ya watu wazima yanawalenga binadamu ambao maishani wana majukumu mbalimbali na kupatwa na majaribu makubwa.

Hivyo imani yao inahitaji mfululizo kuangazwa, kukomazwa na kulindwa ili hekima ya Kikristo iunganishe na kukamilisha mang'amuzi yao yote.

Kwa ajili hiyo, katika kulea wasekulari walei:

- tuyazingatie hayo pamoja na msingi walionao kiroho na kielimu, hali yao ulimwenguni na wito wao wa kulenga ufalme wa Mungu katika kuratibu malimwengu;

- tuimarishe misingi ya imani yao kwa mchango wa akili pia;

- tuwaingize katika kusoma Maandiko katika sala;

- tustawishe maisha yao katika Kristo mfufuka kwa njia ya liturujia, mafungo na uongozi wa kiroho;

- tuwaonyeshe uhusiano kati ya wajibu katika jamii na wajibu katika Kanisa;

- tuangaze maswala ya kisasa kuhusu dini na maadili;

- tuwasaidie kupima mageuzi ya jamii.

 

 

4.9.     INJILI, UTAWA NA UTAMADUNI

 

Yesu Kristo na Injili yake wanapita utamaduni wowote na kuweza kuuboresha mpaka ndani kwa nguvu ya Roho Mtakatifu; upande wake kila utamaduni unahitaji kupenywa na Habari Njema ili uponywe madonda yaliyotokana na dhambi, na ili tunu zake zikamilishwe na hekima ya msalaba.

Utawa pia unahusiana na utamaduni, kwa maana utamaduni unalenga kumwezesha mtu apokee na kutawala hali na maisha yake awe bora zaidi; upande wake tamko la kushika mashauri ya Kiinjili, ingawa linamdai mwamini ajinyime tunu za maana, linachangia sana maendeleo halisi: historia inathibitisha kuwa wengi walikuta utawani nafasi bora ya kujielewa na kukomaa kwa dhati.

Kwa hiyo:

- tuzingatie utamaduni na ujuzi wa mlelewa, ambao hauishii katika elimu inayotolewa shuleni;

- tumsaidie kutamadunisha imani yake ili ipenye maisha yake yote;

- tuandae wanaokwenda kuishi nje ya mazingira ya utamaduni wao wajue na kuheshimu ule wa kigeni;

- tustawishe maisha ya kitawa yaliyotamadunishwa;

- tutathmini maisha yetu kwa kuzingatia tunavyotunza na kuoanisha uaminifu kwa Yesu na Injili yake, kwa Kanisa na umisionari wake, kwa utawa na karama yetu maalumu, kwa binadamu na mahitaji ya nyakati hizi, bila ya kuzidisha upande mmoja na kupungukiwa upande mwingine.

 

 

4.10.            MBINU

 

Malezi ya kisasa yanataka mlelewa awe mtendaji sana, pamoja na kuwa wazi na kushirikiana vizuri na wenzake: mtindo wa kujifunza kwa njia ya kutenda unalingana na mawasiliano halisi kati ya watu.

Hata Mungu katika mpango wake wa kujifunua na kutuokoa anatuita wote tuitikie zawadi yake kwa upokeaji wa sakramenti, liturujia na sala, uwajibikaji katika Kanisa na jamii, matendo ya upendo na ustawishaji wa tunu za kibinadamu (k.mf. uhuru, haki, amani na hifadhi ya mazingira).

Basi, malezi yetu katika kulenga itikio la hiari la mtu na kudai mchango wa utendaji wake, yafungamanishe ujumbe na mbinu za kuutoa: mbinu zinahitajika ili ujumbe upokewe, nazo zinapaswa kulingana na ujumbe wenyewe, na mazingira halisi na hali ya mhusika.

Tangu mwanzo wa malezi tufute udanganyifu wa mtu kuwadai kila kitu wenzake; tumsaidie kuvumbua kwa shukrani yale yote ambayo amekwishasaidiwa na anaendelea kusaidiwa; tumuandae kuwa mjenzi wa jumuia, si mtumiaji tu, yaani awajibike kwa ustawi wa wenzake, awe tayari kupokea na kutoa msaada, mwepesi kushika nafasi ya mwingine na kumuachia nafasi yake mwenyewe.

Vipimo vya ustawi wa utu ni ukomavu katika mawasiliano na mafungamano, uwezo wa kujitolea, msimamo wa tabia, busara katika uamuzi, uwezo wa kujitawala, utaratibu na upendo katika kusema, utulivu wa nafsi, huruma kwa wenye shida, ulinganifu wa maneno na matendo.

Tustawishe yale maadili ambayo yanadaiwa na mafungamano yoyote na kuheshimiwa na watu wowote: adabu njema, uungwana, haki, uaminifu, nidhamu, mshikamano, usemakweli, unyofu, upole na ukunjufu, pamoja na kupima vema watu na matukio, kubuni na kuanzisha mambo ya kufaa.

Tuzoee kuwa na upana wa akili na wa moyo, kujali fumbo la kila mtu na kumheshimu hasa akiwa mzee au mgonjwa, kwa kuona kila mmoja ni wa pekee kwa Mungu na kwetu.

Kujadiliana ni jambo gumu lakini la lazima kati yetu wenyewe, tena kati yetu na wowote; hivyo katika hatua za kuingizwa kila mmoja ajifunze kufanikisha majadiliano, kwa kutambua anavyopaswa kuwa macho kuhusu namna yake ya kukabili maswala, kwa sababu anaathiriwa na mambo mbalimbali ya leo na hasa ya zamani, ya nje na hasa ya ndani mwake.

 

 

4.11.   AFYA YA NAFSI

 

Safari ya kuelekea ukomavu haina mwisho kwa kuwa inadai kutajirika mfululizo sio tu kinafsi, kielimu na kijamii, bali hasa Kiroho; hivyo inaendana na ile ya kuishi Kikristo kweli.

Roho ndiye kipaumbele cha kudumu katika malezi, kwa kuwa lengo hasa ni kuzidi kumzamisha mtu ndani ya Utatu, ulio dira ya maisha yetu.

Mtakatifu Fransisko, kielelezo cha afya ya nafsi, alikuwa tajiri wa miguso na vionjo, tena mwenye uwezo wa kuvitokeza; mwenye adabu na ustaarabu sana; mwenye kuvutiwa na yaliyo mema na mazuri.

Kuwa na upendo wa Kimungu na wa kibinadamu kwa pamoja ni sifa maalumu ya moyo uliofanywa mpya; upendo huo ulio tayari kusaidia kwa heshima na kujitoa bure unakusudiwa kuonjesha ule wa Bwana uliodhihirika hivi msalabani hata tusiweze kutia shakani kwamba tunapendwa na yule aliye upendo.

Ingawa siku hizi ni vigumu kuliko zamani kulinganisha yote ili kumpata mtu aliyekomaa pande zote katika umoja wa dhati, tulenge hali hiyo kwa kushirikisha tunu za Injili kuliko wingi wa habari mchanganyiko.

 

 

4.12.            UKOMAVU

 

Mtazamo wa imani unatakiwa kuhuisha na kukamilisha malezi yote, lakini malezi ya Kiroho yanapotea bure yasipoendana na ustawi wa nafsi ambao ndugu waweze kujipatia tunu za kitawa (hasa usafi kamili) mpaka ndani, wakivuka toka tabia ya kujipendea na kujinufaisha kwa ubinafsi hadi ile ya kupenda na kujitoa kwa wengine.

Matatizo yakija kujitokeza upande huo, mara nyingi yametokana na athari za mambo yaliyotokea kwingine, ambazo hazijarekebishwa.

Kwa kuwa utawa unategemea na kutimiliza ubatizo, wanaoshindwa kutekeleza kwa kiasi kikubwa masharti ya ubatizo kulingana na umri wao, hawawezi kujitwisha mzigo mkubwa zaidi usije ukawalemea kabisa.

Kwa msingi huo wazuiwe wasianze zoezi wale ambao wanashindwa kutawala tamaa ili kutekeleza jinsia yao kwa namna isiyotegemea mwili, au wanataka kushika njia isiyoelekea ndoa wala usafi kamili.

Kama vile ukomavu fulani unavyohitajika ili kuishi kijumuia, upendo wa kidugu unahitajika ili ndugu akomae hata akapenda wito wake na viumbe kadiri ya wito wake, bila ya kuvamia wala kutawala wengine: ndio uhuru wa dhati unaomwezesha kutekeleza vema haja ya kupendana ndani na nje ya jumuia.

Hiyo iwe mahali pa kukomaa kimiguso, ambapo mazingira ya utulivu, uwazi, utayari wa kupokeana yanamwezesha ndugu kustawisha vionjo vyake, kushirikisha shida zake, kuwa na urafiki halisi, kufanya kazi kwa mshikamano na kujilinganisha na watu na hali tofauti.

Pamoja na hayo, tusikose kumpatia kila ndugu ujuzi wa nafsi na mazingira yake ili aishi kwa ukomavu mkubwa zaidi.

Walau ajue motisha za ndani za binadamu; muundo wa nafsi yake; haja kuu na matarajio ya moyoni; maendeleo ya nafsi na hatua za maisha; mang'amuzi yanayoweka wazi kulipokea fumbo la Mungu; hali ya kidini, ya kijamii, ya kiutamaduni na ya kiuchumi zinazomuathiri kimaisha.

 

 

4.13.            JINSIA

 

Mwenyezi Mungu hakuumba watu wa aina moja tu: alipomuumba mtu kama kiumbe mwenye akili na utashi anayeweza kumjua na kumpenda, hakutaka awe peke yake, bali aambatane na mwingine wa jinsia tofauti.

Mafungamano mengi ya wanaume na wanawake na maelekeo ya ulimwengu leo yanadai malezi imara upande wa jinsia, kwa namna ya pekee katika chama chetu chenye watu mchanganyiko.

Kwa kawaida wavulana na wasichana wa siku hizi wanalelewa kwa pamoja bila ya kusaidiwa watambue tunu zao na mipaka yao kijinsia.

Kuchanganyikana mapema si hakika ya kukomaa katika mafungamano ya jinsia mbalimbali, bali ni lazima tulenge ukomavu huo na kuchukua hatua ili usafi wa moyo na pengine useja mtakatifu viweze kutekelezwa kweli.

Wanaume na wanawake wanahitaji kuelewa hali yao tofauti katika mpango wa Muumba na mchango maalumu wanaokusudiwa kuutoa katika kazi ya uumbaji na ya wokovu kadiri ya jinsia yao.

Kwa hiyo tuwaonyeshe ukweli wa kutofautiana na kukamilishana kwao, sio tu upande wa mwili katika ndoa na wa jamii katika kazi za kufanya, bali kimsingi zaidi upande wa nafsi.

 

 

4.14.            WANAWAKE

 

Kwa namna ya pekee Bikira Maria anaangazia ukweli wa mwanamke yeyote aweze kutekeleza ipasavyo jinsia yake na kujikomboa kweli.

Kwa njia yake Kanisa linavumbua katika sura ya wanawake uzuri wa miguso bora ya binadamu: uwezo wa kuhisi shida ya mtu na kumfariji, ukamilifu wa kujitoa kwa upendo, uaminifu mkubwa katika wajibu, utendaji usiokubali kuchoka na nguvu ya kuvumilia lolote.

Kwa mfano wa Maria wanawake wanaitwa kuwa ishara ya hisani ya Mungu kwa kila mtu, na ya sura ya kimama ya Kanisa, ambalo linawategemea sana katika utamaduni na maisha ya kiroho, katekesi, teolojia na maadili, maisha ya kifamilia na ya kijamii, na hasa hadhi yao na utetezi wa uhai.

Wasishindwe na kishawishi cha kuwaiga wanaume, bali katika sekta zote watokeze uwezo asilia waliojaliwa na namna yao maalumu ya kuwaza na kutenda.

Kwa kujijali na kushika nafasi zao bila ya woga wala unyonge, watawasaidia wanaume kuangalia upya namna wanavyojielewa, wanavyotazama mambo na wanavyopanga maisha ya kijamii, ya kisiasa, ya kiuchumi na ya kidini.

Hivyo malezi bora, pamoja na kuwasaidia wanawake kuelewa vipawa vyao, yatachochea ushirikiano unaohitajiwa na jinsia zote mbili.

 

 

 

 

5. HATUA ZA KUINGIZWA

 

5.1.            KUINGIZWA UTAWANI HATUA KWA HATUA

 

Neno "kuingizwa" lina maana ya kusaidiwa kuachana hatua kwa hatua na mtindo fulani wa maisha ili kuingia mtindo mwingine ulio maalumu wa kundi fulani.

Hatua za kuingizwa katika maisha yetu ya Kifransisko zinategemea zile za kuingizwa katika Ukristo, na zinafanana nazo.

Baada ya muda wa mapokezi, ambao ni wa kujisikia kuvutiwa na maisha yetu, ziko hatua tatu, yaani:

- utakaji, ulio hatua ya kuyatafiti na kuyachagua;

- zoezi, lililo hatua ya kukoleza karama ya Kiinjili ya Kifransisko;

- uchipukizi, ulio hatua ya kuimarika kimaisha.

Tuhakikishe hatua hizo zilete maendeleo yaliyotazamiwa kadiri ya lengo maalumu la kila moja na kwa kusonga mbele daima kuelekea ukomavu.

Malengo ya hatua hizo ni vituo vya kufikia na kuondokea kwa wakati mmoja; kwa kifupi ni kuvumbua, halafu kujaribu, hatimaye kuchimba maisha matakatifu ya udugu na udogo.

Ndugu asipige hatua ya mbele kabla hajafikia lengo la awali.

Kwa hiyo, kwa kiasi fulani, urefu wa hatua hizo ulinganishwe na mwendo wa kila ndugu, ambao ni wa pekee kutokana na tofauti za neema za Mungu, itikio la hiari yake, mchango wa jumuia, umri n.k.

Katika safari hiyo ndugu wasaidiwe na ibada maalumu ambazo ziwatakase na kuwategemeza, ziwapatie baraka za Mungu katika kupiga hatua fulani n.k.

Kulingana na mafundisho wanayopata wakabidhiwe Injili, Kanuni ya Imani, Sala ya Bwana na kanuni ya utawa wetu.

 

 

5.2.     HAJA YA UJUZI

 

Katika hatua zote za maisha tunahitaji kujiongezea ujuzi, kila mmoja kadiri ya uwezo na mahitaji yake, ili tuzidi kutambua na kuitikia wito tuliojaliwa na Mungu ndani ya Kanisa.

Ustawi wa Kiroho na wa kitume unatudai daima tukabili masomo yanayotuhusu ili yatusaidie kumjua Yesu, kushika misimamo ya Kanisa, kutekeleza tunu za karama yetu, kukomaa kwa ndani, kushirikisha ujumbe wa wokovu, kuumua utamaduni kwa chachu ya Injili na kuchangia maendeleo kamili ya jamii.

Hasa katika hatua za kuingizwa chama kiwajibike kushirikisha kwa mpango ujuzi unaohitajika, ingawa malezi hayaishii hapo bali ni kumkuza mtu mzima.

Uzingatiwe umoja wa ndani wa mafundisho yote ili ndugu watambue ni elimu ileile ya Injili.

Wahusika wawajibike kuhudhuria kwa kawaida na kwa bidii vipindi walivyopangiwa: wakikosa kuhudhuria thuluthi moja ya vipindi vya kozi fulani, itawabidi kuirudia.

Kwa muda uliopangwa waonyeshe maendeleo yao kwa njia ya majadiliano, maandishi na mitihani.

Watakaoonekana hawajajua vya kutosha (60%) itawabidi warudie mtihani, na wakifeli tena wairudie kozi husika.

 

 

5.3.            UTAKAJI

 

Baada ya mapokezi, wanaoomba kuanza rasmi malezi ya kitawa wanaweza kupokewa katika utakaji.

Ikiwezekana nyumba yao isiwe ile ya zoezi, bali nyingine ambayo ijitegemee hata upande wa mafundisho yanayokazaniwa wakati huo.

Katika utakaji zitolewe kozi zifuatazo, isipokuwa kama mmojawapo hahitaji baadhi yake kwa kuwa ana ujuzi huo tayari au ametangulia kupata kozi nyingine za hatua za mbele: Marko, Tunasadiki, Mungu Baba, Liturujia-msingi, Sakramenti za Kwanza, Misa, Sakramenti za Uponyaji, Maadili-msingi, Amri za Mungu, Sala-msingi, Elimunafsia-Jinsia, Maisha ya Kijumuia.

Mtakaji na chama wanatakiwa kuhusiana sana ili yeye aweze kutambua na kuchagua maisha, nasi tuweze kumfahamu vizuri na kumfikiria kuhusu wito.

Lengo hilo linahitaji mbinu na muda: hivyo tusiogope kuurefusha hadi miaka mitatu, ingawa bila ya kuuzidisha bure, wala kuchelewa kuwaelekeza kwingine wale wasiofaa kwa maisha yetu.

Kazi za mtakaji ni hasa:

- kupunguza uhusiano na ulimwengu;

- kuishi kijumuia kweli;

- kukomaa upande wa hisi na vionjo;

- kujitambua kiutu na Kiroho;

- kuelewa maana na aina za miito;

- kuzoea Biblia, liturujia na sala;

- kujiongezea ujuzi wa imani na maadili.

 

 

5.4.            KABLA YA ZOEZI

 

Matatizo mengi katika malezi mashirikani yanatokana na vijana kuingia unovisi pasipo ukomavu wa kutosha.

Si kwamba wadaiwe kuwa wakamilifu toka mwanzo, bali kwamba waweze kutimiza masharti ya utawa wakimaliza unovisi.

Ili wito wao ueleweke na uwezo huo upimwe, kabla hawajaanza wasaidiwe kuziba mapengo yaliyoachwa na malezi yao ya awali.

Mtumishi anapoingiza zoezini afuate kwa makini katiba yetu akizingatia:

- ukomavu wa kiutu na wa Kikristo unaohitajika ili zoezi lisilazimishwe kurudia misingi tu;

- msimamo wa miguso, hasa upande wa jinsia;

- uwezo wa kuishi kijumuia chini ya viongozi;

- ujuzi wa lugha inayotumika katika zoezi;

- elimu inayodaiwa na serikali kwa wananchi wote.

 

 

5.5.            UNGAMO LA IMANI

 

Tokeo muhimu la urithi hai wa Mitume ni Kanuni ya Imani: hasa katika nafasi ngumu za historia yake, Kanisa likiongozwa na Roho Mtakatifu lilijumlisha vema imani yake likaikabidhi rasmi kwa waamini wapya kabla ya Sala ya Bwana.

Siku hizi ibada hizo zimerudishwa kwa wakatekumeni na kuhimizwa kwa nafasi nyingine ili mwanafunzi wa Yesu apokee kwa ujuzi na ari mafumbo anayopaswa kuyazingatia.

Watakaji wetu, muda mrefu baada ya kukabidhiwa imani hiyo waiungame mbele ya mtumishi na jumuia kabla hawajaanza zoezi.

 

 

5.6.     ZOEZI

 

Lengo la zoezi ni kuingizwa katika mtindo wa maisha wa Mwana wa Mungu, kwa kuzingatia hasa ufukara na unyenyekevu wa Injili yake takatifu.

Wanazoezi wakijaribu kuishi hivyo, jamaa inapima nia na uwezo wao wa kudumu siku za mbele.

Masomo na kazi visivyolenga moja kwa moja malezi hayo haviruhusiwi.

Wanazoezi waongozwe kupata mang'amuzi ya Kiroho ya dhati zaidi kwa:

- kuwajua kwa namna hai Yesu na Baba;

- kustawisha maadili ya kibinadamu na ya Kimungu;

- kuongeza kasi katika kuelekea ukamilifu;

- kutunza kimya, kukazania sala na kujikana;

- kuzama katika mafumbo ya imani;

- kusoma na kutafakari Neno la Mungu na kuona namna ya kuliitikia kwa nguvu zote;

- kumuabudu vema katika liturujia kwa mtindo wa Kifransisko na wa Kiafrika;

- kupenda Kanisa na wachungaji wake;

- kujifunza kutimiza masharti ya maisha yetu, hasa mashauri ya Kiinjili;

- kujua sifa na karama, lengo na sheria, historia na maisha ya familia ya Kifransisko na ya chama chetu.

Katika zoezi zitolewe kozi zifuatazo: Mathayo, Luka, Yesu Kristo, Roho Mtakatifu, Sakramenti za Ushirika, Baba Yetu, Maisha ya Sala, Maisha ya Kiroho - I, Historia ya Wafransisko, Kanuni, Katiba, Mashauri ya Kiinjili, Kujifahamu.

Baadhi yake zinaweza kutangulizwa au kuairishwa katika hatua nyingine za malezi ya awali, isipokuwa kozi za mwisho.

 

 

5.7.            MAZINGIRA YA ZOEZI

 

Ili wanazoezi watie mizizi katika maisha yaliyofichika pamoja na Kristo ndani ya Mungu na waunde akili na moyo kadiri ya karama yetu haifai nyumba iliyozama kati ya watu, bali mazingira na hali vinavyosaidia kuvutiwa na sala.

Isipowezekana kwa mwaka wa kwanza na kwa ule wa mwisho, walau wa pili utumike katika mazingira ya namna hiyo na kwa kuzingatia utulivu wa kukaa na Mungu kuliko utendaji na uhusiano na watu.

Kinyume chake, miaka ya kwanza na mwisho ikitumika jangwani zaidi, mwaka wa pili unaweza ukatumika kumpa mwanazoezi nafasi ya:

- kustawisha uwajibikaji wake katika maisha ya kidugu;

- kung'amua utume wetu maalumu;

- kujifunza kudumisha muungano wake na Mungu katika kazi yoyote, kama tunu mojawapo ya msingi.

Zoezi lote lifanyike katika nchi asili ya mwanazoezi au nyingine inayofanana nayo, tusije tukazidisha ugumu wa hatua hiyo ambapo:

- anapaswa kujipatia msimamo wa ndani;

- mafungamano kati yake na mlezi yanatakiwa kuwa rahisi;

- tunahitaji kuchambua miito midanganyifu inayosukumwa na motisha isiyo ya Kiroho, kama vile kusafiri na kuona mazingira mapya.

 

 

5.8.            UBORA WA KUJITOA MOJA KWA MOJA

 

Mtu yeyote anaweza kupimwa kwa kuzingatia anafungamana na nani na nini.

Hiari yake inaweza kufikia ukomavu mkuu kwa kujifunga kiarusi kupendana na Kristo.

Upendo wake unaweza ukatushika hata tujisikie haja ya kumtolea moyo na maisha yetu yote.

Mwenyewe akitualika tufanye hivyo, haifai kujitoa kwake kwa muda au kwa jaribio.

Kwa kutegemea uaminifu wake na karama ya Roho Mtakatifu tunaweza kujitoa kabisa kwake, halafu kuzidi kujitoa siku kwa siku kwa uhuru na furaha: wakati wa zoezi uonyeshwe uwezekano na ubora wa kujitoa moja kwa moja.

Maana ya kiarusi ya maisha ya wakfu ina umuhimu wa pekee kwa kulikumbusha Kanisa wajibu wa kuwa aminifu kabisa kwa Bwanaarusi wake, ambaye toka kwake linapokea mema yote.

Hasa wanawake wanakuta humo ukweli wa jinsia yao na namna yao maalumu ya kuhusiana na Bwana.

Kielelezo kikuu ni Mama Maria aliyejaliwa kwamba upendo wake wa kibikira umzae Mungu duniani na kuchangia hata leo uzima wa Kimungu upatikane na kustawi ndani ya watu.

Katika hatua zote za kuingizwa tustawishe upendo na ibada kwake, ambaye kila ndugu na jumuia ya malezi wajiaminishe kwake.

 

 

5.9.            KUWEKA AHADI

 

Ahadi ya daima inadai mang'amuzi na maandalizi marefu yanayohakikisha iwezekanavyo udumifu.

Ndiyo sababu Kanisa linaweza likadai utangulie muda wa kuthibitisha uaminifu wa mtawa hata katika nafasi ngumu.

Maadhimisho ya ahadi yawe tofauti sana: ahadi ya muda isiwe na fahari yoyote; kumbe ahadi ya daima ifanyike kwa kuwaalika askofu wa jimbo na waamini wengine, kwa kuwa ni tendo la kuwekwa wakfu na ni ishara ya muungano wa moja kwa moja kati ya Kristo na Kanisa.

Kwa njia ya wenye mamlaka ndani ya chama, lenyewe linazipokea ahadi zetu za daima na za muda vilevile na kuziunganisha na sadaka ya Bwana.

Tufuate kwa makini taratibu zote za katiba kuhusu kuweka ahadi.

 

 

5.10.            KIPINDI CHA MATAKASO

 

Miezi mitatu kabla ya ahadi ya kwanza, anayetaka kuiweka aandike ombi kwa halmashauri ya jamaa.

Nia yake hiyo na kibali cha chama vitangazwe rasmi katika ibada ya kuandikisha jina la kitawa.

Ndiyo mwanzo wa kipindi cha matakaso, ambacho ni kilele cha zoezi na ambacho kiini chake ni ibada tatu zinazohusiana na mashauri matatu ya Kiinjili, yaliyo nguzo za utawa na ambayo yanakazaniwa wakati huo.

Urafiki wa ndani na Yesu ndio neema ambayo inatuwezesha, na kwa namna fulani inatutaka tuwe kitu kimoja naye kimawazo na kimaisha na kuona mengine ni hasara tupu, hata tukaahidi kushika mashauri aliyotuachia kwa mifano na mafundisho yake.

Mashauri hayo ya Kiinjili si kujinyima tu, bali ni kuliishi fumbo la Kristo ndani ya Kanisa kwa ukamilifu ule unaowezekana duniani na kulingana na karama fulani.

Mapokeo ya Mitume yameungama daima ubora wa maisha ya useja, ufukara na utiifu, kwa kuwa ndiyo maisha ya Mwana wa Mungu kama binadamu, yanayotokeza upendo wa Mwana kwa Baba katika umoja wa Roho Mtakatifu, kwa hiyo ni namna ya Kimungu ya kuishi duniani.

Ndiyo changamoto na wajibu mkuu wa maisha ya kitawa: kadiri yanavyolingana na yale ya Yesu, mwenyewe anakuwepo na kuokoa ulimwengu.

Utume wa watawa unatokana na wito huo wa kuungana naye: ni hasa kumfanya awepo ulimwenguni kwa ushuhuda wa maisha yaleyale ya kwake.

Tuwaingize kwa makini wanazoezi katika maana na masharti ya mashauri hayo, upande wa nadharia na wa utekelezaji.

Imani, tumaini na upendo vinatusukuma tuweke ahadi ya kuyashika ili kukwepa vinavyoweza vikazuia ari ya ukamilifu katika kumtumikia Mungu ndani ya Kanisa.

Kila shauri linarekebisha nafsi yetu katika jambo mojawapo la msingi, yaani mapenzi, mali na hiari, hivyo linaweza kutatua tatizo kuu mojawapo linaloutawala na kuuharibu ulimwengu, yaani tamaa za mwili, tamaa za macho na kiburi cha maisha.

Kutimiza vema mashauri hayo kunamkomaza mtu, kunampa uhuru wa Kiroho, kunamtakasa moyo, kunamwasha upendo na kumsaidia kujenga dunia bora.

 

 

5.11.            UCHIPUKIZI

 

Baada ya kuweka ahadi, malezi yanaendelea kuhitajika ili watawa chipukizi, wanapozidi kuingizwa katika maisha yetu yote, wazoee kuoanisha kimaisha juhudi za Kiroho (ambazo zidumu kushika nafasi ya kwanza), za kitume na za kielimu katika jumuia.

Ni hatua mpya inayokusudiwa kufaidika na msukumo na msimamo wa tamko la ahadi; yaani mtawa chipukizi anatakiwa kuchuma matunda ya hatua zilizotangulia na kuendelea kukua kiutu na Kikristo akitekeleza kiaminifu ahadi yake, na kuelekea pengine ile ya daima.

Katika hatua hiyo anahitaji kudumisha juhudi za Kiroho za zoezi hasa kwa sababu ongezeko la kazi na la mafungamano na watu wa nje linasababisha kwa urahisi hali ya ukavu na ya kuyumbayumba.

Hivyo lengo kuu ni kumwezesha afuate wito kwa umoja wa ndani na kukabili vema mvutano kati ya sala na shughuli zinazozidi kumpasa, au kati ya maisha ya kijumuia na utume unaodaiwa na maendeleo yake wakati huo.

Pia aelewe karama yetu zaidi, atimize masharti ya ustawi wake, akubali maisha yetu jinsi yalivyo, aheshimu wengine katika tofauti zao na kuwajibika katika jumuia.

Asikabidhiwe kazi zinazoweza zikayazuia malengo hayo, ila apate mang'amuzi ya Kikanisa na ya kijamii kulingana na karama ya chama na kwa kujitambua daima kuwa si mtendakazi tu, bali ni hasa shahidi hai wa maisha ya Yesu, hivyo utendaji wake unahitaji kufanyiwa utambuzi na kuwekewa masharti.

 

 

5.12.            MALEZI YA UCHIPUKIZI

 

Ni wajibu mzito wa chama kumpatia hali inayomwezesha kukua katika kujitoa kwa Bwana.

Kwanza kimpatie mlezi wa kufaa na jumuia ya nguvu, yaani yenye uongozi imara na ndugu wengiwengi, hata wa mataifa mbalimbali, wanaochanga utajiri wa tunu zao mbalimbali.

Kwa kuwa hatua hiyo, tofauti na zoezi, inahitaji jumuia kubwakubwa, yenye vitabu bora vingivingi pamoja na uwezekano wa kuhudhuria kozi za dini na za elimudunia, ingawa hata kozi kwa njia ya posta zinaweza zikafikiriwa.

Lakini mafunzo mazito ya nadharia na ya ufundi ni vigumu kuyapatanisha na madai ya uchipukizi: kwa hiyo mwaka wa kwanza baada ya ahadi ndugu asifuate mafunzo yasiyo ya dini, isipokuwa pengine ya lugha ya Kiingereza.

Halafu yapangwe si kwa kumridhisha kibinadamu kadiri ya malengo yake binafsi, bali kwa ajili ya utume wa chama kulingana na karama yetu na mahitaji ya Kanisa na ya jamii.

Tena yalinganishwe na malezi yote ya hatua hiyo, ambayo yawe na malengo yaleyale kwa wote, hata wasipokaa nyumba moja miaka yote mitatu.

Ni jukumu la mtumishi pamoja na mlezi kulinganisha mpango wa jumla na mahitaji ya watawa, nyakati na mahali.

Kwa vyovyote, ndugu akiishi nje ya jumuia ya uchipukizi, arudi humo walau miezi miwili kwa mwaka kwa kuhudhuria kozi zifuatazo (zisipotarajiwa baadaye katika malezi ya daraja takatifu): Zaburi, Yohane, Historia ya Kanisa, Mababu, Matapo ya Kiroho, Mtaguso, Sheria za Kanisa, Kanisa Barani Afrika, Maisha ya Kiroho - II, Fransisko-maadili, Sheria Ndogondogo, Ushauri, Elimu ya Malezi, Utamaduni, Elimujamii, Mawasiliano, Katekesi, Uchungaji, Ekumeni, Umisionari, Uislamu, Tunu za Afrika, Sayansi, Falsafa, Teolojia-msingi, Teolojia ya Historia.

Watawa chipukizi (na vilevile wanaosomea daraja au fani maalumu) wapaswe kumtii mlinzi, lakini wawe chini ya mlezi wao, hivi kwamba mlinzi asiamue lolote juu yao asipokubaliana na mlezi.

 

 

 

 

6. MALEZI YA KUDUMU

 

6.1.     HAJA YAKE

 

Ufafanuzi ufuatao unahitajika ili kila mmojawetu awe na mpango tayari kwa maisha yake yote, kusudi azidi kukua kama mtu na kama mfuasi, bila ya kujitenga na wenzake wala kujiamini mno: hakuna wakati wa kujisikia tumekamilika.

Hasa aliyemaliza muda wa uchipukizi hawezi kujidai yuko imara kwa maisha yake yote, yawe yaweje; ila anakusudiwa kuwa amejipatia ari na mbinu za kujirekebisha na kujiendeleza sikuzote katika namna ya kuishi, kufikiri na kutenda ili akabili vema zaidi na zaidi hali zozote, za zamani na mpya, za ndani na za nje.

Awe amejifunza jinsi ya kujifunza, kwa kumuendea Mungu upwekeni, kujisomea hasa Neno lake na hati za Kanisa, kuchunguza ishara za nyakati na kutambua itikio la kufaa, kuchimba karama yetu, kufaidika na maneno na mang'amuzi ya wengine asidhuriwe nayo, kuhudhuria semina, mikutano n.k.

Ndugu mwenyewe ndiye wa kwanza kupaswa na malezi yake ya kudumu, kulingana na maongozi ya Mungu, mahitaji ya Kanisa na ya ulimwengu.

Pamoja na kuwa mtendaji wa malezi katika hatua zote za maisha yake, ndiye mlengwa pia katika utu wake wote unaoitwa kuwapenda kabisa Mungu na jirani.

Upendo huo ndio unaoweza kuchochea daima uaminifu na ustawi.

 

 

6.2.            MPANGO WAKE KATIKA MTIRIRIKO WA MAISHA

 

Malezi ya kudumu yanaanza miaka mitatu baada ya kumaliza zoezi na yanachukua miaka ya ukomavu wa mtu, halafu ile inayolazimisha kupunguza kazi na kujiandaa kukutana na Bwana moja kwa moja.

Miaka ya kwanza ya kufanya utume muda mwingi kila siku pasipo usimamizi ni hatua ngumu inayotutaka tuwajibike kikamilifu kwa msaada wa ndugu zetu kutekeleza ari ya upendo.

Hatua inayofuata inaweza ikaleta hatari ya kuzoea hata kukinai maisha na kazi, pamoja na kishawishi cha kukata tamaa kwa kuona matunda machache ya Kiroho na ya kitume: hapo tunahitaji tena msaada tujitoe tu, bila ya kujali matokeo yanayoonekana bali kwa kuzingatia upya yale ambayo peke yake ni ya lazima.

Umri wa makamo unaweza ukaleta hatari mbalimbali: kupatwa na ubinafsi au hofu ya kupitwa na wakati, kushikilia namna fulani tu, kujifanya lengo la yote na kupotewa na juhudi; hapo tunahitaji kuinua maisha ya Kiroho na ya kitume ili kuzaa sana kwa kujitoa kwa Mungu kwa ukweli na ukarimu mkubwa zaidi, na kujitoa kwa watu kwa utulivu, usahili na hekima kubwa zaidi.

Uzee unaweza ukaleta matatizo mapya ambayo tuyakabili Kiroho mapema, tukijiandaa kupokea changamoto za umri huo: kupunguza polepole utendaji wetu ni namna mpya ya kuishi inayoweza kutufanya tung'amue kuwa ubora wa utawa hautegemei uwezo wa kuendesha shughuli; hata maumivu ni fursa ya kujiunga na Kristo mteswa na kujiaminisha mikononi mwa Baba.

Wasiojiweza tena wasijione mzigo, bali wasadiki kuwa wamealikwa mbele zaidi katika fumbo la Pasaka, wachangie ustawi wa chama na wa utume wake kwa sala na sadaka: matunda yataonekana Bwana atakaporudi.

Wawe pia tayari kutoa huduma ya uongozi wa Kiroho; wasipofikiria matatizo yao tu, bali wakidumisha upendo, furaha, amani na tumaini, wanaweza kumtegemeza sana kijana: shuhuda, busara na sala zao zinamtia moyo mfululizo katika safari yake.

Kusudi wasijione pembeni katika maisha ya jamaa, tuthamini uwepo wao na kupokea utendaji wao, pamoja na kuwapatia kidugu misaada wanayohitaji kwa roho na mwili, tukithibitisha ukweli wetu kama familia iliyokusanyika kwa jina la Bwana.

Saa ya kufa katika Bwana iandaliwe na kungojewa kama tendo kuu la kujitoa kwake kwa upendo, kwa kuwa ndipo Baba anapoikamilisha kazi ambayo aliianza ndani mwetu akaifanya kwa miaka kadhaa.

 

 

6.3.            NAFASI ZA PEKEE

 

Bila ya kutegemea hatua hizo, tunaweza tukapatwa na magumu kwa sababu za nje (k.mf. uhamisho, kazi mpya, matatizo ya kazi, uhaba wa matunda katika utume, misiba, hisi ya kutoeleweka au kutengwa) au za ndani (k.mf.ugonjwa, ukavu rohoni, vishawishi vikali, wasiwasi juu ya imani au wito, hisi ya kutokuwa na maana).

Tuyakabili hayo yote kwa hakika ya kuwa kilicho muhimu ni kudumu kiaminifu katika wito: udumifu huo unashuhudia vema fumbo la Pasaka, yaani imani katika Bwana mshindi anayeshika mikononi mwake watu binafsi na mataifa, miundo yao na historia yote.

Tuyatazame majaribu yenyewe kama njia za kulelewa na Baba na za kuokolewa na nguvu ya msalaba.

Uaminifu unapokuwa wa shida, mtawa asaidiwe na ndugu binafsi na jumuia nzima kwa upendo na tumaini: hasa ujirani wa mtumishi na wa mlinzi ni wa lazima.

Hao na ndugu wahusika wafanye juhudi za pekee katika malezi kwenye nafasi zifuatazo: wakati wa uhamisho kati ya watu wa utamaduni tofauti, miaka ya kwanza baada ya upadirisho, vipindi vigumu vya binafsi, jubilei n.k.

Miaka kumi baada ya ahadi ya kwanza ndugu anaweza kutumia mwaka mzima asisitize kipaumbele cha uhusiano na Mungu, kwa kuwa maisha yetu ni hasa itikio la upendo kwa upendo wake mkuu.

Asiyejisikia hamu ya mwaka huo wa Sabato, aombe walau mwezi mmoja wa mazoezi ya Kiroho ili kutambua kinachomfanya asiwe na hamu ya kukaa zaidi na Bwana.

 

 

6.4.            MSINGI WAKE: MAISHA YA KIROHO

 

Bila ya shaka maisha ya Kiroho ndiyo msingi, kwa kuwa ndiyo njia ya kujitambua mbele ya Mungu, kupokea kila siku changamoto za Neno na za maisha, kufuata karama tuliyojaliwa na kuonja amani ya dhati.

Chini ya Roho Mtakatifu ndugu ajihakikishie nafasi za kimya na kujiombea mfululizo ushindi katika mapigano.

Wito wa Mungu na itikio la mtu vinaendelea maisha yote kwa namna ambazo pengine hazieleweki wala kutarajiwa, ila zinamdai daima mtu awe tayari kumfuata Mwanakondoo kokote.

Uhai wa Kiroho unadumu pale ambapo katika hatua yoyote mtu anatafuta na kuona namna maalumu za kuishi, kutumikia na kupenda upya.

Ustawi wa mtawa binafsi ni baraka kwa chama kizima na chemchemi ya nguvu katika utume kwa manufaa ya watu tunaowalenga.

Vilevile mwamko wa jumuia unaimarisha maisha ya pamoja na ushirikiano kati ya ndugu tofauti kwa asili, umri, elimu n.k. na hivyo unakuza ushuhuda wetu wa Kiinjili.

 

 

6.5.            KUJENGA JUMUIA

 

Malezi ya kudumu hayamlengi tu ndugu binafsi, bali jumuia pia ikomae katika upendo kwa Mungu na kwa ndugu wote, wa ndani na wa nje yake.

Ombi la umoja la Bwana Yesu linatuita mfululizo tuukaribie zaidi na zaidi kwa njia ya usikivu kwa Neno na kwa lishe ya Mwili na Damu: ndio chakula cha sikuzote kwa safari ya kumrudia Baba.

Mezani hapo hotuba inatakiwa kututia moyo tuanze upya kila leo.

Huduma ya Neno ina namna nyingine pia, kama vile:

- kusoma na kutafakari pamoja Maandiko, hasa kwa njia ya lectio divina ili kuyaitikia Kikanisa na kijumuia;

- kuchambua matukio kwa msaada wa mafundisho ya Kanisa kuhusu jamii ili kupima kama yanalingana au kupishana na Injili;

- kufafanua liturujia ili kuzidi kung'amua maana ya sala, ishara na vitendo, namna ya kushiriki, kunyamaza na kuzama katika mafumbo yanayoadimishwa;

- kutoa mawaidha ya dharura yanayojaribu kufasiri nafasi maalumu za maisha ya mtu, jumuia, Kanisa na jamii ili kuziishi kwa imani;

- kuhimiza mikakati ya Kiroho ili kuimarisha misimamo, kupanua mitazamo na kudumisha sala na uwajibikaji;

- kuchimba kwa mpango imani ya Kikristo ili kukuza ujuzi wake na kumwezesha kila ndugu ashuhudie ulimwenguni sababu za kutumaini.

 

 

6.6.           NDANI YA CHAMA

 

Sawa na hatua za kuingizwa, malezi ya kudumu yanafanyika ndani ya jamaa na kwa kushirikiana na watumishi na walinzi waliokabidhiwa na Kanisa mamlaka na majukumu ya kufundisha, kutakasa na kuongoza wanachama wenzao, wakichochea karama yao wasichoke.

Maisha yenyewe, yakifuatwa kwa dhati, kulingana na Injili na mazingira tuliyopangiwa na Mungu ndiyo jambo la kwanza, la thamani na la kudumu linalochangia ustawi wetu.

Pamoja na hayo, halmashauri kuu ielekeze njia za kukomaa hasa Kiroho na nafasi za kuchimba ujuzi unaotuhusu, kadiri tunavyoweza na tunavyohitaji, bila ya kutegemea mno taasisi za nje.

Kwa ajili hiyo imteue ndugu mwenye jukumu la kushughulikia malezi ya kudumu katika jamaa nzima kama jambo la lazima kwa wote.

Mawasiliano ni moja kati ya mambo ya kibinadamu yenye uzito mkubwa kwa jumuia za kitawa: ili tuwe ndugu ni lazima tufahamiane, na ili tufahamiane ni muhimu kufungamana kwa upana na kwa undani.

Kwa kawaida mikutano, ziara, barua, majarida, vikilingana na mtindo wetu hasa upande wa ufukara, vinaimarisha roho ya kifamilia, hamu ya kujihusisha na maisha ya chama, na umoja katika utume.

 

 

6.7.           MIKUTANO NA USHIRIKISHANO

 

Mikutano juu ya hati za Kanisa na juu ya maswala yetu inafaa pia kwa kusikiliza wenzetu, kushirikisha mawazo, kukosoana kidugu, kukagua maisha, kutathmini yaliyopita na kupanga pamoja.

Udugu unaimarika kadiri yalivyo muhimu yale tunayoshirikishana, kama vile Neno, imani na mang'amuzi ya Kiroho.

Kosa la kutoshirikishana vya kutosha mambo hayo linaweza likachangia ubinafsi na kishawishi cha kujali mafungamano na watu wa nje kuliko yale na ndugu wa ndani.

Fursa hizo zinahitajika hasa katika jumuia kubwa au wakiishi pamoja watawa mbalimbali kwa asili, umri, elimu na mang'amuzi, waweze kuungana kwa kutumia utajiri huo wote.

Katika utekelezaji mlinzi ana nafasi muhimu, hivyo asaidiwe kuzifanikisha.

 

 

6.8.           UAMINIFU KWA KARAMA

 

Malezi ya kudumu si kujiendeleza upande wa elimu na kazi tu, bali ni kujifanya upya mfululizo kwa kuchochea karama yetu na kustawisha uaminifu kwa ahadi yetu katika kila nafasi ya maisha.

Kwa ahadi kila mmojawetu amejitoa kwa Baba ndani ya chama, hivyo anaitwa daima azidi kuungana na ndugu wengine katika kumfuata Yesu kadiri ya karama ya Kifransisko.

Hiyo ni sharti la msingi la umoja wetu katika jumuia na katika utume, kwa hiyo tuielewe sawasawa, tuzidi kujisomea na kuhudhuria kozi kuhusu mwanzilishi, roho, historia na umisionari wa familia yake, kanuni na katiba zetu, ili tuwe pamoja hata tunapokabili hali mpya za maisha.

Tukumbuke pia kuwa karama yoyote inazaliwa ndani ya Kanisa kwa ajili ya uzima wa ulimwengu; hivyo itakuwa hai kadiri inavyozingatia asili yake hiyo na lengo lake hilo.

 

 

6.9.           MASOMO

 

Masomo yanatakiwa kutokeza hamu isiyozimika ya kumjua zaidi Mungu, asili ya mwanga na ukweli wote: kwa hiyo elimu yote iendelee kujengeka juu ya ujuzi imara wa mafundisho ya imani.

Badala ya kusomasoma magazeti kwa udadisi, tunahitaji juhudi za kudumu upande wa akili kama njia ya kujilea na kujikamilisha iliyo muhimu hasa leo, tunapokabiliana na mabadiliko yanayoyumbisha.

Lengo lisiwe kuabudu elimu wala kujidai, bali kukuza sala na ushirikiano, uwezo wa kupima na kuchuja mambo, pamoja na kuelewa watu na maisha yao, tusije tukaishia katika sura za nje na mitazamo ya juujuu, wala kujihisi tumebaki nyuma na kuanzisha mambo kwa pupa tu.

Wajibu wa kusoma hauishii katika malezi ya msingi wala katika kujipatia vyeti na digrii.

Hivyo wakati wowote wa maisha yetu tunaweza tukaitwa kufuata masomo maalumu: hicho ni kipindi nyeti hasa tusipoweza kuyaendesha wenyewe.

Ikiwabidi ndugu waishi nje ya jumuia zetu, halmashauri kuu iwachagulie kituo ambacho kinahakikisha malezi bora ya Kiroho na ya kitume, ya kinadharia na ya kiutendaji, na kuwezesha kushika masharti yetu ya udugu na udogo, ufukara, sala na uaminifu kwa Ualimu wa Kanisa.

Wenyewe wajitahidi binafsi na kwa pamoja kulinganisha masomo wanayofuata na tunu za Kifransisko, wakisaidiwa na mlezi wao na wataalamu.

Tujiendeleze vilevile kuhusu ufundi ili kutumia misaada ya maendeleo, mradi tusiachane na ufukara wetu.

Tujihadhari na vipingamizi vya malezi ya kudumu: kuzama katika kazi, kupuuzia haja ya kujiendeleza mfululizo na kuogopa utambuzi wa hali halisi ya roho.

 

 

 

 

7. HATIMA: MAMA MARIA

 

7.1.            MARIA NA UTATU

 

Maria, mfano bora wa upokeaji wa neema, anatukumbusha kwamba Mungu Baba ndiye anayeanza na kuwezesha daima mema yote.

Kwa jinsi alivyoishi na Yesu Nazareti na kuhudhuria nafasi muhimu za utume wake, anatufundisha kumfuata pasipo masharti na kumtumikia kwa ukarimu.

Akiwa hekalu la Roho Mtakatifu, ndani mwake unang'aa uumbaji mpya.

Maria anafungamana sana na Kanisa pia kama kiungo bora na mama.

Tukimtazama hivyo kama kielelezo cha kuwekwa wakfu kwa Baba, kuungana na Mwana hadi msalabani na kuwa wazi kwa Roho, tuelewe na kuonyesha ya kuwa kufuata maisha manyenyekevu na safi ya Yesu ni kuiga maisha ya Maria pia.

 

 

7.2.            MARIA NA WITO

 

Daima yeye anashiriki kazi ya Roho Mtakatifu, kama katika umwilisho na siku ya Pentekoste.

Aliyoyafanya karibu na Yesu anayaendeleza kwa manufaa ya Mwili wake mzima na ya kila Mkristo, hasa yule anayewajibika kumfuata Mwanae kwa karibu zaidi.

Mama Maria yupo pale wito unapoanza, unapoundwa na unapostawi: uwepo huo ni muhimu kwa kila mmoja na kwa uimara na umoja wa jumuia nzima.

Kwa hiyo fungamano na Bikira Maria lizingatiwe katika hatua zote.

Tuwaombee watumishi, walinzi, walezi na ndugu wote wadumu kwa uaminifu chini ya ulinzi wake.

 

 

7.3.            KUMUIGA MARIA

 

Katika maneno yake ya "Fiat" na "Magnificat" tunakuta ukamilifu wa imani, tumaini na upendo katika kukubali mpango wa Baba na wa furaha inayotokana na hali hiyo.

Malezi yote yaelekeze njia hiyo ya hakika katika kusikiliza na kutekeleza Neno na hivyo kufanikisha lengo la utawa.

Bikira wa Maamkio na wa Kana atusaidie kuitikia shida za watu kwa kuleta msaada, lakini hasa kwa kumleta na kumdhihirisha Yesu ili wafanye yote atakayowaambia, halafu watangaze pamoja naye maajabu ambayo Mwenyezi Mungu anawatendea wanyonge wanaokiri jina lake takatifu.

LINKS:

 

WIMBO WA TAIFA

Mungu Ibariki Afrika

Wabariki viongozi wake

Hekima, umoja na amani

Hizi ni ngao zetu

Afrika na watu wake. 

CHORUS:    

Ibariki, Afrika

Ibariki, Afrika

Tubariki, watoto wa Afrika

Morogoro: cappella maschile - Morogoro: kikanisa chajumuia ya kiume - Morogoro: the chapel of the brothers